Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 5/15 kur. 10-15
  • Tuna Furaha kwa Sababu Yehova Hutuonyesha Njia Yake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tuna Furaha kwa Sababu Yehova Hutuonyesha Njia Yake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova Aonyesha Njia
  • Wengine Walitembea Katika Njia ya Yehova
  • Kwa Nini Wengine Waliiacha Njia ya Yehova
  • Kielelezo Kibaya cha Ahazi
  • Wayahudi Wakiwa na Yeremia Misri
  • Yehova Huwabariki Wale Wanaotembea Katika Njia Yake
  • Mtumaini Yehova Ukabilipo Janga
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Kesi ya Mahakama ya Ulimwengu Wote Mzima Ambayo Inakuhusisha Wewe Ndani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Mashahidi Dhidi ya Miungu Bandia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Shauri la Yehova Dhidi ya Mataifa
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 5/15 kur. 10-15

Tuna Furaha kwa Sababu Yehova Hutuonyesha Njia Yake

“Mungu njia yake ni kamilifu; ahadi ya BWANA imehakikishwa.”—2 SAMWELI 22:31.

1, 2. (a) Wanadamu wote wana uhitaji wa msingi wa kupata nini? (b) Itakuwa vema tufuate kielelezo cha nani?

WANADAMU wote wana uhitaji wa msingi wa kupata mwongozo. Kwa kweli, tunahitaji msaada wa kutuongoza maishani. Ni kweli kwamba Yehova ametupa kiasi fulani cha akili na dhamiri inayotusaidia kufahamu lililo jema na lililo baya. Lakini dhamiri yetu yahitaji kuzoezwa ikiwa itatuongoza kwa njia yenye kutegemeka. (Waebrania 5:14) Nayo akili yetu yahitaji habari sahihi—na vilevile mazoezi ya kuichanganua habari hiyo—ikiwa tutafanya maamuzi mazuri. (Mithali 2:1-5) Lakini hata baada ya kufanya hivyo, huenda maamuzi yetu yakakosa kuwa vile tunavyotaka kwa sababu ya ukosefu wa uhakika maishani. (Mhubiri 9:11) Tukijitegemea, sisi hatuna njia inayotegemeka ya kujua mambo ya wakati ujao.

2 Kwa sababu hizo na nyingine nyingi, nabii Yeremia aliandika hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Yesu Kristo, yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, alikubali mwelekezo. Alisema hivi: “Mwana hawezi kufanya hata kitu kimoja kwa uanzisho wake mwenyewe, ila tu kile atazamacho Baba akifanya. Kwa maana mambo yoyote yale Huyo hufanya, mambo hayo Mwana pia hufanya kwa namna kama hiyo.” (Yohana 5:19) Basi, ni jambo la hekima kama nini kumwiga Yesu na kumtegemea Yehova atupe msaada wa kuzielekeza hatua zetu! Mfalme Daudi aliimba hivi: “Mungu njia yake ni kamilifu; ahadi ya BWANA imehakikishwa; yeye ndiye ngao yao wote wanaomkimbilia.” (2 Samweli 22:31) Tukijitahidi kutembea katika njia ya Yehova badala ya kufuata hekima yetu wenyewe, tutapata mwongozo mkamilifu. Kuikataa njia ya Mungu husababisha msiba.

