Funzo la Biblia la Jamaa—Jambo la Kwanza kwa Wakristo
1 Mara nyingi mahali ambapo kuna matatizo na washiriki wa jamaa wanaoitikadi, hasa na matineja, funzo la Biblia la jamaa halijapokea fikira inavyohitajiwa. Inasikitisha kusema, jamaa nyingi, kutia na zile za wazee fulani na watumishi wa huduma, zinapata matatizo ya watoto wao wanaoenda shuleni kushindwa na mavutano ya kilimwengu.
2 Hivi majuzi mwangalizi wa mzunguko mmoja aliandika juu ya akina ndugu ambao wanapata matatizo pamoja na watoto wao. Yeye alipata kuona kwamba chanzo cha tatizo karibu sikuzote ni ukosefu wa kuelekezea fikira funzo la Biblia nyumbani. Uchunguzi wa hivi karibuni uliofanywa na mwangalizi wa mzunguko mmoja ulionyesha kwamba katika makundi fulani kufikia asilimia 50 hawana funzo la Biblia la jamaa la kawaida.
JAMBO LA KWANZA
3 Yehova aliwapa wazazi onyo la upole katika Israeli: “Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” (Kum. 6:6, 7) Ndiyo, wazazi katika Israeli waliagizwa kufikiria jambo hili kwa uzito sana.
4 Lazima wakati uwekwe kando kwa ukawaida kwa ajili ya funzo la jamaa ikiwa washiriki wa jamaa watafuata miongozo inayotolewa katika Neno la Mungu. Vichwa vya jamaa wanapaswa kuendelea kwa bidii-endelevu katika kuongoza funzo la Biblia la jamaa kwa ukawaida, na vilevile washiriki wengine wa jamaa wanapaswa kusaidia kufanya upande huu wa ibada ya jamaa uwe wenye mafanikio kwa manufaa ya jamaa nzima. Wote wanahitaji kuthamini kwamba wasipoelekezea fikira mahitaji ya kiroho ya jamaa sasa, inaelekea sana watalazimika kushughulikia matatizo mazito na hata yenye kutia uchungu wakati ujao.
JINSI YA KUREKEBISHA PROGRAMU YA FUNZO
5 Funzo lapaswa kuongozwa jinsi gani? Ni nini kinachopaswa kudarisiwa? Linapaswa kufanywa wakati gani, na kwa muda gani? Unaweza kuwa na uhakika jinsi gani kwamba unafikia moyo wa mtoto? Ili kupata majibu kwa maswali haya, tafadhali zungumzia Mnara wa Mlinzi wa Novemba 1, 1986, ukurasa 24.
6 Vitu vya maana kabisa ili kuwa na funzo la jamaa lenye mafanikio ni shangwe na idili inayodhihirishwa na wazazi. (Linganisha Zaburi 40:8) Pia, wazazi wanahitaji kuwasifu watoto kwa jitihada zao na kuwatia moyo watumie kanuni za Yehova.
7 Dada mmoja alijifunza ukweli wakati wanane wa watoto wake walikuwa wangali wanaishi nyumbani. Ingawa alikuwa na mume asiyeitikadi na asiyeshirikiana naye, yeye alihakikisha kwamba hali ya kiroho ya watoto wake ilielekezewa fikira inayofaa. Yeye aliweka kielelezo kizuri katika utumishi wa shambani na katika ushiriki wake kwenye mkutano. Baada ya utumishi wa shambani, yeye alikuwa akitazama nyuso za watoto wake na kuona ikiwa zilionyesha shangwe. Ikiwa hazikuonyesha, mara moja yeye alihakikisha kwamba anawapa kitia-moyo. Ikiwa wao wakijitenga na kukaa chumbani mwao, yeye alikuwa akizungumza nao kwa upendo na kuwavuta ili waseme na kuwatia moyo kwa Neno la Mungu. Kama matokeo, watoto wake wote wamo katika ukweli. Watatu wamekuwa mapainia wa kawaida, na wawili kati ya hawa walitumikia katika Betheli pia. Jitihada zake zilithawabishwa sana kwa sababu sikuzote yeye aliweka kwanza hali yao ya kiroho.—Linganisha 3 Yohana 4.
8 Mibaraka mingi inaweza kufurahiwa sasa na wakati ujao ikiwa wazazi daima wanaelekezea fikira mahitaji ya kiroho ya watoto wao. Watoto wanapoona thamani ya sheria ya Mungu na wanasadikishwa kwamba ni nzuri kweli kweli na yenye manufaa, hawatajizuia kuwajulisha wengine kile ambacho wao wanaitikadi kwa neno na tendo. (Zab. 119:165) Basi, wazazi, kwa shangwe lipeni funzo la jamaa lenu sehemu ya muhimu linalostahili.