Jinsi Tuwezavyo Kusitawisha Wema wa Adili
KAMUSI za kisasa hufasiri “wema wa adili” kuwa “ubora wa kiadili; wema.” Kuonyesha wema wa adili ni “kutenda na kufikiri ifaavyo; tabia njema.” Mtunga-kamusi Marvin R. Vincent asema kwamba maana halisi ya awali ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa “wema wa adili” huonyesha “ubora wa aina yoyote.” Kwa hiyo si ajabu kwamba wakati fulani sifa kama vile busara, ujasiri, nidhamu, kutopendelea, huruma, uvumilivu, unyofu, unyenyekevu, na uaminifu-mshikamanifu zimetajwa kuwa wema wa adili. Wema wa adili umefasiriwa pia kuwa “kujipatanisha na kiwango cha haki.”
Twapaswa kujipatanisha na viwango vya nani vya ubora, wema, na haki? “Kulingana na wafuasi mashuhuri wa falsafa ya maadili,” likasema gazeti Newsweek, “mashaka yaliyoanzishwa na Enlightenment (Harakati ya Wanafalsafa ya Karne ya 18) yamefanya maoni yote kuhusu mema na mabaya kuwa mapendezi ya kibinafsi, mapendezi ya kihisia-moyo au uchaguzi wa kitamaduni.” Lakini, je, inaridhisha kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya kwa kutegemea tu mapendezi ya mtu? La. Ili tusitawishe wema wa adili, twahitaji kiwango chenye kutegemeka cha mema na mabaya—kiwango ambacho chaweza kutumiwa kuamua iwapo tendo, mtazamo, au sifa fulani ni nzuri au ni mbaya.
Chanzo cha Kweli na cha Pekee cha Viwango vya Adili
Kuna Chanzo kimoja tu cha kweli cha viwango vya adili—Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu. Punde tu baada ya kuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, Yehova Mungu alitoa amri hii kwa mwanadamu huyo: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Yehova Mungu aliupa mti huo jina hilo la pekee ili kuonyesha kwamba yeye pekee ndiye aliyekuwa na haki ya kuamua mema na mabaya kwa ajili ya viumbe wake. Kwa hiyo, viwango vya Mungu vya mema na mabaya vikawa msingi wa kuhukumu au kupima matendo, mtazamo, na tabia za mtu. Bila viwango hivyo hatungeweza kupambanua mema na mabaya kwa usahihi.
Amri iliyohusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya iliwapa Adamu na Hawa uchaguzi—kutii au kutotii. Ili waonyeshe wema wa adili walihitaji kutii amri hiyo. Baada ya muda, Yehova alifunua zaidi mambo yanayompendeza na yale yasiyompendeza, na kuhakikisha yameandikwa katika Biblia kwa ajili yetu. Hivyo basi, kusitawisha wema wa adili kwahusisha kujipatanisha na viwango vya uadilifu vya Yehova vilivyo katika Maandiko.
Fahamu Kikamili Viwango vya Mungu
Kwa kuwa Yehova Mungu ameweka viwango vya mema na mabaya na kuvifunua katika Biblia, je, hatupaswi kuvifahamu kikamili? Mtume Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili,mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.
Kwa mfano, fikiria hali ya kutoelewana aliyokabili Kunihito, ambaye ametajwa katika makala iliyotangulia, alipodhihirisha wema wa adili kulingana na utamaduni wake. Baadaye alisaidiwa kuwa na mtazamo uliosawazika kwa kuchunguza kwa makini viwango vya Kimaandiko. Bila shaka, Biblia hututia moyo tuwe na kiasi, na hutushauri tusiwe na uhakika kupita kiasi au kuwa na kimbelembele. (Mithali 11:2; Mika 6:8) Hata hivyo, alipokuwa akionyesha sifa za “cheo cha mwangalizi,” mtume Paulo alisema juu ya “kufikilia” pendeleo hilo. (1 Timotheo 3:1) “Kufikilia” huko hakupasi kufanywa kwa kujisifu au kwa kimbelembele, na pia kwa kujidhalilisha isivyo lazima.
Biblia husema nini kuhusu ubora wa kiadili katika sehemu za biashara? Kutumia njia zenye kutilika shaka au kukwepa kanuni za serikali na sheria zinazohusu kodi ni zoea la kawaida katika ulimwengu wa kibiashara wa leo. Hata hivyo, bila kujali wengine wanafanya nini, kiwango cha Biblia ni kwamba twapaswa “kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Hivyo, tunasitawisha wema wa adili kwa kuwa wanyofu na kutopendelea waajiri, waajiriwa, wateja, na serikali. (Kumbukumbu la Torati 25:13-16; Waroma 13:1; Tito 2:9, 10) Bila shaka unyofu hukuza itibari na nia njema. Mara nyingi kuandika mapatano huzuia kutoelewana na magumu yanayoweza kutokea kwa sababu ya “tukio lisilotazamiwa.”—Mhubiri 9:11 NW; Yakobo 4:13, 14.
Twahitaji pia kusitawisha wema wa adili kwa habari ya mavazi na mapambo yetu. Aina za mavazi hutofautiana kulingana na utamaduni, na huenda kukawa na msongo mwingi wa kufuata mitindo ya karibuni. Lakini kwa nini tufuate kila mtindo unaotokea? Biblia hutushauri ‘tukome kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo.’ (Waroma 12:2) Badala ya kuweka sheria nyingi, mtume Paulo aliandika hivi chini ya upulizio: “Natamani wanawake wajirembe wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mvao ulio ghali sana, bali katika njia inayofaa wanawake wanaodai kumstahi Mungu.” (1 Timotheo 2:9, 10) Kiwango hiki cha msingi chatumika kwa wanaume na wanawake vilevile. Bila shaka, mtu aweza kuchagua mitindo ya aina mbalimbali inayopendeza ikitegemea utamaduni au mapendezi ya kibinafsi.
Biblia pia hutaja mazoea yasiyo ya adili yanayolaumiwa waziwazi na Mungu. Kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10, twasoma onyo hili: “Ama! Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawatarithi ufalme wa Mungu? Msiongozwe vibaya. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.” Andiko hilo lilimsaidia Maria, aliyetajwa hapo awali, kuona kwamba kulingana na kiwango bora cha maadili kilichowekwa na Muumba, hakupaswa kuwa na uhusiano na Juan na lazima aukomeshe ili apate kibali cha Mungu. Ni wazi kwamba, ili kusitawisha wema wa adili, twahitaji kufahamu viwango vya Yehova kikamili.
Jifunze kwa Moyo
Wema wa adili si kuepuka tu lililo baya. Una nguvu za kiadili. Mtu mwenye wema wa adili ni mwema. Profesa mmoja asema kwamba “mtu ahitaji kujifunza wema wa adili kwa moyo na vilevile kwa akili.” Kwa hiyo, kusitawisha wema wa adili kwahusisha mengi zaidi ya kufahamu kikamili Neno la Mungu. Hutaka tutafakari mambo yaliyoandikwa humo ili mioyo yetu ijawe na shukrani kwa Yehova na hivyo tuchochewe kutumia kanuni za Kimaandiko maishani mwetu.
“Sheria yako naipenda mno ajabu,” mtunga-zaburi akatamka. “Ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Naye Mfalme Daudi aliandika hivi: “Nimezikumbuka siku za kale, nimeyatafakari matendo yako [ya Mungu] yote, naziwaza kazi za mikono yako.” (Zaburi 143:5) Sisi pia twahitaji tufanye kutafakari kwa bidii kuwe sehemu muhimu ya funzo letu la Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia.
Ni kweli kwamba, si rahisi kupata wakati wa kujifunza kwa bidii na kutafakari. Lakini ili kufuatia wema wa adili, twahitaji kununua wakati kutoka kwenye utendaji mbalimbali. (Waefeso 5:15, 16) Aaron, mwenye umri wa miaka 24, hununua wakati huo kila siku kwa kuamka dakika 30 kabla ya wakati aliokuwa akiamka hapo awali. Asema hivi: “Kwanza, nilikuwa nikisoma Biblia tu kwa muda huo wote wa nusu saa. Nimetambua umuhimu wa kutafakari hivi majuzi tu. Kwa hiyo sasa ninatumia nusu ya wakati huo kutafakari mambo ambayo nimesoma. Nimethawabishwa kwelikweli kwa kufanya hivyo.” Mtu aweza kutafakari nyakati nyingine. Daudi alimwimbia Yehova hivi kwa sauti tamu: “Nakutafakari Wewe makesha yote ya usiku.” (Zaburi 63:6) Nayo Biblia husema: “Isaka akatoka ili kutafakari kondeni wakati wa jioni.”—Mwanzo 24:63.
Kutafakari ni kwenye thamani sana katika kusitawisha wema wa adili, kwa kuwa kunatufanya tuhisi kama Yehova na kuwa na maoni kama yake. Kwa mfano, Maria alijua kwamba Mungu anakataza uasherati. Lakini ili ‘akirihi lililo ovu na kuambatana na lililo jema,’ alihitaji kutafakari maandiko muhimu ya Biblia. (Waroma 12:9) Alisaidiwa kuona uhitaji wa kufanya marekebisho baada ya kusoma Wakolosai 3:5, andiko linalotuhimiza ‘tufishe viungo vya mwili wetu kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa.’ Ilimbidi Maria ajiulize hivi: ‘Ni tamaa gani ya ngono ninayohitaji kufisha? Niepuke nini ambacho chaweza kuchochea tamaa zisizo safi? Je, nahitaji kufanya mabadiliko fulani kuhusu namna ninavyowatendea watu wa jinsia tofauti?’
Kutafakari kwahusisha kufikiria matokeo ya tendo fulani. Paulo awahimiza Wakristo wajiepushe na uasherati na wajidhibiti ili “yeyote asifikie hatua ya kudhuru na kuziingilia haki za ndugu yake.” (1 Wathesalonike 4:3-7) Maswali mazuri ya kufikiria ni kama haya: ‘Ni madhara gani yatakayonipata mimi mwenyewe, familia yetu, au wengine kwa kufanya tendo hilo? Nitaathiriwaje kiroho, kihisia-moyo, na kimwili? Wengine ambao walivunja sheria ya Mungu hapo zamani walipatwa na nini?’ Kutafakari maswali hayo kulifanya Maria awe thabiti hata zaidi, nasi twaweza kusaidiwa kufanya hivyo pia.
Jifunze Kutokana na Vielelezo
Je, wema wa adili waweza kufundishwa darasani? Swali hilo limewatatanisha watu wenye kufikiri kwa milenia nyingi. Plato, mwanafalsafa Mgiriki, alifikiri inawezekana. Kwa upande mwingine, Aristotle alisababu kwamba mtu husitawisha wema wa adili kwa kujizoeza. Mwandishi-habari mmoja alieleza hivi kwa ufupi kuhusu mjadala huo: “Kwa ufupi mtu hawezi kujifunza maadili ya wema akiwa peke yake. Wala hawezi kujifunza sifa hiyo kwa kusoma vitabu. Tabia njema hutokana na kuishi katika jumuiya . . . ambapo watu hutiwa moyo kuonyesha wema wa adili na huthawabishwa kwa kufanya hivyo.” Lakini ni wapi tuwezapo kupata watu wenye wema wa adili wa kweli? Ingawa tamaduni nyingi zina vielelezo kadhaa vya wema wa adili, angalau katika hadithi na ngano zinazotaja mashujaa wao, Biblia ina vielelezo vingi vya kweli.
Yehova ndiye kielelezo chenye kutokeza zaidi cha wema wa adili. Sikuzote, yeye hutenda kwa njia yenye wema wa adili na hufanya mambo ya haki na mema. Twaweza kusitawisha wema wa adili kwa kuwa “waigaji wa Mungu.” (Waefeso 5:1) Naye Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, ‘alituachia kigezo ili tufuate hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Isitoshe, Biblia ina masimulizi ya watu wengi waaminifu, kama vile, Abrahamu, Sara, Yosefu, Ruthu, Yobu, na Danieli na Waebrania wenzake watatu. Twaona pia vielelezo vya wema wa adili miongoni mwa watumishi wa Yehova wa siku ya kisasa.
Twaweza Kufaulu
Je, kwa kweli twaweza kufaulu kufanya mambo yenye wema wa adili machoni pa Mungu? Kwa kuwa tumerithi kutokamilika, huenda nyakati nyingine tukakabili pambano kali baina ya akili na mwili—kati ya kufanya jambo lenye wema wa adili na kutii mielekeo yetu yenye dhambi. (Waroma 5:12; 7:13-23) Lakini twaweza kushinda pigano hilo kwa msaada wa Mungu. (Waroma 7:24, 25) Yehova ameandaa Neno lake na vichapo vinavyotegemea Biblia. Kwa kujifunza Maandiko kwa bidii na kuyatafakari kwa sala, twaweza kuwa safi moyoni. Moyo huo ulio safi utatokeza mawazo, maneno, na matendo yenye wema wa adili. (Luka 6:45) Kwa kutegemea kielelezo cha Yehova Mungu na Yesu Kristo, twaweza kusitawisha utu wa kimungu. Na bila shaka twaweza kujifunza mengi kutoka kwa watu wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu leo.
Mtume Paulo aliwahimiza wasomaji wake ‘waendelee kufikiria’ mambo yaliyo ya wema wa adili na ya kustahili sifa. Bila shaka kufanya hivyo kutaleta baraka za Mungu. (Wafilipi 4:8, 9) Twaweza kufaulu kusitawisha wema wa adili kwa msaada wa Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Fanya kutafakari kuwe sehemu ya funzo lako la Biblia
[Picha katika ukurasa wa 7]
Sitawisha utu wa kimungu kwa kumwiga Kristo Yesu