Kesheni na Mwe na Bidii Yenye Kuendelea!
“Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui wala siku wala saa.”—MATHAYO 25:13.
1. Mtume Yohana alikuwa akitazamia kwa hamu jambo gani?
KWENYE mazungumzo ya mwisho katika Biblia, Yesu aliahidi hivi: “Mimi ninakuja upesi.” Yohana, mtume wake, alijibu hivi: “Ameni! Njoo, Bwana Yesu.” Mtume huyo hakuwa na shaka yoyote kwamba Yesu angekuja. Yohana alikuwa miongoni mwa mitume ambao walimwuliza Yesu hivi: “Ni wakati gani mambo haya yatakuwa, nayo itakuwa ni nini ishara ya kuwapo [Kigiriki, pa·rou·siʹa] kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Ndiyo, akiwa na uhakika, Yohana alitazamia kwa hamu kuwapo kwa Yesu kwa wakati ujao.—Ufunuo 22:20; Mathayo 24:3.
2. Hali ikoje katika makanisa kuhusiana na kuwapo kwa Yesu?
2 Uhakika kama huo ni nadra sana siku hizi. Makanisa mengi yana fundisho rasmi kuhusu “kuja” kwa Yesu, lakini ni washiriki wachache wa makanisa hayo wanaokutarajia. Wao huishi tu kana kwamba Yesu hatakuja. Kitabu The Parousia in the New Testament chataarifu hivi: “Kuna uvutano hafifu kuhusu tumaini la Parousia katika maisha, maoni na kazi ya kanisa. . . . Uharaka wenye juhudi nyingi ambao kanisa linatakiwa liwe nao katika kutubu na kufanya kazi ya kimishonari ya kutangaza gospeli, umefifia, au umepotea kabisa.” Lakini hali haiko hivyo kwa watu wote!
3. (a) Wakristo wa kweli wana maoni gani kuhusu pa·rou·siʹa? (b) Sasa tutachunguza nini hasa?
3 Wanafunzi wa kweli wa Yesu wanangojea kwa hamu mwisho wa mfumo mwovu wa mambo uliopo. Tuendeleapo kungojea kwa uaminifu-mshikamanifu, twahitaji kuwa na maoni yanayofaa kuelekea mambo yote yanayohusishwa na kuwapo kwa Yesu na tutende kulingana nayo. Hayo yatatuwezesha ‘kuvumilia hadi mwisho na tuokolewe.’ (Mathayo 24:13) Alipokuwa akitoa unabii tunaopata katika Mathayo sura ya 24 na 25, Yesu aliandaa shauri lenye hekima tunaloweza kutumia kwa manufaa yetu yenye kudumu. Sura ya 25 ina mifano ambayo yaelekea unaijua, kutia ndani ule mfano wa mabikira kumi (wale mabikira wenye hekima na wale wapumbavu) na mfano wa talanta. (Mathayo 25:1-30) Tunaweza kunufaikaje na vielezi hivyo?
Ukeshe, Kama Wale Mabikira Watano!
4. Ni yapi mambo makuu katika mfano wa mabikira?
4 Labda ungependa kusoma tena ule mfano wa mabikira, unaopatikana kwenye Mathayo 25:1-13. Hapo pana arusi kubwa ya Kiyahudi ambapo bwana-arusi anaenda kwenye nyumba ya baba ya bibi-arusi ili kumleta bibi-arusi nyumbani kwa bwana-arusi (au kwa baba yake). Huenda mwandamano wa aina hiyo ukatia ndani wanamuziki na waimbaji, na wakati mahususi wa kuwasili kwa mwandamano huo haungejulikana. Katika mfano huo, mabikira kumi walingojea kuwasili kwa bwana-arusi hadi usiku. Kwa upumbavu, watano hawakuwa wamebeba mafuta ya taa ya kutosha na kwa hivyo walilazimika kwenda kununua mafuta zaidi. Kwa hekima, wale wengine watano walikuwa wamebeba mafuta ya ziada katika vyombo vyao ili wazijaze tena taa zao ikiwa wangelazimika kufanya hivyo wanapongojea. Ni hawa watano tu waliokuwepo wakiwa tayari wakati bwana-arusi alipowasili. Kwa hiyo, ni hao tu walioruhusiwa kuingia kwenye karamu. Wakati wale mabikira watano wapumbavu waliporudi, walikuwa wamechelewa mno wasiweze kuingia.
