Fahamu Yaliyo Katika Vitolewaji Vipya vya Mkusanyiko
1 Vitolewaji viwili vipya, kitabu na broshua, vimeongezwa kwenye ugavi wetu wa chakula kingi cha kiroho. Vikitolewa kwenye “Lugha Iliyo Safi” Mikusanyiko ya Wilaya, vichapo hivi vipya hakika vitakuwa na uvutano wenye nguvu katika huduma yetu ya shambani zaidi ya kutusaidia sisi sote tunene lugha iliyo safi kwa wazi zaidi.—Sef. 3:9.
2 Alipokuwa akitoa broshua hiyo mpya, mnenaji wa mkusanyiko alisema hivi: “Katika huduma ya shambani—nyumba kwa nyumba, kwenye ziara za kurudia, na wakati wa mafunzo ya Biblia—mara nyingi tunaulizwa kwa nini sisi hatutakubali kutumia damu. Ili kukusaidia kujibu swali hilo, ni shangwe kutoa kichapo kipya. Ni broshua hii yenye ukubwa wa gazeti, Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako?” Je, wewe umefanya habari katika broshua hii iwe yako mwenyewe kwa kuisoma kwa uangalifu? Ni jambo la maana kwako ufanye hivyo ili kutia nguvu imani yako mwenyewe na kuwa tayari kusaidia wengine waelewe maoni ya Mkristo juu ya damu.—Mdo. 15:28, 29.
3 Habari iliofanyiwa utafiti mwingi katika broshua hii itakutayarisha zaidi ueleze msimamo na matakwa yako kwa daktari yeyote. Hata hivyo, broshua hii mpya haikutolewa sana-sana kwa ajili ya madaktari au wanasheria. Imekusudiwa na kuandikwa hasa kwa ajili ya umma. Unaweza kuona jinsi makusudi yayo mawili yanavyoifanya iwe kifaa chenye thamani sana sana kwa matumizi yetu wakati huu. Inadokezwa kwamba uchukue nakala moja au mbili zayo shambani. Tumia kwa ukamili habari hiyo yenye thamani kwa manufaa yako mwenyewe na kwa kusaidia wengine waonyeshe staha inayofaa kwa damu.
KITABU KIPYA
4 Wazia tu thamani ya kile kitabu kipya Mankind’s Search for God katika kutusaidia katika huduma yetu. Kujifunza hicho kutatupa uelewevu ulio wazi zaidi juu ya dini nyinginezo na msingi wa historia yazo. Kitatusaidia tuwe tayari zaidi kuhubiria watu wa Jumuiya ya Wakristo pamoja na wale wanaoshikamana na dini nyingine. Kwa sababu ya kuhama-hama kwa watu wengi wakati wa hii karne ya 20, huenda tukapata watu wa lugha na dini nyingi tofauti-tofauti tunapohubiri nyumba kwa nyumba. Jambo hilo huwa gumu kweli kweli tunapokuwa hatufamu imani na desturi za watu hao. Kwa msaada wa kitabu hiki kipya, haitupasi kujisikia hatujui la kufanya tukutapo watu wa malezi mbalimbali ya kidini katika eneo letu.
5 Habari iliyomo katika kitabu hiki kipya imefanyiwa utafiti na kupitiwa na watu mmoja mmoja wanaofahamu kabisa habari zinazozungumzwa. Kwa hiyo, twaweza kunena kwa mamlaka tunapotumia taarifa zinazopatikana katika kitabu hicho. Hakika, kuandaa habari kama hiyo wakati huu ni ushuhuda mwingine wa upendo wa Yehova kwa watu wa mataifa yote. Acheni tufanye jitihada yenye bidii ya kufahamu yaliyo katika kichapo hiki kipya na kisha tukitumie kwa mafanikio katika kusaidia watu wenye mioyo myeupe wa malezi tofauti-tofauti ya kitaifa na kidini. Ndiyo, kutumia kichapo hiki kipya kwa mafanikio kutatupa uradhi wa kujua kwamba tunajulisha habari njema kwa watu wa aina zote tuwapatapo katika eneo letu tulilogawiwa.—Mt. 28:19, 20; Tito 2:11.