Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
Jitihada ya Kumtafuta Mungu wa Kweli Yathawabishwa
KATIKA karne ya kumi K.W.K., ibada isiyo ya kweli ilienea katika ufalme wa Yuda wa makabila mawili. Hata hivyo, katikati ya ibada ya sanamu iliyoenea pote, paliishi mtu fulani ambaye moyo wake ulikuwa mnyoofu kuelekea Mungu. Aliitwa Yehoshafati. Nabii Yehu alisema hivi kumhusu: “Yameonekana mema ndani yako, kwa kuwa . . . moyo wako umeukaza kumtafuta Mungu.” (2 Mambo ya Nyakati 19:3) Vivyo hivyo leo, katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” mamilioni ya watu ‘wamekaza mioyo yao’ kumtafuta Mungu wa kweli, Yehova. (2 Timotheo 3:1-5) Hili laonyeshwa na jambo lililoonwa lifuatalo kutoka Togo, Afrika Magharibi.
Casimir alisomea katika shule ya Kikatoliki na alishiriki kula Sakramenti kwa mara ya kwanza alipokuwa na umri wa miaka tisa. Hata hivyo, alipofikisha umri wa miaka 14, Casimir alikuwa ameacha kwenda kanisani. Hili lilimfanya aishi kwa hofu kwa sababu alifikiri kwamba kukosa kuhudhuria Misa kungemfanya aende kwenye helo yenye moto, au akiponea kidogo aende purgatori.
Shuleni Casimir alijiunga na kikundi cha vijana waliokutana mara moja kwa juma kujifunza Biblia. Pia alianza kujisomea Biblia. Katika pindi moja Casimir alisoma katika kitabu cha Ufunuo kuhusu hayawani-mwitu mwenye kuogofya aliyetoka baharini. (Ufunuo 13:1, 2) Alipouliza kiongozi wa kikundi cha kujifunza Biblia kuhusu hayawani-mwitu huyo, aliambiwa kwamba huyo hayawani-mwitu alikuwa halisi na kwamba kwa kweli angetoka baharini. Maelezo hayo yalimsumbua Casimir kwa sababu aliishi karibu na Pwani ya Atlantiki. Alisadiki kwamba angekuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuliwa na huyo hayawani-mwitu.
Casimir alianza kuhifadhi pesa zake ili apate kutorokea jangwa lililokuwa upande wa kaskazini kusudi amwepuke huyo hayawani-mwitu. Alimweleza mwanadarasa mwenzake kuhusu mipango yake. Mwanadarasa mwenzake ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alimweleza kwamba hakuna hayawani-mwitu halisi wa namna hiyo ambaye angetoka baharini. Muda mfupi baada ya hapo, Casimir alialikwa mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme. Alifurahia mikutano hiyo na akaanza kuihudhuria kwa ukawaida. Pia alikubali funzo la Biblia la nyumbani.
Casimir alipoendelea na funzo lake, upinzani kutoka kwa familia ulianza. Familia yao ilikuwa na zoea la kuabudu wazazi waliokufa na kula nyama yenye damu iliyobakia kutoka kwa dhabihu. Casimir alipokataa kwa upole kula nyama hiyo, alitishwa na kuambiwa aondoke nyumbani. Casimir alibaki akiwa mtulivu, na hakutishika. Hata hivyo, kwa miezi mitatu nyama hiyo ndiyo iliyokuwa chakula cha familia hiyo. Casimir alikuwa na tatizo la kupata chakula cha kutosha, lakini alivumilia hili na shida nyinginezo.
Casimir alizidi kufanya maendeleo ya kiroho kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Baadaye, aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma na kuhudhuria darasa la nne la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma katika Togo. Kwa sasa, anafurahia kufanya kazi ya kujitolea kwenye ofisi ya tawi.
Naam, maneno ya Mfalme Daudi yamethibitika kuwa ya kweli kama nini katika visa vingi: “Ukimtafuta [Yehova], ataonekana nawe.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Casimir (kulia) afurahia kazi ya kujitolea kwenye ofisi ya tawi