Wazazi, Kielelezo Chenu Chafundisha Nini?
“Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.”—WAEFESO 5:1, 2.
1. Yehova alitoa mielekezo gani kwa wenzi wa kwanza wa kibinadamu?
YEHOVA ndiye Mwanzilishi wa mpango wa familia. Kila familia hutokana naye kwa sababu yeye ndiye aliyeanzisha familia ya kwanza na kuwapa wenzi wa kibinadamu wa kwanza uwezo wa kuzaa. (Waefeso 3:14, 15) Aliwapa Adamu na Hawa maagizo ya msingi kuhusu madaraka yao na pia akawapa fursa ya kutosha ili wao wenyewe wachukue hatua ya kwanza kuyatimiza. (Mwanzo 1:28-30; 2:15-22) Baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, wanadamu walilazimika kukabili hali ngumu zaidi. Hata hivyo, kwa upendo Yehova aliwatolea mielekezo ambayo ingewasaidia watumishi wake washughulikie hali hizo.
2. (a) Ni kwa njia zipi Yehova ametumia shauri lililoandikwa kuimarisha maagizo ya mdomo? (b) Wazazi wapaswa kujiuliza maswali gani?
2 Akiwa Mfunzi wetu Mtukufu, Yehova amefanya mengi zaidi ya kutuandalia mielekezo iliyoandikwa kuhusu yale tupaswayo kufanya na yale tupaswayo kuepuka. Nyakati za kale aliambatanisha maagizo yaliyoandikwa na maagizo ya mdomo kupitia makuhani na manabii na kupitia vichwa vya familia. Yeye anatumia nani mwingine kutoa maagizo ya mdomo wakati wetu? Wazee Wakristo na wazazi. Ikiwa wewe ni mzazi, je, unatimiza sehemu yako ya kuagiza familia yako katika njia za Yehova?—Mithali 6:20-23.
3. Vichwa vya familia wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kufundisha kwenye matokeo?
3 Maagizo hayo yapasa kutolewaje katika familia? Yehova hutoa kiolezo. Yeye hutaarifu waziwazi yaliyo mema na yaliyo mabaya, naye hurudia mambo mara nyingi. (Kutoka 20:4, 5; Kumbukumbu la Torati 4:23, 24; 5:8, 9; 6:14, 15; Yoshua 24:19, 20) Yeye hutumia maswali yenye kuamsha fikira. (Ayubu 38:4, 8, 31) Huchochea hisia zetu na kuelekeza mioyo yetu kwa kutumia vielezi na mifano halisi. (Mwanzo 15:5; Danieli 3:1-29) Wazazi je, nyinyi hujaribu kuiga kiolezo hicho mnapowafundisha watoto wenu?
4. Twajifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kutia nidhamu, na ni kwa nini nidhamu ni muhimu?
4 Yehova ni imara kuhusu yaliyo sawa, lakini yeye huelewa matokeo ya kutokamilika. Kwa hiyo, kabla ya kutoa adhabu, yeye huwafundisha na kuwatolea maonyo na vikumbusha vingi wanadamu wasiokamilika. (Mwanzo 19:15, 16; Yeremia 7:23-26) Anapotia nidhamu, yeye hufanya hivyo kwa kiwango kifaacho, hapiti kiasi. (Zaburi 103:10, 11; Isaya 28:26-29) Ikiwa hivyo ndivyo sisi hushughulika na watoto wetu, jambo hilo latoa uthibitisho wa kwamba tunamjua Yehova, na itakuwa rahisi zaidi kwa watoto kupata kumjua pia.—Yeremia 22:16; 1 Yohana 4:8.
5. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kusikiliza?
5 Ni jambo la ajabu kwamba Yehova husikiliza kama Baba wa kimbingu mwenye upendo. Yeye hatoi maagizo tu. Yeye hututia moyo tumweleze hisia zetu zote. (Zaburi 62:8) Na ikiwa hisia hizo tunazomweleza hazifai kabisa, yeye hatukemei kwa sauti kubwa kutoka mbinguni. Yeye hutufundisha kwa subira. Hivyo, lafaa kama nini shauri hili la mtume Paulo: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa”! (Waefeso 4:31–5:1) Yehova anawatolea wazazi kielelezo kizuri kama nini wanapojaribu kuwaagiza watoto wao! Ni kielelezo kinachotugusa moyo na kufanya tutake kutembea katika njia yake ya maisha.
