Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 4/1 kur. 20-22
  • Ni Nani Ambaye Huongoza Kufikiri Kwako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Ambaye Huongoza Kufikiri Kwako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusongwa Kulingana na Muundo wa Shetani?
  • Jua Kinachoendelea
  • Kubali Kufanyizwa Katika Muundo wa Yehova
  • Kumthamini Yehova Akiwa Mfinyanzi Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Acha Nidhamu ya Yehova Ikufinyange
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Mruhusu Yehova Afinyange Matendo na Kufikiri Kwako
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2017
  • Pambana Vikali Ili Kulinda Akili Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 4/1 kur. 20-22

Ni Nani Ambaye Huongoza Kufikiri Kwako?

“HAKUNA mtu aniambiaye la kufikiri! Na hakuna mtu aniambiaye la kufanya!” Kusema hivyo kwa mkazo sana kwa kawaida humaanisha kwamba unajitumaini sana na watumaini sana uamuzi wako. Je, wewe huhisi hivyo? Kwa kueleweka, hakuna mtu anayepaswa kukuamulia mambo. Lakini je, ni jambo la hekima kukataa haraka ule ambao waweza kuwa ushauri mzuri? Je, hakuna mtu yeyote kamwe awezaye kukusaidia kufanya uamuzi mzuri? Kwa vyovyote, waweza kuwa na uhakika kwamba mtu fulani, kwa kweli, haongozi kufikiri kwako, bila hata wewe kujua?

Kwa mfano, kabla ya vita ya ulimwengu ya pili, Joseph Goebbels, waziri wa propaganda wa Hitler, alisimamia wizara ya filamu ya Ujerumani. Kwa nini? Kwa sababu alitambua kwamba hiyo ingempa njia yenye nguvu ambayo angeweza “kuathiri itikadi za watu na vilevile tabia yao.” (Propaganda and the German Cinema 1933-1945) Labda wajua jinsi alivyotumia vibaya mbinu hii na njia nyinginezo kuwapotosha watu wa kawaida wafuate falsafa ya Nazi bila kufikiri.

Ukweli ni kwamba, jinsi unavyofikiri, na jinsi unavyotenda, sikuzote huchochewa kwa njia fulani na hisia na maoni ya wale unaowasikiliza. Bila shaka, si lazima hilo liwe jambo baya. Ikiwa ni watu ambao kwa kweli hupendezwa na hali njema yako—kama vile walimu, marafiki, au wazazi—basi utanufaika sana na shauri lao. Lakini kama ni watu ambao hupendezwa tu na mambo yao wenyewe na ambao wamepotoshwa au waliofisidika katika kufikiri kwao, “wadanganyi wa akili,” kama mtume Paulo alivyowafafanua, basi jihadhari!—Tito 1:10; Kumbukumbu la Torati 13:6-8.

Hivyo, usiridhike na kufikiri kwamba hakuna mtu anayeweza kukuathiri. (Linganisha 1 Wakorintho 10:12.) Yaelekea zaidi kwamba yatendeka hivyo tayari—zaidi ya vile uwezavyo kuamini—bila hata kutambua. Chukua kwa mfano, kitu unachoamua kununua unapoenda dukani. Je, sikuzote huo ni uamuzi wa kibinafsi kabisa, na wenye busara? Au je, watu wengine, mara nyingi wasioonekana, huathiri uamuzi wako kwa ujanja lakini kwa nguvu? Mwandishi wa habari mwenye kuchunguza mambo Eric Clark afikiri hivyo. “Kadiri tunavyofurikwa na matangazo mengi,” asema, “ndivyo tukosavyo kugundua athari yake, na bado, kwa hakika, ndivyo tunavyoathiriwa zaidi.” Pia aripoti kwamba watu wanapoulizwa jinsi utangazaji ulivyo na matokeo, “walio wengi hukubali kwamba huo huwa na matokeo, lakini si kwao.” Watu huhisi kwamba kila mtu anadhuriwa, lakini si wao. “Huonekana kwamba, wao peke yao, ndio wasioathirika.”—The Want Makers.

Kusongwa Kulingana na Muundo wa Shetani?