5. Ni maandiko yapi yanayofafanua maana ya kitamathali ya mfano wa wale mabikira kumi?
5 Sehemu nyingi za mfano huo zaweza kueleweka kuwa ni za ufananisho. Kwa kielelezo, Maandiko humtaja Yesu kuwa kama bwana-arusi. (Yohana 3:28-30) Yesu alijifananisha na mwana wa mfalme ambaye aliandaliwa karamu ya ndoa. (Mathayo 22:1-14) Nayo Biblia humlinganisha Kristo na mume. (Waefeso 5:23) Kwa kupendeza, ingawa Wakristo watiwa-mafuta wanafafanuliwa kwingineko kuwa “bibi-arusi” wa Kristo, mfano huo hautaji bibi-arusi. (Yohana 3:29; Ufunuo 19:7; 21:2, 9) Hata hivyo, mfano huo husema juu ya mabikira kumi, nao watiwa-mafuta wanafananishwa mahali kwingineko na bikira ambaye ameposewa Kristo.—2 Wakorintho 11:2.a
6. Yesu alitoa himizo gani alipokuwa akimalizia mfano wa wale mabikira kumi?
6 Mbali na mambo ya kindani kama hayo na matumizi yoyote ya kiunabii, kwa hakika kuna kanuni nzuri tunazoweza kujifunza kutokana na mfano huo. Mathalani, ona kwamba Yesu aliumalizia kwa maneno haya: “Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui wala siku wala saa.” Kwa hiyo, mfano huo waonyesha uhitaji wa kila mmoja wetu kukesha, kuwa chonjo kuelekea mwisho unaokaribia wa mfumo huu mwovu wa mambo. Bila shaka mwisho huo unakuja, hata ingawa hatuwezi kutaja tarehe hususa. Kwa habari hii, ona mitazamo inayodhihirishwa na vikundi hivyo viwili vya mabikira.
7. Ni katika maana gani mabikira watano katika mfano huo walithibitika kuwa wapumbavu?
7 Yesu alisema hivi: “Watano wao walikuwa wapumbavu.” Je, walikuwa hivyo kwa sababu hawakuamini kuwa bwana-arusi anakuja? Je, walikuwa wameenda kutafuta raha? Au je, walidanganywa? Jibu ni la. Yesu alisema kwamba hao watano ‘walitoka wakaenda kukutana na bwana-arusi.’ Walijua kwamba alikuwa anakuja, nao walitaka wahusishwe, na hata washiriki katika “karamu ya arusi.” Ingawa hivyo, je, walikuwa wamejitayarisha vizuri? Walimngojea kwa muda fulani, hadi “katikati kabisa ya usiku,” lakini hawakuwa wamejitayarishia kuwasili kwake wakati wowote ambapo kungetokea—iwe ni mapema au baadaye kuliko vile walivyotarajia hapo awali.
8. Wale mabikira wengine watano katika mfano huo walithibitikaje kuwa wenye busara?
8 Wale wengine watano—ambao Yesu alisema kuwa ni wenye busara—pia walitoka na taa zilizowashwa, wakitarajia kuwasili kwa bwana-arusi. Iliwabidi wangoje pia, lakini walikuwa “wenye busara.” Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “wenye busara,” laweza kumaanisha “mwenye hekima, mwenye akili, mwenye hekima tendaji.” Hao watano walijithibitisha kuwa wenye busara kwa kubeba vyombo vyenye mafuta ya ziada ili kuzijaza tena taa zao ikihitajika. Kwa kweli, walizingatia sana kujitayarishia bwana-arusi hivi kwamba hawangeweza kumpa mwingine mafuta yao. Kukesha huko hakukuwa kazi bure, kama inavyothibitishwa na kuwapo kwao na kuwa kwao tayari kabisa wakati bwana-arusi alipowasili. Hao “waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya arusi; nao mlango ukafungwa.”
9, 10. Ni nini kusudi la mfano wa mabikira, na ni maswali gani tunayopaswa kujiuliza?
9 Yesu hakuwa akifundisha juu ya adabu arusini, wala hakuwa akitoa shauri juu ya kushiriki vitu na wengine. Hoja yake ilikuwa hii: “Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui wala siku wala saa.” Jiulize hivi, ‘Je, ninakesha kwelikweli kuhusiana na kuwapo kwa Yesu?’ Tunaamini kwamba Yesu sasa anatawala mbinguni, lakini sisi tunazingatia kwa kiwango gani ule uhalisi wa kwamba ‘karibuni Mwana wa binadamu atakuja juu ya mawingu ya mbinguni na nguvu na utukufu mkubwa’? (Mathayo 24:30) Kwa hakika, kufikia “katikati kabisa ya usiku,” kuwasili kwa bwana-arusi kulikuwa karibu zaidi kuliko hapo awali ambapo mabikira walitoka kwenda kumlaki. Vivyo hivyo, kuwasili kwa Mwana wa binadamu ili kuuharibu mfumo mwovu wa sasa kuko karibu zaidi kuliko wakati tulipoanza kutazamia kwa hamu kuja kwake. (Waroma 13:11-14) Je, tumedumisha kukesha kwetu, tukiendelea kukesha hata zaidi kadiri wakati huo ukaribiapo?
10 Yahitaji kukesha sikuzote ili kutii amri hii ya “fulizeni kulinda.” Mabikira watano waliacha mafuta yao yakaisha nao wakaenda kununua mengine zaidi. Vivyo hivyo leo, Mkristo anaweza kukengeushwa fikira hivi kwamba asiweze kuwa tayari kabisa kwa ajili ya kuwasili kwa Yesu ambako kuko karibu. Jambo hilo liliwapata baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza. Hilo pia laweza kuwapata baadhi ya Wakristo leo. Kwa hiyo acheni tujiulize hivi, ‘Je, mimi ninapatwa na jambo hilo?’—1 Wathesalonike 5:6-8; Waebrania 2:1; 3:12; 12:3; Ufunuo 16:15.
Uwe na Bidii Yenye Kuendelea Mwisho Ukaribiapo
11. Yesu alifuatisha kutoa mfano gani mwingine, nao ulifanana na nini?
11 Katika mfano wake uliofuata, Yesu alifanya mengi kuliko tu kuwasihi wafuasi wake wakeshe. Baada ya kusimulia kuhusu mabikira wenye hekima na wale wapumbavu, alisimulia kielezi cha talanta. (Soma Mathayo 25:14-30.) Mambo mengi ya kielezi hicho yanafanana na mfano wake wa mapema wa mina, ambao Yesu aliutoa kwa sababu wengi “walikuwa wakiwazia kwamba ufalme wa Mungu ulikuwa ukielekea kujionyesha mara hiyo.”—Luka 19:11-27.
12. Ni yapi mambo makuu katika mfano wa talanta?
12 Katika mfano wa talanta, Yesu alisimulia kuhusu mwanamume ambaye, kabla ya kusafiri nchi ya nje, aliwaita watumwa watatu. Akampa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na wa mwisho talanta moja tu—“kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.” Yaelekea hiyo ilikuwa talanta ya fedha, kiwango rasmi ambacho wakati huo thamani yake ilikuwa sawa na mshahara ambao mfanyakazi angechuma kwa miaka 14—pesa nyingi kwelikweli! Mwanamume huyo aliporudi, aliwataka watumwa watoe hesabu ya kile walichofanya kwa kipindi cha “wakati mrefu” alipokuwa hayupo. Watumwa wa kwanza wawili walikuwa wameongeza maradufu thamani ya kile walichokabidhiwa. Alisema “vema,” akaahidi kila mmoja madaraka zaidi, na kumalizia hivi: “Ingia katika shangwe ya bwana-mkubwa wako.” Mtumwa mwenye talanta moja, huku akidai kwamba bwana-mkubwa alikuwa mwenye kudai mno, hakuitumia talanta kwa njia yoyote yenye faida. Alizificha pesa hizo, bila hata kuziweka akiba katika benki ili zichume riba. Bwana-mkubwa alimtaja kuwa “mwovu na goigoi” kwa sababu alikuwa ametenda kinyume cha masilahi ya bwana-mkubwa wake. Basi, akanyang’anywa talanta hiyo, naye akatupwa nje, “huko ndiko kutoa kwake machozi na kusaga meno” kungekuwa.
13. Yesu alithibitikaje kuwa kama bwana-mkubwa katika mfano huo?
13 Kwa mara nyingine tena, mambo ya ndani ya mfano huo yaweza kueleweka kwa njia ya ufananisho. Kwa kielelezo, Yesu, aliyefananishwa na mwanamume anayesafiri nchi ya nje, angewaacha wanafunzi wake, aende mbinguni, na angoje kwa wakati mrefu hadi wakati ambapo angepokea mamlaka ya kifalme.b (Zaburi 110:1-4; Matendo 2:34-36; Waroma 8:34; Waebrania 10:12, 13) Hata hivyo, twaweza kutambua tena somo kubwa au kanuni ambayo sisi sote twapaswa kuitumia maishani. Ni kanuni gani?
14. Ule mfano wa talanta unakazia uhitaji gani muhimu?
14 Ni wazi kutokana na mfano wa Yesu kwamba twapaswa kuwa tunajikakamua katika utendaji wa Kikristo, iwe kwamba tumaini letu ni kupata uhai usioweza kufa huko mbinguni au uhai udumuo milele katika paradiso duniani. Kwa kweli, ujumbe wa mfano huo waweza kujumlishwa kifupi hivi: bidii yenye kuendelea. Mitume waliweka kiolezo kuanzia Pentekoste 33 W.K. na kuendelea. Twasoma hivi: “Kwa maneno mengine mengi [Petro] akatoa ushahidi kamili na kufuliza kuwahimiza kwa bidii, akisema: ‘Pateni kuokolewa kutokana na kizazi hiki kilicho kombo.’” (Matendo 2:40-42) Naye alipata matokeo mazuri kama nini kwa sababu ya jitihada zake! Wengine walipoendelea kujiunga na mitume katika kazi ya Kikristo ya kuhubiri, wao pia walikuwa na bidii yenye kuendelea, huku habari njema ‘ikiongezeka katika ulimwengu wote.’—Wakolosai 1:3-6, 23; 1 Wakorintho 3:5-9.
15. Ni kwa njia ipi ya pekee twapaswa kuwa tukitumia jambo kuu la mfano wa talanta?
15 Ukumbuke muktadha wa mfano huo—unabii kuhusu kuwapo kwa Yesu. Tuna uthibitisho wa kutosha wa kuonyesha kuwa pa·rou·siʹa ya Yesu inaendelea na kwamba itafikia upeo hivi karibuni. Kumbuka ule ulinganifu ambao Yesu aliweka kati ya “mwisho” na kazi ambayo Wakristo wanahitaji kufanya: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Tukiwa na hayo akilini, je, twafanana na mtumwa yupi? Jiulize hivi: ‘Je, kungekuwa na sababu ya kukata kauli kwamba mimi nafanana na mtumwa yule aliyeficha kile alichokabidhiwa, labda huku akiendelea kushughulikia mambo yake ya kibinafsi? Au je, iko wazi kwamba mimi ni kama wale waliokuwa wema na waaminifu? Je, nimeazimia kabisa kuongeza masilahi ya Bwana-mkubwa kila wakati?’
Kukesha na Kuwa na Bidii Yenye Kuendelea Wakati wa Kuwapo Kwake
16. Ile mifano miwili ambayo tumeizungumzia ina ujumbe gani kwako?
16 Ndiyo, mbali na maana yake ya kitamathali na ya kiunabii, mifano hiyo miwili hutupa kitia-moyo kilicho wazi kitokacho katika kinywa cha Yesu mwenyewe. Huu ndio ujumbe wake: Kesheni; iweni na bidii yenye kuendelea, hasa wakati ishara ya pa·rou·siʹa ya Kristo inapoonekana. Hiyo ni sasa. Kwa hivyo, je, kweli tunakesha na kuwa na bidii yenye kuendelea?
17, 18. Mwanafunzi Yakobo alishauri nini kuhusu kuwapo kwa Yesu?
17 Yakobo, yule ndugu wa kambo wa Yesu, hakuwako kwenye Mlima wa Mizeituni kuweza kusikia unabii wa Yesu; lakini baadaye alijifunza kuuhusu, naye alielewa waziwazi umuhimu wake. Aliandika hivi: “Kwa hiyo, dhihirisheni subira akina ndugu, hadi kuwapo kwa Bwana. Tazameni! Mkulima hufuliza kungojea matunda yenye bei ya dunia, akidhihirisha subira juu yayo mpaka apatapo mvua ya mapema na mvua ya mwisho-mwisho. Nyinyi pia dhihirisheni subira; fanyeni mioyo yenu kuwa imara, kwa sababu kuwapo kwa Bwana kumekaribia.”—Yakobo 5:7, 8.
18 Baada ya kutoa uhakikisho kwamba Mungu atawahukumu vikali wale wanaotumia vibaya mali zao, Yakobo aliwasihi Wakristo wasikose subira wanapomngojea Yehova atende. Huenda Mkristo asiye na subira akawa mwenye kulipiza kisasi, kana kwamba yeye mwenyewe ndiye anayepaswa kusahihisha makosa yaliyofanywa. Hata hivyo, haipasi kuwa hivyo, kwa sababu wakati wa hukumu utafika hakika. Mfano wa mkulima unatolea jambo hilo kielezi, kama Yakobo alivyofafanua.
19. Mkulima Mwisraeli angedhihirisha subira ya aina gani?
19 Ilimbidi mkulima Mwisraeli ambaye alipanda mbegu angoje, kwanza jani litokee, kisha mmea ufikie ukomavu, na mwishowe mavuno. (Luka 8:5-8; Yohana 4:35) Kwa miezi hiyo yote kulikuwa wakati, na labda sababu ya kuhangaika. Je, mvua ya mapema ingenyesha na iwe ya kiasi cha kutosha? Vipi kuhusu mvua ya mwisho-mwisho? Je, huenda wadudu au mvua yenye upepo mkali ikaangamiza mimea? (Linganisha Yoeli 1:4; 2:23-25.) Hata hivyo, kwa ujumla mkulima Mwisraeli angeweza kumtumaini Yehova na duru za asili ambazo ameziweka. (Kumbukumbu la Torati 11:14; Yeremia 5:24) Kwa kweli, subira ya mkulima ingekuja kuwa taraja lenye uhakika. Kwa imani yeye alijua kwamba kile alichokuwa akingojea kingekuja. Hakika kingekuja!
20. Tunaweza kudhihirishaje subira kupatana na shauri la Yakobo?
20 Ingawa mkulima anaweza kujua wakati wa mavuno, Wakristo wa karne ya kwanza hawangeweza kukadiria kihususa wakati wa kuwapo kwa Yesu. Hata hivyo, kwa hakika kuwapo huko kungekuja. Yakobo aliandika hivi: “Kuwapo [Kigiriki, pa·rou·siʹa] kwa Bwana kumekaribia.” Wakati Yakobo alipoyaandika maneno hayo, ishara kubwa, au ya tufeni pote, ya kuwapo kwa Kristo ilikuwa bado haijaonekana. Lakini sasa imeonekana! Kwa hiyo, twapaswa kuhisije katika kipindi hiki? Kwa hakika ishara inaonekana. Tunaiona. Tunaweza kusema kwa uhakika, ‘Ninaona ishara ikitimizwa.’ Tunaweza kusema kwa uhakika kwamba ‘Kuwapo kwa Bwana kumefika, na upeo wa kuwapo huko umekaribia.’
21. Tumeazimia kwa dhati kufanya nini?
21 Kwa kuwa hali iko hivyo, tuna sababu yenye nguvu hata zaidi ya kuzingatia na kutumia masomo muhimu katika mifano miwili ya Yesu ambayo tumeizungumzia. Alisema hivi: “Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui wala siku wala saa.” (Mathayo 25:13) Bila shaka yoyote, sasa ndio wakati wa kuwa na bidii katika utumishi wetu wa Kikristo. Acheni tuonyeshe kila siku katika maisha yetu kwamba tunaelewa hoja ya Yesu. Acheni tukeshe! Acheni tuwe na bidii yenye kuendelea!
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu mambo yenye ufananisho ya mfano huo, ona kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, ukurasa wa 169-211, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Ona kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, ukurasa wa 212-256.
Je, Wakumbuka?
◻ Umejifunza habari gani muhimu kutokana na mfano wa wale mabikira wenye hekima na wale wapumbavu?
◻ Yesu anakutolea shauri gani muhimu kupitia mfano wa zile talanta?
◻ Ni katika maana gani subira yako kuhusiana na pa·rou·siʹa inafanana na ile ya mkulima Mwisraeli?
◻ Ni kwa nini wakati huu tunamoishi ni wenye kusisimua na wenye magumu?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ni masomo gani unayojifunza kutokana na ule mfano wa mabikira na ule wa talanta?