Uwe Mwenye Nafsi Yote Katika Huduma ya Shambani
Sehemu ya 1: Thamani ya Kumthamini Yehova
1 Kuwa mwenye nafsi yote katika huduma hutokana na uthamini wenye kina kwa Yehova na yote ambayo ametufanyia. (2 Sam. 22:2, 3) Maoni yenye kuhurumia hali mbaya ya ainabinadamu yote iliyotenganishwa na Mungu yapasa kutusukuma tujitahidi katika utumishi. (Mt. 9:36; 2 Kor. 5:14, 15) Kwa kadiri tujitoavyo zaidi kwa Yehova na kwa kadiri tuhangaikiavyo zaidi watu, ndivyo tutakavyosukumwa zaidi tushiriki kwa idili katika utumishi wa shambani. (Mt. 22:37-39) Ndipo huduma yetu inapokuwa hazina ya kuonwa kuwa yenye bei sana. (2 Kor. 4:7) Lakini uthamini huo kwa huduma waweza kusitawishwaje?
NJIA ZA KUJENGA UTHAMINI
2 Funzo la Biblia la kibinafsi na la kundi pamoja na kutafakari kwa njia ya sala hutusaidia kusitawisha uhusiano wa kibinafsi na Yehova. Tunapata kutambua uzuri wa sifa na utu wake. Je! wewe hufuata ratiba ya kila juma ya usomaji wa Biblia? Je! wewe hutenga wakati kwa ukawaida ili kujifunza vichapo vya Sosaiti? Je! wewe hutayarisha, kuhudhuria, na kushiriki katika mikutano yote ya kundi? (Ebr. 10:24, 25) Wakati na baada ya kila kipindi cha funzo la kibinafsi, kutafakari kwenye kusudi kutajenga uthamini wa moyo kwa uzuri wa Mungu wetu mwenye moyo mchangamfu na mipango yake ya ibada ya kweli.—Zab. 27:4.
3 Njia nyingine ya kuzidisha kiwango chetu cha uthamini ni kufikiria sana kielelezo cha wahudumu wengine wa Mungu waliojitoa kwa nafsi yote. Nabii Yeremia aliwaka kwa juhudi yenye moto kwa ajili ya kazi aliyoaminishwa. (Yer. 20:9) Yesu aliacha kigezo, akionyesha roho yenye uthamini na bidii. (Yn. 4:34) Kwa kazi zake ngumu katika huduma mtume Paulo alionyesha shukrani zake kwa rehema ya kimungu aliyoonyeshwa. (1 Tim. 1:12, 13, 17) Tutafakaripo vielelezo kama hivyo, pamoja na vielelezo vya nyakati za ki-siku-hizi, twaweza kujenga uthamini ambao utatufanya tuwe wenye nafsi yote katika huduma.
4 Tujifunzapo juu ya fahari yenye utukufu ya adhama ya Yehova na kujishughulisha na kazi zake za ajabu, tunasukumwa tutangaze ukuu wake na kupaaza sauti kwa shangwe kwa sifa yake. (Zab. 145:5-7) Twaonyesha kwamba sisi twahazini fursa zetu za kutolea ushahidi jina la kimungu kwa kutafuta kwa bidii njia za kueneza ujumbe wa Ufalme.—Luka 6:45.
5 Lakini je! kuna mambo mengine ambayo yatachochea ushiriki wetu wa nafsi yote katika huduma? Ikiwa ndivyo, ni yapi? Wazee, watumishi wa huduma, mapainia, na watangazaji wengine wa Ufalme wenye ujuzi waweza kusaidiaje? Miradi inatimiza sehemu gani katika kusitawisha idili? Ni manufaa zipi zinazoweza kutarajiwa? Maswali hayo na mengine yatajibiwa katika mfululizo huu wa sehemu tano, ambao utaendelezwa katika matoleo yatakayofuata ya Huduma ya Ufalme Yetu.