Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w08 6/1 kur. 24-25
  • Alitaka Kusaidia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Alitaka Kusaidia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Habari Zinazolingana
  • Shujaa na Msichana Mdogo
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Alikuwa Mkaidi Lakini Mwishowe Alitii
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • “Jifungeni Unyenyekevu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Msichana Anamsaidia Mwanamume Mwenye Nguvu
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
w08 6/1 kur. 24-25

Wafundishe Watoto Wako

Alitaka Kusaidia

JE, UMEWAHI kumwona mtu fulani aliye mgonjwa sana?— Je, ulitamani kumsaidia?— Namna gani ikiwa alikuwa wa taifa au dini nyingine? Je, bado ungetaka kumsaidia apone?— Msichana mdogo aliyeishi katika nchi ya Israeli miaka 3,000 hivi iliyopita alifanya hivyo. Acha tuzungumzie yaliyotukia.

Msichana huyo anaishi Israeli. Mara nyingi kumekuwa na vita kati ya nchi hiyo na nchi jirani ya Siria. (1 Wafalme 22:1) Siku moja Wasiria wanakuja na kumteka nyara msichana huyo mdogo. Anapelekwa Siria, ambako anakuwa kijakazi wa mkewe Naamani, mkuu wa Jeshi la Siria. Naamani ana ugonjwa mbaya sana unaoitwa ukoma. Ugonjwa huo unaweza kufanya nyama ya mwili wa mtu ikatike-katike.

A servant girl talking to Naaman’s wife
A servant girl talking to Naaman’s wife

Kijakazi huyo anamwambia mkewe Naamani jinsi mume wake anavyoweza kuponywa. Anasema hivi: ‘Ikiwa Naamani angekuwa Samaria, Elisha nabii wa Yehova angemponya ukoma wake.’ Kijakazi huyo anazungumza kumhusu Elisha kwa njia inayomfanya Naamani aamini kwamba kwa kweli nabii huyo anaweza kumponya. Hivyo, akiwa na ruhusa ya Ben-hadadi, mfalme wa Siria, Naamani na watumishi wake wanafunga safari ndefu ya kilomita 150 hivi kumtafuta Elisha.

Kwanza, wanamwendea Yehoramu, mfalme wa Israeli. Wanamwonyesha barua ya Mfalme Ben-hadadi ya kuomba msaada kwa ajili ya Naamani. Lakini Yehoramu hamwamini Yehova wala nabii Elisha. Yehoramu anafikiri kwamba Ben-hadadi anajaribu kuanzisha vita naye. Elisha anaposikia jambo hilo, anamwambia Mfalme Yehoramu: “Tafadhali, mwache aje kwangu.” Elisha anataka kuonyesha kwamba Mungu ana nguvu za kumponya Naamani ugonjwa wake mbaya.—2 Wafalme 5:1-8.

Naamani anapofika nyumbani kwa Elisha akiwa na farasi na magari ya kukokotwa, Elisha anamtuma mjumbe akamwambie hivi: ‘Unapaswa kuoga mara saba katika Mto Yordani, nawe utaponywa.’ Naamani anakasirika. Alitazamia kwamba Elisha angekuja nje na kutikisa mkono wake huku na huku juu ya mahali penye ukoma na kupaponya. Badala yake, anamwona mjumbe tu! Hivyo, Naamani anageuka kwa ghadhabu na kuanza kurudi nyumbani.—2 Wafalme 5:9-12.

Ungefanya nini ikiwa ungekuwa mmoja wa watumishi wa Naamani?— Watumishi wake wanamuuliza hivi: ‘Ikiwa Elisha angekwambia ufanye jambo gumu, je, hungefanya? Hivyo, kwa nini usifanye jambo hili rahisi—kuoga tu na kuwa safi?’ Naamani anawasikiliza. ‘Anashuka na kuanza kujitumbukiza katika Yordani mara saba kisha nyama yake inakuwa kama nyama ya mvulana mdogo.’

Naamani anarudi kwa Elisha na kusema: “Tazama, sasa, hakika ninajua kwamba hakuna Mungu yeyote mahali pengine popote duniani isipokuwa katika Israeli.” Anamwahidi Elisha kwamba “hatatoa tena toleo la kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine yoyote isipokuwa kwa Yehova.”—2 Wafalme 5:13-17.

Je, ungependa kumsaidia mtu fulani kujifunza kumhusu Yehova na kuhusu yale anayoweza kufanya, kama msichana huyo mdogo alivyofanya?— Yesu alipokuwa duniani, mtu fulani aliyekuwa na ukoma alimwamini na kusema: ‘Kwa kweli ikiwa unataka, unaweza kunisaidia.’ Je, unajua jinsi Yesu alivyomjibu?— “Nataka.” Na Yesu akamponya, kama tu Yehova alivyomponya Naamani.—Mathayo 8:2, 3.

Je, unajua kwamba Yehova ataumba ulimwengu mpya ambamo watu wote watakuwa na afya na wataweza kuishi milele?— (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Ikiwa ndivyo, hapana shaka kwamba ungetaka kuwajulisha wengine mambo hayo mazuri ajabu!

Maswali:

  • Msichana mdogo ambaye alitekwa nyara na wanaume wa Naamani alimsaidia jinsi gani?

  • Kwa nini mwanzoni Naamani alikataa kumtii Elisha, lakini ni nini kilichobadili maoni yake?

  • Ili uwe kama msichana huyo mdogo unapaswa kutaka kufanya nini hasa?

  • Yesu alitaka kufanya nini, na kwa nini maisha yatakuwa mazuri ajabu katika ulimwengu mpya wa Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki