Kitabu cha Hekima Chenye Ujumbe Unaofaa Leo
“MFUKO uliojaa hekima una thamani kubwa zaidi kuliko mfuko uliojaa lulu,” akasema Yobu, mzee wa kale wa ukoo, ambaye bila shaka alikuwa mwanamume tajiri zaidi katika wakati wake. (Ayubu 1:3; 28:18; 42:12, NW) Kwa kweli, hekima ina thamani kubwa zaidi kuliko mali za kimwili kwa habari ya kusaidia mtu afanikishe maisha yake. “Hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi,” Mfalme Solomoni mwenye hekima akasema, “na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.”—Mhubiri 7:12.
Lakini hekima kama hiyo yaweza kupatikana wapi leo? Watu huendea waandishi wa makala, wanasaikolojia, madaktari wa magonjwa ya akili na hata watengeneza nywele na madereva wa teksi, ili wapate utatuzi wa matatizo yao ya kibinafsi. Nao wataalamu wengi sana wako tayari kutoa shauri kuhusu karibu habari yoyote—kwa ada ifaayo. Ingawa hivyo, mara nyingi maneno hayo ya “hekima” yamesababisha tu kukata tamaa na hata msiba. Hivyo basi, twaweza kupataje hekima ya kweli?
Yesu Kristo aliyekuwa na ufahamu wenye kina kirefu wa mambo ya kibinadamu alisema hivi wakati mmoja: “Hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi zayo.” (Mathayo 11:19) Acheni tuchunguze matatizo fulani ya kawaida maishani mwa watu na tuone ni maneno gani ya hekima ambayo kwa kweli yamewasaidia na yamethibitika kuwa yenye thamani kubwa kwao kupita “mfuko uliojaa lulu.” Wewe pia waweza kupata “mfuko [huo] uliojaa hekima” na kunufaika kutokana nao.
Je, Unasumbuliwa na Mshuko-Moyo?
Gazeti la International Herald Tribune la London lasema, “Ikiwa karne ya 20 ilileta Enzi ya Wasiwasi, basi mwisho wake unashuhudia mwanzo wa Enzi ya Mshuko-moyo. Laongeza kusema kwamba “uchunguzi wa kwanza wa kimataifa kuhusu mshuko-moyo mkubwa wafunua kuongezeka hatua kwa hatua kwa ugonjwa huo ulimwenguni pote. Katika mataifa yenye watu mbalimbali kama vile Taiwan, Lebanoni, na New Zealand, kila kizazi kinachofuata kinazidi kudhuriwa rahisi na ugonjwa huo.” Wale waliozaliwa baada ya mwaka wa 1955 wanasemekana kuwa wanaelekea kusumbuliwa na mshuko-moyo mkubwa mara tatu zaidi ya babu na nyanya zao.
Hali ya Tomoe, aliyesumbuliwa na mshuko-moyo mkubwa na kutumia wakati wake mwingi zaidi akiwa kitandani, ilikuwa hivyo. Kwa kuwa hangeweza kutunza mwana wake mwenye umri wa miaka miwili, alirudi nyumbani kwa wazazi wake. Punde si punde, jirani aliyekuwa na binti wa rika moja na mwana wa Tomoe, akafanya urafiki naye. Wakati Tomoe alipomwambia jirani huyo jinsi alivyohisi kutofaa kitu, huyo jirani alimwonyesha andiko kutoka katika kitabu fulani. Lilisema hivi: “Jicho haliwezi kuuambia mkono: ‘Sikuhitaji wewe’; au, tena, kichwa hakiwezi kuambia miguu: ‘Siwahitaji nyinyi.’ Lakini badala yake ni kwamba vile viungo vya mwili vionekanavyo kuwa dhaifu zaidi ni vya lazima.”a Macho ya Tomoe yalijaa machozi alipong’amua kwamba kila mtu anafaa katika ulimwengu na anahitajiwa.
Jirani huyo alipendekeza kwamba, Tomoe achunguze kitabu kilichokuwa na maneno hayo. Tomoe alikubali, hata ingawa hadi kufikia wakati huo, alikuwa hawezi kufanya chochote, hata kujipa sharti ya kutoa ahadi sahili. Jirani huyo alimsaidia pia kununua vitu dukani, naye alipika pamoja na Tomoe kila siku. Mwezi mmoja baadaye, Tomoe alikuwa akiamka kila asubuhi, akifua nguo, akisafisha nyumba, akinunua vitu dukani, na kupika chakula, kama vile ambavyo mke yeyote wa nyumbani angefanya. Ilimbidi atatue matatizo mengi, lakini yeye alisema, “Nilikuwa na uhakika kwamba kama ningefuata tu maneno ya hekima niliyopata, basi singekuwa na tatizo.”
Kwa kutumia hekima aliyopata, Tomoe alishinda siku zenye huzuni za mshuko-moyo wake. Sasa Tomoe anafanya kazi wakati wote akiwasaidia watu watumie maneno yaleyale yaliyomsaidia kukabiliana na matatizo yake. Maneno hayo ya hekima yanapatikana katika kitabu fulani cha kale ambacho kina ujumbe unaofaa watu wote leo.
Je, Unakabili Matatizo ya Nyumbani?
Kiwango cha talaka kinazidi kuongezeka ulimwenguni pote. Matatizo ya nyumbani yanaongezeka hata katika nchi za Mashariki, ambako wakati mmoja watu walijivunia familia zao zilizoshikamana kwa ukaribu. Je, tunaweza kupata wapi mwongozo wenye hekima kuhusu ndoa uwezao kutumika?
Fikiria kisa cha Shugo na Mihoko, wenzi ambao walikuwa na matatizo mengi sana ya ndoa. Waligombana juu ya kila jambo dogo. Shugo alikuwa mwepesi wa hasira, naye Mihoko alikuwa akimjibu kwa ukali kila wakati alipompata na kosa. Mihoko hata akafikiri, ‘Haiwezekani kwetu kukubaliana juu ya jambo lolote.’
Siku moja mwanamke fulani alimtembelea Mihoko na kumsomea maneno haya kutoka katika kitabu fulani: “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.”b Ingawa hakupendezwa na dini, Mihoko alikubali kujifunza kitabu kilichokuwa na maneno hayo. Alipendezwa na kuboresha maisha yake ya familia. Kwa hiyo, alipoalikwa kuhudhuria mkutano ambapo kitabu chenye kichwa Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha kilikuwa kikizungumziwa, Mihoko—na mume wake—walikubali mara moja.c
Kwenye mkutano huo, Shugo aliona kwamba waliohudhuria walikuwa kwa kweli wakitumia yale waliyokuwa wakijifunza, nao walionekana kuwa wenye furaha. Aliamua kuchunguza kitabu ambacho mke wake alikuwa akijifunza. Taarifa moja ilimvutia mara moja: “Asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi; bali mwenye roho ya hamaki hutukuza upumbavu.”d Ingawa ilimchukua muda kutumia kanuni hiyo maishani mwake, mabadiliko aliyofanya hatua kwa hatua yalikuwa dhahiri kwa wale waliokuwa karibu naye, kutia ndani mke wake.
Kuona mabadiliko ambayo mume wake alikuwa amefanya, Mihoko pia alianza kutumia yale aliyokuwa akijifunza. Kanuni moja iliyothibitika kuwa hasa yenye kumsaidia ilikuwa: “Komeni kuhukumu ili msipate kuhukumiwa; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa.”e Kwa hiyo, Mihoko na mume wake waliamua kwamba wangezungumzia sifa zao njema na jinsi ambavyo wangeweza kufanya maendeleo badala ya kulalamikiana. Matokeo yalikuwa nini? Mihoko akumbuka: “Jambo hilo limenifurahisha kwelikweli. Tumekuwa tukifanya hivyo wakati wa chakula kila jioni. Hata mwana wetu mwenye umri wa miaka mitatu hujiunga na mazungumzo hayo. Hilo limekuwa jambo lenye kutuburudisha kwelikweli!”
Wakati familia hiyo ilipotumia shauri hilo lenye maana walilopokea, waliweza kutatua matatizo yaliyokuwa yamedhoofisha uhusiano wao hadi kufikia kiwango cha kuvunjika. Je, hilo si lenye thamani kubwa zaidi kuliko mfuko uliojaa lulu?
Je, Unataka kufanikisha Maisha Yako?
Mradi wa watu wengi leo ni kurundika mali. Hata hivyo, mfanya-biashara tajiri wa Marekani ambaye ametoa mamilioni ya dola kwa mashirika ya kusaidia wenye shida alisema hivi wakati mmoja: “Pesa huvutia watu fulani, lakini hakuna awezaye kuvaa jozi mbili za viatu wakati mmoja.” Ni watu wachache wanaokubali uhakika huo, nao wanaoacha kufuatia mali ni wachache hata zaidi.
Hitoshi alikua akiwa maskini, kwa hiyo alikuwa na tamaa kubwa ya kuwa tajiri. Baada ya kuona namna wenye kudai walivyowatumia kwa hila wadeni wao, yeye aliamua hivi: “Yule anyakuaye pesa nyingi zaidi ndiye mshindi.” Hitoshi alikuwa na imani kubwa katika uwezo wa pesa hivi kwamba alifikiri hata uhai wa wanadamu ungeweza kununuliwa kwa pesa. Ili kurundika mali, alifanya biashara yake ya ufundi-bomba kwa bidii, akiifanya mwaka wote, bila kupumzika hata siku moja. Punde si punde, Hitoshi, akiwa mwana-kandarasi msaidizi, aling’amua kwamba hata kama angejitahidi kadiri gani, hangekuwa na uwezo sawa na wenye kandarasi ambao walimwajiri. Kuvunjika moyo na kuhofia kufilisika yakawa mambo aliyolazimika kukabili kila siku.
Ndipo mwanamume fulani akamtembelea Hitoshi na kumwuliza kama alijua kwamba Yesu Kristo alikufa kwa ajili yake. Kwa kuwa Hitoshi alifikiri kwamba hakuna yeyote ambaye angekufa kwa ajili ya mtu kama yeye, alitaka kujua zaidi naye akakubali mazungumzo zaidi. Juma lililofuata, alihudhuria hotuba fulani na kushtuka kusikia onyo juu ya ‘kuweka jicho likiwa sahili.’ Msemaji alieleza kwamba jicho “sahili” ni lile ambalo huzingatia mambo ya baadaye na hukazwa juu ya mambo ya kiroho; ilhali jicho lenye “husuda” hukazwa tu juu ya tamaa za kimwili za wakati huohuo na halizingatii mambo ya baadaye. Shauri, “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia,” lilimgusa moyo.f Kuna jambo fulani lililo muhimu zaidi kuliko kupata mali! Hakuwa amewahi kusikia jambo kama hilo.
Akiwa amevutiwa sana, alianza kufanya yale aliyokuwa akijifunza. Badala ya kuchoka akitafuta pesa, alianza kutanguliza mambo ya kiroho maishani mwake. Pia, alitumia wakati kushughulikia hali njema ya kiroho ya familia yake. Bila shaka, hilo lilimaanisha kwamba angetumia wakati mchache zaidi kazini, hata hivyo, biashara yake ilisitawi. Kwa nini?
Alipoitikia shauri alilopewa, utu wake wenye ugomvi ulibadilika akawa mpole na mwenye amani. Alivutiwa hasa na onyo hili la upole: “Kwa kweli yawekeni mbali nanyi hayo, hasira ya kisasi, hasira, ubaya, usemi wenye kuudhi, na maongezi yenye aibu kutoka katika kinywa chenu. Msiwe mkiambiana uwongo. Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea ya huo, na mjivike wenyewe utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.”g Kufuata shauri hilo hakukumfanya tajiri, lakini ‘utu wake mpya’ uliwavutia sana wateja wake, wakawa na itibari na uhakika katika yeye. Naam, maneno ya hekima aliyopata yalimsaidia kufanikisha maisha yake. Kwake, maneno hayo yalikuwa yenye thamani kubwa kuliko mfuko uliojaa lulu au pesa.
Je, Utaufungua Mfuko Huo?
Je, unaweza kuutambua mfuko huo uliojaa hekima ambao umethibitika kuwa wenye thamani kwa watu mmoja-mmoja katika vielelezo vilivyopo juu? Ni hekima ipatikanayo katika Biblia, kitabu ambacho kimetawanywa zaidi sana na ambacho hupatikana kwa urahisi zaidi duniani. Labda una nakala au waweza kupata moja kwa urahisi. Hata hivyo, kuwa na Biblia tu hakungekuwa na thamani yoyote sawa na vile kuwa na mfuko uliojaa lulu zenye thamani na kutozitumia hakungemsaidia mwenye kuzimiliki. Kwa nini usiufungue mfuko huo, kusema kitamathali, na kutumia shauri la Biblia la hekima na mawaidha ya wakati ufaao, na kuona jinsi Biblia iwezavyo kukusaidia kushughulika kwa mafanikio na matatizo ya maisha.
Kama kwa vyovyote ungepewa mfuko uliojaa lulu, je, usingeshukuru na kujaribu kutafuta mfadhili wako ni nani ili uweze kumshukuru? Kwa habari ya Biblia, je, unajua ni nani aliye Mpaji?
Biblia hufunua Chanzo cha hekima ipatikanayo ndani yake inaposema hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa.” (2 Timotheo 3:16) Hiyo pia hutuambia kwamba “neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Hiyo ndiyo sababu maneno yenye hekima yapatikanayo katika Biblia yanafaa na ni yenye matokeo kwetu leo. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza juu ya Mpaji huyu mkarimu, Yehova Mungu, ili uwe na taraja la kunufaika na ‘mfuko huo uliojaa hekima’ iliyomo katika Biblia—kitabu cha hekima chenye ujumbe kwa ajili ya watu leo.
[Maelezo ya Chini]
a Nukuu hilo linatoka katika 1 Wakorintho 12:21, 22.
c Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
f Mathayo 6:21-23, NW, (ya Kiingereza); kielezi-chini.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]
Maneno ya Hekima ili Kudumisha Usawaziko wa Kihisia-Moyo
“BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha, ili Wewe uogopwe.”—Zaburi 130:3, 4.
“Moyo wa furaha huchangamsha uso; bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.”—Mithali 15:13.
“Usiwe na haki kupita kiasi; wala usijiongezee hekima mno; kwani kujiangamiza mwenyewe?”—Mhubiri 7:16.
“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
“Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.”—Waefeso 4:26.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]
Maneno ya Hekima ili Kuwa na Maisha ya Familia Yenye Furaha
“Pasipo mashauri makusudi hubatilika; bali kwa wingi wa washauri huthibitika.”—Mithali 15:22, UV, chapa ya 1989.
“Moyo wa mwenye busara hupata maarifa; na sikio la mwenye hekima hutafuta maarifa.”—Mithali 18:15.
“Neno linenwalo wakati wa kufaa. Ni kama machungwa katika vyano vya fedha.”—Mithali 25:11.
“Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:13, 14.
“Jueni hili, ndugu zangu wapendwa. Kila mtu lazima awe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema, wa polepole juu ya hasira ya kisasi.”—Yakobo 1:19.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
Maneno ya Hekima ili Kufanikisha Maisha
“Mizani ya hadaa ni chukizo kwa BWANA; bali vipimo vilivyo sawasawa humpendeza.”—Mithali 11:1.
“Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.”—Mithali 16:18.
“Asiyetawala roho yake ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.”—Mithali 25:28.
“Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.”—Mhubiri 7:9.
“Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.”—Mhubiri 11:1.
“Msiache usemi uliooza utoke kinywani mwenu, bali usemi wowote ule ulio mwema kwa ajili ya kujenga kama vile kuwezavyo kuwa na uhitaji, ili huo upate kuwapa wasikiaji lililo la kupendeleka.”—Waefeso 4:29.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kujifunza Biblia ndiyo hatua ya kwanza ya kunufaika na “mfuko uliojaa hekima”