Familia za Kambo Zinaweza Kufanikiwa
JE, INAWEZEKANA KUWA NA FAMILIA ZA KAMBO ZENYE MAFANIKIO? NDIYO, HASA IKIWA WOTE wanaohusika wanakumbuka kwamba “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16) Kila mmoja anapotumia kanuni za Biblia, kufanikiwa karibu kunahakikishwa.
Sifa Iliyo ya Msingi
Biblia hutoa sheria chache tu halisi za kuongoza mahusiano ya kibinadamu. Hiyo, hasa hututia moyo kusitawisha sifa na mitazamo mizuri ambayo hutuongoza kutenda kwa hekima. Mitazamo hiyo mizuri na vilevile sifa nzuri ndio msingi wa maisha ya familia yenye furaha.
Laweza kuonekana kuwa jambo lililo wazi, lakini hata hivyo, yastahili kusema kwamba sifa ya msingi ya kufanikiwa kwa familia ni upendo. Mtume Paulo alisema: “Acheni upendo wenu uwe bila unafiki. . . . Katika upendo wa kidugu iweni na shauku nyororo kwa mtu na mwenzake.” (Waroma 12:9, 10) Neno “upendo” hutumiwa vibaya mara nyingi, lakini sifa ambayo Paulo alirejezea hapa ni ya pekee. Alirejezea upendo wa kimungu, nao “haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:8) Biblia huufafanua upendo huo kuwa usio na ubinafsi na ulio tayari kutumikia. Huo hufanya kazi kwa bidii ili kunufaisha wengine. Ni wenye subira na fadhili, hauna wivu kamwe, wala kujisifu, wala kujivuna. Hautafuti masilahi yake wenyewe. Unakuwa tayari sikuzote kuachilia mambo, kuitibari, kutumaini na kuvumilia chochote chenye kutokea.—1 Wakorintho 13:4-7.
Upendo wa kweli husaidia kupunguza kutopatana na huunganisha watu wenye malezi mbalimbali na nyutu tofauti sana. Nao husaidia kushinda hali yenye kuvunja moyo inayotokana na talaka au kifo cha mzazi halisi. Mwanamume mmoja aliyepata kuwa baba wa kambo afafanua matatizo yake hasa: “Mara nyingi nilihangaikia hisia zangu mno nisiweze kuchanganua hisia-moyo za watoto wangu wa kambo au hata za mke wangu. Ilinibidi nijifunze kutokuwa na hisia nyepesi mno. Jambo muhimu zaidi ni kwamba nilijifunza kuwa mnyenyekevu.” Upendo ulimsaidia kufanya marekebisho yaliyohitajika.
Mzazi Halisi
Upendo waweza kusaidia katika kushughulika na uhusiano wa watoto pamoja na baba yao halisi ambaye sasa hayupo. Baba wa kambo afunua siri hii: “Nilitaka watoto wangu wa kambo wanipende zaidi ya vile walivyompenda baba yao halisi. Walipomtembelea baba yao halisi, sikuweza kukinza kishawishi cha kumchambua. Waliporudi baada ya kuwa na wakati mzuri pamoja naye, nilihisi vibaya sana. Walipokuwa na wakati mbaya, nilifurahi. Kwa kweli nilihofia kupoteza shauku yao kwangu. Jambo lililokuwa gumu zaidi ni kung’amua na kukubali umuhimu wa fungu la baba halisi katika maisha ya watoto wangu wa kambo.”
Upendo wa kweli ulimsaidia baba huyo wa kambo kukabili uhakika wa kwamba halikuwa jambo la akili kutarajia kupendwa “mara moja.” Hakupaswa kuhisi amekataliwa wakati watoto walipokosa kumkubali mara moja. Alikuja kung’amua kwamba huenda asiweze kamwe kuchukua kabisa mahali pa baba halisi katika mioyo ya watoto wake. Hao watoto walimjua mwanamume huyo tangu walipokuwa wachanga kabisa, ilhali huyo baba wa kambo alikuwa mtu mpya ambaye ingembidi ajitahidi ili apate kupendwa na watoto hao. Mtafiti Elizabeth Einstein adhihirisha jambo linalowapata watu wengi anaposema hivi: “Mahali pa baba halisi hapawezi kamwe kuchukuliwa na mwingine—kamwe. Hata mzazi aliyekufa au aliyewaacha watoto huendelea kuwa na ushawishi muhimu katika maisha ya watoto hao.”
Nidhamu—Suala Nyeti
Biblia huonyesha kwamba nidhamu yenye upendo ni muhimu kwa vijana, nao hutia ndani watoto wa kambo. (Mithali 8:33) Wataalamu kadhaa wameanza kukubaliana na yale ambayo Biblia husema kuhusu jambo hilo. Profesa Ceres Alves de Araújo alisema: “Kiasili hakuna yeyote apendaye kuwekewa mipaka, lakini hiyo inahitajika. ‘La’ ni neno litoalo kinga.”
Hata hivyo, katika familia zenye mzazi wa kambo, maoni kuhusu nidhamu yaweza kutokeza ugomvi mkubwa. Watoto wa kambo wameathiriwa kwa kadiri fulani na mtu mzima ambaye sasa hayupo. Yaelekea wana tabia au desturi ambazo huenda zikamwudhi mzazi wa kambo. Na yawezekana hawaelewi ni kwa nini mzazi wa kambo anashikilia sana mambo fulani. Utaishughulikiaje hali hiyo kwa mafanikio? Paulo ahimiza kwa bidii hivi: “Fuatia . . . upendo, uvumilivu, tabia-pole.” (1 Timotheo 6:11) Upendo wa Kikristo husaidia wazazi wa kambo na watoto wawe wapole na wenye subira wanapojifunza kuelewana. Ikiwa mzazi wa kambo anakosa subira, ‘hasira, hasira ya kisasi, usemi wenye kuudhi’ waweza kuharibu haraka uhusiano wowote ambao umepatikana.—Waefeso 4:31.
Ufahamu wenye kina kuhusu yale yatakayosaidia katika jambo hilo ulitolewa na nabii Mika. Yeye alisema: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema [“fadhili,” NW], na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” (Mika 6:8) Haki ni jambo muhimu nidhamu inapotolewa. Lakini namna gani fadhili? Mzee mmoja Mkristo asimulia kwamba mara nyingi ilikuwa vigumu kuwaamsha watoto wake wa kambo Jumapili asubuhi ili washiriki katika ibada ya kutaniko. Badala ya kuwakemea vikali, alijaribu kuwa mwenye fadhili. Aliamka mapema, akatayarisha kiamsha-kinywa, kisha akapelekea kila mmoja wao kinywaji chenye joto. Tokeo likawa kwamba walielekea zaidi kusikiza ombi lake la kuwataka waamke.
Profesa Ana Luisa Vieira de Mattos alitoa maelezo yafuatayo yenye kupendeza: “Kilicho muhimu si aina ya familia bali ni ubora wa uhusiano huo. Katika utafiti wangu nimeng’amua kwamba vijana walio na matatizo ya kitabia karibu sikuzote hutoka katika familia ambamo mna usimamizi dhaifu wa wazazi, ukosefu wa sheria na mawasiliano.” Yeye pia alisema: “Yapaswa kukaziwa sana kwamba kulea watoto kwamaanisha uhitaji wa kusema la.” Kwa kuongezea, Madakt. Emily na John Visher walisema: “Kimsingi, nidhamu huwa na matokeo wakati ambapo mtu anayeipokea anajali juu ya itikio la mwenye kuitoa na vilevile uhusiano wake pamoja naye.”
Maneno hayo yanagusia suala la ni nani katika familia za kambo apaswaye kutoa nidhamu. Ni nani apaswaye kusema la? Baada ya kuzungumzia mambo hayo, wazazi wengine wameamua kwamba, mwanzoni, mzazi halisi ndiye apaswaye kuwa mdhibiti-nidhamu mkuu ili kumpa mzazi wa kambo muda wa kujenga uhusiano wa karibu zaidi na watoto. Acheni watoto wajifunze kuwa na uhakika kwamba mzazi wao wa kambo anawapenda kabla yeye hajaanza kuwatia nidhamu.
Namna gani ikiwa baba ndiye mzazi wa kambo? Je, Biblia haisemi kwamba baba ndiye kichwa cha familia? Ndiyo. (Waefeso 5:22, 23; 6:1, 2) Hata hivyo, huenda baba wa kambo akataka kumwachia mke daraka la kutoa nidhamu kwa muda mfupi, hasa ikiwa nidhamu hiyo yahusisha kutia adhabu. Huenda akawaruhusu watoto watii ‘sheria ya mama yao’ huku akiwawekea msingi wa ‘kusikiliza nidhamu ya baba yao [mpya].’ (Mithali 1:8; 6:20; 31:1) Ushuhuda waonyesha kwamba, mwishowe, jambo hilo halipingi kanuni ya ukichwa. Kwa kuongezea, baba mmoja wa kambo alisema: “Nilikumbuka kwamba nidhamu hutia ndani kuonya kwa upole, kusahihisha, na kukaripia. Kwa kawaida nidhamu huwa na matokeo inapotolewa katika njia ya haki, yenye upendo, na yenye huruma na kutegemezwa kwa kielelezo cha wazazi.”
