Hazina Yetu Katika Vyombo vya Udongo
“Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.”—2 WAKORINTHO 4:7.
1. Kielelezo cha Yesu chapaswa kututiaje moyo?
ALIPOKUWA akifinyangwa na Yehova hapa duniani, Yesu alipata kujua moja kwa moja udhaifu mbalimbali wa wanadamu. Kielelezo chake cha kushika uaminifu-maadili chapaswa kututia moyo kama nini! Mtume atuambia: “Kwa kweli, kwenye mwendo huu mliitwa, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Kwa kunyenyekea chini ya kufinyangwa huko, Yesu aliushinda ulimwengu. Pia, aliwajasirisha mitume wake wawe washindi. (Matendo 4:13, 31; 9:27, 28; 14:3; 19:8) Na ni kitia-moyo kikubwa kama nini alichotoa katika umalizio wa hotuba yake ya mwisho! Alitangaza hivi: “Nimewaambia nyinyi mambo haya ili kupitia mimi mpate kuwa na amani. Ulimwenguni mnakuwa na dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:33.
2. Tofauti na hali ya upofu ya ulimwengu, sisi tuna mmuliko gani?
2 Vilevile, baada ya kutofautisha hali ya upofu iliyoletwa na “mungu wa huu mfumo wa mambo” na “mmuliko wa habari njema yenye utukufu,” mtume Paulo alisema hivi kuhusu huduma yetu yenye thamani: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe. Twasongwa katika kila njia, lakini hatufinywi kupita tuwezavyo kusonga; twafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa; twateswa, lakini hatuachwi kabisa bila msaada; twaangushwa chini, lakini hatuangamizwi.” (2 Wakorintho 4:4, 7-9) Ingawa sisi ni “vyombo vya udongo” vilivyo dhaifu, Mungu ametufinyanga sana kwa roho yake takatifu hivi kwamba twaweza kuushinda kabisa ulimwengu wa Shetani.—Waroma 8:35-39; 1 Wakorintho 15:57.
Kufinyanga Katika Israeli la Kale
3. Isaya alifafanuaje kufinyangwa kwa taifa la Kiyahudi?
3 Yehova hufinyanga watu mmoja-mmoja na pia mataifa mazima-mazima. Kwa kielelezo, Israeli la kale liliponyenyekea ufinyanzi wa Yehova, lilisitawi. Lakini hatimaye likajifanya kuwa gumu na kukosa kutii. Tokeo lilikuwa kwamba Mfinyanzi wa Israeli alileta “ole” juu ya taifa hilo. (Isaya 45:9) Katika karne ya nane K.W.K., Isaya alizungumza na Yehova kuhusu hali yenye dhambi ya Israeli iliyokuwa dhahiri, akisema: “Ee BWANA, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu; sisi sote tu kazi ya mikono yako. . . . Vitu vyetu vyote vyenye kupendeza vimeharibika.” (Isaya 64:8-11) Israeli lilikuwa limefinyangwa kuwa chombo kilichofaa tu kuharibiwa.
4. Ni kielezi kipi ambacho kiliigizwa na Yeremia?
4 Karne moja baadaye, siku ya kutoa hesabu ilipokaribia, Yehova alimwambia Yeremia achukue gudulia la udongo na aende pamoja na wanaume wazee wa Yerusalemu kwenye Bonde la Hinomu, akimwagiza hivi: “Hapo utalivunja gudulia lile, mbele ya macho ya watu wale waendao pamoja nawe, na kuwaambia, BWANA wa majeshi asema hivi, Hivyo ndivyo nitakavyowavunja watu hawa, na mji huu, kama mtu avunjavyo chombo cha mfinyanzi, kisichoweza kutengenezwa tena na kuwa kizima.”—Yeremia 19:10, 11.
5. Hukumu ya Yehova dhidi ya Israeli ilikuwa kubwa kadiri gani?
5 Katika 607 K.W.K., Nebukadneza aliharibu Yerusalemu kabisa pamoja na hekalu lake na kuwapeleka Wayahudi walionusurika utekwani huko Babiloni. Lakini baada ya miaka 70 uhamishoni, Wayahudi wenye kutubu waliweza kurudi na kujenga upya Yerusalemu na hekalu lake. (Yeremia 25:11) Hata hivyo, kufikia karne ya kwanza W.K., taifa hilo lilikuwa limemwacha tena Mfinyanzi Mkuu, na hatimaye hali yake ya kiadili ikashuka kufikia kiwango cha kufanya uhalifu mbaya sana wa kumwua Mwana wa Mungu. Katika 70 W.K., Mungu alitumia Serikali ya Ulimwengu ya Roma kama mfishaji wake katika kufutilia mbali mfumo wa mambo wa Kiyahudi na kuponda tikitiki Yerusalemu na hekalu lake. Taifa la Israeli halingefinyangwa tena kamwe kwa mkono wa Yehova likiwa kitu ‘kitakatifu na kizuri.’a
Kufinyanga Taifa la Kiroho
6, 7. (a) Paulo anafafanuaje kufinyangwa kwa Israeli wa kiroho? (b) Idadi kamili ya “vyombo vya rehema” ni gani, nayo ilifanyizwaje?
6 Wayahudi waliomkubali Yesu walifinyangwa wakawa washiriki wa msingi wa taifa jipya, “Israeli wa Mungu” wa kiroho. (Wagalatia 6:16) Basi, maneno haya ya Paulo yanafaa: “Ama je, mfinyanzi hana mamlaka juu ya udongo wa mfinyanzi kufanya kutokana na donge lilelile chombo kimoja kwa utumizi wenye kuheshimika, kingine kwa utumizi usio wenye kuheshimika? . . . Mungu, ingawa anayo nia ya kuonyesha hasira ya kisasi yake na kujulisha nguvu yake, alivumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa vifae kuharibiwa, ili apate kujulisha utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema, alivyotayarisha kimbele kwa ajili ya utukufu.”—Waroma 9:21-23.
7 Yesu aliyefufuliwa alijulisha baadaye kwamba idadi ya “vyombo [hivyo] vya rehema” ingekuwa 144,000. (Ufunuo 7:4; 14:1) Kwa kuwa Israeli la asili halikuwa limetoa idadi hiyo ikiwa kamili, Yehova aliwaonyesha watu wa mataifa rehema. (Waroma 11:25, 26) Kutaniko jipya la Kikristo lilipanuka haraka. Katika muda wa miaka 30 habari njema ilikuwa “[iki]hubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23) Jambo hilo lilihitaji kuyaweka makutaniko mengi ya mahali hapo yaliyokuwa yametawanyika chini ya uangalizi ufaao.
8. Ni nani waliofanyiza baraza linaloongoza la kwanza, na kikundi hicho kilikuaje?
8 Yesu alikuwa ametayarisha mitume 12 ili wawe baraza linaloongoza la kwanza, akiwazoeza mitume hao pamoja na watu wengine kwa ajili ya huduma. (Luka 8:1; 9:1, 2; 10:1, 2) Siku ya Pentekoste 33 W.K., kutaniko la Kikristo lilianzishwa, na kwa wakati upasao baraza lake linaloongoza likapanuliwa kutia ndani “mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu.” Yaonekana, Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, alitumikia kwa kipindi kirefu akiwa mwenyekiti, ingawa yeye hakuwa mtume. (Matendo 12:17; 15:2, 6, 13; 21:18) Kulingana na mwanahistoria Eusebius, mitume walikuwa shabaha ya pekee ya mnyanyaso nao walitawanyika katika maeneo mengine. Muundo wa baraza linaloongoza ulirekebishwa kulingana na hali.
9. Ni tukio gani lenye kusikitisha ambalo Yesu alitabiri lingetokea?
9 Mwishoni mwa karne ya kwanza, ‘yule adui, ambaye ni Ibilisi,’ alianza ‘kupanda magugu’ miongoni mwa warithi wa “ufalme wa mbingu” walio kama ngano. Yesu alikuwa ametabiri kwamba tukio hilo lenye kusikitisha lingeruhusiwa hadi wakati wa kuvuna katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” Ndipo, ‘waadilifu wangeng’aa tena kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.’ (Mathayo 13:24, 25, 37-43) Huo ungekuwa wakati gani?
Kufinyanga Israeli la Mungu Leo
10, 11. (a) Kufinyangwa kwa Israeli wa Mungu wa siku hizi kulianzaje? (b) Ni mafundisho gani yenye kutofautiana ambayo yangepatikana katika Jumuiya ya Wakristo na miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia wenye bidii?
