Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w08 4/1 kur. 5-8
  • Har-magedoni—Vita Vya Mungu Vya Kukomesha Vita Vyote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Har-magedoni—Vita Vya Mungu Vya Kukomesha Vita Vyote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vita Vilivyopiganwa Karibu na Megido
  • Har–Magedoni Katika Biblia
  • Kwa Nini Har–Magedoni Inahitajiwa?
  • Kuchukua Har–Magedoni kwa Uzito
  • Har-magedoni—Mwanzo Wenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Har–Magedoni—Si Mambo Haya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Har-magedoni Lini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vita vya Har-Magedoni Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
w08 4/1 kur. 5-8

Har-magedoni—Vita Vya Mungu Vya Kukomesha Vita Vyote

“Wanaona kuua kiumbe mwenzao kuwa ukatili mkubwa; hivyo, machoni pao vita ni kitu kisichowazika na chenye kuchukiza, na hata lugha yao haina neno ‘vita.’” —UFAFANUZI KUWAHUSU WATU WA INUIT WANAOISHI GREENLAND ULIOFANYWA NA FRIDTJOF NANSEN, MVUMBUZI KUTOKA NORWAY MNAMO 1888.

NI NANI ambaye hangependa kuishi katika jamii ya watu ambao waliona vita kuwa “kitu kisichowazika na chenye kuchukiza”? Ni nani ambaye hatamani kuishi katika ulimwengu ambamo hata hauna neno vita kwa sababu haujui vita? Huenda ulimwengu kama huo ukaonekana kuwa ndoto tu, hasa ikiwa tunawatumainia wanadamu wautokeze.

Hata hivyo, katika unabii wa Isaya, Mungu mwenyewe anaahidi kutokeza ulimwengu kama huo: “Watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”—Isaya 2:4.

Kwa wazi, leo ulimwengu ulio na askari-jeshi milioni 20 walio vitani na ambamo vita 20 hivi vinaendelea kupiganwa ungehitaji mabadiliko makubwa ili ahadi hiyo itimie. Haishangazi kwamba Mungu mweza-yote, Yehova atahitaji kuingilia kati shughuli za wanadamu. Hatua hiyo ya Yehova kuingilia kati ndiyo itakayofikia upeo katika kile kinachoitwa na Biblia Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.

Ingawa katika nyakati za karibuni neno “Har–Magedoni” limetumiwa kumaanisha maangamizi makubwa ya nyuklia, kamusi moja inaeleza maana ya msingi ya neno hilo hivi: “Mahali pa mapambano makubwa ya mwisho kati ya majeshi ya wema na uovu.” Je, kweli wema utawahi kushinda uovu, ama vita hivyo ni ndoto tu?

Tunaweza kufarijika kujua kwamba Biblia inazungumzia tena na tena kuhusu mwisho wa uovu. Mtunga-zaburi alitabiri hivi: “Watenda-dhambi watamalizwa kabisa kutoka duniani; nao waovu, hawatakuwapo tena.” (Zaburi 104:35) Methali inasema: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”—Methali 2:21, 22.

Pia, Biblia inafunua wazi kwamba waovu hawataachilia mamlaka yao kwa amani; na hiyo ndiyo sababu Mungu atahitaji kuchukua hatua ya kukata maneno kukomesha uovu wote, kutia ndani uovu wa vita. (Zaburi 2:2) Jina ambalo Biblia inayapa mapambano hayo ya pekee, yaani, Har–Magedoni, lina maana kubwa sana.

Vita Vilivyopiganwa Karibu na Megido

Neno “Har–Magedoni” linamaanisha “Mlima wa Megido.” Jiji la kale la Megido, pamoja na Nchi Tambarare ya Yezreeli ni mahali ambapo vita vingi vya kukata maneno vilipiganwa. “Katika historia yote, Megido na Bonde la Yezreeli yamekuwa maeneo ya vita ambavyo vimebadili kabisa ustaarabu,” anaandika mwanahistoria Eric H. Cline katika kitabu chake (The Battles of Armageddon).

Kama Cline anavyosema, mara nyingi vita vilivyopiganwa Megido vilikuwa vya kukata maneno. Majeshi ya Mongolia, ambayo yalishambulia sehemu kubwa ya Asia katika karne ya 13, yalishindwa kwa mara ya kwanza katika bonde hilo. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, majeshi ya Uingereza yakiwa chini ya Jenerali Edmund Allenby, yaliwashinda Waturuki katika eneo lililo karibu na Megido. Mwanahistoria wa masuala ya kijeshi alifafanua ushindi wa Allenby kuwa “mojawapo ya mapambano ya kukata maneno yaliyomalizika upesi zaidi katika historia yote.”

Vita mbalimbali vya kukata maneno vinavyotajwa katika Biblia pia vilipiganwa karibu na Megido. Huko ndiko Mwamuzi Baraka alikoyashinda majeshi ya Sisera Mkanaani. (Waamuzi 4:14-16; 5:19-21) Gideoni akiwa na kikundi chake cha wanaume 300 alishinda jeshi kubwa la Wamidiani karibu na eneo hilo. (Waamuzi 7:19-22) Majeshi ya Wafilisti yaliposhinda jeshi la Israeli, Mfalme Sauli na mwana wake Yonathani walikufa katika Mlima Gilboa ulio karibu na eneo hilo.—1 Samweli 31:1-7.

Kwa kuwa eneo la Megido na bonde linalolizunguka liko mahali pazuri, vita vingi vimepiganwa huko katika miaka 4,000 iliyopita. Mwanahistoria mmoja alisema kwamba vita 34 hivi vilipiganwa katika eneo hilo!

Bila shaka, neno “Har–Magedoni” linapotumiwa kwa njia ya mfano ni kwa sababu ya historia ya Megido na eneo hilo liko mahali panapofaa kwa ajili ya vita. Ingawa neno hilo linatajwa mara moja tu katika Biblia, muktadha wake katika kitabu cha Ufunuo unaonyesha waziwazi kwamba Har–Magedoni itakuwa na matokeo katika maisha ya kila mtu duniani.

Har–Magedoni Katika Biblia

Ingawa vita vingi vilivyopiganwa karibu na Megido vilikuwa vya kukata maneno, havikukomesha uovu. Hakuna yoyote kati ya vita hivyo vilivyokuwa kati ya majeshi ya wema na uovu. Ni jambo linalopatana na akili kwamba vita vya aina hiyo vitaanzishwa na Mungu. Yesu alisema hivi pindi moja: “Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.” (Luka 18:19) Isitoshe, Biblia inataja kihususa kwamba Har–Magedoni ni vita vya Mungu.

Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinasema kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watakusanywa pamoja “kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufunuo 16:14) Kisha simulizi la kinabii linaongeza hivi: “Nayo yakawakusanya pamoja mahali panapoitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.”a (Ufunuo 16:16) Sura zinazofuata za Ufunuo zinasema kwamba ‘wafalme wa dunia na majeshi yao watakusanywa pamoja ili kupigana vita na yule anayeketi juu ya farasi na jeshi lake.’ (Ufunuo 19:19) Mpanda-farasi huyo si mwingine ila Yesu Kristo.—1 Timotheo 6:14, 15; Ufunuo 19:11, 12, 16.

Mistari hiyo inatufanya tukate kauli gani? Har–Magedoni ni vita kati ya Mungu na majeshi ya wanadamu wasiotii. Kwa nini Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo wapigane vita hivyo? Sababu moja ni kwamba Har–Magedoni ‘itawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Kwa kuongezea, italeta ulimwengu wenye amani, ‘dunia mpya ambayo tunangojea kulingana na ahadi ya Mungu ambamo uadilifu utakaa.’—2 Petro 3:13.

Kwa Nini Har–Magedoni Inahitajiwa?