Uvutano Unaotokezwa na Kielelezo
6. Mtazamo na kielelezo cha wazazi kina uvutano gani kwa watoto wao?
6 Kwa kuongezea maagizo ya mdomo, kielelezo pia kina uvutano mkubwa kwa wachanga. Wazazi wapende wasipende, watoto wao watawaiga. Huenda wazazi wakapendezwa—nyakati nyingine wakashtuka—kusikia watoto wao wakisema mambo ambayo wazazi wenyewe wameyasema. Mwenendo na mtazamo wa wazazi unapoonyesha kwamba wanathamini sana mambo ya kiroho, jambo hilo huwa na matokeo yafaayo kwa watoto.—Mithali 20:7.
7. Yeftha alimwekea binti yake kielelezo akiwa mzazi wa aina gani, na matokeo yakawa nini?
7 Biblia inatoa vielezi vizuri juu ya matokeo ya kielelezo cha wazazi. Yeftha, aliyetumiwa na Yehova kuongoza Waisraeli kuwashinda Waamoni, alikuwa baba pia. Rekodi ya jibu lake kwa mfalme wa Amoni yaonyesha kwamba ni lazima Yeftha awe alisoma mara nyingi historia ya jinsi Yehova alivyoshughulika na Israeli. Angeweza kunukuu historia hiyo bila tatizo, naye alionyesha imani yenye nguvu katika Yehova. Haikosi kielelezo chake kilimsaidia binti yake asitawishe imani na roho ya kujinyima aliyoionyesha kwa kuchukua daraka la kumtumikia akiwa mseja mwanamke aliyejitoa kwa Yehova.—Waamuzi 11:14-27, 34-40; linganisha Yoshua 1:8.
8. (a) Wazazi wa Samweli walionyesha mtazamo gani mzuri? (b) Jambo hilo lilimnufaishaje Samweli?
8 Katika maisha yake yote, Samweli alikuwa kielelezo chema akiwa mtoto na vilevile nabii mwaminifu kwa Mungu. Je, ungependa watoto wako wapate kuwa kama yeye? Ebu changanua kielelezo kilichowekwa na Elkana na Hana, wazazi wa Samweli. Ingawa hali katika familia yao haikuwa nzuri kabisa, walienda kuabudu huko Shilo kwa ukawaida, mahali ambapo tabenakulo takatifu lilikuwa. (1 Samweli 1:3-8, 21) Ona jinsi Hana alivyosali kwa hisia nyingi. (1 Samweli 1:9-13) Ona jinsi wote wawili walivyohisi kuhusu umuhimu wa kutimiza ahadi yoyote waliyomtolea Mungu. (1 Samweli 1:22-28) Haikosi kielelezo chao chema kilimsaidia Samweli asitawishe sifa zilizomsaidia afuatie mwenendo ufaao—hata wakati ambapo watu waliokuwa karibu naye, ambao walitarajiwa kumtumikia Yehova, walikosa kabisa kustahi njia za Mungu. Baada ya muda Yehova alimtwika Samweli daraka la kuwa nabii Wake.—1 Samweli 2:11, 12; 3:1-21.
9. (a) Ni hali gani za nyumbani zilizokuwa na uvutano mzuri kwa Timotheo? (b) Timotheo alipata kuwa mtu wa aina gani?
9 Je, ungetaka mwana wako awe kama Timotheo, ambaye akiwa kijana alipata kuwa mshiriki wa mtume Paulo? Baba ya Timotheo hakuwa mwamini, lakini mama na nyanya yake walimwekea kielelezo kizuri cha kuthamini mambo ya kiroho. Yaelekea jambo hilo lilisaidia kumwekea Timotheo msingi mzuri akiwa Mkristo. Tunaambiwa kwamba Eunike mama yake, na Loisi nyanya yake, walikuwa na “imani . . . isiyo na unafiki wowote.” Maisha yao wakiwa Wakristo hayakuwa yenye unafiki; kwa hakika waliishi kupatana na yale waliyodai kuamini, nao wakamfundisha kijana Timotheo kufanya vivyo hivyo. Timotheo alithibitisha kwamba alikuwa mwenye kutegemeka, na kwamba alijali kikweli hali njema ya wengine.—2 Timotheo 1:5; Wafilipi 2:20-22.