10 Katika mwaka wa 1870, Charles Taze Russell alifanyiza kikundi cha kujifunza Biblia katika Pittsburgh, Pennsylvania, Marekani. Katika mwaka wa 1879 alianza kuchapisha gazeti la kila mwezi ambalo leo laitwa Mnara wa Mlinzi. Punde si punde, wanafunzi hao wa Biblia, kama walivyoitwa, walifahamu kwamba Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imekubali mafundisho ya kipagani yasiyo ya Kimaandiko, kama vile kutokufa kwa nafsi, moto wa helo, purgatori, mungu wa Utatu, na ubatizo wa vitoto vichanga.
11 Ingawa hivyo, jambo la muhimu zaidi ni kwamba hawa wapenda-kweli ya Biblia walirudisha mafundisho ya msingi ya Biblia, kama vile ukombozi kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu, na kufufuliwa kwenye uhai udumuo milele katika dunia paradiso yenye amani chini ya Ufalme wa Mungu. Zaidi ya yote, mkazo uliwekwa juu ya kutetewa karibuni kwa Yehova Mungu kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Wanafunzi wa Biblia waliamini kwamba Sala ya Bwana ilikuwa karibu kujibiwa: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:9, 10) Walikuwa wakifinyangwa na roho takatifu ya Mungu kuwa jamii ya ulimwenguni pote ya Wakristo wapenda-amani.
12. Wanafunzi wa Biblia walikuja kufahamuje tarehe fulani muhimu?
12 Funzo barabara la Danieli sura ya 4 na unabii mwingine mbalimbali uliwasadikisha Wanafunzi wa Biblia kwamba kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme wa Kimesiya lazima kulikuwa kumekaribia. Walifahamu kwamba mwaka wa 1914 ungekuwa tarehe ya kumalizika kwa “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa.” (Luka 21:24; Ezekieli 21:26, 27) Hao Wanafunzi wa Biblia walipanua utendaji wao kwa haraka, wakifanyiza madarasa ya Biblia (ambayo baadaye yaliitwa Makutaniko) kotekote Marekani. Mwanzoni mwa miaka ya 1900, kazi yao ya kufundisha Biblia ilipanuliwa hadi Ulaya na Australasia. Kuwepo kwa mpango mzuri kukawa jambo la lazima.
13. Wanafunzi wa Biblia walipata uhalali gani wa kisheria, naye msimamizi wa kwanza wa Sosaiti alitoa utumishi gani wenye kutokeza?
13 Ili kuwapa Wanafunzi wa Biblia uhalali wa kisheria, Zion’s Watch Tower Tract Society lilifanywa kuwa shirika mwaka wa 1884 huko Marekani, makao makuu yakiwa Pittsburgh, Pennsylvania. Waelekezi wake walitumika wakiwa Baraza kuu Linaloongoza, wakisimamia kuhubiriwa tufeni pote kwa Ufalme wa Mungu. Msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, Charles T. Russell, aliandika mabuku sita ya Studies in the Scriptures na kufanya safari ndefu za kuhubiri. Pia alichanga fedha nyingi alizokuwa amekusanya kabla ya kuanza kujifunza Biblia, kwa ajili ya kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote. Katika mwaka wa 1916, huku Vita Kuu ikiendelea vikali huko Ulaya, Ndugu Russell aliyekuwa mchovu alikufa akiwa katika safari ya kuhubiri. Alikuwa ametoa kila kitu kwa ajili ya kupanua kutolewa kwa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu.
14. J. F. Rutherford ‘alipiganaje pigano bora’? (2 Timotheo 4:7)
14 Joseph F. Rutherford, ambaye kwa muda alikuwa hakimu katika Missouri, akawa msimamizi aliyefuata. Kwa sababu ya kutetea kwake kweli ya Biblia bila hofu, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo waliungana na wanasiasa katika ‘kutunga madhara kwa njia ya sheria.’ Katika Juni 21, 1918, Ndugu Rutherford na Wanafunzi wa Biblia wengine saba wenye kuongoza walifungwa jela, wakiwa wamehukumiwa vifungo mbalimbali vya miaka 10 au 20 ambavyo wangetumikia wakati uleule. Wanafunzi hao wa Biblia walijitetea. (Zaburi 94:20; Wafilipi 1:7) Walipokata rufani, waliachiliwa Machi 26, 1919, na baadaye shtaka la uwongo la uchochezi likaondolewa kabisa.b Jambo hilo lililowapata liliwafinyanga wakawa watetezi hodari wa ile kweli. Kwa msaada wa Yehova walijaribu kila njia iwezekanayo kushinda katika pigano la kiroho la kuhubiri habari njema, licha ya upinzani wa Babiloni Mkubwa. Pigano linaloendelea hadi mwaka huu wa 1999.—Linganisha Mathayo, sura ya 23; Yohana 8:38-47.
