Wakati na Umilele Tunajua Nini Hasa Kuzihusu?
“WAKATI waonekana kuwa mojawapo ya mambo yaliyo magumu zaidi kwa mwanadamu kuelewa,” ensaiklopedia moja yaeleza. Naam, kufafanua wakati kwa maneno sahili ni jambo ambalo ni kama haliwezekani. Twaweza kusema kwamba wakati “hupita,” “huenda,” “huyoyoma,” na hata kusema kwamba sisi wenyewe tunaenda na “mkondo wa wakati.” Lakini hatujui hasa lile tunalozungumzia.
Wakati umefafanuliwa kuwa “umbali uliopo baina ya matukio mawili.” Hata hivyo, mambo tunayoyafahamu yaonekana yanatujulisha kwamba wakati hautegemei matukio; waonekana kuendelea tu, iwe jambo fulani latukia au la. Mwanafalsafa mmoja adai kwamba kwa kweli wakati haupo, bali ni kitu tu cha kuwaziwa. Je, yawezekana kwamba kile ambacho tumetegemea sana, yaani wakati, kiwe kitu tunachowazia tu?
Maoni ya Biblia juu ya Wakati
Biblia haitoi ufafanuzi wowote juu ya wakati, hilo likidokeza kwamba labda mwanadamu hawezi kabisa kuuelewa. Wakati unafanana na uwazi wa anga ambao hauna mwisho, na ambao pia tunaona ugumu wa kuelewa. Yaonekana wakati ni mojawapo ya mambo ambayo Mungu pekee ndiye awezaye kuyaelewa kabisa, kwa kuwa yeye peke yake ndiye wa “tangu milele hata milele.”—Zaburi 90:2.
Biblia hutaja wakati kuwa halisi, hata ingawa haiufafanui. Kwanza, Biblia hutuambia kwamba Mungu aliumba “mianga”—jua, mwezi, na nyota— iwe alama za wakati, ili “iwe ndiyo dalili na majira na siku na miaka.” Matukio mengi yaliyoandikwa katika Biblia yanafuata kabisa mkondo wa wakati. (Mwanzo 1:14; 5:3-32; 7:11, 12; 11:10-32; Kutoka 12:40, 41) Biblia pia hutaja wakati kuwa kitu ambacho twapaswa kutumia kwa hekima ili tuweze kupata baraka za Mungu za wakati wa umilele—taraja la kuishi milele.—Waefeso 5:15, 16.
Uhai Udumuo Milele—Je, Wazo Hilo Linapatana na Akili?
Ingawa ni jambo linalovuruga akili kujaribu kuelewa wakati ni nini hasa, watu wengi hutatanishwa hata zaidi na wazo la uhai udumuo milele, au kuishi milele. Sababu moja inayofanya watatanike yaweza kuwa kwamba sikuzote tumeelewa kwamba wakati umehusianishwa na mzunguko wa kuzaliwa, kukua, kuzeeka, na kufa. Hivyo, sisi huhusianisha kupita kwa wakati na kuzeeka kwenyewe. Kwa wengi, kuwa na maoni yaliyo tofauti kungeonekana kuwa ukiukaji wa ile dhana hasa ya wakati. ‘Kwa nini wanadamu wawe tofauti na viumbe wengine wote walio hai kwa habari ya kuzeeka?’ huenda wakauliza.
Kusababu kwa aina hiyo mara nyingi hupuuza uhakika wa kwamba, katika hali nyingi, tayari wanadamu ni tofauti na viumbe wengine wote. Kwa mfano, wanyama hawana uwezo wa kiakili ambao wanadamu wanao. Licha ya madai mengine, wanyama hawatumii akili kuliko vile silika zao huwasukuma kufanya. Hawana vipawa vya kisanaa wala uwezo wa kuonyesha upendo na uthamini, sifa ambazo wanadamu wanazo. Ikiwa wanadamu wamepewa sifa na uwezo mwingi wa aina hiyo, ambao hufanya maisha yawe na maana, kwa nini wasiweze kupewa wakati mrefu zaidi kwa habari ya uhai wenyewe?
Kwa upande mwingine, je, haishangazi kwamba katika visa fulani miti isiyoweza kufikiri huishi kwa maelfu ya miaka, ilhali wanadamu wenye akili wanaweza kuishi kwa miaka 70 hadi 80 tu kwa wastani? Je, si jambo lililo kinyume kwamba kobe, ambao hawana uwezo wa kufikiri au wa kisanii, wanaweza kuishi kwa zaidi ya miaka 200, ilhali wanadamu, ambao wamepewa uwezo huo kwa wingi sana, huishi kwa muda wa miaka inayopungua nusu ya hiyo?
Ingawa mwanadamu hawezi kuelewa kikamili wakati na umilele, ahadi ya uhai udumuo milele ingali tumaini lenye msingi mzuri katika Biblia. Katika Biblia, neno “uhai udumuo milele” linaonekana karibu mara 40. Lakini ikiwa kusudi la Mungu ni kwamba wanadamu waishi milele, kwa nini halijatimizwa tayari? Swali hilo litazungumziwa katika makala ifuatayo.