Kuiga Yehova kwa Kuzoea Haki
1 “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. . . . Yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kum. 32:4) Maneno haya ya wimbo wa kale yanakazia mojapo sifa kuu za Yehova, ile ya haki. Kwa kutuumba katika mfano na sura yake, kwa kufaa Yehova anatazamia sisi ‘tutende haki katika kutembea pamoja na Mungu wetu.’—Mika 6:8, NW; Mwa. 1:26.
2 Jitihada zetu za kuiga Yehova zitadhihirishwa waziwazi kwenye “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya yote iliyoratibiwa kwa ajili ya tawi letu. (Efe. 5:1) Wengi wa ndugu zetu wamehusika kwa idili katika kufanya matayarisho yanayohitajiwa, nasi sote tunatazama mbele kwenye “Haki ya Kimungu” mikusanyiko tukiwa na hamu nyingi. Je! wewe umefanya mipango mahususi ili uwepo kwa kila pindi?
3 Kuanzia Alhamisi hadi Jumapili, kiasi kingi cha chakula cha kiroho chenye kukazia uhitaji wa kushikilia haki ya kimungu kitatolewa kupitia kwa hotuba, mawonyesho, mahojiano, na drama za Biblia.
4 Kwa kuongezea, programu hiyo itatia ndani mambo yaliyoonwa na habari zinazohusu utendaji wa ndugu na dada wanaotumikia katika kazi ya kimisionari. Huenda baadhi ya wamisionari hawa wakahudhuria mkusanyiko wako na wakawa katika programu. Kielelezo chao cha kuwa imara kwa ajili ya haki ya kimungu, mara nyingi katikati ya mastakimu zenye magumu, kinaweza kutuchochea tuishi na kutenda kulingana na haki ya kimungu katika shughuli zetu zote.
KUWASAIDIA WENGINE ‘WAONE HAKI’
5 Je! wewe binafsi umealika wanafunzi wako wa Biblia wahudhurie mkusanyiko wa wilaya? Je! haingekuwa sababu ya shangwe ikiwa watu wote wenye kupendezwa waliohudhuria sherehe ya Ukumbusho mwaka huu wangehudhuria pia mkusanyiko wa wilaya? Wangeweza kujionea wenyewe furaha ya watu wa Yehova na kupokea habari za kuwasadikisha juu ya uwezo na nia ya Yehova ya kukomesha kabisa ukosefu wa haki. Mkusanyiko huo ungetokeza badiliko kubwa katika maisha yao, ukiwasukuma wachukue msimamo mahususi kwa ajili ya Mungu wa haki.
6 Ingawa tutahudhuria mkusanyiko na wengi watachukua likizo wakati wa miezi hiyo, tutataka kudumisha ratiba nzuri kwa ajili ya utumishi wa shambani, tukiwaelekeza watu wenye kupendezwa kwenye tumaini la Ufalme. Kabla ya kuondoka kwenda kwenye mkusanyiko au likizo yako, fanya mipango ili utoe ushuhuda unaposafiri. Tafuta fursa za kusema na wengine katika pindi zote zinazofaa.
7 Na tujishughulishe kikamili na utendaji wa kitheokrasi. Tunapokusanyika pamoja kwa ajili ya “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya na tunaposhiriki katika huduma ya shambani, tutataka kudhihirisha upendo wetu kwa ajili ya haki, tukiiga Yehova Mungu wetu, ‘mpenda haki.’—Zab. 37:28.