Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
Kutia Maji Mbegu za Kweli Nchini Chile
KATIKA jangwa lililopo sehemu ya kaskazini ya Chile, huenda mvua isinyeshe kwa miaka kadhaa. Lakini hatimaye, mvua inaponyesha, ardhi hiyo kavu yenye mawe-mawe, hugeuka kuwa kama zulia la maua yenye rangi nyingi. Maua hayo maridadi huwavutia watalii kutoka sehemu zote za nchi.
Hata hivyo, jambo lenye kupendeza hata zaidi linatukia miongoni mwa watu wa Chile. Maji ya kweli ya Biblia yanatiririka kuelekea sehemu zote za nchi, na watu wengi wanyofu “wanasitawi” na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Njia moja ya kueneza maji hayo ya kweli ni kupitia simu. Matokeo mazuri yanayopatikana kwa kutumia njia hii ya kutoa ushahidi huthibitishwa na mambo yaliyoonwa yafuatayo.
• Mweneza-evanjeli wa wakati wote aitwaye Karina aliombwa aonyeshe jinsi ya kutoa ushahidi kupitia simu katika kusanyiko la mzunguko. Hata hivyo, Karina hakuwahi kamwe kutoa ushahidi kupitia njia hiyo. Ili kumtia Karina moyo kushiriki katika programu ya kusanyiko mzee mmoja pamoja na mke wake walipitia mambo kadhaa kuhusu jinsi ya kutoa ushahidi kupitia simu. Pia walimtia moyo atoe sala kwa Yehova ili apate uongozi katika jambo hilo. Ndivyo alivyofanya, na hatimaye akaamua kujaribu kutoa ushahidi kupitia simu.
Karina alichagua namba ya simu ya kijiji kilichokuwa karibu. Mpokeaji simu alichukua simu na Karina akaeleza kusudi la kumpigia. Mpokeaji simu alikubali ujumbe, na mpango ukafanywa wa kuendeleza mazungumzo hayo baada ya siku tatu. Karina alifanya ziara ya kurudia kupitia simu, akaanzisha funzo la Biblia akitumia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Tangu wakati ule wamekuwa na funzo lenye kupendeza na la kusisimua, naye Karina amemtumia mwanamke huyo vichapo ili kujibu maswali yake.
• Bernarda alimtolea ushahidi mwanamume mmoja aliyepiga namba yake ya simu kimakosa. Badala ya kuudhika Bernarda alijitambulisha kama mmoja wa Mashahidi wa Yehova, akajitolea kumsaidia. Mazungumzo yalianza, na mwanamume huyo alisikiliza Bernarda alipoeleza jinsi Ufalme wa Mungu utakavyoondoa udhalimu hivi karibuni. Mwanamume huyo alimpa Bernarda namba yake ya simu, naye alifanya ziara za kurudia kupitia simu. Katika mojawapo ya mazungumzo yao, Bernarda alimsomea sehemu katika kitabu cha Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Mwanamume huyo aliuliza jinsi angeweza kupata nakala ya kitabu hicho, naye Bernarda alimtumia nakala moja pamoja na Biblia. Mipango ilifanywa ili ndugu mmoja wa mahali hapo amtembelee, naye anaendelea “kutilia maji mmea” huo unaositawi.
Naam, katika udongo mkavu wa ulimwengu huu, mbegu zilizofichwa zangojea kuchipuka zitakapofikiwa na maji ya kweli yenye kuhuisha. Maelfu ya watu wenye kiu waendelea “kuchipuka” na “kusitawi” na kuwa watumishi waaminifu wa Yehova Mungu.—Isaya 44:3, 4.