Je, unashangaa kwamba Yehova, “Mungu wa upendo,” anaweza kumwagiza Mwana wake, “Mkuu wa Amani,” apigane katika vita? (2 Wakorintho 13:11; Isaya 9:6) Bila shaka ukielewa kusudi lao mambo yatakuwa wazi. Kitabu cha Zaburi kinamfafanua Yesu kuwa shujaa aliyepanda farasi. Kwa nini anapigana vita? Zaburi inaeleza kwamba Kristo anapanda ili “kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu.” Anapigana vita kwa sababu anapenda uadilifu na kuchukia uovu.—Zaburi 45:4, 7.

Vivyo hivyo, Biblia inaeleza maoni ya Yehova kuhusu ukosefu wa haki unaotukia duniani leo. Nabii Isaya anaandika hivi: “BWANA ameona haya, naye anachukizwa kwamba hakuna haki. Atavaa haki kama vazi la chuma na nguvu ya kuokoa kama kofia ya chuma. Yeye mwenyewe atajivika tamaa kubwa ya kunyoosha mambo na kutoa adhabu na kulipiza kisasi makosa ambayo yamewaletea watu mateso.”—Isaya 59:15, 17, Today’s English Version.

Maadamu watu waovu wanatawala, watu waadilifu hawatakuwa na amani na usalama. (Methali 29:2; Mhubiri 8:9) Kwa kweli, hatuwezi kuutenganisha uovu au ufisadi na watu wanaoufanya. Kwa hiyo, ili amani na haki ya kudumu ipatikane ni lazima waovu waondolewe. Sulemani aliandika hivi: “Mwovu ni fidia ya mwadilifu.”—Methali 21:18.

Kwa kuwa Mungu ndiye Mwamuzi, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hukumu yoyote juu ya waovu itafanywa kwa uadilifu. Abrahamu aliuliza hivi: “Je, Mwamuzi wa dunia yote hatafanya lililo sawa?” Kutokana na jibu alilopata, Abrahamu alijua kwamba sikuzote Yehova anafanya yaliyo sawa! (Mwanzo 18:25) Zaidi ya hayo, Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova hafurahii kuwaharibu waovu; anafanya hivyo ikiwa tu hakuna njia nyingine.—Ezekieli 18:32; 2 Petro 3:9.

Kuchukua Har–Magedoni kwa Uzito

Utamuunga nani mkono wakati wa mapambano hayo ya kukata maneno? Wengi wetu tunadhani kwamba tunaunga mkono majeshi ya wema. Lakini tunaweza kuwa na uhakika jinsi gani? Nabii Sefania anahimiza hivi: “Utafuteni uadilifu, utafuteni upole.” (Sefania 2:3) Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli,” anasema mtume Paulo.—1 Timotheo 2:4.

Kujifunza ukweli kuhusu Yehova na kusudi lake la kuondoa uovu duniani ni hatua ya kwanza ya kupata wokovu. Kutenda kwa uadilifu ni hatua ya pili itakayotuletea kibali na ulinzi wa Mungu.

Tukichukua hatua hizo muhimu, tunaweza kutazamia kwa hamu Har–Magedoni, vita vitakavyokomesha kabisa vita vya wanadamu. Vita hivyo vitakapokwisha, watu ulimwenguni pote wataona vita kuwa kitu kisichowazika na chenye kuchukiza. “Hawatajifunza vita tena.”—Isaya 2:4.

[Maelezo ya Chini]

a Ili kujua kama Har–Magedoni ni mahali halisi, ona makala “Wasomaji Wetu Wanauliza,” kwenye ukurasa wa 31.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Har–Magedoni ni hatua ya Mungu ya kuingilia kati shughuli za wanadamu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Megido

[Picha katika ukurasa wa 6]

Gideoni na kikundi chake walishinda vita vya kukata maneno karibu na Megido

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Vita vya Har–Magedoni vitakapokwisha, watu ulimwenguni pote wataona vita kuwa kitu kisichowazika na chenye kuchukiza

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kujifunza ukweli kuhusu Yehova na kusudi lake ni hatua ya kwanza ya kupata wokovu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki