Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w10 1/15 kur. 24-28
  • Utawala wa Shetani Utashindwa Kabisa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Utawala wa Shetani Utashindwa Kabisa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Njia Inayoongoza Kwenye Msiba
  • Kwa Nini Mungu Aliruhusu Hali Hiyo?
  • Uasi Ambao Umefanya Yehova Atukuzwe
  • Kwa Nini Ulimwengu Una Ugonjwa?
  • Utawala wa Yehova Umethibitika Kuwa Bora!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Kwa Nini Mungu Ameruusu Uovu Yetu ya Leo?
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Watawala Katika Makao ya Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Kwa Nini Kuna Mateso Mengi Ulimwenguni?
    Biblia Inatufundisha Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
w10 1/15 kur. 24-28

Utawala wa Shetani Utashindwa Kabisa

“Mambo hayatakuwa mema kwa mwovu.”—MHU. 8:13.

1. Kwa nini hukumu inayokuja ya waovu ni habari yenye kufariji?

PUNDE si punde, waovu watahukumiwa. Wataadhibiwa kwa sababu ya makosa yao. (Met. 5:22; Mhu. 8:12, 13) Hiyo ni habari yenye kufariji, hasa kwa wale ambao wanapenda uadilifu na ambao wametendewa isivyo haki na kuteswa na waovu. Atakayekuwa wa kwanza kabisa kuhukumiwa kati ya waovu, ni baba ya uovu Shetani Ibilisi.—Yoh. 8:44.

2. Kwa nini muda ulihitajiwa ili kutatua suala ambalo lilitokezwa katika Edeni?

2 Katika bustani ya Edeni, Shetani alijiona kuwa mtu wa maana sana, akawafanya wanadamu wakatae utawala wa Mungu. Kwa hiyo, wazazi wetu wa kwanza walijiunga na Shetani katika kutilia shaka haki ya Yehova ya kutawala na hivyo wakawa watenda-dhambi. (Rom. 5:12-14) Bila shaka, Yehova alijua matokeo ya kumwasi na kutomheshimu. Hata hivyo, viumbe wote wenye akili walipaswa kuona wazi matokeo hayo ambayo hayangeweza kuepukika. Basi, muda ulihitajiwa ili suala hilo litatuliwe na kuthibitisha kwa uhakika kwamba waasi hao walikuwa wamekosea kabisa.

3. Tuna maoni gani kuhusu serikali za wanadamu?

3 Kwa kuwa wanadamu walikuwa wamekataa kuongozwa na Yehova, walilazimika kuanzisha serikali zao wenyewe. Mtume Paulo alipokuwa akiwaandikia waamini wenzake huko Roma, aliziita serikali hizo za wanadamu “mamlaka zilizo kubwa.” Katika siku za Paulo, mamlaka kubwa ilikuwa hasa serikali ya Roma iliyoongozwa na Maliki Nero, ambaye alitawala kuanzia mwaka wa 54-68 W.K. Paulo alisema kwamba mamlaka kama hizo zilizo kubwa “zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.” (Soma Waroma 13:1, 2.) Je, hilo linamaanisha kwamba Paulo alikuwa akitetea utawala wa wanadamu kuwa ni bora kuliko utawala wa Mungu? Bila shaka hapana. Badala yake, alikuwa akisema kwamba maadamu Yehova anaruhusu utawala wa wanadamu uendelee kuwapo, Wakristo wanapaswa kuheshimu “mpango wa Mungu” na kuwatii watawala hao.

Njia Inayoongoza Kwenye Msiba

4. Eleza ni kwa nini utawala wa wanadamu utashindwa kwa hakika.

4 Bila shaka, utawala wa wanadamu unaoongozwa na Shetani utashindwa. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba utawala huo hautegemei hekima ya Mungu. Yehova peke yake ndiye aliye na hekima kamilifu. Hivyo basi, yeye ndiye chanzo pekee cha mwongozo unaotegemeka kuhusu utawala wenye mafanikio. (Yer. 8:9; Rom. 16:27) Sikuzote, Yehova anajua njia bora zaidi ya kufanya mambo, tofauti na wanadamu ambao mara nyingi wanajifunza kwa kukisia-kisia tu. Serikali yoyote ambayo haifuati mwongozo wa Mungu haiwezi kufanikiwa. Kwa sababu hiyo na kwa sababu ya mwelekeo mwovu wa Shetani, njia yake ya kuongoza kupitia utawala wa wanadamu haingefanikiwa tangu mwanzoni.

5, 6. Inaelekea ni nini kilichomwongoza Shetani amwasi Yehova?

5 Kwa kawaida, mtu mwenye busara hawezi kuanza kufanya jambo ambalo halitafanikiwa. Ikiwa atasisitiza kufanya jambo hilo, atalazimika kutambua makosa yake. Historia imethibitisha tena na tena kwamba hakuna faida yoyote inayotokana na kumpinga Muumba mweza-yote. (Soma Methali 21:30.) Hata hivyo, Shetani alimwasi Yehova kwa kuwa alipofushwa na kiburi chake, naye alijiona kuwa mtu wa maana sana. Hivyo, Ibilisi alichagua kimakusudi kufuata njia ambayo ingemwongoza kwenye msiba tu.

6 Mtazamo wa Shetani wa kimbelembele ulionyeshwa baadaye na mtawala wa Babiloni ambaye Biblia inasema alijigamba hivi: “Nitaenda juu mbinguni. Nitakiinua kiti changu cha ufalme juu ya nyota za Mungu, nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, katika sehemu za mbali zaidi za kaskazini. Nitaenda juu ya mahali palipo juu pa mawingu; mimi nitajifananisha na Aliye Juu Zaidi.” (Isa. 14:13-15) Jitihada za mtawala huyo asiye na busara hazikufanikiwa, na kwa aibu utawala wa Babiloni ulishindwa. Hivi karibuni, Shetani atashindwa kabisa vivyo hivyo pamoja na ulimwengu wake.

Kwa Nini Mungu Aliruhusu Hali Hiyo?

7, 8. Wanadamu wamefaidika jinsi gani kwa sababu ya Yehova kuruhusu uovu uendelee kuwapo kwa muda?

7 Huenda watu fulani wakauliza kwa nini Yehova hakuwazuia wanadamu wajiunge na Shetani na kufuata utawala ambao kwa hakika ungeshindwa. Akiwa Mungu Mweza-Yote, bila shaka angeweza kuwazuia. (Kut. 6:3) Hata hivyo, hakuwazuia. Kwa sababu ya hekima yake, alitambua kwamba ikiwa angewaruhusu wanadamu waendelee na uasi wao kwa muda fulani, mwishowe matokeo yangekuwa mazuri. Hatimaye, Yehova angethibitika kuwa Mtawala mwadilifu na mwenye upendo, na wanadamu waaminifu wangefaidika kutokana na uamuzi wa Mungu.

8 Familia ya wanadamu ingeepuka mateso mengi ikiwa wanadamu wangekataa kudanganywa na Shetani na kama hawangeasi utawala wa Mungu! Hata hivyo, uamuzi wa Yehova wa kuwaruhusu wanadamu wajitawale kwa muda fulani umekuwa na faida. Hatua hiyo imewasaidia sana watu wenye mioyo minyoofu kuona kwamba ni jambo la hekima kumsikiliza Mungu na kumtegemea. Kwa karne nyingi, wanadamu wamejaribu aina mbalimbali za serikali, lakini hakuna hata moja ambayo imethibitika kuwa inafaa kabisa. Jambo hilo la hakika limefanya waabudu wa Mungu wasadiki kabisa kwamba utawala wa Yehova ndio utawala bora zaidi. Ni kweli kwamba kwa sababu Yehova ameruhusu utawala mwovu wa Shetani uendelee kuwapo, wanadamu wote wameteseka, kutia ndani wale ambao wanamwabudu Mungu kwa uaminifu. Hata hivyo, waabudu hao waaminifu wamefaidika kwa sababu Yehova ameruhusu uovu uendelee kuwapo kwa muda.

Uasi Ambao Umefanya Yehova Atukuzwe

9, 10. Eleza jinsi ambavyo utawala wa Shetani umefanya Yehova atukuzwe.

9 Uhakika wa kwamba Yehova amewaruhusu wanadamu washawishiwe na Shetani na kujitawala, hauthibitishi kamwe kwamba utawala wa Yehova haufai. Badala yake, historia inathibitisha ukweli wa maneno ya Yeremia ambayo alisema akiongozwa na roho ya Mungu kwamba wanadamu hawawezi kujitawala. (Soma Yeremia 10:23.) Kwa kuongezea, uasi wa Shetani umempa Yehova nafasi ya kuonyesha sifa Zake nzuri kwa njia iliyo wazi zaidi. Jinsi gani?

10 Matokeo mabaya ya utawala wa Shetani yamefunua waziwazi zaidi sifa kamilifu za Yehova ambazo huenda hatungeziona. Kwa hiyo, ametukuzwa machoni pa wale ambao wanampenda. Ndiyo, ingawa huenda likaonekana kuwa jambo la kushangaza, kwa kweli utawala wa Shetani umefanya Mungu atukuzwe. Hilo limeonyesha wazi kwamba Yehova ameshughulika na upinzani huo kuelekea enzi yake kuu kwa njia bora zaidi. Ili kuthibitisha ukweli huo, acheni tuchunguze kwa ufupi sifa fulani za Yehova na tuone jinsi ambavyo utawala mwovu wa Shetani umemfanya Yehova aonyeshe sifa hizo kwa njia nyingine nyingi.

11. Yehova ameonyesha upendo jinsi gani?

11 Upendo. Maandiko yanatuambia kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Kwanza kabisa, Mungu alionyesha upendo wake kwa kuwaumba wanadamu. Kwa kuongezea, miili yetu iliyoumbwa kwa njia ya ajabu na yenye kustaajabisha inathibitisha pia upendo wa Mungu. Pia, kwa upendo Yehova aliwapa wanadamu makao mazuri sana ambayo yalikuwa na kila kitu walichohitaji ili kuwa na furaha. (Mwa. 1:29-31; 2:8, 9; Zab. 139:14-16) Lakini familia ya wanadamu ilipotumbukia katika dhambi, Yehova alionyesha upendo wake kwa njia nyingine mpya. Jinsi gani? Mtume Yohana ananukuu maneno haya ya Yesu: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Mungu aliwaonyesha wanadamu upendo wake kwa njia kubwa zaidi alipomtuma Mwana wake mzaliwa-pekee aje duniani kuwakomboa watenda-dhambi. (Yoh. 15:13) Uthibitisho huo mkubwa wa upendo uliwawekea pia wanadamu mfano wa kuiga, na umewapa nafasi ya kuonyesha upendo wa Mungu wa kujidhabihu katika maisha yao ya kila siku, kama Yesu alivyofanya.—Yoh. 17:25, 26.

12. Nguvu za Yehova zinaonekana jinsi gani?

12 Nguvu. “Mungu, Mweza-Yote” ndiye peke yake aliye na nguvu za kuumba uhai. (Ufu. 11:17; Zab. 36:9) Mwanadamu anapozaliwa anaweza kulinganishwa na karatasi ambayo haina maandishi yoyote. Wakati wa kifo, anakuwa amejaza kwenye karatasi hiyo maamuzi, matendo, na mambo mbalimbali aliyopitia maishani ambayo yalifinyanga utu wake. Habari hiyo inaweza kuhifadhiwa katika kumbukumbu ya Yehova. Wakati ukifika, Yehova anaweza kumfufua mtu huyo, akiwa na utu wake wa pekee. (Yoh. 5:28, 29) Kwa hiyo, ingawa hapo mwanzoni Mungu hakukusudia wanadamu wafe, kifo kimempa Yehova nafasi ya kuonyesha kwamba ana nguvu za kuwafufua wafu. Kwa kweli, Yehova ni “Mungu, Mweza-Yote.”

13. Dhabihu ya Yesu ilionyesha jinsi gani haki kamilifu ya Yehova?

13 Haki. Yehova hasemi uwongo; wala hatendi kamwe isivyo haki. (Kum. 32:4; Tito 1:2) Sikuzote anashikamana na viwango vya juu zaidi vya kweli na haki, hata ikiwa inaonekana kwamba kufanya hivyo kutamgharimu sana. (Rom. 8:32) Bila shaka, Yehova alihisi uchungu sana alipomwona Mwana wake mpendwa akifa kwenye mti wa mateso kana kwamba Yesu alikuwa mwasi aliyekuwa amekufuru. Hata hivyo, akichochewa na upendo kuelekea wanadamu wasio wakamilifu, Yehova alikuwa tayari kuruhusu tukio hilo lenye kuumiza litendeke ili ashikamane na viwango vyake vikamilifu vya haki. (Soma Waroma 5:18-21.) Ulimwengu uliojaa ukosefu wa haki ulimpa Yehova nafasi ya kuthibitisha kwamba yeye ndiye mfano bora zaidi katika kuonyesha haki.

14, 15. Yehova ameonyesha subira na hekima yake isiyo na kifani kwa njia gani mbalimbali?

14 Hekima. Mara tu baada ya Adamu na Hawa kufanya dhambi, Yehova alifunua jinsi ambavyo angeondoa madhara yote yaliyosababishwa na uasi wao. (Mwa. 3:15) Yehova alionyesha wazi kabisa hekima yake kwa kuchukua hatua ya haraka na kufunua hatua kwa hatua kusudi lake kuelekea watumishi wake. (Rom. 11:33) Hakuna jambo lolote linaloweza kumzuia Yehova asitimize makusudi yake. Katika ulimwengu uliojaa watu wenye maadili mapotovu, wanaopenda vita, wasio na usawaziko, wasiotii, wasio na rehema, wenye ubaguzi, na wanafiki, Yehova amekuwa na nafasi ya kutosha ya kuwaonyesha viumbe wake hekima ya kweli. Mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.”—Yak. 3:17.

15 Subira na Ustahimilivu. Sifa za Yehova za subira na ustahimilivu hazingeonekana wazi zaidi ikiwa hangelazimika kushughulika na wanadamu wasio wakamilifu, wenye dhambi, na wanaokosea. Kwa kukubali kushughulika na wanadamu kwa maelfu ya miaka, Yehova ameonyesha kwamba ana sifa hizo nzuri ajabu kwa kiwango kikamilifu, na hivyo tunapaswa kumshukuru sana. Kwa kufaa, mtume Petro alisema kwamba tunapaswa ‘kuiona subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.’—2 Pet. 3:9, 15.

16. Kwa nini utayari wa Yehova wa kusamehe unatuletea shangwe nyingi sana?

16 Yuko Tayari Kusamehe. Sisi sote ni watenda-dhambi na tunajikwaa mara nyingi. (Yak. 3:2; 1 Yoh. 1:8, 9) Tunapaswa kushukuru sana kwamba Yehova yuko tayari kusamehe “kwa njia kubwa”! (Isa. 55:7) Fikiria pia ukweli huu: Kwa sababu tumezaliwa tukiwa watenda-dhambi wasio wakamilifu, tunaweza kupata shangwe nyingi sana Mungu anapotusamehe makosa yetu. (Zab. 51:5, 9, 17) Sifa hiyo ya Yehova yenye kugusa moyo inatuchochea sisi binafsi kumpenda zaidi na inatutia moyo kuiga mfano wake tunaposhughulika na wengine.—Soma Wakolosai 3:13.

Kwa Nini Ulimwengu Una Ugonjwa?

17, 18. Utawala wa Shetani umeshindwa jinsi gani?

17 Kwa karne nyingi, mfumo wote wa ulimwengu wa Shetani ambao unatokana na utawala wake, umeshindwa kufanikiwa. Mwaka wa 1991, gazeti moja (The European) lilisema hivi: “Je, ulimwengu una ugonjwa? Bila shaka ndiyo, lakini . . . ugonjwa huo haujasababishwa na Mungu, ugonjwa wa ulimwengu umesababishwa na wakaaji wake.” Hilo ni kweli kabisa! Wakichochewa na Shetani, wazazi wetu wa kwanza walichagua utawala wa wanadamu badala ya utawala wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, walianzisha utawala ambao bila shaka ungeshindwa. Maumivu na mateso ambayo wanadamu wanapata ulimwenguni pote ni ishara ya kwamba utawala wa wanadamu umeshikwa na ugonjwa hatari.

18 Utawala wa Shetani unachochea uchoyo. Hata hivyo, uchoyo au ubinafsi hauwezi kamwe kuushinda upendo, ambao ni msingi wa utawala wa Yehova. Utawala wa Shetani umeshindwa kuleta amani, furaha, na usalama. Ni wazi kwamba utawala wa Yehova ndio utawala bora kabisa! Je, leo kuna uthibitisho wowote unaoonyesha hivyo? Ndiyo, kama tutakavyoona katika habari inayofuata.

Tumejifunza Nini Kuhusu Utawala kwa Kusoma . . .

• Waroma 13:1, 2?

• Methali 21:30?

• Yeremia 10:23?

• Wakolosai 3:13?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Utawala wa Shetani haujawanufaisha kamwe wanadamu

[Hisani]

U.S. Army photo

WHO photo by P. Almasy

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yehova ana nguvu za kuwafufua wafu

[Picha katika ukurasa wa 27]

Yehova alionyesha hekima na upendo wake kupitia dhabihu ya Mwana wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki