Programu Mpya ya Kusanyiko la Pekee
Kichwa cha programu ya kusanyiko la pekee la mwaka wa utumishi wa 2008 ni “Sisi Ni Udongo—Yehova Ni Mfinyanzi Wetu,” nacho kinategemea Isaya 64:8. Himizo la Kimaandiko litakalotolewa katika programu hiyo litatusaidia tuelewe na kuthamini zaidi hekima, haki, nguvu, na upendo wa Yehova akiwa Mfinyanzi Mkuu.
Hotuba ya mwangalizi wa mzunguko yenye kichwa, “Kutumikia Tukiwa Vyombo Vyenye Kuheshimika Katika Huduma,” itaonyesha jinsi ambavyo watu wengi wanazidi kupata baraka nyingi ya kujua kweli na kuwaambia wengine kweli hiyo. Hotuba yenye kichwa, “Kutafakari Kutakulinda” itafunua jinsi ambavyo kutafakari kanuni za uadilifu za Yehova hutulinda. Msemaji anayezuru atatoa hotuba zenye kichwa, “Tusifanyizwe Kulingana na Mfumo Huu wa Mambo” na “Ufinyangwe na Mfinyanzi Mkuu.” Wazazi na vijana watatiwa moyo na hotuba “Vijana Wanaotumiwa na Yehova” na “Daraka Muhimu la Wazazi Katika Kufinyanga.” Kupitia maonyesho na mahojiano, tutafurahia kusikia na kuona yale ambayo ndugu na dada zetu wanatimiza katika huduma yao. Wale ambao wangetaka kuonyesha wakfu wao kwa Mungu kwa kubatizwa katika maji wanapaswa kumjulisha mwangalizi-msimamizi haraka iwezekanavyo. Usisahau kubeba gazeti la Mnara wa Mlinzi litakalosomwa juma hilo la kusanyiko la pekee.
Chochote Mfinyanzi Mkuu anachokusudia anakitimiza. Lakini ni juu yetu kuamua jinsi tutakavyotenda anapotufinyanga. Wale wanaokubali viwango vya Yehova na kusafishwa naye, wanaweza kufinyangwa na kisha kung’arishwa na kutengenezwa kuwa vyombo vyenye matumizi yanayofaa kama vile donge la udongo katika gurudumu la mfinyanzi. Tunaposhirikiana na Yehova, tunakweza enzi yake kuu na kupata baraka nyingi.