Unapenda Neno la Mungu Kadiri Gani?
“Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.”—ZABURI 119:97.
1. Watu wenye kumcha Mungu huonyesha kwa njia gani moja kwamba wanapenda Neno la Mungu?
MAMIA ya milioni ya wanaume na wanawake wana Biblia. Lakini kuna tofauti kati ya kuwa na Biblia na kupenda Neno la Mungu. Je, kweli mtu anaweza kudai kwamba anapenda Neno la Mungu ikiwa yeye hulisoma mara chache tu? Bila shaka la! Tofauti na hivyo, wengine ambao zamani hawakuiheshimu Biblia sasa huisoma kila siku. Wao wamejifunza kupenda Neno la Mungu, na kama mtunga-zaburi, sasa wao hulitafakari Neno la Mungu “mchana kutwa.”—Zaburi 119:97.
2. Imani ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova ilitegemezwaje katika hali ngumu?
2 Nasho Dori alijifunza kupenda Neno la Mungu. Akiwa pamoja na waamini wenzake, alivumilia kwa miongo mingi akitumikia Yehova katika nchi yao ya Albania. Kwa kipindi kirefu cha muda huo, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku, na Wakristo hao waaminifu walikuwa wakipokea fasihi chache za Biblia. Lakini imani ya Ndugu Dori ilidumu ikiwa imara. Kwa njia gani? “Lengo langu,” akasema, lilikuwa “kusoma Biblia kwa angalau muda wa saa moja kila siku, na nilifanya hivyo kwa miaka ipatayo 60 kabla ya macho yangu kudhoofika.” Hadi hivi karibuni, Biblia nzima haikuwako katika Kialbania, lakini Ndugu Dori alijifunza Kigiriki akiwa mtoto mdogo, kwa hiyo alikuwa akisoma Biblia katika Kigiriki. Kusoma Biblia kwa ukawaida kulimtegemeza Ndugu Dori katika majaribu mengi, na kunaweza kututegemeza sisi vilevile.
“Fanyizeni Hamu Sana” ya Neno la Mungu
3. Wakristo wanapaswa kukuza mtazamo gani kuhusu Neno la Mungu?
3 “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni,” akaandika mtume Petro, “fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno.” (1 Petro 2:2) Kama vile mtoto hutamani sana maziwa ya mamake, Wakristo ambao wanaona uhitaji wao wa kiroho wanapaswa kufurahia sana kusoma Neno la Mungu. Je, ndivyo unavyohisi? Kama sivyo, usikate tumaini. Wewe pia unaweza kufanyiza hamu sana ya Neno la Mungu.
4. Ni nini kinachohusika ili uwe na desturi ya kusoma Biblia kila siku?
4 Ili ufanye hivyo, kwanza jitie nidhamu ili uwe na desturi ya kusoma Biblia kwa ukawaida, kila siku ikiwezekana. (Matendo 17:11) Huenda usiweze kutumia muda wa saa moja kila siku kusoma Biblia kama Nasho Dori, lakini yaelekea sana unaweza kutenga wakati fulani kila siku ili usome Neno la Mungu. Wakristo wengi huamka dakika chache mapema kidogo ili watafakari fungu fulani la Biblia. Je, kweli kuna njia nzuri kuliko hiyo ya kuanza siku? Wengine hupendelea kumaliza siku kwa kusoma Biblia kabla tu ya kulala. Wengine nao husoma Biblia wakati mwingine unaowafaa. Jambo muhimu ni kusoma Biblia kwa ukawaida. Kisha, tafakari kwa muda mfupi yale ambayo umesoma. Ebu tuone vielelezo vya watu ambao walinufaika kutokana na kusoma Neno la Mungu na kulitafakari.
Mtunga-Zaburi Aliyependa Sheria ya Mungu
5, 6. Ijapokuwa huenda tusijue jina la mwandikaji wa Zaburi ya 119, twaweza kujifunza nini juu yake kwa kusoma na kutafakari mambo aliyoyaandika?
