Yule Mfinyanzi Mkuu na Kazi Yake
“[Uwe] chombo kwa kusudi lenye kuheshimika, . . . kilichotayarishwa kwa kila kazi njema.”—2 TIMOTHEO 2:21.
1, 2. (a) Uumbaji wa Mungu wa mwanamume na mwanamke ulikuwaje kazi yenye kutokeza? (b) Mfinyanzi Mkuu aliwatokeza Adamu na Hawa kwa kusudi gani?
YEHOVA ndiye Mfinyanzi Mkuu. Kuumbwa kwa Adamu, mzazi wetu wa kwanza, kulikuwa kazi yenye kutokeza zaidi kati ya uumbaji wake. Biblia hutuambia: “Yehova Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai,” yaani, “kiumbe kinachopumua.” (Mwanzo 2:7, NW, kielezi-chini) Mwanadamu wa kwanza kuumbwa alikuwa mkamilifu, amefanyizwa hasa kwa mfano wa Mungu, uthibitisho wa hekima Yake ya kimungu na kupenda kwake uadilifu wa kweli na pia haki.
2 Akitumia ubavu wa Adamu, Mungu pia alifinyanga—mwanamke—kikamilisho na msaidizi wa mwanamume. Urembo wa Hawa usio na dosari ulipita kabisa hata ule wa wanawake ambao ni warembo zaidi siku hizi. (Mwanzo 2:21-23) Isitoshe, wenzi wa kwanza wa kibinadamu walipewa miili na uwezo mbalimbali uliobuniwa kikamilifu ili kutimiza mradi waliogawiwa wa kufanya dunia hii kuwa paradiso. Walipewa pia uwezo wa kutekeleza amri ya Mungu iliyotolewa kwenye Mwanzo 1:28: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” Hatimaye, mabilioni ya wanadamu wenye shangwe wangekuwa wakazi wa bustani hii ya ulimwenguni pote, wakiwa wameunganishwa pamoja katika aina ya upendo ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14.
3. Wazazi wetu wa kwanza walikuja kuwa vyombo visivyoheshimika jinsi gani, na matokeo yakawa nini?
3 Kwa kusikitisha, wazazi wetu wa kwanza waliamua kuasi dhidi ya mamlaka ya Muumba wao Mwenye Enzi Kuu, Mfinyanzi Mkuu. Mwenendo wao ukawa kama ifafanuliwavyo kwenye Isaya 29:15, 16: “Ole wao wanaojitahidi kumficha BWANA mashauri yao, na matendo yao yamo gizani, nao husema, Ni nani atuonaye? nani atujuaye? . . . . Je! mfinyanzi ahesabiwe kuwa kama udongo; kitu kilichofinyangwa kimnene yeye aliyekifinyanga, Hakunifinyanga huyu; au kitu kilichoumbwa kimnene yeye aliyekiumba, Yeye hana ufahamu?” Upotovu wao ulitokeza msiba—hukumu ya kifo cha milele. Isitoshe, jamii yote ya kibinadamu iliyotokana nao ilirithi dhambi na kifo. (Waroma 5:12, 18) Uzuri wa uumbaji wa Mfinyanzi Mkuu ukatiwa dosari kubwa.
4. Sisi twaweza kutumikia kusudi gani lenye kuheshimika?
4 Hata hivyo, hata tukiwa katika hali yetu ya sasa isiyo kamilifu, sisi wazao wa Adamu mwenye dhambi twaweza kumsifu Yehova kwa maneno ya Zaburi 139:14: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” Ingawa hivyo, inasikitisha kama nini kwamba kazi ya mikono ya awali ya Mfinyanzi Mkuu imetiwa dosari kubwa hivyo!
Mfinyanzi Apanua Kazi Yake
5. Ustadi wa Mfinyanzi Mkuu ungetumikaje?
5 Kwa kufurahisha, mbali na uumbaji wake wa kwanza wa wanadamu, Muumba wetu angetumia ustadi wake akiwa Mfinyanzi Mkuu kwa kiwango kikubwa hata zaidi. Mtume Paulo atuambia: “Basi, Ewe mtu, kwa kweli wewe ni nani hata uwe ukimjibu Mungu? Hakika je, kitu kilichofinyangwa kitamwambia yeye aliyekifinyanga, ‘Kwa nini ulinifanya mimi kwa njia hii?’ Ama je, mfinyanzi hana mamlaka juu ya udongo wa mfinyanzi kufanya kutokana na donge lilelile chombo kimoja kwa utumizi wenye kuheshimika, kingine kwa utumizi usio wenye kuheshimika?”—Waroma 9:20, 21.
6, 7. (a) Wengi leo huamuaje kufinyangwa kwa ajili ya kutoheshimika? (b) Waadilifu hufinyangwa namna gani kwa utumizi wenye kuheshimika?
6 Naam, baadhi ya vyombo vya Mfinyanzi Mkuu vitafinyangwa kwa utumizi wenye kuheshimika, ilhali vingine vitafinyangwa kwa utumizi usio wenye kuheshimika. Wale wanaoamua kufuatana na ulimwengu unapoingia ndani zaidi na zaidi katika hali ya kutomcha Mungu wanafinyangwa kwa njia ya kuwatambulisha ili waharibiwe. Wakati Mfalme mtukufu, Yesu Kristo, ajapo kuhukumu, vyombo hivyo visivyoheshimika vitatia ndani wanadamu wakaidi walio kama mbuzi ambao, kama vile andiko la Mathayo 25:46 lisemavyo, “wataondoka kuingia katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele.” Lakini “waadilifu” walio kama kondoo ambao walifinyangwa kwa utumizi “wenye kuheshimika,” watarithi “uhai udumuo milele.”
7 Kwa unyenyekevu, waadilifu hao watakuwa wamejitiisha chini ya ufinyanzi wa kimungu. Wameingia katika njia ya Mungu ya maisha. Wamekubali shauri hili lipatikanalo kwenye 1 Timotheo 6:17-19: ‘Weka tumaini lako, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.’ Wamejitahidi “kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili wao wapate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.” Kweli ya kimungu huwafinyanga nao hudhihirisha imani thabiti katika uandalizi wa Yehova kupitia Kristo Yesu, “aliyejitoa mwenyewe kuwa fidia inayolingana” ili arudishe kilichopotea kwa sababu ya dhambi ya Adamu. (1 Timotheo 2:6) Basi, twapaswa kunyenyekea kwa utayari ulioje shauri la Paulo la “[kujivika] wenyewe utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya [unafinyangwa] kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba”!—Wakolosai 3:10.
Wewe Utakuwa Chombo cha Aina Gani?
8. (a) Ni nini kinachoamua mtu anakuwa chombo cha aina gani? (b) Ni mambo gani mawili ambayo huelekeza jinsi mtu atavyofinyangwa?
8 Ni nini kinachoamua mtu anakuwa chombo cha aina gani? Ni mtazamo wake na mwenendo wake. Hizo husababishwa kwanza na tamaa na mielekeo ya moyo. Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema: “Moyo wa mtu huifikiri njia yake; bali BWANA huziongoza hatua zake.” (Mithali 16:9) Pili, husababishwa na mambo yaliyosikiwa na kuonwa, mashirika na pia mambo yaliyompata mtu. Kwa hiyo, ni muhimu jinsi gani kusikiza shauri hili: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Kama vile andiko la 2 Petro 1:16 lituonyavyo, twapaswa kuepuka kufuata “hadithi zisizo za kweli zilizotungwa kwa usanifu mwingi,” au kulingana na tafsiri ya Katoliki ya Roma ya Knox, “hekaya zilizobuniwa na mwanadamu.” Hadithi hizo zingetia ndani mengi ya mafundisho na misherehekeo ya Jumuiya ya Wakristo iliyoasi.
9. Twaweza kuitikiaje kwa njia ifaayo kufinyangwa na Mfinyanzi Mkuu?
9 Basi, Mungu aweza kutufinyanga kulingana na itikio letu. Twaweza kurudia kwa unyenyekevu mbele za Yehova sala ya Daudi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu; uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu, ukaniongoze katika njia ya milele.” (Zaburi 139:23, 24) Yehova anafanya ujumbe wa Ufalme uhubiriwe. Mioyo yetu imeitikia kwa uthamini habari njema na miongozo zaidi kutoka kwake. Kupitia tengenezo lake yeye hututolea mapendeleo mbalimbali yanayohusiana na kuhubiri habari njema; acheni tuyapokee mapendeleo hayo na kuyathamini sana.—Wafilipi 1:9-11.
10. Twapaswa kujitahidije katika kufuata programu za kiroho?
10 Ni muhimu sana kwamba tukazie Neno la Mungu uangalifu daima, tukifuata programu ya kila siku ya usomaji wa Biblia na kufanya Maandiko na utumishi wa Yehova uwe msingi wa mazungumzo katika familia zetu na miongoni mwa marafiki wetu. Programu ya ibada ya asubuhi, ambayo hufanywa wakati wa kifungua-kinywa na kila familia ya Betheli na pia wamishonari wanaoishi kwenye makao ya wamishonari ya Mashahidi wa Yehova, kwa kawaida hutia ndani usomaji mfupi wa Biblia au kitabu Yearbook cha wakati huo, kila kimoja kikisomwa katika juma tofauti. Je, familia yako yaweza kuwa na mpango kama huo? Sote pia hupokea manufaa zilizoje, kupitia ushirika katika kutaniko la Kikristo, kukutana kwetu pamoja, na hasa kushiriki katika funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma!
Waliofinyangwa Kukabiliana na Majaribu
11, 12. (a) Twaweza kutumiaje shauri la Yakobo kuhusu majaribu katika maisha yetu ya kila siku? (b) Jambo lililompata Yobu latutiaje moyo kushika uaminifu-maadili?
11 Katika maisha yetu ya kila siku, Mungu huruhusu hali fulani zitokee na huenda tukaziona baadhi ya hali hizo kuwa ngumu. Twapaswa kuzionaje? Kama andiko la Yakobo 4:8 linavyoshauri, na tusiwe na uchungu kamwe, bali acheni tumkaribie Mungu, tukimtumaini kwa moyo wetu wote, tukiwa na uhakika kwamba ‘tunapomkaribia, atatukaribia.’ Ni kweli kwamba tutavumilia shida na majaribu, lakini yanaruhusiwa ili yasaidie katika kufinyangwa kwetu, kukiwa na matokeo yenye furaha. Andiko la Yakobo 1:2, 3 latuhakikishia hivi: “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.”
12 Yakobo pia asema: “Wakati yuko chini ya jaribu, acheni yeyote asiseme: ‘Mimi ninajaribiwa na Mungu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote. Lakini kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yakobo 1:13, 14) Majaribu yetu yaweza kuwa mengi na ya namna mbalimbali, lakini kama hali ya Yobu ilivyokuwa, hayo yote hutimiza fungu fulani katika kufinyangwa kwetu. Ni uhakikisho mkubwa jinsi gani ambao Maandiko yanatutolea kwenye Yakobo 5:11: “Tazameni! Twawatamka kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia. Nyinyi mmesikia juu ya uvumilivu wa Yobu na mmeona tokeo alilotoa Yehova, kwamba Yehova ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema.” Tukiwa kama vyombo mikononi mwa Mfinyanzi Mkuu, na tushike uaminifu-maadili nyakati zote, tukiwa na uhakika kama wa Yobu katika lile litakalotokea!—Ayubu 2:3, 9, 10; 27:5; 31:1-6; 42:12-15.
Kufinyanga Vijana Wetu
13, 14. (a) Wazazi wapaswa kuanza kufinyanga watoto wao lini, wakitazamia matokeo gani hatimaye? (b) Waweza kutaja matokeo gani yenye furaha?
13 Wazazi wanaweza kushiriki kufinyanga vijana wao, tangu utotoni, nao vijana wetu wanaweza kushika uaminifu-maadili kwa njia nzuri kama nini! (2 Timotheo 3:14, 15) Hilo limepata kuwa hivyo hata wakati ambapo majaribu yamekuwa makali mno. Miaka kadhaa iliyopita, mnyanyaso ulipokuwa mkali sana katika nchi fulani ya Afrika, familia yenye kutumainika ilishughulikia uchapaji wa Mnara wa Mlinzi katika kibanda kilichokuwa nyuma ya nyumba yao. Siku moja askari-jeshi walikuwa wakija barabarani, wakiwasaka wanaume vijana kutoka nyumba hadi nyumba ili wawaingize jeshini. Wakati ulikuwa ungali upo kwa wavulana wawili wa familia hiyo kujificha, lakini msako wa askari-jeshi ambao ungefuata ungefichua hiyo matbaa kwa hakika. Jambo hilo lingesababisha kuteswa au labda kuuawa kwa familia yote. Ni nini kingeweza kufanywa? Hao wavulana wawili walisema bila woga, wakitaja kwa ujasiri Yohana 15:13: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” Walisisitiza kuendelea kukaa sebuleni. Askari-jeshi hao wangewapata na yaelekea wangewatesa au hata kuwaua wakikataa kuingizwa jeshini. Lakini hawangeendelea na msako wao. Matbaa na washiriki wengine wa familia wangenusurika. Hata hivyo, kulikuwa na matokeo yenye kutokeza. Kwa kweli, askari-jeshi hao waliruka nyumba hiyo na kuelekea kwenye nyumba nyingine! Vyombo hivyo vya kibinadamu ambavyo viliundwa kwa utumizi wenye kuheshimika vilinusurika, pamoja na matbaa na kuendelea kuchapisha chakula cha kiroho kwa wakati ufaao. Mmojawapo wa wavulana hao wawili na dada yake, sasa wanatumikia katika Betheli; na mvulana huyo angali anaendesha mashine hiyo iliyozeeka.
14 Vijana wanaweza kufunzwa namna ya kusali, naye Mungu hujibu sala zao. Mfano wenye kutokeza wa jambo hilo ulitokea wakati wa mauaji ya kinyama ya Rwanda. Wakati binti mwenye umri wa miaka sita na wazazi wake walipowekwa tayari na waasi ili wauawe kwa kombora la kutupwa kwa mkono, binti huyo alisali kwa Yehova kwa sauti kubwa na kwa bidii waweze kunusurika ili waendelee na utumishi wao kwa Yehova. Wale ambao wangewaua kimakusudi walisukumwa kuwanusuru, wakisema, “Hatuwezi kuwaua kwa sababu ya huyu msichana mdogo.”—1 Petro 3:12.
15. Paulo alionya juu ya uvutano gani wenye kufisidi?
15 Vijana wetu walio wengi hawalazimiki kukabiliana na hali ngumu kama hizo ambazo zimefafanuliwa hapo juu, lakini kuna majaribu mengi ambayo siku hizi wanakabiliana nayo shuleni na katika jamii zenye ufisadi: lugha chafu, ponografia, vitumbuizo vilivyoshuka, na kusongwa na marika ili washiriki mazoea mabaya yameenea mahali pengi. Mtume Paulo alionya tena na tena juu ya uvutano huo.—1 Wakorintho 5:6; 15:33, 34; Waefeso 5:3-7.
16. Mtu aweza kuwaje chombo kwa utumizi wenye kuheshimika?
16 Baada ya kuvirejezea vyombo vinavyowekwa ‘baadhi yavyo kwa kusudi lenye kuheshimika lakini vingine kwa kusudi lenye kukosa heshima,’ Paulo asema: “Kwa hiyo, ikiwa yeyote ajiepusha kabisa na hawa wa mwisho, atakuwa chombo kwa kusudi lenye kuheshimika, kilichotakaswa, chenye mafaa kwa mmiliki wacho, kilichotayarishwa kwa kila kazi njema.” Kwa hiyo acheni tuwatie moyo vijana wetu wawe waangalifu kuhusu mashirika yao. Acheni ‘wakimbie tamaa zenye kutukia ujanani, lakini wafuatie uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale wamwitiao Bwana kutokana na moyo safi.’ (2 Timotheo 2:20-22) Programu ya familia kwa ajili ya “kujengana” yaweza kuwa yenye manufaa sana katika kufinyanga vijana wetu. (1 Wathesalonike 5:11; Mithali 22:6) Kusoma na kujifunza Biblia kila siku, ukitumia vichapo vya Sosaiti vifaavyo kwaweza kuwa msaada mzuri.
Kufinyangwa kwa Watu Wote
17. Nidhamu itatufinyanga namna gani, kukiwa na matokeo gani yenye shangwe?
17 Ili kutufinyanga, Yehova hututolea shauri kutoka katika Neno lake na kupitia tengenezo lake. Usikinze kamwe shauri hilo la kimungu! Liitikie kwa hekima, na acha likufinyange kwa ajili ya kutumiwa na Yehova katika utumizi wenye kuheshimika. Andiko la Mithali 3:11, 12 latushauri: “Mwanangu, usidharau kuadhibiwa na BWANA, wala usione ni taabu kurudiwa naye. Kwa kuwa BWANA ampendaye humrudi, kama vile baba mwanawe ampendezaye.” Isitoshe, shauri la kibaba latolewa kwenye Waebrania 12:6-11: “[Yule] ambaye Yehova ampenda humtia nidhamu . . . Kweli, hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” Lazima Neno la Mungu lililopuliziwa liwe ndilo njia kuu ya kutolea nidhamu kama hiyo.—2 Timotheo 3:16, 17.
18. Kuhusu toba, twajifunza nini kutokana na Luka sura ya 15?
18 Yehova pia ni mwenye rehema. (Kutoka 34:6) Toba ya kutoka moyoni ionyeshwapo hata ikiwa dhambi nzito sana imetendwa, yeye husamehe. Hata ‘wapotevu’ wa siku hizi waweza kufinyangwa kuwa vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika. (Luka 15:22-24, 32) Huenda dhambi zetu zisiwe nzito kama zile za mwana mpotevu. Lakini itikio letu la unyenyekevu kwa shauri la Kimaandiko litafanya sikuzote tufinyangwe kuwa vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika.
19. Twaweza kuendeleaje kutumikia tukiwa vyombo vyenye kuheshimika mikononi mwa Yehova?
19 Tulipojifunza kweli mara ya kwanza, tulionyesha utayari wa kumwacha Yehova atufinyange. Tuliacha njia za kilimwengu, tukaanza kuvaa utu mpya, tukawa Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa. Tulitii shauri la Waefeso 4:20-24, ‘tukiweka mbali utu wa hapo zamani uliofuatana na njia yetu ya kwanza ya mwenendo, pamoja na tamaa zake za udanganyifu, na kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ Sisi binafsi na twendelee kuwa wenye kupindika kwa urahisi mikononi mwa Yehova, Mfinyanzi Mkuu, tukitumikia sikuzote kama vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika!
Kwa Kupitia
◻ Kusudi la Mfinyanzi Mkuu kuelekea dunia yetu ni nini?
◻ Waweza kufinyangwa namna gani kwa utumizi wenye kuheshimika?
◻ Watoto wetu waweza kufinyangwa namna gani?
◻ Twapaswa kuwa na maoni gani kuhusu nidhamu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Je, wewe utafinyangwa kwa utumizi wenye kuheshimika au utakataliwa?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Wachanga waweza kufinyangwa tangu utotoni