Utasema Nini Unaporudi?
1 Ili kuwa wenye matokeo katika huduma yetu, kutayarisha kunatakiwa ili tunaporudia wale walioonyesha kupendezwa mwanzoni, tuweze kuamsha kupendezwa kwao na kuendelea na mazungumzo yetu. Tunaweza kufanyaje hivyo?
2 Kwa kuwa Wakristo wa kweli hupendezwa na wengine kwa moyo mnyoofu, huenda kwanza ukarejezea jambo ulilojifunza kuhusu mwenye nyumba katika ziara iliyopita.
Kwa mtu aliyefunua hangaiko lake kuhusu uhalifu, ungeweza kusema:
◼ “Tulipozungumza wakati uliopita ulisema unahangaishwa na ongezeko la uasi wa sheria unaoonekana wazi. Je! unafikiri kwamba kuongeza idadi ya polisi kutasuluhisha tatizo hilo?”
Ikiwa mtu alionyesha wasiwasi juu ya matukio ya hivi karibuni katika hali ya ulimwengu, ungeweza kusema:
◼ “Mara ya mwisho tulipozungumza ulisema jambo lenye kupendeza kuhusu ukosefu wa amani ulimwenguni. Je! unafikiri kwamba viongozi wa ulimwengu wataleta utaratibu wa ulimwengu mpya?”
Kwa mtu anayetaabishwa na ubinafsi wa wengine, ungeweza kusema:
◼ “Tulipozungumza wakati uliopita ulisema jambo zuri sana kuhusu pupa tunayoona katika watu kwa ujumla. Wewe unafikiri maoni ya Mungu ni nini kuhusu watu wenye pupa? [Ruhusu itikio.] Hivi ndivyo Biblia husema kwenye Waefeso 5:5.”
3 Maelezo mengine ambayo yametumiwa kwa matokeo yanatia ndani:
◼ “Nilifurahia sana mazungumzo yetu ya wakati uliopita, kwa hiyo nilifanya utafiti wa wazo hili fupi ili nikuonyeshe jinsi Yehova hutambua shida za wasio na makao. Ona Isaya 65:21-23.”
◼ “Uliuliza swali la kupendeza juu ya kama dini zote hukubaliwa na Mungu.”
◼ “Ulinifanya nifikirie sana yale uliyosema kuhusu kuamuliwa kimbele.”
◼ “Nimekuwa nikifikiria mazungumzo yetu, na kuna jambo fulani katika kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani ambalo ninafikiri utalifurahia. [Unaweza kumwonyesha mwenye nyumba mambo yaliyoteuliwa katika kitabu.]”
Matangulizi kama hayo huonyesha kwamba tulithamini mazungumzo yetu ya wakati uliopita na kwamba tunapendezwa kuzungumza tena na mwenye nyumba.
4 Kabla ya kufanya ziara ya kurudia, fikiria yale utakayosema. Tunga utoaji wako umfae kila mtu.
5 Ikiwa mtu tunayezuru ana shughuli, bado tunaweza kuwa wenye matokeo kwa kusema:
◼ “Ninajua kwamba una dakika chache tu, lakini hapa pana jambo unaloweza kufikiria huku ukimalizia kazi yako. [Soma Mathayo 5:3.]”
Au ungeweza kusema:
◼ “Nilikuandikia maandiko haya matatu. Kwa kuwa huu si wakati mzuri wa kuzungumza, acha nikuachie, na nitakaporudi, nitataka kutumia dakika tano kuyazungumza na wewe.”
6 Njia Zisizofaa za Kuanzisha Mazungumzo Zipaswazo Kuepukwa: Maswali yanayoweza kuleta itikio lisilofaa au yanayoweza kumwaibisha mwenye nyumba huwa mara nyingi hayana matokeo mazuri. Hayo yanatia ndani: “Je! ulisoma habari niliyokuachia?” “Je! una maswali yoyote?” “Je! unanikumbuka?” “Nimerudi ili niulize kama bado unapendezwa kuzungumzia makusudi ya Mungu kwa dunia hii.”
7 Tutakuwa na hamu ya kuwarudia watu mmoja mmoja walioonyesha kupendezwa hapo mbeleni ikiwa tutatayarisha kimbele ili kuwapa msaada ambao ni wenye maana kwelikweli.