5 Kwa hakika mwandikaji wa Zaburi ya 119 alithamini sana Neno la Mungu. Ni nani aliyeandika zaburi hiyo? Mwandikaji huyo hatajwi katika Biblia. Lakini, tunajifunza mambo fulani juu yake kutokana na muktadha, na twajua kwamba alikuwa na matatizo maishani. Baadhi ya watu aliowajua ambao walipaswa kuwa waabudu wa Yehova hawakupenda kanuni za Biblia kama yeye. Lakini, huyo mtunga-zaburi hakuruhusu mtazamo wao umzuie asifanye yaliyo sawa. (Zaburi 119:23) Ikiwa unaishi au kufanya kazi na mtu ambaye haheshimu kanuni za Biblia, unaweza kuona jinsi hali yako inavyofanana na hali ya mtunga-zaburi.
6 Japo mtunga-zaburi alikuwa mcha Mungu, hakujiona kamwe kuwa mwadilifu. Alikiri wazi kutokamilika kwake. (Zaburi 119:5, 6, 67) Lakini, hakuruhusu dhambi imtawale. “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” akauliza. Akajibu: “Kwa kutii, akilifuata neno lako.” (Zaburi 119:9) Kisha, akikazia jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu za kutokeza mema, mtunga-zaburi aliongezea: “Moyoni mwangu nimeliweka neno lako, nisije nikakutenda dhambi.” (Zaburi 119:11) Nguvu iwezayo kutusaidia kuepuka kutenda dhambi dhidi ya Mungu ina uwezo kwelikweli!
7. Kwa nini vijana wanapaswa hasa kuona uhitaji wa kusoma Biblia kila siku?
7 Inafaa vijana Wakristo wazingatie maneno ya mtunga-zaburi. Leo vijana Wakristo wanashambuliwa. Ibilisi angependa sana kufisidi kizazi hiki kichanga cha waabudu wa Yehova. Shetani analenga kuwashawishi vijana Wakristo washindwe na tamaa za kimwili na kuvunja sheria za Mungu. Mara nyingi sinema na programu za televisheni huonyesha fikira za Ibilisi. Watu wanaohusika katika programu hizo huonekana kuwa wenye kuvutia na wenye kupendeka; mahusiano yasiyo ya kiadili kati yao hayaonwi kuwa mabaya. Twapewa ujumbe gani? ‘Si vibaya kwa watu ambao hawajafunga ndoa kufanya ngono maadamu kwa kweli wanapendana.’ Kwa kusikitisha, kila mwaka vijana kadhaa Wakristo huona mambo kwa njia hiyo. Imani za wengine huvunjika. Kwa hiyo, mkazo upo! Lakini, je, mkazo huo ni mkali sana hivi kwamba nyinyi vijana hamwezi kuushinda? La hasha! Yehova ameandaa njia ambayo vijana Wakristo wanaweza kushinda tamaa zisizofaa. Wanaweza kukinza silaha yoyote ambayo Ibilisi anaweza kubuni ‘kwa kutii, na kulifuata Neno la Mungu, na kuliweka Neno la Mungu moyoni mwao.’ Je, wewe binafsi hutumia muda gani kusoma Biblia kwa ukawaida na kuitafakari?