10. (a) Ni vielelezo gani viwezavyo kuathiri watoto wetu nje ya nyumbani? (b) Tufanyeje uvutano huo ukijidhihirisha katika usemi na mtazamo wa watoto wetu?
10 Si vielelezo vyote vinavyoathiri watoto ambavyo hupatikana nyumbani. Kuna watoto wanaosoma nao shuleni, walimu ambao kazi yao ni kufinyanga akili changa, watu ambao hushikilia kwa dhati kwamba kila mtu apaswa kufuata desturi za kikabila zilizo imara kabisa, wachezaji maarufu ambao mafanikio yao husifiwa na wengi, na maofisa wa umma ambao mwenendo wao hutajwa mara nyingi katika vyombo vya habari. Mamilioni ya watoto pia wameona ukatili wa vita. Je, tushangae uvutano huo ukijidhihirisha katika usemi na mtazamo wa watoto wetu? Tufanyeje inapokuwa hivyo? Je, kemeo au karipio kali linatatua tatizo hilo? Badala ya kuwajibu watoto wetu haraka-haraka, je, haingekuwa afadhali kujiuliza, ‘Je, kuna jambo lolote katika njia ambayo Yehova hushughulika nasi linaloweza kutusaidia kufahamu jinsi ya kushughulikia hali hii?’—Linganisha Waroma 2:4.
11. Mtazamo wa watoto waweza kuathiriwaje wazazi wanapokosea?
11 Bila shaka, si sikuzote wazazi wasiokamilika watashughulikia hali katika njia ifaayo kabisa. Watafanya makosa. Watoto wakitambua hivyo je, jambo hilo halitaharibu staha yao kwa wazazi wao? Linaweza, hasa wazazi wakijaribu kupunguza uzito wa makosa yao kwa kusisitiza mamlaka yao kwa ukali. Lakini matokeo yanaweza kuwa tofauti kabisa wazazi wakiwa wanyenyekevu na wanakubali makosa yao kwa hiari. Kwa kufanya hivyo wanaweza kuwawekea watoto wao, ambao pia wanahitaji kufanya vivyo hivyo, kielelezo chenye thamani.—Yakobo 4:6.
Mambo Ambayo Kielelezo Chetu Chaweza Kufundisha
12, 13. (a) Watoto wahitaji kujifunza nini kuhusu upendo, na jambo hilo laweza kufundishwaje kwa matokeo zaidi? (b) Kwa nini ni muhimu kwa watoto kujifunza kuhusu upendo?
12 Kuna masomo mengi yenye thamani yawezayo kufundishwa kwa matokeo zaidi wakati maagizo ya mdomo yanapoambatanishwa na kielelezo kizuri. Fikiria machache.
13 Kuonyesha upendo usio na ubinafsi: Mojawapo ya masomo muhimu ambayo huimarishwa kwa kielelezo ni maana ya upendo. “Twapenda, kwa sababu [Mungu] alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Yeye ndiye Chanzo na kielelezo bora kabisa cha upendo. Upendo huu wa kanuni, a·gaʹpe, umetajwa katika Biblia zaidi ya mara 100. Ni sifa ambayo hutambulisha Wakristo wa kweli. (Yohana 13:35) Upendo huo wapaswa uonyeshwe kwa Mungu na Yesu Kristo, na wanadamu pia wapaswa kuonyeshana upendo huo—hata kuuonyesha kwa wanadamu ambao huenda tusipendezwe nao sana. (Mathayo 5:44, 45; 1 Yohana 5:3) Ni lazima upendo huo uwe mioyoni mwetu na udhihirike maishani mwetu kabla ya kuweza kuufundisha watoto wetu kwa matokeo. Muungwana ni kitendo. Katika familia, watoto wanahitaji kuona na kuonyeshwa upendo na sifa nyinginezo zinazohusiana na upendo, kama vile shauku. Bila mambo hayo, ukuzi wa mtoto kimwili, kiakili, na kihisia-moyo unazuiwa. Watoto wanahitaji kuona namna ambavyo Wakristo wenzetu, ambao si wa familia yetu, huonyeshwa upendo na shauku ifaavyo.—Waroma 12:10; 1 Petro 3:8.
14. (a) Watoto waweza kufundishwaje kufanya kazi nzuri inayoridhisha? (b) Hilo laweza kufanywaje katika familia yako?
14 Kujifunza jinsi ya kufanya kazi: Kazi ni sehemu muhimu ya maisha. Mtu anahitaji kujifunza kufanya kazi vizuri ili apate kujistahi. (Mhubiri 2:24; 2 Wathesalonike 3:10) Mtoto akipewa kazi ambazo hajaonyeshwa vizuri jinsi ya kuzifanya, kisha akemewe kwa kutozifanya vizuri, haielekei atajifunza kufanya kazi nzuri. Lakini watoto wanapojifunza hasa kwa kufanya kazi pamoja na wazazi wao na kusifiwa ifaavyo, yaelekea zaidi watajifunza kufanya kazi inayoridhisha. Kielelezo cha wazazi kikiambatanishwa na maelezo, watoto wanaweza kujifunza jinsi ya kufanya kazi vizuri na pia jinsi ya kutatua matatizo, jinsi ya kuendelea kufanya kazi hadi inapoisha, na jinsi ya kusababu na kufanya maamuzi. Katika hali hiyo wanaweza kusaidiwa kufahamu kwamba Yehova pia hufanya kazi, kwamba yeye hufanya kazi nzuri, na kwamba Yesu humwiga Baba yake. (Mwanzo 1:31; Mithali 8:27-31; Yohana 5:17) Ikiwa familia inafanya kazi ya ukulima au biashara, baadhi ya washiriki wa familia hiyo wanaweza kufanya kazi pamoja. Au labda mama anaweza kumfundisha mwana wake au binti yake kupika na kusafisha vyombo baada ya mlo. Baba anayefanya kazi ya kuajiriwa mbali na nyumbani anaweza kupanga kuwa na kazi za kufanya nyumbani akiwa pamoja na watoto. Ni jambo lenye kunufaisha kama nini wazazi wanapokumbuka kwamba wanawaandaa watoto wao kwa muda wa maisha yao yote bali si wamalize tu kufanya kazi fulani ya wakati huo!
15. Masomo katika imani yanaweza kufundishwa katika njia zipi? Toa kielezi.
15 Kudumisha imani wakati wa janga: Imani pia ni sehemu muhimu ya maisha yetu. Imani inapozungumziwa katika funzo la familia, watoto wanaweza kujifunza kuifafanua. Wanaweza pia kufahamu uthibitisho unaofanya imani ianze kukua mioyoni mwao. Lakini wanapoona wazazi wao wakionyesha imani thabiti wanapopatwa na majaribu, jambo hilo laweza kuathiri maisha yao yote. Mwanafunzi mmoja wa Biblia wa Panama alitishwa na mumewe kufukuzwa nyumbani kwao asipoacha kumtumikia Yehova. Hata hivyo, yeye pamoja na watoto wake wanne, walitembea kwa ukawaida umbali wa kilometa 16, kisha wakasafiri kwa basi kilometa nyingine 30 ili kufika kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa karibu zaidi. Kwa kutiwa moyo na kielelezo chake, washiriki wapatao 20 wa familia yao walikubali njia ya ile kweli.
Kuweka Kielelezo Katika Usomaji wa Biblia wa Kila Siku
16. Kwa nini usomaji wa Biblia wa kila siku unapendekezwa?
16 Mojawapo ya desturi zenye thamani zaidi ambazo familia yaweza kuanzisha—desturi itakayowanufaisha wazazi na kuwa kielelezo kwa watoto—ni usomaji wa Biblia wa kawaida. Ikiwezekana, someni Biblia kila siku. Kilicho muhimu zaidi si ukubwa wa sehemu inayosomwa bali ni ukawaida na namna usomaji huo unavyofanywa. Mbali na usomaji wa Biblia, watoto wanaweza pia kusikiliza kaseti za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, ikiwa zinapatikana katika lugha yenu. Kusoma Neno la Mungu kila siku hutusaidia kutanguliza mawazo ya Mungu. Na ikiwa usomaji huo unafanywa na familia, wala si mtu mmoja-mmoja, jambo hilo laweza kusaidia familia nzima itembee katika njia za Yehova. Familia zilitiwa moyo ziwe na desturi ya kufanya hivyo katika drama Familia—Fanyeni Usomaji wa Biblia Kila Siku Uwe Njia Yenu ya Maisha! kwenye Mikusanyiko ya hivi majuzi ya “Njia ya Mungu ya Maisha.”—Zaburi 1:1-3.
17. Usomaji wa Biblia wa familia na kukariri maandiko muhimu husaidiaje kutumia shauri lililo kwenye Waefeso 6:4?
17 Usomaji wa Biblia wa familia wapatana na yale mtume Paulo aliyopuliziwa kuandika katika barua yake kwa Wakristo wa Efeso, yaani: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Hilo lamaanisha nini? “Rekebisho la akilini” kihalisi humaanisha “kutia akili katika”; kwa hiyo, baba Wakristo wanahimizwa kutia akili ya Yehova Mungu katika watoto wao—kuwasaidia watoto wapate kujua mawazo ya Mungu. Kuwatia moyo watoto wakariri maandiko muhimu, kwaweza kusaidia kutimiza jambo hilo. Lengo ni kufanya mawazo ya Yehova yaongoze kufikiri kwa watoto ili hatua kwa hatua tamaa zao na mwenendo wao upate kudhihirisha viwango vya Mungu, iwe wazazi wako pamoja na watoto hao au la. Kufikiri kwa aina hiyo hutokana na Biblia.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.
18. Wakati wa kuisoma Biblia ni nini ambacho huenda kikahitajiwa ili (a) kuielewa vizuri? (b) kunufaishwa na shauri lake? (c) kuitikia yale ifunuayo kuhusu kusudi la Yehova? (d) kunufaishwa na yale isemayo kuhusu mitazamo na matendo ya watu?
18 Bila shaka, ikiwa Biblia itaathiri maisha yetu, twahitaji kuelewa yale isemayo. Kwa wengi, hilo huenda likahitaji wasome sehemu mbalimbali mara kadhaa. Ili kuelewa vizuri semi fulani, huenda tukahitaji kuangalia maneno katika kamusi au katika Insight on the Scriptures. Ikiwa andiko linatoa shauri au amri, chukua wakati wa kuzungumzia hali za wakati wetu zinazofanya hilo lifae. Kisha unaweza kuuliza, ‘Twaweza kunufaikaje kwa kutumia shauri hili?’ (Isaya 48:17, 18) Ikiwa andiko hilo lasimulia sehemu fulani ya kusudi la Yehova, uliza, ‘Andiko hili laathirije maisha yetu?’ Labda unasoma simulizi linalotaja mitazamo na matendo ya watu. Ni mikazo gani ya maisha waliyokuwa wakivumilia? Walishughulikiaje mikazo hiyo? Twaweza kunufaishwaje na kielelezo chao? Ruhusu wakati sikuzote wa kuzungumzia maana ya simulizi hilo katika maisha yetu leo.—Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:11.
19. Kwa kuwa waigaji wa Mungu, tutakuwa tukiwaandalia watoto wetu nini?
19 Hiyo ni njia nzuri kama nini ya kukazia mawazo ya Mungu katika akili na mioyo yetu! Hivyo tutasaidiwa kwelikweli kuwa ‘waigaji wa Mungu, tukiwa watoto wapendwa.’ (Waefeso 5:1) Nasi tutatoa kielelezo ambacho kwa kweli chastahili kuigwa na watoto wetu.
Je, Wakumbuka?
◻ Wazazi waweza kunufaishwaje na kielelezo cha Yehova?
◻ Kwa nini ni lazima kufundisha watoto kwa maneno kuambatanishwe na kielelezo kizuri cha wazazi?
◻ Ni baadhi ya masomo gani yawezayo kufundishwa vizuri zaidi kwa kielelezo cha wazazi?
◻ Twaweza kunufaikaje kikamili kutokana na usomaji wa Biblia?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wengi hufurahia kusoma Biblia kila siku wakiwa familia