Mkaribie Mungu
Mungu Anatuona Kuwa Wenye Thamani
“HUENDA mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia.” Kwa maneno hayo, Biblia inakubali kwamba nyakati nyingine huenda mioyo yetu ikatuchambua kupita kiasi. Kwa kweli, huenda mioyo yetu ikasisitiza kwamba hatustahili kupendwa na kutunzwa na Mungu. Hata hivyo, Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Mungu anatujua vizuri kuliko tunavyojijua. Huenda maoni yake kutuhusu yakawa tofauti kabisa na jinsi ambavyo tunajiona. Hivyo basi, je, sisi ni wenye thamani machoni pa yule mtu muhimu zaidi, yaani, Yehova Mungu? Jibu la swali hilo linapatikana katika mfano wenye kugusa moyo ambao Yesu aliutumia pindi mbili tofauti.
Pindi moja, Yesu alisema kwamba ‘shomoro wawili huuzwa kwa sarafu ya thamani ndogo.’ (Mathayo 10:29, 31) Kulingana na Luka 12:6, 7, Yesu alisema hivi pia: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao husahaulika mbele za Mungu. . . . Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.” Mfano huo rahisi lakini wenye nguvu unatufunza jinsi ambavyo Yehova anamwona kila mmoja wa waabudu wake.
Shomoro au shore walikuwa miongoni mwa ndege wa bei ya chini zaidi waliotumiwa kwa chakula. Bila shaka, Yesu alikuwa amewaona wanawake maskini, pengine hata mama yake mwenyewe, wakinunua ndege hao wadogo sokoni ili kulisha familia zao. Kwa sarafu moja ya asarioni yenye thamani inayopungua senti tano za Marekani, mtu angeweza kununua shomoro wawili. Ndege hao walikuwa na thamani ndogo sana hivi kwamba kwa sarafu mbili, mtu angepewa shomoro watano badala ya wanne, yule wa tano akiongezwa bila malipo ya ziada.
Yesu alisema kwamba hakuna hata shomoro mmoja “husahaulika mbele za Mungu” au hakuna hata mmoja wao anayeanguka “chini bila” Baba kujua. (Mathayo 10:29) Yehova anajua kila mara shomoro anapoanguka chini, iwe ni kwa sababu ameumia au ili kutafuta chakula. Ndege hao ambao huonwa kuwa wasio na thamani, si wadogo sana kwa Yehova kuwaumba au kuwakumbuka. Kwa kweli, anawathamini kwa kuwa hao ni viumbe hai. Je, unaona somo la mfano wa Yesu?
Katika mafundisho yake, mara nyingi Yesu alilinganisha mambo. Alitumia mifano rahisi, kisha akaonyesha jinsi mifano hiyo inavyoweza kutumiwa kuhusu mambo muhimu. Kwa mfano, Yesu alisema hivi: “Kunguru hawapandi mbegu wala hawavuni, nao hawana bohari wala ghala, na bado Mungu huwalisha. Ninyi ni wenye thamani kama nini kuliko ndege?” (Luka 12:24) Sasa somo katika mfano wa Yesu wa shomoro linakuwa wazi: Ikiwa Yehova anawatunza ndege hao wadogo, je, hatawatunza hata zaidi wanadamu wanaompenda na kumwabudu?
Tunapofikiria maneno ya Yesu, hatupaswi kuhisi kwamba hatuna thamani yoyote kustahili kutambuliwa na kutunzwa na Mungu ambaye ni “mkuu kuliko mioyo yetu.” Je, haifariji kujua kwamba Muumba wetu anaweza kuona sifa ambazo huenda sisi wenyewe hatuzioni?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]
Sparrows: © ARCO/D. Usher/age fotostock