Matatizo ya Pekee ya Familia za Kambo
INAWEZEKANA KUWA NA FAMILIA ZA KAMBO ZENYE FURAHA! NAMNA GANI?
Familia ya kambo imekuwa ya kawaida katika sehemu nyingi za ulimwengu. Hata hivyo, familia za kambo huwa na matatizo ya pekee. Bila shaka, tatizo lililo gumu zaidi ni kulea watoto. Hata hivyo, kama vile makala mbili zifuatazo zitakavyojaribu kuonyesha, yawezekana kulea watoto kwa mafanikio katika familia ya kambo.
KIDESTURI, BABA WA KAMBO NA MAMA WA KAMBO WAMESEMWA VIBAYA. TULIPOKUWA WATOTO, wengi wetu tulisikia masimulizi fulani ya ile hadithi kuhusu Cinderella, ambaye aliteswa sana na mama yake wa kambo aliyekuwa mkatili. Huko Ulaya, watoto pia hujifunza hadithi iitwayo Snow White and the Seven Dwarfs. Mama wa kambo wa Snow White alithibitika kuwa mchawi mwovu!
Je, hadithi hizo hutoa maoni sahihi kuhusu familia za kambo? Je, kwa kweli wazazi wote wa kambo ni wabaya hivyo? La. Wengi wao hutaka kuwanufaisha zaidi watoto ambao wao hurithi kupitia ndoa. Lakini wao hulazimika kukabili matatizo fulani magumu yaliyo asili ya maisha ya familia ya kambo.
Matatizo ya Kulea Watoto
Wakati ndoa ya kwanza inapovunjika, mara nyingi sababu inakuwa kutokomaa kwa wenzi. Katika ndoa ya pili, kushughulika na watoto kwaweza kuleta mkazo juu ya uhusiano huo. Rekodi fulani huonyesha kwamba katika miaka mitano ya kwanza, familia 4 kati ya 10 zenye mzazi wa kambo huishia katika talaka.
Huenda wenzi wapya wa ndoa wasing’amue msukosuko wa kihisia-moyo, matatizo katika kuonyesha uaminifu-mshikamanifu, na hisia za wivu na uchungu wa moyo ambao kufika kwa mzazi wa kambo husababisha katika watoto hao wa kambo. Huenda watoto hao wakawaza kwamba mzazi wao halisi anampenda huyo mzazi wa kambo zaidi yao. Isitoshe, huenda mzazi halisi aliyeachwa na mwenzi akashindwa kuelewa upendo wenye kuendelea kati ya watoto na mwenzi wa kwanza. Mvulana mmoja alijaribu kueleza uhusiano wake mzuri pamoja na baba yake halisi, akisema, “Mama, ninajua Baba alikutesa, lakini amekuwa mwema kwangu!” Usemi kama huo, ingawa ni wa moyo mnyofu, waweza kumfanya mama aone uchungu mwingi kuelekea baba ya mtoto huyo.
Baba mmoja wa kambo aliungama: “Kwa kweli sikuwa tayari kushughulika na matatizo yote yanayohusiana na kulea watoto wangu wa kambo. Niliingia katika hali hiyo nikifikiri kwamba kwa kuwa sasa nilikuwa nimeoa mama yao, nilikuwa baba yao. Kwangu, hilo lilionekana kuwa jambo lisilo gumu sana! Sikuelewa upendo ambao watoto hao walikuwa nao kwa baba yao halisi, nami nilifanya makosa mengi sana.”
Mikazo inaweza kuzuka hasa kuhusiana na nidhamu. Watoto huhitaji nidhamu yenye upendo, lakini mara nyingi wao huikinza hata inapotoka kwa mzazi wao halisi. Basi, inakuwa vigumu zaidi kama nini kwao kuipokea kutoka kwa mzazi wa kambo! Kwa kawaida, anapokabiliwa na nidhamu kama hiyo, mtoto wa kambo atasema maneno kama, “Wewe si baba yangu halisi!” Maneno kama hayo yanaweza kumvunja moyo kama nini mzazi mwenye nia njema!
Je, watoto wanaweza kulelewa kwa mafanikio katika familia zenye mzazi wa kambo? Je, wazazi wa kambo wanaweza kutimiza fungu lifaalo katika kujenga familia ya kambo yenye mafanikio? Jibu kwa maswali yote mawili ni ndiyo ikiwa wote wanaohusika watafuata shauri la Neno la Mungu lililopuliziwa, Biblia.
[Picha katika ukurasa wa 3]
“Wewe si baba yangu halisi!”