Yehova Aonyesha Njia

3. Yehova aliwaongozaje Adamu na Hawa, naye aliwatolea matazamio gani?

3 Fikiria kisa cha Adamu na Hawa. Walihitaji mwelekezo hata ingawa hawakuwa na dhambi. Yehova hakuacha Adamu ajipangie kila jambo katika bustani maridadi ya Edeni. Badala yake, Mungu alimpa kazi ya kufanya. Kwanza, Adamu alipaswa kuwapa wanyama majina. Kisha, Yehova akawapa Adamu na Hawa miradi ya muda mrefu. Walipaswa kuitiisha dunia, kuijaza kwa uzao wao, na kuwatunza wanyama wa dunia. (Mwanzo 1:28) Hiyo ingekuwa kazi kubwa mno, lakini matokeo ya mwisho yangekuwa paradiso ya ulimwenguni pote iliyojaa jamii kamilifu ya kibinadamu inayoishi kwa upatano na wanyama walioumbwa. Lilikuwa tazamio zuri kama nini! Na zaidi, maadamu Adamu na Hawa wangeendelea kutembea kwa uaminifu katika njia ya Yehova, wangewasiliana naye. (Linganisha Mwanzo 3:8.) Lilikuwa pendeleo la kustaajabisha kama nini—kuwa na uhusiano wenye kuendelea na wa kibinafsi pamoja na Muumba!

4. Adamu na Hawa walionyeshaje ukosefu wa tumaini na uaminifu-mshikamanifu, na matokeo yenye msiba yalikuwa gani?

4 Yehova aliwakataza wanadamu wawili wa kwanza kula kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya uliokuwa katika Edeni, na hilo liliwapa fursa ya papohapo ya kuonyesha utii wao—tamaa yao ya kutembea katika njia ya Yehova. (Mwanzo 2:17) Hata hivyo, baada ya muda mfupi, utii huo ulijaribiwa. Shetani alipokuja na maneno yake ya udanganyifu, Adamu na Hawa walihitaji kuonyesha uaminifu-mshikamanifu wao kwa Yehova na kuzitumaini ahadi Zake ikiwa wangedumisha utii. Kwa kusikitisha, walikosa uaminifu-mshikamanifu na tumaini. Shetani alipomtolea Hawa uhuru wa kujitegemea na kumshtaki Yehova isivyo kweli kwamba anasema uwongo, Hawa alidanganyika, akakataa kumtii Mungu. Naye Adamu akajiunga naye katika dhambi. (Mwanzo 3:1-6; 1 Timotheo 2:14) Walipata hasara kubwa mno kutokana na jambo hilo. Kutembea katika njia ya Yehova kungewapa shangwe yenye kuongezeka daima huku wakitimiza mapenzi yake hatua kwa hatua. Badala yake, maisha yao yakajawa na kukata tamaa na maumivu hadi kifo.—Mwanzo 3:16-19; 5:1-5.

5. Kusudi la Yehova la muda mrefu ni nini, naye huwasaidiaje wanadamu waaminifu kuona utimizo wake?

5 Hata hivyo, Yehova hakubadili kusudi lake kwamba siku moja dunia itakuwa makao ya paradiso kwa wanadamu wakamilifu, wasio na dhambi. (Zaburi 37:11, 29) Naye hajawahi kamwe kukosa kutoa mwongozo mkamilifu kwa wale wanaotembea katika njia yake na kutumaini kuona utimizo wa ahadi hiyo. Kwetu sisi tulio na masikio ya kusikia, sauti ya Yehova iko nyuma yetu, ikisema hivi: “Njia ni hii, ifuateni.”—Isaya 30:21.

Wengine Walitembea Katika Njia ya Yehova

6. Ni wanaume gani wa kale wawili waliotembea katika njia ya Yehova, na matokeo yakawa nini?

6 Kulingana na rekodi ya Biblia, ni watu wachache tu kati ya uzao wa Adamu na Hawa waliotembea katika njia ya Yehova. Wa kwanza kati yao ni Abeli. Ingawa alikufa kifo cha mapema, alikufa akiwa katika upendeleo wa Yehova na hivyo ana tazamio hakika la kufufuliwa katika “ufufuo wa waadilifu,” katika wakati alioweka Mungu. (Matendo 24:15) Yeye ataona utimizo wa mwisho wa kusudi kubwa la Yehova kwa dunia na wanadamu. (Waebrania 11:4) Mwingine aliyetembea katika njia ya Yehova ni Enoki, ambaye unabii wake kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo umehifadhiwa katika kitabu cha Yuda. (Yuda 14, 15) Enoki pia alikufa kifo cha mapema. (Mwanzo 5:21-24) Ingawa hivyo, “alikuwa na ushahidi kwamba alikuwa amempendeza Mungu vema.” (Waebrania 11:5) Alipokufa, yeye, sawa na Abeli, alikuwa na tazamio hakika la ufufuo, naye atakuwa miongoni mwa wale watakaoona makusudi ya Yehova yakitimizwa.

7. Noa na familia yake walionyeshaje uaminifu-mshikamanifu na tumaini kwa Yehova?

7 Ulimwengu wa kabla ya Furiko ulipozidi kujaa uovu, utii kwa Yehova ukaendelea zaidi na zaidi kuwa jaribu la uaminifu-mshikamanifu. Kufikia mwisho wa ulimwengu huo, ni kikundi kidogo tu kilichopatikana kikitembea katika njia ya Yehova. Noa na familia yake walimsikiliza Mungu na kutumaini yale aliyosema. Walitimiza kwa uaminifu kazi walizopewa nao wakakataa kuingizwa katika mazoea yenye uovu ya ulimwengu wa siku hizo. (Mwanzo 6:5-7, 13-16; Waebrania 11:7; 2 Petro 2:5) Tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa sababu ya utii wao wenye uaminifu-mshikamanifu na tumaini. Kwa sababu ya utii huo, waliokoka Furiko, wakawa mababu wetu.—Mwanzo 6:22; 1 Petro 3:20.

8. Kutembea katika njia ya Mungu kulitia ndani nini kwa taifa la Israeli?

8 Baadaye, Yehova alifanya agano na wazao wa Yakobo mwaminifu, nao wakawa taifa la pekee kwake. (Kutoka 19:5, 6) Yehova aliwaelekeza watu wake wa agano kupitia Sheria iliyoandikwa, ukuhani, na mwongozo wenye kuendelea wa kiunabii. Lakini lilikuwa daraka la Waisraeli kufuata mwelekezo huo. Yehova alimwagiza nabii wake awaambie Waisraeli hivi: “Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana; baraka ni hapo mtakapoyasikia maagizo ya BWANA, Mungu wenu, niwaagizayo leo; na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya BWANA, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua.”—Kumbukumbu la Torati 11:26-28.

Kwa Nini Wengine Waliiacha Njia ya Yehova

9, 10. Ni kwa sababu ya hali gani Waisraeli walihitaji kumtumaini Yehova na kusitawisha uaminifu-mshikamanifu kwake?

9 Waisraeli, sawa tu na Adamu na Hawa, walihitaji kumtumaini Yehova na kuwa waaminifu-washikamanifu kwake ikiwa wangedumu wakiwa watiifu. Israeli lilikuwa taifa dogo lililozungukwa na jirani wagomvi. Misri na Ethiopia zilikuwa upande wa kusini-magharibi. Siria na Ashuru zilikuwa kaskazini-mashariki. Filistia, Amoni, Moabu, na Edomu zilikuwa katika ujirani wa karibu. Hizi nchi zote zilithibitika kuwa adui za Israeli nyakati mbalimbali. Na zaidi, zote zilifuata dini isiyo ya kweli, iliyojulikana kwa ibada ya sanamu, unajimu, na katika visa vingine, sherehe za kingono zilizopotoka kabisa na kudhabihu watoto kikatili. Jirani za Israeli walitegemea miungu yao iwape familia kubwa, mavuno mengi, na ushindi vitani.

10 Taifa la Israeli pekee ndilo lililomwabudu Mungu mmoja, Yehova. Aliwaahidi baraka za familia kubwa, mavuno mengi, na usalama dhidi ya adui ikiwa wangezitii sheria zake. (Kumbukumbu la Torati 28:1-14) Kwa kusikitisha, wengi katika Israeli hawakufanya hivyo. Wengi waliotembea katika njia ya Yehova waliteswa kwa sababu ya uaminifu-mshikamanifu wao. Hata baadhi yao waliteswa vikali, wakadhihakiwa, wakapigwa mijeledi, wakafungwa gerezani, wakapigwa mawe, na kuuawa na Waisraeli wenzao. (Matendo 7:51, 52; Waebrania 11:35-38) Hayo yalikuwa majaribu makali kama nini kwa waaminifu hao! Hata hivyo, kwa nini wengi walitoka katika njia ya Yehova? Vielelezo viwili kutoka katika historia ya Israeli vinatusaidia kuona kufikiri kwao kusikofaa.

Kielelezo Kibaya cha Ahazi

11, 12. (a) Siria lilipomtisha Ahazi, yeye alikataa kufanya nini? (b) Ahazi alitafuta usalama kutoka vyanzo gani viwili?

11 Ahazi alitawala ufalme wa kusini wa Yuda katika karne ya nane K.W.K. Utawala wake haukuwa wa amani. Wakati mmoja, Siria na ufalme wa kaskazini wa Israeli waliungana vitani dhidi yake, na “moyo wake ukataharuki, na moyo wa watu wake.” (Isaya 7:1, 2) Hata hivyo, Yehova alipotaka kumsaidia na kumwalika Ahazi amjaribu, Ahazi alikataa katakata! (Isaya 7:10-12) Matokeo yakawa kwamba, Yuda lilishindwa vitani na watu wake wengi wakauawa.—2 Mambo ya Nyakati 28:1-8.

12 Ingawa Ahazi alikataa kumjaribu Yehova, alinyenyekea, akamwomba mfalme wa Ashuru msaada. Na bado, Yuda liliendelea kuteseka mikononi mwa jirani zake. Ashuru pia lilipomgeuka Ahazi na ‘kumfadhaisha,’ mfalme “akaitolea dhabihu miungu ya Dameski iliyompiga, akasema, Kwa sababu miungu ya Wafalme wa Shamu [“Siria,” NW] imewasaidia wao, mimi nitaitolea dhabihu, ili inisaidie mimi.”—2 Mambo ya Nyakati 28:20, 23, Union Version, Chapa ya 1989.

13. Ahazi alionyesha nini kwa kuigeukia miungu ya Siria?

13 Baadaye, Yehova aliliambia Israeli hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye katika njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Hatua ya Ahazi ya kuigeukia miungu ya Siria ilionyesha tu vile alivyokuwa amepotoka sana kutoka ‘katika njia impasayo kuifuata.’ Kufikiri kwa mataifa kulimpotosha kabisa, naye akategemea vyanzo bandia vya usalama badala ya kumtegemea Yehova.

14. Ni kwa nini Ahazi hakuwa na sababu ya kuigeukia miungu bandia?

14 Kwa muda mrefu miungu ya mataifa, kutia ndani ile ya Siria, ilikuwa imethibitishwa kwa muda mrefu kuwa “vinyago vya miungu.” (Isaya 2:8, BHN) Mapema, wakati wa utawala wa Mfalme Daudi, ukuu wa Yehova juu ya miungu ya Siria ulionekana waziwazi wakati Wasiria walipofanywa watumishi wa Daudi. (1 Mambo ya Nyakati 18:5, 6) Ni Yehova pekee, aliye “Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya” awezaye kutoa usalama wa kweli. (Kumbukumbu la Torati 10:17) Ingawa hivyo, Ahazi alimkataa Yehova na kuitegemea miungu ya mataifa ili kupata usalama. Matokeo yalikuwa msiba kwa Yuda.—2 Mambo ya Nyakati 28:24, 25.

Wayahudi Wakiwa na Yeremia Misri

15. Wayahudi walifanyaje dhambi huko Misri katika siku ya Yeremia?

15 Yehova aliwaruhusu Wababiloni waliharibu Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 607 K.W.K., kwa sababu watu wake walikuwa na ukosefu mbaya sana wa uaminifu-mshikamanifu. Wengi katika taifa hilo walihamishiwa Babiloni. Hata hivyo, watu kadhaa walibaki, nabii Yeremia akiwa miongoni mwao. Liwali Gedalia alipouawa kihila, kikundi hicho kilikimbilia Misri na kumchukua Yeremia pamoja nao. (2 Wafalme 25:22-26; Yeremia 43:5-7) Wakaanza kuitolea miungu bandia dhabihu wakiwa huko. Yeremia alisababu kwa bidii na Wayahudi hao wasio waaminifu, lakini wakawa wakaidi. Walikataa kumgeukia Yehova na kusisitiza kwamba wangeendelea kumtolea “malkia wa mbinguni” uvumba. Kwa nini? Kwa sababu wao na baba zao wa zamani walikuwa wakifanya hivyo ‘katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu; walipokuwa na chakula tele, na kufanikiwa, wala hawakuona mabaya.’ (Yeremia 44:16, 17) Pia, Wayahudi walibisha hivi: “Tulipoacha kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, tumepungukiwa na vitu vyote; na kuangamizwa kwa upanga, na kwa njaa.”—Yeremia 44:18.

16. Ni kwa nini Wayahudi waliokuwa Misri walikosea kabisa katika kusababu kwao?

16 Kwa kweli kumbukumbu yaweza kuhifadhi tu yale yanayotupendeza! Ukweli ulikuwa nini? Ni kweli kwamba Wayahudi waliitolea miungu bandia dhabihu katika nchi aliyowapa Yehova. Nyakati nyingine, kama katika siku za Ahazi, waliteseka kwa sababu ya uasi-imani. Hata hivyo, Yehova hakuwa “mwepesi wa hasira” kwa watu wake wa agano. (Kutoka 34:6; Zaburi 86:15) Aliwatuma manabii wake ili wawasihi watubu. Mara kwa mara, mfalme alipokuwa mwaminifu, Yehova alimbariki, nao watu wakafaidika kutokana na baraka hiyo hata ingawa wengi wao hawakuwa waaminifu. (2 Mambo ya Nyakati 20:29-33; 27:1-6) Wayahudi hao huko Misri walikosea kama nini kwa kudai kuwa ufanisi wowote walioufurahia wakiwa nchini mwao ulikuwa umetoka kwa miungu yao bandia!

17. Kwa nini Yuda lilipoteza nchi na hekalu lake?

17 Kabla ya mwaka wa 607 K.W.K., Yehova alikuwa amewasihi watu wa Yuda hivi: “Sikilizeni sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu; mkaende katika njia ile yote nitakayowaamuru mpate kufanikiwa.” (Yeremia 7:23) Wayahudi walipoteza hekalu na nchi yao hasa kwa sababu walikataa kutembea ‘katika njia ile yote ambayo Yehova alikuwa amewaamuru.’ Acheni tuepuke kabisa kufanya kosa lenye kuangamiza kama hilo.

Yehova Huwabariki Wale Wanaotembea Katika Njia Yake

18. Ni lazima wale wanaotembea katika njia ya Yehova wafanye nini?

18 Leo, sawa na zamani, yahitaji uaminifu-mshikamanifu ili kutembea katika njia ya Yehova—azimio la kumtumikia yeye pekee. Inahitaji tumaini—imani kamili kwamba ahadi za Yehova zinategemeka na zitatimia. Yahitaji utii ili kutembea katika njia ya Yehova—tukifuata sheria zake bila kukengeuka na kushika viwango vyake vya juu. “BWANA ndiye mwenye haki, apenda matendo ya haki.”—Zaburi 11:7.

19. Watu wengi leo huabudu miungu ipi, na matokeo ni nini?

19 Ahazi aliitegemea miungu ya Siria ili apate usalama. Waisraeli huko Misri walitumaini kwamba “malkia wa mbinguni,” mungu wa kike aliyeabudiwa sana katika Mashariki ya kale ya Kati, angewapa ufanisi wa mali. Miungu mingi leo si sanamu halisi. Yesu alionya dhidi ya kutumikia “Utajiri” badala ya Yehova. (Mathayo 6:24) Mtume Paulo alisema kuhusu “tamaa, amba[y]o ni ibada ya sanamu.” (Wakolosai 3:5) Alisema pia kuhusu wale ambao “mungu wao ni tumbo lao.” (Wafilipi 3:19) Naam, baadhi ya miungu mikuu inayoabudiwa leo ni pesa na vitu vya kimwili. Kwa kweli, wengi zaidi—kutia ndani watu wengi wa dini—‘wanaweka tumaini lao juu ya mali zisizo hakika.’ (1 Timotheo 6:17) Wengi hufanya bidii sana kuitumikia miungu hiyo, na baadhi yao hupata thawabu—kuishi katika makao bora, kuwa na vitu vya bei ghali, na kula milo ya anasa. Hata hivyo, sio wote wanaofurahia utajiri kama huo. Na hata wale walio na utajiri wanagundua hatimaye kwamba huo wenyewe hauridhishi. Huo hauna uhakika, ni wa muda mfupi, na hautoshelezi mahitaji ya kiroho.—Mathayo 5:3.

20. Twahitaji kudumisha usawaziko gani?

20 Ni kweli kwamba tunapaswa kuwa wenye busara tuendeleapo kuishi katika siku za mwisho za huu mfumo wa mambo. Tunahitaji kuchukua hatua zifaazo ili kuandalia familia zetu mahitaji ya kimwili. Lakini tukikazia sana kiwango cha juu cha maisha, kufuatia pesa, au vitu kama hivyo badala ya kumtumikia Mungu, tutakuwa tumeingia katika namna fulani ya ibada ya sanamu nasi tutakuwa hatuendelei tena kutembea katika njia ya Yehova. (1 Timotheo 6:9, 10) Ingawa hivyo, itakuwaje tukikabiliwa na matatizo ya afya, ya kifedha, au mengineyo? Acheni tusiwe kama Wayahudi huko Misri waliosema kuwa kumtumikia Mungu ndiko kulikosababisha matatizo yao. Badala yake, acheni tumjaribu Yehova, jambo ambalo Ahazi alikataa kufanya. Mgeukie Yehova Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu ili akuongoze. Fuata mwongozo wake kwa kumtumaini, na kusali ili upate nguvu na hekima ya kushughulikia hali yoyote. Kisha, ngojea kwa uhakika baraka ya Yehova.

21. Wale wanaotembea katika njia ya Yehova wanapata baraka zipi?

21 Yehova aliwabariki sana wale waliotembea katika njia yake kwa historia yote ya Israeli. Mfalme Daudi aliimba hivi: “BWANA, uniongoze kwa haki yako, kwa sababu yao wanaoniotea.” (Zaburi 5:8) Yehova alimpa ushindi wa kivita dhidi ya mataifa jirani ambayo baadaye yalimsumbua Ahazi. Chini ya utawala wa Solomoni, Waisraeli walibarikiwa kwa kupewa amani na ufanisi ambao Wayahudi huko Misri walitamani sana baadaye. Hata Yehova alimpa Hezekia mwana wa Ahazi ushindi dhidi ya Ashuru lenye nguvu. (Isaya 59:1) Naam, mkono wa Yehova haukuwa mfupi kuelekea waaminifu-washikamanifu wake, ambao hawakusimama “katika njia ya wakosaji” bali walipendezwa na sheria ya Mungu. (Zaburi 1:1, 2) Hali ingali hivyo leo. Hata hivyo, tunaweza kuwaje na uhakika kwamba tunatembea katika njia ya Yehova? Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

Je, Wakumbuka?

◻ Ni sifa zipi zilizo muhimu ikiwa tutatembea katika njia ya Yehova?

◻ Kwa nini kufikiri kwa Ahazi hakukustahili?

◻ Kwa nini kusababu kwa Wayahudi huko Misri kulikuwa na makosa?

◻ Twaweza kutiaje nguvu azimio letu la kutembea katika njia ya Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ahazi aliitegemea miungu ya Siria badala ya kumtegemea Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki