Kujenga juu ya Misingi ya Kipagani
PANTHEON ni mojawapo ya majengo mengi yenye kuvutia ambayo hutembelewa na watalii wanaoenda Roma, Italia. Jengo hilo ambalo ni kazi bora ya usanifu-ujenzi wa Kiroma, ni mojawapo ya majengo machache huko ambayo kwa kiwango kikubwa yamebaki vile yalivyokuwa nyakati za kale. Jengo hilo lilianza kujengwa na Agripa wapata mwaka wa 27 K.W.K. na kujengwa upya na Hadrian wapata mwaka wa 120 W.K. Sehemu yenye kutokeza zaidi ya jengo hilo ni kuba lake lenye kipenyo cha meta 43, majengo ya nyakati za kisasa tu yakiwa ndiyo yenye upana mkubwa kushinda wa jengo hilo. Awali jengo hilo la Pantheon lilikuwa hekalu la kipagani, “mahali pa miungu yote,” ambayo ndiyo maana ya neno la awali la Kigiriki. Leo, jengo hilo lingali laonwa kuwa kanisa Katoliki. Badiliko hilo lenye kushangaza liliwezekanaje?
Hekalu hilo ambalo kwa muda mrefu halikuwa likitumiwa, liliwekwa wakfu tena kuwa kanisa la “Kikristo” na Papa Boniface wa Nne katika mwaka wa 609 W.K. Wakati huo liliitwa Kanisa la Santa Maria Rotunda. Kulingana na makala iliyochapishwa mwaka wa 1900 katika gazeti La Civiltà Cattolica la Wayesuiti wa Italia, Boniface alikusudia kutumia hekalu hilo hasa “kutukuza pamoja wafia-imani wote wa milki ya Kikristo, au kwa hakika, watakatifu wote, Bikira Mama ya Mungu akiwa ndiye wa kwanza kabisa.” Majina ambayo Kanisa Katoliki limelipa jengo la Pantheon leo—Santa Maria ad Martyres au, kwa jina jingine, Santa Maria Rotunda —yaonyesha kusudi hilo lisilo la Kimaandiko.—Linganisha Matendo 14:8-15.
“Ni mambo machache tu yaliyohitajika kufanywa” ili kugeuza Pantheon lifae matumizi yake mapya, makala hiyo yaendelea kusema. “Boniface alifuata sheria sahili na njema ambazo tayari zilikuwa zimeanzishwa na Mtk. Gregory Mkuu [Papa Gregory wa Kwanza] aliyemtangulia, ambaye alikuwa msanii wa muziki na pia kiolezo katika kugeuza mahekalu ya kipagani ili yatumiwe kwa ibada ya Kikristo.” Sheria hizo zilikuwa gani?
Katika barua iliyoandikiwa mishonari aliyekuwa akinuia kwenda Uingereza ya kipagani mwaka wa 601 W.K., Gregory alitoa agizo hili: “Mahekalu ya sanamu katika nchi ambayo imetajwa hayapaswi kuharibiwa; ila tu sanamu ambazo huenda zikawa humo . . . Ikiwa mahekalu hayo yamejengwa vizuri, basi yasitumiwe kuabudia mashetani bali yageuzwe kwa ajili ya utumishi wa Mungu wa kweli.” Wazo la Gregory lilikuwa kwamba ikiwa wapagani wangeona mahekalu yao ya zamani yakiwa hayajaharibiwa, huenda wakawa na mwelekeo zaidi wa kuendelea kuyazuru mara nyingi. Kwa kuwa wapagani walikuwa “wakiua mafahali wengi kuwatoa dhabihu kwa mashetani,” papa akaandika, sasa ilitumainiwa kwamba “hawatoi wanyama dhabihu tena kwa ibilisi bali wanawaua ili wale kwa kusudi la kumsifu Mungu.”
Dini ya Katoliki “ilibatilisha” ibada ya wapagani kwa kuanzisha makanisa yaliyowekwa wakfu kwa walezi “Wakristo” karibu na mahekalu ya zamani. Sherehe za kale zilikubaliwa kirasmi na kupewa umuhimu wa “Kikristo.” Kwa kueleza jambo hilo kulingana na maneno ya gazeti La Civiltà Cattolica: “Wasomi wote wa siku hizi wanajua uhakika wa kwamba desturi na maadhimisho fulani ya kidini ya Wakristo wa mapema yalihusiana sana na mazoea na njia fulani za kipagani. Yalikuwa mazoea yaliyopendwa sana na watu, desturi zilizoimarika sana na kufanywa kuwa sehemu muhimu ya maisha ya hadharani na ya faraghani katika ulimwengu wa kale. [Kanisa Katoliki], lenye fadhili na hekima, halikuonelea kwamba lilipaswa kuzibatilisha; badala ya hivyo, kwa kuzigeuza kuwa na maana ya Kikristo, na kuzikweza kuwa bora na kuzihuisha upya, kanisa hilo lilizishinda kwa njia zenye nguvu lakini zenye uanana, ili kushawishi nafsi za watu wa kawaida na pia watu wenye elimu.”
Bila shaka, Krismasi ni mojawapo ya vielelezo vyenye kujulikana sana vya kule kukubali kirasmi sherehe za kipagani. Desemba 25, kwa kweli, ilikuwa tarehe ambayo Waroma wa kale waliadhimisha dies natalis Solis Invicti, yaani, “kuzaliwa kwa jua lisiloweza kushindwa.”
Kwa hiyo, kanisa lilishindwa kushikamana na kweli kwa sababu ya tamaa yake ya kutaka kushawishi mioyo ya wapagani. Lilitetea zoea la kuchanganya itikadi mbalimbali, kutwaa itikadi na mazoea “yaliyopendwa sana na watu wa kawaida.” Hali hiyo ilitokeza kanisa lenye mchanganyiko wa itikadi na lenye kuasi imani, mambo ambayo ni kinyume kabisa na mafundisho ya Ukristo wa kweli. Kwa kufikiria hayo, labda haishangazi kwamba hekalu la zamani la Kiroma lililokuwa la “miungu yote”—Pantheon—lilipata kuwa kanisa Katoliki lililowekwa wakfu kwa Maria na kwa “watakatifu” wote.
Hata hivyo, ni jambo lipaswalo kuwa wazi kwamba kuweka hekalu wakfu tena au kubadilisha jina la sherehe fulani hakutoshi kugeuza ‘ibada ya mashetani kuwa utumishi wa Mungu wa kweli.’ “Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu?” akauliza mtume Paulo. “‘Tokeni miongoni mwao, na jitengeni wenyewe,’ asema Yehova, ‘na komeni kugusa kitu kisicho safi’; ‘na hakika mimi nitawakaribisha ndani.’ ‘Na mimi nitakuwa baba kwenu, na nyinyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,’ asema Yehova Mweza-Yote.”—2 Wakorintho 6:16-18.