Wazazi Wahitaji Kuwasiliana
Andiko la Mithali 15:22 lasema: “Pasipo mashauri [“mazungumzo ya siri,” NW] makusudi hubatilika.” Mazungumzo ya siri yaliyo matulivu na wazi baina ya wazazi ni muhimu katika familia ya kambo. Mwandishi wa makala katika gazeti la habari la O Estado de S. Paulo alisema: “Sikuzote watoto wana mwelekeo wa kujaribu mipaka iliyowekwa na wazazi.” Huenda jambo hilo likawa kweli kabisa katika familia za kambo. Kwa sababu hiyo, wazazi wahitaji kukubaliana katika mambo tofauti-tofauti ili watoto waone kwamba wao ni wenye muungano. Ingawa hivyo, namna gani mzazi wa kambo akitenda kwa njia ambayo mzazi halisi anahisi si ya haki? Basi, wote wawili wapaswa kusuluhisha jambo hilo faraghani, sio mbele ya watoto.
Mama mmoja aliyeolewa tena asimulia: “Jambo lililo gumu zaidi kwa mama ni kuona baba wa kambo akiwatia watoto wake nidhamu, hasa ikiwa yeye ahisi kwamba anatenda kwa haraka-haraka au ni mwenye ubaguzi. Hilo humvunja moyo mama, naye hutaka kuwatetea watoto wake. Nyakati kama hizo, ni vigumu kuendelea kuwa mtiifu kwa mume wako na kumwunga mkono.
“Pindi moja, wavulana wangu wawili, wenye umri wa miaka 12 na 14, waliomba baba yao wa kambo ruhusa ya kufanya kitu fulani. Yeye alikataa mara moja, kisha akaondoka chumbani bila kuwapa wavulana hao fursa yoyote ya kueleza ni kwa nini ombi hilo lilikuwa muhimu kwao. Wavulana hao walikuwa tayari kulia, nami niliduwaa. Mvulana mwenye umri mkubwa zaidi alinitazama na kusema: ‘Mama, umeona vile amefanya?’ Nikajibu: ‘Ndiyo, nimeona. Lakini yeye bado ni kichwa cha nyumba hii, na Biblia hutuambia tustahi ukichwa.’ Walikuwa wavulana wazuri nao walikubaliana na jambo hilo na kutulia kidogo. Jioni hiyohiyo, nilimweleza mume wangu juu ya mambo hayo, naye aling’amua kwamba alikuwa ametumia mamlaka kupita kiasi. Alienda moja kwa moja chumbani mwa wavulana hao na kuwaomba radhi.
“Tulijifunza mengi kutokana na tukio hilo. Mume wangu alijifunza kusikiliza kabla ya kufanya maamuzi. Nilijifunza kuunga mkono kanuni ya ukichwa, hata linapokuwa jambo lenye kunitia uchungu. Wavulana walijifunza umuhimu wa kuwa watiifu. (Wakolosai 3:18, 19) Nao uombaji radhi wenye kuhisiwa moyoni wa mume wangu ukatufunza sote somo muhimu la unyenyekevu. (Mithali 29:23) Leo, wana hao wawili ni wazee Wakristo.”
Makosa yatafanywa. Watoto watasema au kufanya mambo yenye kutia uchungu. Mikazo wanayokuwa nayo wakati fulani itafanya wazazi wa kambo watende bila kutumia busara. Hata hivyo, maneno haya sahili, “Naomba radhi, tafadhali nisamehe,” yaweza kufanya mengi kuondoa uchungu.
Kuimarisha Muungano wa Familia
Inachukua muda kujenga uhusiano mchangamfu katika familia ya kambo. Ikiwa wewe ni mzazi wa kambo, wahitaji kuonyesha hisia-mwenzi. Uwe mwenye uelewevu na tayari kutumia wakati pamoja na watoto. Cheza na watoto wachanga. Uwe tayari kuzungumza na walio na umri mkubwa zaidi. Tafuta fursa za kutumia wakati pamoja—kwa kielelezo, waombe watoto wakusaidie kufanya kazi za nyumbani, kama kutayarisha mlo wa mchana au kusafisha gari. Waalike waende nawe na kukusaidia unapoenda sokoni. Kwa kuongezea, ishara kidogo za shauku zaweza kuonyesha upendo ulio nao. (Bila shaka, baba wa kambo wapaswa kuwa waangalifu kuweka mipaka ifaayo wanaposhughulika na binti zao wa kambo na kutowatia wasiwasi. Mama wa kambo wapaswa kukumbuka kwamba wavulana wana mipaka pia.)
Familia za kambo zaweza kufanikiwa. Nyingi zinafanikiwa. Zilizofanikiwa zaidi ni zile ambamo wote, hasa wazazi, husitawisha mitazamo ifaayo na matarajio yawezekanayo. Mtume Yohana aliandika hivi: “Wapendwa, acheni tuendelee kupendana, kwa sababu upendo ni wa kutoka kwa Mungu.” (1 Yohana 4:7) Naam, upendo wenye kuhisiwa moyoni ndio siri hasa ya kuwa na familia ya kambo yenye furaha.
[Picha katika ukurasa wa 7]
FAMILIA ZA KAMBO ZENYE FURAHA
hutumia wakati pamoja . . .
hujifunza Neno la Mungu pamoja . . .
huzungumza pamoja . . .
hufanya kazi pamoja . . .