Ikiwa waathiriwa na matangazo ya kila siku huenda hilo lisiwe na matokeo makubwa. Hata hivyo, kuna uvutano mwingine, ambao ni hatari zaidi. Biblia huonyesha wazi kwamba Shetani ni stadi katika kuongoza kwa hila. (Ufunuo 12:9) Falsafa yake yafanana kimsingi na kufikiri kwa mtangazaji mmoja aliyesema kwamba kuna njia mbili za kuwavutia wateja—“kwa kuwashawishi au kwa kuwapatanisha na hali.” Ikiwa wanapropaganda na watangazaji wanaweza kutumia mbinu kama hizo zenye hila kuelekeza akili zako, lazima Shetani awe ana ustadi mwingi zaidi kwa kutumia mbinu kama hizo!—Yohana 8:44.

Mtume Paulo alijua jambo hilo. Alihofu kwamba baadhi ya Wakristo wenzake huenda wangekosa kuwa macho na kuwa wahasiriwa wa udanganyaji wa Shetani. Yeye aliandika hivi: “Naogopa kwamba kwa njia fulani, kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja wake, huenda akili zenu zikafisidiwa kutoka kwenye weupe wa moyo na usafi wa kiadili ambao wamstahili Kristo.” (2 Wakorintho 11:3) Chukulia onyo hilo kwa uzito. La sivyo, waweza kuwa kama watu wale ambao huamini kwamba propaganda na kupatanishwa na hali huwa na matokeo—“lakini si kwao.” Uhakika wa kwamba propaganda ya kishetani hufanya kazi waonekana wazi kutuzunguka katika ukatili, upotovu, na unafiki, tabia ambazo huonyeshwa na kizazi hiki.

Kwa hiyo, Paulo aliomba Wakristo wenzake ‘wakome kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo.’ (Waroma 12:2) Mtafsiri mmoja wa Biblia alisimulia kwa maneno mengine maneno ya Paulo kwa njia hii: “Msiache ulimwengu unaowazunguka uwasonge katika muundo wake.” (Waroma 12:2, Phillips) Shetani atajaribu kila njia kukuelekeza kwa nguvu kama atakavyo, kama vile mfinyanzi wa zamani aliyeufinyanga udongo kwa nguvu na kuutandaza ili kutia alama alizotaka juu ya udongo. Shetani anatumia siasa za ulimwengu, biashara, dini, na vitumbuizo kufanya hivyo. Lakini ushawishi wake umeenea kadiri gani? Umeenea sana kama vile ulivyokuwa siku za mtume Yohana. “Ulimwengu mzima,” akasema Yohana, “unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19; ona pia 2 Wakorintho 4:4.) Ikiwa una shaka lolote kuhusu uwezo wa Shetani wa kushawishi watu na kufisidi kufikiri kwao, kumbuka jinsi alivyofanya hivyo kwa matokeo kwa taifa zima la watu, Waisraeli, ambao walikuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu. (1 Wakorintho 10:6-12) Je, jambo lile lile laweza kukupata? Huenda likakupata ukiacha akili yako iwe wazi kushawishiwa na uvutano wa Shetani.

Jua Kinachoendelea

Mara nyingi, kani hizo zenye hila zitaathiri kufikiri kwako ukiziacha zifanye hivyo tu. Katika kitabu chake The Hidden Persuaders, Vance Packard alisema hivi: “Tungali na kinga yenye nguvu iliyopo dhidi ya washawishi hao [waliofichika]: twaweza kuamua kutoshawishiwa. Katika karibu visa vyote tungali na uchaguzi, nasi hatuwezi kuongozwa kwa hila sana kama twajua kinachoendelea.” Ndivyo ilivyo pia kuhusu propaganda na udanganyi.

Bila shaka, ili “kujua kinachoendelea,” lazima uache akili yako ikiwa imefunguka na tayari kupokea uvutano mwema. Kama vile mwili wenye afya, akili yenye afya, huhitaji kulishwa vizuri ikiwa itafanya kazi vizuri. (Mithali 5:1, 2) Ukosefu wa uelewevu waweza kuwa jambo la hatari kama vile kupotoshwa. Kwa hiyo, ijapokuwa wahitaji kulinda akili yako na mawazo na falsafa zilizopotoka, jaribu kutositawisha maoni ya husuda na ya madharau kuelekea ushauri wote au habari yote unayopewa.—1 Yohana 4:1.

