Je, Unafanya Mawazo ya Yehova Kuwa Mawazo Yako?
“Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.”—ROM. 12:2.
1, 2. Tunapoendelea kukua kiroho, tunajifunza kufanya nini? Toa mfano.
MTOTO mdogo anapokea zawadi. Wazazi wake wanamwambia, “Sema asante.” Mtoto huyo anatii, ingawa anafanya hivyo ili tu kutimiza wajibu. Anapoendelea kukua, anaanza kuthamini hata zaidi njia ya kufikiri ya wazazi wake na matendo ya fadhili anayofanyiwa na wengine. Sasa anaonyesha shukrani kwa utayari zaidi, kutoka moyoni. Kwa nini? Kwa sababu kuonyesha shukrani kumekuwa sehemu ya njia yake ya kufikiri.
2 Vivyo hivyo, tulipoanza kujifunza kweli, tulijifunza umuhimu wa kutii matakwa ya msingi ya Yehova. Lakini kadiri tunavyoendelea kukua kiroho, tunajifunza mengi zaidi kuhusu njia ya Yehova ya kufikiri, yaani, mambo anayopenda na asiyopenda, na maoni yake kuhusu mambo mbalimbali. Tunapojifunza kufikiri kama yeye na kuruhusu njia yake ya kufikiri iongoze matendo na maamuzi yetu ya kibinafsi, tunaonyesha kwamba tunafanya mawazo ya Yehova kuwa mawazo yetu.
3. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kufanya mawazo ya Yehova kuwa mawazo yetu?
3 Ingawa ni jambo lenye kufurahisha kujifunza kufikiri kama Yehova, inaweza pia kuwa vigumu kufanya hivyo. Nyakati nyingine tunashindwa kufikiri kama Yehova kwa sababu sisi si wakamilifu. Kwa mfano, huenda ikawa vigumu kuelewa maoni ya Yehova kuhusu usafi wa kiadili, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, kazi ya kuhubiri, matumizi yasiyofaa ya damu, au mambo mengine. Tunaweza kufanya nini? Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kujitahidi kufanya mawazo ya Mungu kuwa mawazo yetu? Na kufanya hivyo kunapaswa kuwa na matokeo gani katika matendo yetu ya sasa na ya wakati ujao?
KUFANYA MAWAZO YA MUNGU KUWA MAWAZO YETU
4. Ni mambo gani yanayohusika ili kufuata himizo la Paulo la “kufanya upya akili [zetu]”?
4 Soma Waroma 12:2. Mtume Paulo anafafanua mambo yanayohusika ili mtu ajifunze kufikiri kama Yehova. Makala iliyotangulia ilitusaidia kuelewa kwamba ili “[tuache] kufinyangwa na mfumo huu wa mambo,” ni lazima tukatae kujilisha mitazamo na njia ya kuona mambo ya ulimwengu huu. Lakini Paulo anataja pia kwamba tunahitaji “kufanya upya akili [zetu].” Jambo hilo linahusisha kujifunza Neno la Mungu tukiwa na lengo la kuelewa mawazo yake, kuyatafakari, na kupatanisha njia yetu ya kufikiri na njia ya Mungu.
5. Eleza tofauti iliyopo kati ya kusoma kijuujuu na kujifunza.
5 Kujifunza kunahusisha mengi zaidi ya kusoma habari fulani kijuujuu au kupigia tu mistari majibu ya maswali yanayoulizwa. Tunapojifunza, tunachunguza mambo ambayo habari hiyo inatufundisha kumhusu Yehova, njia zake, na njia yake ya kufikiri. Tunajitahidi kuelewa kwa nini Mungu anaamuru tufanye jambo fulani na kutukataza kufanya jambo lingine. Tunafikiria pia mabadiliko tunayohitaji kufanya maishani mwetu na katika njia yetu ya kufikiri. Ingawa huenda tusifanye mambo hayo yote kila mara tunapojifunza, tutanufaika kwa kutumia wakati—labda nusu ya wakati tunaotumia kujifunza—kutafakari kwa kina mambo tunayosoma.—Zab. 119:97; 1 Tim. 4:15.
6. Ni nini ambacho hutendeka tunapotafakari kuhusu mawazo ya Yehova?
6 Kadiri tunavyotafakari kwa ukawaida Neno la Mungu, jambo fulani la pekee sana hutendeka. ‘Tunajihakikishia wenyewe,’ naam, tunajisadikishia kwamba njia ya Yehova ya kufikiri na ya kuona mambo ni kamilifu. Tunaanza kuona mambo kama anavyoyaona, na tunaanza kukubaliana na njia yake ya kuona mambo. Akili zetu ‘zinafanywa upya,’ na tunaanza kusitawisha njia mpya kabisa ya kufikiri. Hatua kwa hatua, tunaanza kufanya mawazo ya Yehova kuwa mawazo yetu.
MAWAZO YETU HUONGOZA MATENDO YETU
7, 8. (a) Maoni ya Yehova ni nini kuhusu ufanisi wa mambo ya kimwili? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Ikiwa tutafanya maoni yake kuwa maoni yetu, tutatanguliza nini nyakati zote?
7 Hatupaswi kufikia mkataa kwamba kufikiri ni jambo tu la kuchangamsha akili. Kufikiri na kutenda ni mambo yanayoenda sambamba. (Marko 7:21-23; Yak. 2:17) Tunaweza kuelewa vizuri zaidi jambo hilo kwa kuchunguza mifano michache. Kwa mfano, vitabu vya Injili hutusaidia kuelewa vizuri maoni ya Yehova kuhusu vitu vya kimwili. Mungu mwenyewe ndiye aliyewachagua wazazi ambao wangemlea Mwana wake—wenzi wa ndoa waliokuwa na maisha ya hali ya chini. (Law. 12:8; Luka 2:24) Yesu alipozaliwa, Maria “[alimlaza] katika hori, kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba za wageni.” (Luka 2:7) Ikiwa Yehova angetaka, angetumia njia yoyote ile kuandaa mahali pazuri ambapo Mwana wake angezaliwa. Hata hivyo, jambo aliloona kuwa muhimu zaidi Kwake ni mazingira ya kiroho ambayo Yesu angetunzwa na kulelewa.
8 Simulizi hilo la Biblia kuhusu kuzaliwa kwa Yesu, linaweza kutusaidia kuelewa maoni ya Yehova kuhusu vitu vya kimwili. Wazazi fulani wameazimia kwamba lazima watoto wao wawe na vitu bora zaidi vya kimwili, hata ikiwa kufanya hivyo kutahatarisha hali nzuri ya kiroho ya watoto wao. Hata hivyo, ni wazi kwamba Yehova anaona mambo ya kiroho kuwa ya muhimu zaidi. Je, umefanya maoni ya Yehova kuwa maoni yako? Matendo yako yanafunua nini?—Soma Waebrania 13:5.
9, 10. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna maoni kama ya Yehova kuhusu kuwakwaza wengine?
9 Mfano mwingine ni maoni ya Mungu kuhusu kuwakwaza wengine. Yesu alisema hivi: “Yeyote anayemkwaza mmoja wa hawa wadogo walio na imani, ingekuwa afadhali ikiwa jiwe la kusagia ambalo huzungushwa na punda lingefungwa shingoni mwake kisha atupwe baharini.” (Marko 9:42) Maneno hayo yanaonyesha hisia kali! Kwa kuwa Yesu alionyesha kikamilifu sifa za Baba yake, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova pia ana hisia kali kama hizo kumwelekea mtu yeyote anayetenda bila kujali na kumkwaza mmoja wa wafuasi wa Yesu.—Yoh. 14:9.
10 Je, maoni yetu ni kama ya Yehova na Yesu? Je, tumefanya njia yao ya kuona mambo kuwa njia yetu ya kuona mambo? Matendo yetu yanafunua nini? Kwa mfano, tuseme kwamba tunavutiwa na mtindo fulani wa mavazi au wa kujipamba ambao huenda ukawakwaza baadhi ya ndugu na dada kutanikoni, au unaoweza kuchochea akilini mwa watu hamu ya kufanya ngono. Je, tamaa yetu ya kuwajali kwa upendo waamini wenzetu itatusukuma tusitangulize mapendezi yetu binafsi inapohusu mitindo ya mavazi?—1 Tim. 2:9, 10.
11, 12. Kusitawisha maoni ya Mungu kuhusu uovu na kusitawisha sifa ya kujizuia kutatulindaje tusitende mambo mabaya?
11 Mfano wa tatu: Yehova anachukia ukosefu wa uadilifu. (Isa. 61:8) Ingawa Yehova anajua kwamba tuna mwelekeo usiofaa kwa sababu tumerithi hali ya kutokamilika, anatuhimiza tuchukie ukosefu wa uadilifu kama anavyouchukia. (Soma Zaburi 97:10.) Kutafakari kuhusu kwa nini Yehova anachukizwa na uovu kutatusaidia kufanya njia yake ya kuona mambo kuwa njia yetu ya kuona mambo, na hilo litatusaidia kuimarisha azimio letu la kukataa kabisa kutenda mambo mabaya.
12 Kusitawisha maoni ya Yehova kuhusu ukosefu wa uadilifu kutatusaidia pia kutambua kwamba mazoea fulani ni mabaya hata ingawa hayajatajwa moja kwa moja katika Neno la Mungu. Kwa mfano, dansi ya kukata kiuno huku mtumbuizaji akiwa ameketi kwenye mapaja ya mteja (lap dancing), ni aina ya dansi chafu sana kiadili ambayo imeanza kupendwa sana ulimwenguni. Huenda baadhi ya watu wakasema kwamba dansi hiyo si mbaya, wakidai kwamba kufanya hivyo si sawa na kufanya ngono.a Lakini je, mambo kama hayo yanapatana na njia ya Mungu ya kufikiri, ambaye anachukia kila aina ya uovu? Acheni tujitenge kabisa na mambo yote mabaya kwa kusitawisha sifa ya kujizuia na kuchukia kabisa mambo ambayo Yehova anachukia.—Rom. 12:9.
TAFAKARI MAPEMA JINSI UTAKAVYOSHUGHULIKIA HALI MBALIMBALI
13. Kwa nini tunapaswa kutafakari mapema maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali?
13 Tunapojifunza, inafaa kutafakari maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali kwa sababu kufanya hivyo kutatusaidia kujua jinsi tunavyoweza kushughulika na hali tofauti-tofauti wakati ujao. Kwa njia hiyo, ikiwa tutakumbana na hali fulani ambayo itatulazimu tufanye uamuzi papo hapo, tutajua mara moja jambo tunalopaswa kufanya. (Met. 22:3) Fikiria mifano ifuatayo ya Biblia.
14. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yosefu alivyomkataa mke wa Potifa?
14 Yosefu alipokataa mara moja vishawishi vya kufanya ngono na mke wa Potifa, alionyesha kwamba alikuwa ametafakari mapema maoni ya Yehova kuhusu uaminifu katika ndoa. (Soma Mwanzo 39:8, 9.) Zaidi ya hilo, alipomwambia mke wa Potifa: “Ninawezaje kufanya uovu huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” alionyesha kwamba maoni ya Mungu kuhusu ndoa ndiyo yaliyokuwa maoni yake pia. Namna gani sisi? Ungetendaje ikiwa mfanyakazi mwenzako anaanza kukuchezea kimapenzi. Au vipi ikiwa unapokea kwenye simu yako ujumbe au picha chafu kuhusu ngono?b Itakuwa rahisi zaidi kwako kuchukua hatua inayofaa ikiwa tayari umetafakari mapema na kusitawisha maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo na ikiwa uliazimia mapema hatua utakayochukua.
15. Kama ilivyokuwa kwa wale Waebrania watatu, tunaweza kufanya nini ili tusikubali kushinikizwa kuvunja ushikamanifu wetu kwa Yehova?
15 Sasa fikiria mfano wa Waebrania watatu walioitwa Shadraki, Meshaki, na Abednego. Azimio lao thabiti la kutoiabudu sanamu ya dhahabu iliyokuwa imesimamishwa na Mfalme Nebukadneza na jibu la moja kwa moja walilompa, lilionyesha kwamba walikuwa wametafakari mapema yote ambayo yangehusika ili waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. (Kut. 20:4, 5; Dan. 3:4-6, 12, 16-18) Tuseme kwamba mwajiri wako anakuomba utoe mchango kwa ajili ya sherehe fulani ya dini ya uwongo ambayo inatarajiwa kufanywa. Ungefanya nini? Badala ya kusubiri hadi hali hiyo itokee, kwa nini usitafakari sasa maoni ya Yehova kuhusu mambo kama hayo? Kisha hali kama hiyo itakapotokea, itakuwa rahisi kwako kujua jambo unalopaswa kusema, kama walivyofanya wale Waebrania watatu.
Je, umefanya utafiti, umejaza hati ya kitiba, na kuzungumza na daktari wako? (Tazama fungu la 16)
16. Kuelewa vizuri njia ya Yehova ya kufikiri kunaweza kutusaidiaje kujitayarisha iwapo tutahitaji matibabu ya dharura?
16 Kutafakari mapema kuhusu umuhimu wa kuendelea kuwa washikamanifu kunaweza pia kutusaidia tunapohitaji matibabu ya dharura. Ingawa tumeazimia kabisa kuepuka kutiwa damu mishipani, iwe ni damu nzima au sehemu zake kuu nne, kuna matibabu fulani yanayohusisha damu ambayo yanahitaji tufanye uamuzi wa kibinafsi unaotegemea kanuni za Biblia zinazofunua njia ya Yehova ya kufikiri. (Mdo. 15:28, 29) Kwa kweli, wakati mzuri wa kufikiria mambo kama hayo si tukiwa hospitalini, wakati ambapo huenda tuna maumivu na tuko chini ya mkazo wa kufanya uamuzi wa haraka. Sasa ndio wakati wa kufanya utafiti, kujaza hati ya kitiba inayoonyesha matibabu ambayo tungependa kupokea, na kuzungumza na daktari wetu.c
17-19. Kwa nini ni muhimu tujifunze sasa kuhusu njia ya Yehova ya kuona mambo? Toa mfano wa hali ambayo tunahitaji kujua jinsi ya kushughulika nayo kabla haijatokea.
17 Mwishowe, fikiria jibu la papo hapo ambalo Yesu alimpa Petro baada ya kumpa ushauri huu wenye kasoro: “Bwana jihurumie.” Ni wazi kwamba Yesu alikuwa ametafakari kwa kina kuhusu mambo ambayo Mungu alitaka afanye na Maandiko yaliyohusu maisha na kifo chake hapa duniani. Ujuzi huo ulimsaidia aendelee kushikamana na uamuzi wake wa kudumu akiwa mwaminifu na kuishi maisha ya kujidhabihu bila kutetereshwa na chochote.—Soma Mathayo 16:21-23.
18 Leo, Mungu anawataka watu wake wasitawishe urafiki pamoja naye na washiriki kufanya kazi yake kwa kadiri kubwa iwezekanavyo. (Mt. 6:33; 28:19, 20; Yak. 4:8) Kama ilivyokuwa kwa Yesu, huenda watu wenye nia nzuri wakajaribu kutushawishi tuache kufuata njia hiyo. Kwa mfano, vipi ikiwa mwajiri wako anakuahidi kwamba atakupandisha cheo na kukupa mshahara mkubwa zaidi lakini cheo hicho kitavuruga ratiba yako ya mambo ya kiroho? Au vipi ikiwa wewe ni mwanafunzi na umepata fursa ya kuhamia mbali na nyumbani ili upate elimu ya ziada? Hali kama hiyo ikitokea, je, huo ndio wakati wa kusali na kufanya utafiti, kuzungumza na watu wa familia yako au labda wazee, na kisha kufanya uamuzi? Kwa nini usijifunze sasa njia ya Yehova ya kufikiri kuhusu mambo hayo na kujitahidi kufanya mawazo yake kuwa mawazo yako? Kisha, ikiwa hali kama hiyo itakupata, jambo hilo halitakuwa kishawishi kwako kwa sababu malengo yako ya kiroho yako wazi, umeazimia moyoni mwako, na kilichobaki sasa ni kutekeleza uamuzi ambao tayari umefikia.
19 Unaweza kufikiria hali nyingine kama hizo zinazoweza kutokea ghafla, bila kutarajia. Ni kweli kwamba hatuwezi kujitayarisha kwa ajili ya kila hali inayoweza kutokea. Hata hivyo, ikiwa tutatumia wakati wa kujifunza kibinafsi kutafakari kuhusu njia ya Yehova ya kufikiri, itakuwa rahisi zaidi kwetu kukumbuka na kutumia maishani mambo tuliyojifunza wakati uliopita ili kushughulikia hali tunayokabili. Hivyo basi, acheni tuwe macho kutambua jinsi Yehova anavyoona mambo, tufanye njia yake ya kuona mambo kuwa njia yetu ya kuona mambo, na tufikirie jinsi njia ya Mungu ya kuona mambo inavyofinyanga au kuongoza matendo yetu ya sasa na ya wakati ujao.
MAWAZO YA YEHOVA NA WAKATI WETU UJAO
20, 21. (a) Kwa nini tutafurahia kuwa huru katika ulimwengu mpya? (b) Tunaweza kufanya nini ili tufurahie kionjo cha shangwe hiyo hata sasa?
20 Tunatarajia kwa hamu ulimwengu mpya. Wengi wetu tunatarajia maisha yasiyo na mwisho katika dunia itakayokuwa paradiso. Chini ya Ufalme wa Mungu, wanadamu watawekwa huru kutokana na mambo yenye kuhuzunisha ambayo ni ya kawaida katika mfumo huu wa mambo. Bila shaka, hata wakati huo, watu wataendelea kuwa na uhuru wa kuchagua. Kila mtu atachagua mambo anayofurahishwa nayo au kutamani.
21 Bila shaka, uhuru huo utakuwa na mipaka. Inapohusu kuchagua kati ya lililo sawa na lililo kosa, wapole wataongozwa na sheria za Yehova na njia yake ya kufikiri. Watafurahia kufanya hivyo, nao watapata shangwe nyingi sana na amani tele. (Zab. 37:11) Kwa sasa, tunaweza kufurahia kionjo cha shangwe hiyo tunapojitahidi kufanya mawazo ya Yehova kuwa mawazo yetu.
a Aina hiyo ya dansi “ni dansi ambapo mtumbuizaji ambaye kwa kawaida huwa nusu uchi hukata kiuno na kujizungusha-zungusha akiwa ameketi juu ya mapaja ya mteja.” Ikitegemea na mambo halisi ambayo yalitokea katika kisa kinachohusika, jambo hilo linaweza kusemwa kuwa ni uasherati na hatua ya kihukumu inaweza kuchukuliwa. Mkristo ambaye amehusika katika dansi kama hiyo anapaswa kuomba msaada kutoka kwa wazee.—Yak. 5:14, 15.
b Kutuma ujumbe mchafu (Sexting), kunatia ndani kutuma ujumbe wa maneno, picha, na video za ngono kupitia simu ya mkononi. Ikitegemea na hali ambazo zimehusika, hatua ya kihukumu inaweza kuchukuliwa. Katika visa fulani vijana ambao hawajatimiza umri wa miaka 18, ambao wamewatumia wengine ujumbe mchafu wameshtakiwa kwa makosa ya kingono. Kwa habari zaidi, nenda kwenye Tovuti ya jw.org/sw na usome makala yenye kichwa, “Vijana Huuliza—Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu?” (Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MATINEJA.) Au tazama makala yenye kichwa, “Jinsi ya Kuzungumza na Kijana Wako Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu” iliyo katika gazeti la Amkeni! toleo la Novemba 2013, uku. 4-5.
c Kanuni za Biblia zinazohusika zimezungumziwa katika machapisho yetu. Kwa mfano, tazama kitabu Dumu Katika Upendo wa Mungu, uku. 246-2499.