15. Kwa nini mwaka wa 1931 ulikuwa muhimu kihistoria?
15 Katika miaka ya 1920 na 1930 Israeli watiwa-mafuta wa Mungu waliendelea kufinyangwa chini ya mwelekezo wa Mfinyanzi Mkuu. Nuru ya kiunabii kutoka katika Maandiko iliangaza, ikitoa utukufu kwa Yehova na kukazia Ufalme wa Kimesiya wa Yesu. Katika mwaka wa 1931 Wanafunzi wa Biblia walishangilia kupokea jina jipya, Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10-12; Mathayo 6:9, 10; 24:14.
16 na sanduku kwenye ukurasa wa 19. Idadi kamili ya wale 144,000 ilikamilika lini, na kuna uthibitisho gani wa jambo hilo?
16 Katika miaka ya 1930, idadi ya “wale walioitwa na waliochaguliwa na walio waaminifu,” wale 144,000, ilionekana kuwa imekamilika. (Ufunuo 17:14; ona sanduku kwenye ukurasa wa 19.) Hatujui ni wangapi wa watiwa-mafuta waliokusanywa katika karne ya kwanza na waliokusanywa kutoka miongoni mwa “magugu” wakati wa karne za giza za uasi-imani mkubwa wa Jumuiya ya Wakristo. Lakini mwaka wa 1935 kulikuwa na jumla ya wahubiri 52,465 ulimwenguni pote, kati ya kilele cha wahubiri 56,153, walioonyesha tumaini lao la kimbingu kwa kushiriki mifano ya Ukumbusho. Je, ni nini ingekuwa hali ya baadaye ya wengi ambao walikuwa bado wakusanywe?
“Tazama! Umati Mkubwa”
17. Ni tukio gani la kihistoria lililotokea mwaka wa 1935?
17 Kwenye mkusanyiko uliofanywa kutoka Mei 30 hadi Juni 3, 1935, huko Washington, D.C., Marekani, Ndugu Rutherford alitoa hotuba muhimu yenye kichwa “Ile Halaiki Kubwa.”c Kikundi hiki, ‘ambacho hakuna mtu aliyeweza kukihesabu,’ kingetokea wakati ambapo kutiwa muhuri kwa wale 144,000 wa Israeli wa kiroho kungekuwa kukikaribia kukamilika. Hao wa kikundi hicho pia wangedhihirisha imani katika nguvu za kufidi za “damu ya Mwana-Kondoo,” Yesu, na kutoa utumishi mtakatifu katika mpango wa hekalu wa Yehova wa ibada. Wakiwa kikundi, ‘wangetoka katika dhiki kubwa’ wakiwa hai, ili kurithi Paradiso ya kidunia ambapo “kifo hakitakuwapo tena.” Miaka kadhaa kabla ya mkusanyiko huo, kikundi hiki kilikuwa kimesemwa kuwa cha Wayonadabu.—Ufunuo 7:9-17; 21:4; Yeremia 35:10.
18. Mwaka wa 1938 ulikuwa muhimu katika njia zipi?
18 Mwaka wa 1938 ulikuwa muhimu katika kutambulisha waziwazi jamii hizi mbili. Matoleo ya Mnara wa Mlinzi (ya Kiingereza) ya Machi 15 na Aprili 1, 1938, yalikuwa na funzo lenye sehemu mbili lenye kichwa “Kundi Lake” na lilionyesha wazi mahali panapowahusu mabaki watiwa-mafuta na waandamani wao, umati mkubwa. Kisha matoleo ya Juni 1 na Juni 15 (ya Kiingereza) yalikuwa na makala za kujifunza juu ya “Tengenezo,” zilizotegemea Isaya 60:17. Makutaniko yote yaliombwa yatoe ombi kwa Baraza Linaloongoza ili liweke rasmi watumishi katika makutaniko yao, hivyo wakianzisha mpango wa kitheokrasi ulioboreka, wenye kuagizwa na Mungu. Makutaniko yalifanya vivyo hivyo tu.
19 na kielezi-chini. Ni mambo gani ya hakika yathibitishayo kwamba mwito wa kijumla wa “kondoo wengine” umekuwa ukiendelea sasa kwa zaidi ya miaka 60?
19 Ripoti iliyo katika 1939 Yearbook of Jehovah’s Witnesses ilisema: “Wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo Yesu waliomo duniani leo ni wachache, na idadi yao haitaongezeka kamwe. Hawa wanatambulishwa katika Maandiko kuwa ‘mabaki’ ya wazao wa Zayoni, tengenezo la Mungu. (Ufu. 12:17) Sasa Bwana anajikusanyia ‘kondoo wengine,’ ambao watafanyiza ile ‘halaiki kubwa.’ (Yohana 10:16) Wale wanaokusanywa sasa ni waandamani wa mabaki, ambao wanafanya kazi pamoja na mabaki. Tangu sasa na kuendelea, idadi ya wale wanaofanyiza ‘kondoo wengine’ itaongezeka hadi pale ‘halaiki kubwa’ itakapokusanywa.” Mabaki watiwa-mafuta walikuwa wamefinyangwa ili kushughulikia kukusanywa kwa umati mkubwa. Hao pia lazima sasa wafinyangwe.d
20. Ni mabadiliko gani ya kitengenezo ambayo yametokea tangu mwaka wa 1942?
20 Katika Januari 1942, wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa imechacha zaidi, Joseph Rutherford alikufa naye Nathan Knorr akachukua mahali pake akiwa msimamizi. Msimamizi wa tatu wa Sosaiti anakumbukwa kwa shauku kwa kuanzisha shule za kitheokrasi makutanikoni na Shule ya Gileadi ya kuzoeza wamishonari. Kwenye mkutano wa kila mwaka wa Sosaiti katika 1944, yeye alitangaza kwamba hati ya katiba ya Sosaiti ilikuwa ikisahihishwa ili uanachama utegemee, si michango ya vitu vya kimwili, bali hali ya kiroho. Kipindi cha miaka 30 iliyofuata, idadi ya wafanyakazi wa shambani iliongezeka kutoka watu 156,299 hadi watu 2,179,256 duniani pote. Katika mwaka wa 1971-1975 mabadiliko zaidi ya kitengenezo yalihitajiwa. Haingewezekana tena kwa mtu mmoja aliyetumikia akiwa msimamizi atoe uangalizi kamili wa kazi ya Ufalme ulimwenguni pote. Baraza Linaloongoza, likiwa na mwenyekiti aliyetumika kwa zamu, lilipanuliwa kuwa na washiriki 18, ambao karibu nusu yao sasa wamemaliza mwendo wao duniani.
21. Ni nini kimewafanya washiriki wa kundi dogo wastahili Ufalme?
21 Washiriki wanaobaki wa kundi dogo wamefinyangwa kupitia miongo mingi ya majaribu. Wao ni wenye moyo mkuu, wakiwa wamepokea waziwazi ‘ushahidi wa roho.’ Yesu amewaambia: “Nyinyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami nafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu amefanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa kwenye meza yangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.”—Waroma 8:16, 17; Luka 12:32; 22:28-30.
22, 23. Kundi dogo na kondoo wengine wanafinyangwa namna gani?
22 Kwa kuwa idadi ya mabaki waliotiwa mafuta kwa roho imepungua, ndugu wakomavu wa umati mkubwa wamepewa usimamizi wa karibu makutaniko yote duniani pote. Na wakati Mashahidi watiwa-mafuta wa mwisho walio wazee wamalizapo mwendo wao wa kidunia, sa·rimʹ, yaani, wakuu wa kifalme wa kondoo wengine watakuwa wamezoezwa vizuri kutekeleza wajibu mbalimbali wa kiutawala wakiwa jamii ya mkuu duniani.—Ezekieli 44:3; Isaya 32:1.
23 Kundi dogo na vilevile kondoo wengine wanaendelea kufinyangwa kuwa vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika. (Yohana 10:14-16) Tumaini letu liwe katika “mbingu mpya” au liwe katika “dunia mpya,” na tuitikie kwa moyo wote mwaliko wa Yehova: “Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.” (Isaya 65:17, 18) Acheni sisi viumbe dhaifu tutumikie sikuzote kwa unyenyekevu, tukifinyangwa na “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida”—nguvu ya Mungu ya roho takatifu!—2 Wakorintho 4:7; Yohana 16:13.
[Maelezo ya chinis]
a Acheni Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi, iliyofananishwa na Israeli la kale, ipate onyo kuhusu hukumu sawa na hiyo kutoka kwa Yehova.—1 Petro 4:17, 18.
b Hakimu Manton, Mkatoliki wa Kiroma ambaye alikataa kuachilia Wanafunzi wa Biblia kwa dhamana, baadaye yeye mwenyewe alifungwa jela kwa kupatikana na hatia ya kupokea rushwa.
c Ile Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, iliyotolewa mwaka wa 1950, hutumia “umati mkubwa,” kama tafsiri bora ya neno la Kigiriki lililopuliziwa.
d Katika mwaka wa 1938 hudhurio la Ukumbusho la ulimwenguni pote lilikuwa 73,420, na watu 39,225—asilimia 53 ya wale waliokuwapo—walishiriki mifano. Kufikia mwaka wa 1998 hudhurio lilikuwa limeongezeka likafikia watu 13,896,312, na watu 8,756 tu ndio walioshiriki mifano, wastani unaopungua mshiriki mmoja kwa kila makutaniko 10.
Je, Wakumbuka?
◻ Yesu alikuwaje Kielelezo chema kwetu katika kunyenyekea kufinyangwa na Baba yake?
◻ Ni kufinyanga kupi kulikotokea katika Israeli la kale?
◻ “Israeli wa Mungu” wamefinyangwa namna gani hadi kufikia sasa?
◻ “Kondoo wengine” wamefinyangwa kwa kusudi gani?
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
Kufinyanga Zaidi Katika Jumuiya ya Wakristo
Ripoti moja kutoka shirika la habari la Associated Press la Athens, Ugiriki, ilisema yafuatayo juu ya kuwekwa rasmi kwa kiongozi wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki: “Anapaswa kuwa mjumbe wa amani. Lakini kiongozi wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki anavuma zaidi kama jemadari anayejitayarishia pigano.
“‘Tuko tayari, ikiwa lazima, kumwaga damu na kutoa dhabihu. Sisi kama kanisa, twaombea amani . . . Lakini twabariki silaha takatifu hali ikitutaka tufanye hivyo,’ Askofu mkuu Christodoulos alisema hivyo hivi majuzi katika siku takatifu ya Kupazwa kwa Bikira, ambayo pia husherehekewa ikiwa siku ya majeshi ya Ugiriki.”
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
“Hakuna Kuongezwa Wengine Zaidi!”
Wakati wa kuhitimu huko Gileadi mwaka wa 1970, Frederick Franz, aliyekuwa wakati huo makamu-msimamizi wa Watch Tower Society, aliwaambia wanafunzi juu ya uwezekano wa kwamba wao, wote wakiwa wa kondoo wengine wenye matumaini ya kidunia, huenda wangebatiza mtu ambaye angeweza kudai kuwa wa mabaki watiwa-mafuta. Je, hilo lawezekana? Alieleza kwamba Yohana Mbatizaji alikuwa wa kondoo wengine, na alimbatiza Yesu na baadhi ya mitume. Kisha akauliza kama bado kulikuwa na mwito wa kukusanya mabaki zaidi. “La, hakuna kuongezwa wengine zaidi!” akasema. “Mwito huo ulikoma huko nyuma katika 1931-1935! Hakuna kuongezwa wengine zaidi. Basi, ni nani wale washiriki wapya wachache ambao wanashiriki mifano ya Ukumbusho? Ikiwa wao ni kati ya mabaki, basi wao wanachukua mahali pa wengine! Wao si wengine zaidi ambao wameongezwa wawe mabaki, lakini wanachukua mahali pa wengine ambao huenda wameasi.”
[Picha katika ukurasa wa 15]
Twathamini kama nini hazina yetu ya utumishi!
[Picha katika ukurasa wa 16]
Israeli la kale lilikuja kuwa chombo kilichofaa tu kuharibiwa