8. Vielelezo ambavyo vimetajwa katika fungu hili vinaweza kukusaidiaje uzidi kuthamini Sheria ya Kimusa?
8 Mwandikaji wa Zaburi ya 119 alikazia: “Sheria yako naipenda mno ajabu.” (Zaburi 119:97) Alimaanisha sheria gani? Alimaanisha neno la Yehova lililofunuliwa, kutia ndani Sheria ya Kimusa. Kijuujuu wengine wanaweza kupuuza hiyo kanuni ya Sheria kuwa ya kikale na kujiuliza jinsi mtu awezavyo kuipenda. Lakini, tunapotafakari sehemu mbalimbali za Sheria ya Kimusa, kama alivyofanya mtunga-zaburi, tunaweza kuona hekima iliyotokezwa na Sheria hiyo. Mbali na mambo mengi ya kiunabii ya Sheria, kuna maagizo yahusuyo usafi na ulaji, ambayo yaliendeleza usafi na afya njema. (Mambo ya Walawi 7:23, 24, 26; 11:2-8) Sheria iliwatia moyo Waisraeli wafuatie haki katika biashara na kuwahimiza wawaonyeshe hisia-mwenzi waabudu wenzao waliokuwa na uhitaji. (Kutoka 22:26, 27; 23:6; Mambo ya Walawi 19:35, 36; Kumbukumbu la Torati 24:17-21) Maamuzi ya hukumu yalipasa kufanywa bila upendeleo. (Kumbukumbu la Torati 16:19; 19:15) Kwa kadiri mwandikaji wa Zaburi 119 alivyozidi kupata ujuzi maishani, inaelekea ndivyo alivyoona jinsi wale waliotumia Sheria ya Mungu walivyofaulu, na ndivyo alivyozidi kupenda Sheria hiyo. Leo vilevile, kadiri Wakristo wapatavyo mafanikio wanapotumia kanuni za Biblia, ndivyo wao huzidi kupenda Neno la Mungu na kulithamini.
Mwana-Mfalme Aliyekuwa na Ujasiri wa Kuwa Tofauti
9. Mfalme Hezekia alikuza mtazamo gani kuhusu Neno la Mungu?
9 Yaliyomo katika Zaburi ya 119 yanapatana vizuri na mambo tunayojua kuhusu Hezekia alipokuwa angali mwana-mfalme kijana. Wasomi wengine wa Biblia hudokeza kwamba Hezekia ndiye aliyeandika zaburi hii. Ingawa jambo hilo si hakika, twajua kwamba Hezekia aliheshimu sana Neno la Mungu. Kupitia mwenendo wake maishani, alionyesha kwamba alikubaliana kabisa na maneno ya Zaburi 119:97. Biblia yasema hivi juu ya Hezekia: “Alishikamana na BWANA, hakuacha kumfuata, bali alizishika amri zake BWANA alizomwamuru Musa.”—2 Wafalme 18:6.
10. Kielelezo cha Hezekia kinatiaje moyo Wakristo ambao hawakulelewa na wazazi wenye kumcha Mungu?
10 Ripoti zaonyesha kwamba Hezekia hakulelewa katika nyumba inayomcha Mungu. Babake, Mfalme Ahazi, alikuwa mwabudu-sanamu asiye na imani ambaye alichoma motoni angalau mmojawapo wa wana wake—ndugu halisi wa Hezekia—akiwa hai awe dhabihu kwa mungu asiye wa kweli! (2 Wafalme 16:3) Japo mfano huo mbaya, Hezekia aliweza ‘kusafisha njia yake’ kutokana na uvutano wa kipagani kwa kulifahamu Neno la Mungu.—2 Mambo ya Nyakati 29:2.
11. Mbele ya macho ya Hezekia, mambo yalikuwaje kwa babake asiye mwaminifu?
11 Hezekia alipokuwa akikua, alijionea jinsi babake mwenye kuabudu sanamu alivyoshughulikia mambo ya Taifa. Yuda lilikuwa limezingirwa na maadui. Resini mfalme wa Siria alikuwa amejiunga na Mfalme Peka wa Israeli kuzingira Yerusalemu. (2 Wafalme 16:5, 6) Waedomu na Wafilisti pia walikuwa wameshambulia Yuda kwa mafanikio na hata wakateka baadhi ya majiji ya Yudea. (2 Mambo ya Nyakati 28:16-19) Ahazi alishughulikiaje matatizo hayo? Badala ya kumwomba Yehova amsaidie dhidi ya Siria, Ahazi alimwendea mfalme wa Ashuru, akimhonga kwa dhahabu na fedha, kutia ndani zile alizotoa kwenye hazina ya hekalu. Lakini jambo hilo halikuletea Yuda amani ya kudumu.—2 Wafalme 16:6, 8.
12. Hezekia angeweza kuepuka kuyarudia makosa ya babake kwa kufanya nini?
12 Hatimaye, Ahazi akafa na Hezekia akawa mfalme akiwa na umri wa miaka 25. (2 Mambo ya Nyakati 29:1) Japo alikuwa angali kijana kwa kadiri, hiyo haikumzuia asiwe mfalme mwenye mafanikio. Badala ya kuiga mwenendo wa babake asiye mwaminifu, yeye alishikamana na Sheria ya Yehova. Hiyo ilitia ndani amri ya kipekee kwa wafalme: “[Mfalme] aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, kufuata hicho kilicho mbele ya makuhani Walawi; na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii.” (Kumbukumbu la Torati 17:18, 19) Kwa kusoma Neno la Mungu kila siku, Hezekia angejifunza kumcha Yehova na kuepuka kuyarudia makosa ya babake ambaye hakumcha Mungu.
13. Mkristo anawezaje kuwa na hakika kwamba kwa njia ya kiroho, kila alitendalo litafanikiwa?
13 Si wafalme wa Israeli tu waliotiwa moyo kufikiria Neno la Mungu daima, bali pia Waisraeli wote wenye kumcha Mungu walitakiwa wafanye hivyo. Zaburi ya kwanza yafafanua mtu mwenye furaha kwelikweli kuwa yule ambaye “sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Mtunga-zaburi asema hivi juu ya mtu kama huyo: “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Kwa kutofautisha, Biblia yasema hivi kumhusu mtu ambaye hana imani katika Yehova Mungu: “Yeye ni mtu wa kusitasita kuamua, asiye imara katika njia zake zote.” (Yakobo 1:8) Sisi sote twataka kuwa wenye furaha na wenye mafanikio. Kusoma Biblia kwa ukawaida na kwa njia ya maana kwaweza kuchangia furaha yetu.
Neno la Mungu Lilimtegemeza Yesu
14. Yesu alionyeshaje kwamba anapenda Neno la Mungu?
14 Katika pindi moja, wazazi wa Yesu walimpata akiwa ameketi kati ya walimu katika hekalu huko Yerusalemu. Wataalamu hao wa Sheria ya Mungu “walikuwa katika mshangao wa daima [kama nini] juu ya uelewevu wake na majibu yake”! (Luka 2:46, 47) Wakati huo Yesu alikuwa na umri wa miaka 12. Ndiyo, hata alipokuwa mchanga, kwa wazi Yesu alipenda Neno la Mungu. Baadaye, Yesu alitumia Maandiko kumkemea Ibilisi, akisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:3-10) Punde tu baadaye, Yesu aliwahubiria wakazi wa nyumbani kwao Nazareti, akitumia Maandiko.—Luka 4:16-21.
15. Yesu aliwekaje kielelezo alipokuwa akiwahubiria wengine?
15 Yesu alinukuu Neno la Mungu mara nyingi ili kutegemeza mafundisho yake. Wasikilizaji wake ‘walishangaa juu ya njia yake ya kufundisha.’ (Mathayo 7:28) Na si ajabu—mafundisho ya Yesu yalitoka kwa Yehova Mungu mwenyewe! Yesu alisema: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma. Yeye ambaye husema kwa ubuni wake mwenyewe anatafuta sana utukufu wake mwenyewe; bali yeye atafutaye utukufu wake aliyemtuma, huyu ni wa kweli, na hakuna ukosefu wa uadilifu katika yeye.”—Yohana 7:16, 18.
16. Yesu alionyesha upendo wake kwa Neno la Mungu kufikia hatua gani?
16 Tofauti na mwandikaji wa Zaburi 119, ‘hakukuwa na ukosefu wa uadilifu’ katika Yesu. Alikuwa Mwana wa Mungu asiye na dhambi ambaye “alijinyenyekeza mwenyewe akawa mtiifu hadi kifo.” (Wafilipi 2:8; Waebrania 7:26) Lakini, japo alikuwa mkamilifu, Yesu alijifunza Sheria ya Mungu na kuitii. Hilo lilikuwa jambo kuu lililomwezesha kudumisha uaminifu wake wa maadili. Petro alipotumia upanga kujaribu kuzuia Bwana-Mkubwa wake asikamatwe, Yesu alimkemea mtume huyo na kuuliza: “Wafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika? Katika kisa hicho, Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke kwa njia hii?” (Mathayo 26:53, 54) Naam, utimizo wa Maandiko ulikuwa muhimu zaidi kwa Yesu kuliko kuepuka kifo kikatili na chenye kufedhehesha sana. Huo ni wonyesho wenye kutokeza kama nini wa kupenda Neno la Mungu!
Waigaji Wengine wa Kristo
17. Neno la Mungu lilikuwa muhimu kadiri gani kwa mtume Paulo?
17 Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Kama Bwana-Mkubwa wake, Paulo alikuza upendo kwa Maandiko. Alikiri hivi: “Ndani kabisa katika moyo wangu naifurahia sheria ya Mungu.” (Waroma 7:22, Biblia Habari Njema) Paulo alinukuu Neno la Mungu mara nyingi. (Matendo 13:32-41; 17:2, 3; 28:23) Paulo alipompa Timotheo, mhudumu mwenzake mpendwa, maagizo ya mwisho, alikazia fungu muhimu ambalo Neno la Mungu lapaswa kutimiza katika maisha ya kila siku ya kila “mtu wa Mungu.”—2 Timotheo 3:15-17.
18. Taja kielelezo cha mtu ambaye alistahi Neno la Mungu katika nyakati hizi.
18 Watumishi wengi waaminifu wa Yehova katika nyakati hizi vilevile wameiga jinsi Yesu alivyopenda Neno la Mungu. Mapema katika karne hii, kijana mmoja alipokea Biblia kutoka kwa rafikiye mmoja. Kijana huyo akaeleza matokeo ya zawadi hiyo aliyoithamini: “Nikaazimia maishani kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku.” Kijana huyo ni Frederick Franz, na upendo wake kwa Biblia ulifanya afurahie maisha marefu na yenye mafanikio katika utumishi wa Yehova. Yeye anakumbukwa kwa upendo kuwa mwenye uwezo wa kunukuu sura nzima-nzima za Biblia kutoka akilini.
19. Wengine huweka ratiba gani ya kusoma Biblia kila juma kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?
19 Mashahidi wa Yehova hukazia sana kusoma Biblia kwa ukawaida. Kila juma, wanapotayarisha mojawapo ya mikutano yao ya Kikristo, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, wao husoma sura kadhaa za Biblia. Mambo makuu ya sehemu wanayosoma katika usomaji wa Biblia huzungumziwa kwenye mkutano huo. Mashahidi wengine hupendelea kugawanya usomaji wa Biblia wa juma katika sehemu saba ndogondogo na kusoma sehemu moja kila siku. Wasomapo, wao hutafakari habari hiyo. Inapowezekana, wao hufanya utafiti wa ziada wakitumia vichapo vinavyotegemea Biblia.
20. Ni nini kinachohitajika ili kupata wakati wa kusoma Biblia kwa ukawaida?
20 Huenda ukahitaji ‘kununua wakati’ kutoka kwenye utendaji mwingine ili usome Biblia kwa ukawaida. (Waefeso 5:16) Na utapata manufaa nyingi kushinda dhabihu zozote utakazofanya. Kadiri ukuzavyo tabia ya kusoma Biblia kila siku, ndivyo utakavyozidi kupenda Neno la Mungu. Muda usio mrefu, utasukumwa kusema kama mtunga-zaburi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Mtazamo kama huo unanufaisha sana sasa na katika wakati ujao, kama makala ifuatayo itakavyoonyesha.
Je, Wakumbuka?
◻ Mwandikaji wa Zaburi 119 alionyeshaje kwamba anapenda sana Neno la Mungu?
◻ Twaweza kupata masomo gani kutokana na vielelezo vya Yesu na Paulo?
◻ Sisi binafsi twaweza kukuzaje upendo wetu kwa Neno la Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wafalme waaminifu walipaswa kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida. Je, wewe hufanya hivyo?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Hata alipokuwa mvulana, Yesu alipenda Neno la Mungu