Wasomaji Wetu Wanauliza
Vita Vya Har-magedoni Vitapiganwa Wapi?
Vita vya Har–Magedoni havitapiganwa mahali fulani hususa. Badala yake, dunia nzima itakuwa uwanja wa vita. Kwa nini? Wanaohusika katika vita hivyo ni wengi sana wasiweze kutoshea mahali fulani hususa.
Har–Magedoni, inaitwa pia “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Yehova Mungu atamtumia Mwana wake, Kristo Yesu, kukusanya jeshi la malaika wapigane na majeshi yaliyoungana ya watawala wote waovu wa dunia.—Ufunuo 16:14; 19:11-16.
Kwa njia fulani mataifa yanashawishiwa na majeshi ya kishetani ili yajiunge katika vita. Biblia inasema kwamba “maneno yanayoongozwa na roho waovu” yanaelekezwa “kwa wafalme wa dunia nzima inayokaliwa, ili kuwakusanya pamoja . . . mahali panapoitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.”—Ufunuo 16:14-16.
Kitabu cha Ufunuo kimechochea akili za wasomaji wengi wa Biblia kuliko kitabu kingine katika Biblia. Wasomaji wengi wanaofikiri unabii wa kitabu hicho unapaswa kuchukuliwa kihalisi wametaja mahali hususa ambapo wanaamini vita hivyo vitapiganwa, na wamekuwa wakichunguza kwa woga mambo yanayotendeka katika eneo hilo. Wazo la kwamba Har–Magedoni inarejelea mahali hususa linaweza kupatikana katika maandishi ya mapema zaidi ya Kigiriki kuhusu kitabu cha Ufunuo, yaliyoandikwa na Oecumenius katika karne ya sita W.K.
Akitaja tena maoni ya viongozi wengi wa kidini wenye imani kali, John F. Walvoord, aliyekuwa msimamizi wa Chuo cha Theolojia cha Dallas, anasema kwamba Har–Magedoni ni “vita vya mwisho vya ulimwengu vya kujitoa mhanga visivyo na tumaini vitakavyopiganwa katika Mashariki ya Kati.” Walvoord anasema pigano hilo kubwa la wakati ujao litapiganwa katika “‘Mlima wa Megido,’ kilima kilicho kaskazini mwa Palestina mwishoni mwa bonde pana.”
Hata hivyo, kitabu cha Ufunuo hakikukusudiwa kuonyesha mahali hususa panapoitwa Har–Magedoni. Maneno ya utangulizi yanaonyesha kwamba masimulizi ya kitabu hicho yametolewa “kwa njia ya ishara.” (Ufunuo 1:1) Tangu zamani Mashahidi wa Yehova walisema hivi katika kitabu chao (Studies in the Scriptures, Buku la Nne): “Hatupaswi kutazamia kwamba watu watakusanyika kihalisi kwenye Mlima wa Megido.”
Mambo yaliyotendeka zamani huko Megido yanadokeza hali ya kutokuwa na nafasi ya kutorokea itakayowapata maadui wa Mungu. Hivyo, wakati wa Har–Magedoni, Mungu atahakikisha kwamba ufisadi na uovu wote, haidhuru unapatikana wapi ulimwenguni, utakomeshwa kabisa.—Ufunuo 21:8.
Wale wanaompenda Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, hawana sababu ya kuogopa Har–Magedoni. Mungu atapiga vita dhidi ya wanadamu anaowaona kuwa waovu kabisa. Hatawaangamiza watu bila kubagua. “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu,” inasema Biblia. (2 Petro 2:9) Ahadi hii yenye kugusa moyo inatolewa katika Zaburi 37:34: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.”