Rashi Mfafanuzi wa Biblia Mwenye Uvutano Mkubwa
NI KIPI kimojawapo cha vitabu vya kwanza kabisa kuchapishwa katika Kiebrania? Ni kitabu cha ufafanuzi wa Pentateuki (vile vitabu vitano vya Musa). Kilichapishwa huko Reggio Calabria, Italia, mwaka wa 1475. Mtungaji wake alikuwa nani? Mwanamume aliyeitwa Rashi.
Kwa nini kitabu cha ufafanuzi kipewe heshima hiyo ya pekee? Katika kitabu chake Rashi—The Man and His World, Esra Shereshevsky asema kwamba kitabu cha Rashi cha ufafanuzi “kilipata kuwa maandishi ya msingi katika nyumba za Wayahudi na katika nyumba za kujifunzia. Hakuna kitabu kingine kati ya fasihi ya Kiyahudi kilichowahi kupewa tathmini kama hiyo . . . Kuna zaidi ya vitabu 200 vinavyotambuliwa ambavyo hutoa ufafanuzi wa ziada na wa moja kwa moja kuhusu kitabu cha Rashi cha ufafanuzi wa Pentateuki.”
Je, ni Wayahudi pekee ambao wamevutiwa na kitabu cha Rashi cha ufafanuzi? Ingawa hakitambuliwi na wengi, kitabu cha Rashi cha ufafanuzi wa Maandiko ya Kiebrania kimekuwa na uvutano juu ya tafsiri za Biblia kwa karne nyingi. Lakini Rashi alikuwa nani, na ni jinsi gani yeye alikuja kuwa na uvutano mkubwa hivyo?
Rashi Alikuwa Nani?
Rashi alizaliwa huko Troyes, Ufaransa, mwaka wa 1040.aAkiwa kijana, alisomea katika vyuo vya elimu ya kidini vya Kiyahudi huko Worms na Mainz katika eneo la Rhineland. Huko alifundishwa na wasomi Wayahudi waliokuwa mashuhuri zaidi katika Ulaya. Akiwa na umri upatao miaka 25, hali zake za kibinafsi zilimlazimisha kurudi Troyes. Akiwa tayari ametambuliwa kuwa msomi mwenye kutokeza, upesi Rashi akawa kiongozi wa kidini wa jamii ya Kiyahudi ya huko, na kuanzisha chuo chake mwenyewe cha kidini. Baada ya muda, chuo hicho kipya cha kujifunzia mambo yenye kuhusiana na Wayahudi kikawa chenye uvutano mkubwa kuliko vyuo vya walimu wa Rashi vilivyokuwa Ujerumani.
Wakati huo Wayahudi huko Ufaransa walifurahia amani na utulivu wa kadiri pamoja na majirani wao waliodai kuwa Wakristo, jambo hilo likimpa Rashi uhuru mkubwa zaidi wa kufuatia mambo ya kisomi. Hata hivyo, yeye hakuwa msomi mwenye kujitenga. Licha ya fahari yake kuu akiwa mwalimu na msimamizi wa chuo, Rashi alijiruzuku kwa kutengeneza divai. Ujuzi huo mkubwa wa biashara za kawaida ulimwezesha kuwa na ukaribu zaidi na Wayahudi wa kawaida, ukimsaidia kuelewa na kuonea huruma hali zao. Mahali jiji la Troyes lilipokuwa palimsaidia Rashi pia kupata ujuzi huo. Likiwa limejengwa mahali palipokuwa na njia kuu za biashara, jiji hilo lilikuwa kitovu cha kimataifa, na jambo hilo likamwezesha Rashi kufahamu vyema adabu na desturi za mataifa mbalimbali.
Kwa Nini Kitabu cha Ufafanuzi Kilihitajiwa?
Wayahudi walijulikana kuwa watu wa kitabu. Lakini ‘kitabu hicho’—Biblia—kilikuwa katika Kiebrania, na “watu” walizungumza Kiarabu, Kifaransa, Kihispania, Kijerumani, na lugha nyingine nyingi. Ingawa Wayahudi wengi walikuwa wangali wakifunzwa Kiebrania kutoka utotoni, hawakuelewa vizuri maneno mengi ya Kibiblia. Kwa kuongezea, kwa karne nyingi mwelekeo wenye nguvu katika Dini ya Kiyahudi ya kirabi ulivunja watu moyo wasichunguze maana halisi ya maandishi ya Kibiblia. Mafafanuzi yasiyo dhahiri na hekaya zilizohusu maneno na mistari ya Kibiblia zilikuwa nyingi. Mengi ya mafafanuzi hayo na hekaya zilirekodiwa katika mabuku makubwa, ambayo kwa ujumla huitwa Midrash.b
Mjukuu wa Rashi, Rabbi Samuel ben Meir (Rashbam), alikuwa pia msomi wa Biblia. Katika kitabu chake cha ufafanuzi wa Mwanzo 37:2, yeye alisema kwamba “wafafanuzi wa awali [kabla ya Rashi] . . . walikuwa na mwelekeo wa kutoa mahubiri (derashot), jambo waliloliona kuwa lengo muhimu zaidi, [lakini] hawakuwa na desturi ya kuchunguza sana maana halisi ya maandiko ya Kibiblia.” Akieleza juu ya mwelekeo huo, Dakt. A. Cohen (mhariri mkuu wa vitabu Soncino Books of the Bible) aandika: “Ni kweli kwamba Marabi walipitisha sheria kwamba hakuna fasiri yoyote ingekubaliwa ambayo ilipingana na peshat au maana dhahiri ya maandiko; lakini kihalisi walipuuza sheria hiyo.” Katika hali ya kidini kama hiyo, Myahudi wa kawaida alikosa uhakika alipoanza kuyasoma maandiko ya Kibiblia naye aliona uhitaji wa kifaa fulani chenye kufafanua.
Mradi wa Rashi na Njia Zake
Mradi wa maisha wa Rashi ulikuwa kufanya Maandiko ya Kiebrania yaeleweke kwa Wayahudi wote. Ili kutimiza mradi huo, alianza kukusanya daftari zenye kufafanua maneno na mistari hususa ambayo yeye alihisi yangemtatiza msomaji. Maandishi ya Rashi yataja ufafanuzi wa walimu wake na yatokana na ujuzi wake mkubwa wa fasihi yote ya marabi. Katika utafiti wa lugha, Rashi alitumia vitabu vyote vya marejeo alivyoweza kupata. Alikuwa makini sana juu ya jinsi alama za kutua na za kimatamshi za Wamasora zilivyoathiri uelewevu wa maandiko. Ili kufafanua wazi maana ya neno, kitabu chake cha ufafanuzi wa Pentateuki mara nyingi hurejezea ile tafsiri ya Kiaramu (Targum of Onkelos). Rashi alionyesha utayari wa kubadilikana na vilevile ustadi alipochunguza uwezekano mbalimbali wa kufafanua vihusishi, viunganishi, maana ya vitenzi, na sehemu nyingine za sarufi na mpangilio wa maneno ya kisarufi ambao haukuwa umechunguzwa hapo awali. Mafafanuzi hayo yalitoa msaada wenye thamani katika kuelewa mpangilio wa maneno ya kisarufi na pia sarufi ya lugha ya Kiebrania.
Kinyume cha mwelekeo ulioenea sana katika Dini ya Kiyahudi ya kirabi, sikuzote Rashi alijaribu kukazia maana halisi na sahili ya andiko. Lakini fasihi ya Kimidrash iliyokuwa nyingi mno, ambayo Wayahudi waliijua vizuri sana, haingeweza kupuuzwa. Sehemu yenye kutokeza ya kitabu cha ufafanuzi cha Rashi ni njia ambayo yeye hufafanua yale maandishi ya Kimidrash ambayo mara nyingi yalificha maana halisi ya maandiko ya Biblia.
Katika ufafanuzi wake wa andiko la Mwanzo 3:8, Rashi aeleza: “Kuna midrashim, yenye masimulizi mengi (aggadicc) ambayo Watu wetu Wenye Hekima tayari wamepanga ifaavyo katika diwani ya Bereshit Rabbah na diwani nyingine za Kimidrash. Hata hivyo, mimi ninapendezwa tu na maana iliyo wazi (peshat) ya mstari, na zile aggadot, (yaani masimulizi), zenye kufafanua simulizi la Kimaandiko katika muktadha wake.” Kwa kuteua na kuhariri midrash ile tu ambayo kulingana na maoni yake ilisaidia kubainisha maana au muktadha wa mstari, Rashi aliondoa, au kutoa, midrash iliyosababisha upingamizi na utatanishi. Tokeo la uhariri huo likawa kwamba vizazi vya baadaye vya Wayahudi vilikuja kufahamiana hasa na sehemu bora kabisa za Midrash ambazo ziliteuliwa na Rashi.
Ingawa aliwasifu sana walimu wake, Rashi hakusita kutokubaliana nao alipohisi kwamba ufafanuzi wao ulipingana na mantiki iliyo wazi juu ya andiko. Aliposhindwa kuelewa kifungu fulani au kuhisi kwamba hapo awali alikuwa amekifafanua isivyo sahihi, alikuwa tayari kukiri jambo hilo, hata kutaja visa ambapo wanafunzi wake walisaidia kusahihisha uelewevu wake.
Hali za Wakati Wake Zawa na Uvutano juu Yake
Rashi aliishi kulingana na nyakati zake kabisa. Kwa muhtasari, mwandishi mmoja alieleza jambo hilo hivi: “[Rashi] alisaidia sana maisha ya Wayahudi kwa kufasiri tena vifungu vyote vyenye kuwahusu katika lugha ya wenyeji ya wakati huo, akifanya hivyo kwa lugha wazi na yenye kueleweka, kwa uchangamshi na ufikirio, kwa ustadi na usomi usio wa kawaida, hivi kwamba vitabu vyake vya ufafanuzi vilipata kustahiwa kama vile vifungu vya maandiko vistahiwavyo na kupendwa kama vile fasihi ipendwavyo. Rashi aliandika Kiebrania kwa akili na kwa usanifu kana kwamba kilikuwa Kifaransa. Wakati wowote alipokosa neno sahihi la Kiebrania, yeye alitumia neno la Kifaransa, akiliendeleza kwa herufi za Kiebrania.” Maneno hayo ya Kifaransa yaliyotoholewa—Rashi alitumia zaidi ya maneno 3,500—yamekuwa chanzo chenye thamani kwa wanafunzi wa taaluma ya ukuzi wa lugha na matamshi ya Kifaransa cha Zamani.
Ingawa maisha ya Rashi yalianza katika hali yenye utulivu wa kadiri fulani, katika miaka yake ya baadaye alishuhudia uvutano kati ya Wayahudi na waliodai kuwa Wakristo. Katika mwaka wa 1096, Krusedi ya Kwanza iliangamiza jamii za Wayahudi wa Rhineland, ambako Rashi alisomea. Maelfu ya Wayahudi waliuawa kinyama. Yaonekana kuwa habari za mauaji hayo ya kinyama ziliathiri afya ya Rashi (ambayo ilizidi kudhoofika hadi alipokufa mwaka wa 1105). Tangu wakati huo na kuendelea, kulikuwa na badiliko kubwa katika vitabu vyake vya ufafanuzi wa Maandiko. Kielelezo kimoja chenye kutokeza ni Isaya sura ya 53, ambayo yazungumzia mtumishi wa Yehova mwenye kuteseka. Awali, Rashi alitumia maandiko hayo kurejezea Mesiya, kama vile Talmud ifanyavyo. Lakini yaonekana kwamba baada ya Krusedi, alifikiri kwamba mistari hiyo ilirejezea Wayahudi, waliokuwa wamekabili kuteseka kusiko kwa haki. Huo ulithibitika kuwa wakati wa badiliko kubwa katika ufasiri wa maandiko hayo.d Hivyo, tabia ya Jumuiya ya Wakristo isiyo ya Kikristo ilikuwa ikifanya wengi, kutia ndani Wayahudi, wasijue kweli kumhusu Yesu.—Mathayo 7:16-20; 2 Petro 2:1, 2.
Alikuwa na Uvutano Gani juu ya Kutafsiriwa kwa Biblia?
Punde si punde, uvutano wa Rashi uliathiri watu wengine wasiokuwa wa Dini ya Kiyahudi. Mfafanuzi wa Biblia Nicholas wa Lyra (1270-1349), aliyekuwa mtawa wa Kifransiska wa Ufaransa, alirejezea mara nyingi sana maoni ya “Rabbi Solomon [Rashi]” hivi kwamba alipewa jina la utani “Mwigaji wa Solomon.” Naye Lyra alikuwa na uvutano juu ya wafafanuzi na watafsiri wengi, kutia ndani wale waliotangulia kutafsiri Biblia ya Kiingereza ya King James Version na pia yule mleta-mabadiliko, Martin Luther, ambaye alibadili kabisa utafsiri wa Biblia huko Ujerumani. Luther alimtegemea Lyra sana hivi kwamba ubeti ambao ulipendwa sana ulikaririwa hivi: “Ikiwa Lyra hangepiga kinubi, Luther hangecheza dansi.”
Fikira za marabi ambazo zilipingana na kweli ya Kikristo zilikuwa na uvutano mkubwa juu ya Rashi. Hata hivyo, kwa ufahamu wenye kina wa maneno ya Kibiblia ya Kiebrania, mpangilio wa maneno ya kisarufi, na sarufi yenyewe na jitihada yake yenye kuendelea ya kufahamu maana sahili na halisi ya andiko, Rashi aandaa chanzo chenye maana cha ulinganisho kwa watafiti na watafsiri wa Biblia.
[Maelezo ya Chini]
a “Rashi” ni akronimi ya Kiebrania, iliyofanyizwa kwa herufi za kwanza za maneno “Rabbi Shlomo Yitzḥaqi [Rabbi Solomon ben Isaac].”
b Neno “Midrash” hutokana na mzizi wa neno la Kiebrania linalomaanisha “kuuliza, kujifunza, kuchunguza,” na kwa maana pana zaidi, “kuhubiri.”
c Neno Aggadah (wingi aggadot) kihalisi lamaanisha “masimulizi” nalo hurejezea sehemu muhimu zisizo za kisheria katika maandishi ya kirabi, nyakati nyingine yakihusisha ngano zisizo za Kibiblia za wahusika wa Kibiblia, au hekaya kuhusu marabi.
d Ili kupata habari zaidi kuhusu kifungu hiki cha Maandiko, ona sanduku “Mtumishi Wangu”—Yeye Ni Nani?, kwenye ukurasa wa 28 wa broshua Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Maandiko: Per gentile concessione del Ministero dei Beni Culturali e Ambientali