Kuishi Katika Hali Zenye Hatari
“Lolote ufanyalo kila siku—kutia ndani kulala—laweza hata kuhatarisha uhai wako.”—gazeti Discover.
MAISHA yamelinganishwa na kutembea katika eneo lililotegwa mabomu ardhini, kwa kuwa unaweza kujeruhiwa au kufa wakati wowote, mara nyingi bila hata onyo. Mambo yaletayo hatari yanatofautiana kutoka nchi moja kwenda nyingine. Yanatia ndani aksidenti za magari, vita vya wenyewe kwa wenyewe, njaa kuu, UKIMWI, kansa, maradhi ya moyo, na mambo mengine mengi. Kwa mfano, katika mwaka wa hivi karibuni, UKIMWI ambao umekuwa kisababishi kikuu cha vifo katika eneo la Afrika lililo kusini ya Sahara, “uliua watu milioni 2.2, mara 10 zaidi ya watu waliouawa katika vita vyote vya wenyewe kwa wenyewe barani Afrika,” lasema gazeti la U.S.News & World Report.
Wakati huohuo, ulimwengu hutumia pesa nyingi sana kurefusha maisha na kupunguza hatari ya kupatwa na magonjwa na ulemavu. Nyingi za dhana zinazoendelezwa, kama vile kula na kunywa ifaavyo na pia kufanya mazoezi ya kimwili, zinaweza kuwa na manufaa fulani. Hata hivyo, kuna chanzo cha habari yenye kuaminika inayogusa kila sehemu muhimu ya maisha ambacho chaweza kukusaidia ufurahie maisha yaliyo salama zaidi. Chanzo hicho ni Biblia. Biblia ina miongozo inayoonyesha jinsi ya kushughulika na mahangaiko mengi yanayoathiri afya na hali njema yetu. Ni kweli kwamba Biblia haishughulikii kila tatizo kwa undani. Hata hivyo, inatoa kanuni bora sana za kutuongoza katika mambo kama ulaji, afya ya kimwili, mtazamo wa kiakili, ngono, matumizi ya vileo, tumbaku, na zile ziitwazo eti dawa za kujiburudisha, na mambo mengine mengi.
Wengi pia wana mahangaiko mengi ya kifedha. Biblia hutusaidia pia katika jambo hilo. Hututia moyo tuwe na maoni yenye hekima kuhusu pesa na matumizi yake na pia hutuonyesha vile tuwezavyo kuwa waajiriwa au waajiri bora. Kwa ufupi, Biblia ni mwongozo mzuri, si wa kupata usalama wa kifedha na afya bora tu, bali pia wa kupata uhai. Je, ungependa kujua jinsi Biblia iwezavyo kutumika leo? Basi, tafadhali endelea kusoma.