Kusaidia Wengine Tunapokuwa Katika Utumishi wa Shambani
1 Tangu mwanzo walo, kundi la Kikristo limekuwa tengenezo la waeneza evanjeli. Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kibinafsi katika utendaji wa kuhubiri na “akaanza kuwatuma wawili wawili.” (Mk. 6:7; Luka 8:1) Mtume Paulo alitaja “wafanyakazi wenzi” katika kundi la Filipi ambao ‘walijitahidi kando kwa kando pamoja naye katika zile habari njema.’ (Flp. 4:3) Ijapokuwa haihitajiwi sikuzote kuwa na mwenzi katika huduma, walio wengi wetu huthamini wengine wakiandamana nasi. (Mhu. 4:9) Ni jinsi gani, basi, tuwezavyo kuwa wenye kutia moyo na kusaidia mmoja na mwenzake tunapohubiri?
2 Kusudi moja la mikutano yetu ya utumishi wa shambani ni kutoa usaidizi kwa wahubiri wapya zaidi au wale wasio na ujuzi mwingi. (omSW kur. 76, 97) Hata mapainia waliowekwa karibuni huenda wakataka kufanya kazi na wahubiri wenye ujuzi zaidi au na mzee au mtumishi wa huduma. Ni fursa nzuri kama nini ya “badilishano la kitia-moyo”!—Rum. 1:12, NW.
3 Kwa sababu za usalama, huenda ikawa afadhali wahubiri wafanye kazi pamoja katika maeneo fulani. Au nyakati nyingine huenda ikahitajiwa kubadili mipango iliyotangulia kupangwa ya kufanya kazi na mtu fulani ili kuwatia ndani wahubiri wasio na ujuzi mwingi waliomo katika mkutano wa utumishi wa shambani. Tukiombwa tufanye hivyo, ungekuwa kweli kweli mwendo wa upendo kwetu kufanya marekebisho yoyote yanayohitajiwa ili “kuwasaidia wanyonge,” hata ingawa huenda kwa kawaida tukawa tumezoea kufanya kazi na mwenzi fulani.—Mdo. 20:35.
FANYENI KAZI KWA UPATANO
4 Wakati wowote tunapoandamana na wengine katika utumishi wa shambani, sisi twataka kufanya kazi kwa upatano kama timu. (Linganisha 1 Wakorintho 3:6, 9.) Wote wawili wanaweza kushiriki kutoa ushuhuda, labda wakipokezana zamu kuanzisha mazungumzo milangoni. Adabu nzuri zingeonyesha kwamba yatupasa kusikiliza kwa heshima na kwa makini wakati mwenzi wetu anapoongea.
5 Ijapokuwa huenda ikafaa kujiunga katika mazungumzo nyakati nyingine wakati mwenzi wetu anapoongoza, hilo lataka uamuzi mzuri. Hatutaki kukatiza kutoa sababu kuzuri kunakotumiwa kwa matokeo mazuri pamoja na mwenye nyumba. Bila shaka, ikiwa mhubiri asiye na ujuzi mwingi aanza kupata magumu katika kushughulika na kipingamizi, pasipo shaka angethamini usaidizi ulioelekezwa vizuri.—Mhu. 4:12.
6 Twaweza kutumia vizuri wakati wa kwenda kutoka mlango mmoja kwenda mwingine kuzungumzia njia ambazo katika hizo twaweza kufanyia maendeleo utoaji wetu. Labda kutumia mojayapo matangulizi katika kibabu Kutoa Sababu au dokezo lililoonyeshwa katika Huduma ya Ufalme Yetu lingethibitika kuwa lenye mafanikio zaidi. Pia kufanya kazi pamoja hutupa fursa ya kupata kujuana vizuri zaidi, na kutia nguvu vifungo vya udugu wetu wa Kikristo.
7 Kweli kweli huduma yetu ni hazina yenye thamani kubwa. (2 Kor. 4:1, 7) Tuwapo na fursa ya kufanya kazi pamoja na wengine katika utumishi wa shambani, twaweza kujenga katika mmoja na mwenzake uthamini wenye kina kwa ajili ya kazi yetu takatifu. Wakati ule ule, tutapokea kitia-moyo na kujifunza kutoka kwa mmoja na mwenzake. Matokeo yatakuwa shangwe iliyoongezeka, mafanikio zaidi katika kutoa ushuhuda, na hisia yenye kutosheleza ya umoja wa ndugu na dada zetu.—Zab. 133:1.