Ushawishi wa haki si sawa na propaganda iliyofichika. Kwa hakika mtume Paulo alimwonya kijana Timotheo awe macho kuhusu “watu waovu na walaghai [ambao] wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi, wakiongoza vibaya na kuwa wenye kuongozwa vibaya.” Lakini Paulo aliongezea hivi: “Hata hivyo, wewe endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishwa kuamini, ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo.” (2 Timotheo 3:13, 14) Kwa kuwa kila kitu unachoruhusu kiingie katika akili yako kitakuathiri kwa kiwango fulani, jambo la maana ni ‘kujua ni kutoka kwa watu gani ambao unajifunza mambo,’ ili uhakikishe ni watu wanaopendezwa kikweli na masilahi yako, wala si na masilahi yao wenyewe.

Uchaguzi ni wako. Waweza kuchagua “kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo” kwa kuacha falsafa na kanuni za ulimwengu zitawale kufikiri kwako. (Waroma 12:2) Lakini ulimwengu huu haupendezwi kikweli na masilahi yako. Kwa hiyo, “jihadharini,” aonya mtume Paulo, “labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.” (Wakolosai 2:8) Kusongwa kuwa katika muundo wa Shetani kwa njia hii, au ‘kuchukuliwa kama windo lake,’ hakuhitaji jitihada. Ni kama moshi wenye kupita. Waweza kuathiriwa kwa kupumua tu hewa iliyochafuka.

Waweza kuepuka kupumua “hewa” hiyo. (Waefeso 2:2) Badala yake, fuata ushauri wa Paulo: “Mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Kufanya hivyo hutaka jitihada. (Mithali 2:1-5) Kumbuka kwamba, Yehova haongozi kwa hila. Yeye huandaa habari yote inayohitajiwa, lakini ili unufaike nayo, lazima uisikilize na uiache iathiri kufikiri kwako. (Isaya 30:20, 21; 1 Wathesalonike 2:13) Lazima uwe tayari kujaza akili yako na kweli iliyo katika “maandishi matakatifu,” Neno la Mungu lililopulizwa, Biblia.—2 Timotheo 3:15-17.

Kubali Kufanyizwa Katika Muundo wa Yehova

Yehova alipomwambia nabii Yeremia atembelee nyumba ya mfinyanzi, hicho kilikuwa kielezi cha kuonyesha uvutano wa kufinyangwa katika muundo wa Yehova. Ili unufaike wahitaji kuitikia kwa utayari na kuwa mtiifu. Yeremia aliona mfinyanzi akibadili nia yake kuhusu jambo la kufanya na chombo kimoja wakati chombo alichokuwa akijaribu kukifanya “kilipoharibika mkononi mwake yule mfinyanzi.” Ndipo Yehova akasema: “Je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? . . . Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli.” (Yeremia 18:1-6) Je, hilo lilimaanisha kwamba watu katika Israeli walikuwa tu kama mabonge yasiyo na uhai ya udongo mikononi mwa Yehova ili ayafanyize katika muundo kiholela kutoka katika namna moja ya chombo hadi nyingine?

Yehova hatumii kamwe nguvu yake ya uwezo wote kufanya watu wafanye mambo yaliyo kinyume cha mapenzi yao; wala hana daraka kwa matokeo yao mabaya, kama vile ilivyo na mfinyanzi mwanadamu. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kasoro hutokea wakati wale ambao Yehova hujaribu kuwaunda katika muundo wake kwa njia ifaayo hukataa mwelekezo wake. Hii ndiyo tofauti moja kubwa zaidi kati yako na bonge la udongo lisilo na uhai. Wewe una uhuru wa kuchagua. Kwa kuudhihirisha, waweza kuchagua kukubali uvutano wa Yehova wa kukufinyanga au kuukataa kimakusudi.

Hilo ni somo linalohitaji kufikiriwa kama nini! Itafaa kama nini kusikiliza sauti ya Yehova badala ya kusisitiza kwa kiburi, “Hakuna mtu aniambiaye la kufanya”! Sisi sote twahitaji mwongozo wenye uvutano wa Yehova. (Yohana 17:3) Uwe kama mtunga-zaburi Daudi, aliyesali hivi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.” (Zaburi 25:4) Kumbuka yale ambayo Mfalme Solomoni alisema: “Mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu.” (Mithali 1:5) Je, utasikiliza? Ukifanya hivyo, basi “busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi.”—Mithali 2:11.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki