“Kwa Nini Mungu Hakufanya Chochote?”
“KILA MARA SWALI LINALOKUJA AKILINI NI: KWA NINI MUNGU HAKUFANYA CHOCHOTE?”—Papa Benedict wa 16, alipotembelea majengo yaliyokuwa kambi ya mateso ya Auschwitz, Poland.
MAJANGA YANAPOTOKEA, JE, WEWE HUJIULIZA, ‘KWA NINI MUNGU HAKUFANYA CHOCHOTE?’ AU KWENYE MAISHA YAKO MWENYEWE, JE, UMEWAHI KUPATWA NA HALI ILIYOFANYA UJIULIZE IKIWA KWELI MUNGU ANAKUJALI?
Huenda unahisi kama Sheila, ambaye anaishi nchini Marekani. Sheila alilelewa katika familia ya kidini. Anasema hivi: “Tangu nilipokuwa mdogo, nilivutiwa na Mungu kwa sababu yeye ni Muumba wetu. Hata hivyo, sikuwahi kuhisi nikiwa karibu naye. Nilihisi ananitazama, lakini akiwa mbali nami. Nilijua kwamba hanichukii, lakini sikuamini kama ananijali mimi binafsi.” Kwa nini Sheila alihisi hivyo? Anasema: “Familia yetu ilipatwa na pigo moja baada ya jingine, na ilionekana kwamba Mungu hakuwa akitusaidia hata kidogo.”
Kama Sheila, huenda wewe pia unaamini kwamba Mungu Mweza-Yote yupo. Hata hivyo, huenda huna uhakika ikiwa kweli anakujali wewe binafsi. Mwanamume mwadilifu, Ayubu, ambaye aliamini kwamba Muumba ana nguvu na hekima, alihisi hivyo pia. (Ayubu 2:3; 9:4) Baada ya Ayubu kupigwa na janga moja baada ya jingine, bila kuwa na tumaini lolote, alimuuliza Mungu hivi: “Kwa nini unauficha uso wako na kuniona kuwa adui yako?”—Ayubu 13:24.
Biblia inasema nini? Je, Mungu ndiye husababisha majanga? Je, kuna chochote kinachothibitisha kwamba Mungu anawajali wanadamu wote kwa ujumla na pia tukiwa mtu mmoja-mmoja? Tunapofikiria hali zetu binafsi, je, tunaweza kuwa na uhakika ikiwa Mungu anatuona na kututambua, anatuelewa, anahisi maumivu yetu, au kutusaidia kukabiliana na matatizo yetu?
Katika makala zinazofuata, tutachunguza jinsi ambavyo uumbaji unaonyesha kwamba Mungu anatujali. (Waroma 1:20) Kisha, tutachanganua maoni ya Biblia kuhusu suala hilo. Kadiri ‘unavyomjua’ Mungu kupitia uumbaji na Neno lake, ndivyo utakavyozidi kuwa na uhakika kwamba ‘anakujali.’—1 Yohana 2:3; 1 Petro 5:7.