“Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1992
1 Yesu alisema wafuasi wake wangekuwa “nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14) Kwa kutofautisha, giza la ulimwengu la kiroho na kiadili linazidi kuongezeka siku baada ya siku. (Isa. 60:2; Rum. 1:21) Daraka letu tukiwa wachukuaji nuru linakuwa la maana zaidi tunapokaribia mwisho wa mfumo huu. Kwa kutambua jukumu muhimu tulilo nalo, tunatazamia kwa hamu nyingi kuhudhuria “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1992. Mkusanyiko wa kwanza kati ya mfululizo huo utaanza Ijumaa, Oktoba 30.
2 Mkusanyiko wa Siku Tatu: Mwaka huu tumepanga kuwa na jumla ya mikusanyiko 16 katika eneo letu. Programu nzima itatolewa katika Kiamhari, Kiarabu, Kiingereza, Kinyarwanda, Kiswahili, Kitigrinya na Kiganda. Programu itaanza saa 4:20 Ijumaa asubuhi na kumalizika kwa wimbo na sala saa 10:15 hivi Jumapili alasiri. Milango itafunguliwa saa 1:30 asubuhi, na hakuna atakayeruhusiwa kuingia kabla ya wakati huo isipokuwa awe amegawiwa kazi. Watu wote wa Yehova watataka kuhudhuria programu nzima. Je! umefanya uamuzi wa kibinafsi kuwapo kwa siku zote tatu? Hakikisha kusali ili kupata baraka za Yehova juu ya jitihada zako.
3 Kuanzia hotuba ya kufungua Ijumaa asubuhi hadi maelezo ya kufunga Jumapili alasiri, twapaswa tuelekeze fikira zetu zote kwenye programu nzima. Habari zenye kuchochea zitakuzwa na kutolewa kwa hotuba, maonyesho, mahoji, na drama moja. Panga kuwa umeketi mapema kabla ya programu kuanza Ijumaa. Kwa kawaida, katika siku ya kwanza wakati mwingi zaidi unahitajiwa wa kuegesha magari, kupata viti, na kadhalika. Kwa hiyo jipatie mwenyewe wakati wa kutosha. Kwa kusikiliza vipindi vyote na kubaki kwa ajili ya wimbo na sala ya kumalizia, tunapata manufaa kamili ya programu na kuonyesha uthamini wetu kwa fursa yetu ya kutumikia tukiwa wachukuaji nuru.
4 Sikio Lako na Lisikilize: Mtunga zaburi alitangaza: “Nitazitafakari shuhuda [vikumbusho, NW] zako. Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zab. 119:95b, 97) Katika kila pindi tukutanapo ili kuagizwa na Yehova, kuna uhitaji wa kutoa uangalifu na kusikiliza si kwa masikio yetu tu bali pia kwa moyo wetu. Hata hivyo, uhitaji wa hilo ni mkubwa zaidi, tunapohudhuria vikusanyiko vikubwa kama vile mkusanyiko wa wilaya. Kuna mengi ya macho kuona na masikio kusikia. Ingekuwa hasara iliyoje kwetu binafsi ikiwa tungetoa wakati na fedha kuhudhuria mkusanyiko na kurudi nyumbani tukiwa twakumbuka kidogo mambo yale madogo-madogo juu ya jinsi tunavyoweza kufanya maendeleo tukiwa wachukuaji nuru! Ni lazima tufanye yote tuwezayo kukinza vikengeusha fikira vyovyote ikiwa tutanufaika kikamili na programu. Tunaweza kuhakikishaje kwamba habari hiyo itakazwa kikiki moyoni na akilini mwetu kwenye umalizio wa programu ya mkusanyiko?
5 Kusikiliza ni ustadi ambao ni lazima usitawishwe na kuzoewa. Neno “sikiliza” humaanisha “kusikia kwa uangalifu wenye fikira.” Fikiria madokezo haya machache: (1) Tia kila jitihada kuwasili kwenye mahali pa mkusanyiko ukiwa umepumzika vya kutosha kila asubuhi. Hilo litataka mpango na ushirikiano wa familia. Ikiwa umechoka kwa sababu ya kukosa usingizi au una njaa kwa sababu hukula kiamshakinywa, au ikiwa neva zako si tulivu kwa sababu ya kulazimika kwenda haraka-haraka, utanufaika kidogo na programu. (2) Sitawisha mtazamio kuhusu jinsi kichwa kitakavyokuzwa. Majuma kadhaa kabla ya mkusanyiko, likiwa sehemu ya funzo lenu la familia, kwa nini kila mshiriki asieleze yale yanayomaanishwa na kuwa mchukuaji nuru. Mkiwa kwenye mkusanyiko, pitieni kila sehemu ya siku hiyo kabla ya programu kuanza. (3) Vaa ifaavyo, na uepuke kula na kunywa wakati wa vipindi. Wachache wameonekana kwenye majumba au stediamu katika sehemu za kukaliwa wakila au kunywa wakati wa programu. Hilo ni jambo la kukosa staha, hukengeusha fikira za wengine, na huonyesha kukosa kujidhibiti.—Ona Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1991, kurasa 8-18.
6 Tunataka tutoe uangalifu wa kipekee kwenye jambo la kuandika habari. Kukifanywa ifaavyo, kutakusaidia kufuatana na wasemaji kwa uangalifu zaidi na kukumbuka yale unayosikia. Kwa kuwa sisi hufikiri mara nne upesi zaidi ya vile tunavyosema, njia bora zaidi ya kuzuia kutangatanga kwa akili ni kuandika habari. Kama vile mwandikaji mmoja alivyoonelea, “Mara nyingi kusikiliza hotuba huwa kugumu kuliko kutoa hotuba.” Huenda ukakumbuka kwamba inasemekana Wakristo wa mapema walichukua vigae kwenda mikutanoni na kuandika maandiko juu yavyo kwa wino. Ni shukrani, kijitabu kidogo cha kuandikia na kalamu ya wino au penseli inatufaa sana. Kuwa wastadi katika kuandika habari humaanisha kuandika mambo ya kutosha tu ili kupata wazo kuu bali si kuandika mambo mengi sana hivi kwamba wakati wote twawa tunaandika. Hilo halingetimiza kusudi letu na lingetufanya tukose mambo ya maana yanayosemwa na msemaji. Andika maneno makuu, na kutumia vifupisho vya maneno. Maandishi yako yatakusaidia sana ikiwa unayapitia jioni hiyo na tena kabla ya mazungumzo ya mambo makuu ya programu katika Mkutano wa Utumishi kundini.
7 Wimbo na Sala Yenye Kuhisiwa Moyoni: Kumwimbia Yehova sifa na kumfikia kwa sala yenye kicho ni sehemu muhimu za ibada yetu. (2 Nya. 30:21, 27) Hizo ni sehemu za maana za mkusanyiko ambazo sote tunaweza kushiriki. Katika siku tatu za “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya wetu, tutaimba nyimbo 18 za sifa kwa Yehova na tuunganike katika sala nane kwa Baba yetu wa kimbingu. Kwa kweli hayo ni mapendeleo yasiyo na kifani. Yehova atatupa zaidi ya saa 12 za elimu na mazoezi ya kiroho. Wakati wa dakika chache zilizotengwa kwa ajili ya wimbo na sala, tunamshukuru Yehova kwa zawadi zake za ukarimu na kumsifu. Kwa kuwa tunakuja mbele za Yehova katika sala tukiwa kikundi kilichokutanika, je! tungependa yeye atuone kuwa watu wachoyo na wasio na shukrani kwa sababu tulishindwa kujiunga katika wimbo na sala kwa sababu tu ya mipango mibaya? Tena, ugavi wa fasihi mwaka huu utakuwa mwingi kwenye kila mkusanyiko, kwa hiyo wale ambao kwa kufaa watabaki kwenye viti hadi kipindi kinapokamilika hawatakosa kuvipata. Vivyo hivyo, hakuna mtu anayepaswa kuondoka kabla ya kumalizika kwa kipindi ili akapange mstari kwa ajili ya chakula kabla ya wengine.—Mt. 7:12; Rum. 12:10; Flp. 2:1-4.
8 Ili kuwawezesha mjizoeze nyimbo kimbele kusudi mwe na ushiriki kamili katika kumwimbia Yehova sifa wakati wa mkusanyiko, ifuatayo ni orodha ya nyimbo zilizoteuliwa kwa ajili ya programu: 33, 91, 111, 38, 221, 217, 43, 128, 152, 177, 207, 201, 35, 89, 50, 168, 42, na 45.
9 Fanya Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu: Kila mwaka tunapewa vikumbusho vya fadhili kuhusu umaana wa tabia njema na mwenendo unaofaa kwenye mkusanyiko. Walio wengi wanastahili pongezi kwa kutii vikumbusho hivyo kwa kudhamiria. Mfumo huu unapokaribia kwisha, tunazidi kulazimika kuwa katika ushirikiano na watu kazini na shuleni ambao mwenendo wao ni kama ule uliotabiriwa kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Ushirika huo waweza kuwa na uvutano mbaya juu yetu ikiwa hatuendelei kujikinga wenyewe. Hatutaki kamwe kumpa yeyote sababu ya ‘kutusingizia kuwa watenda mabaya.’ (1 Pet. 2:12) Hilo lataka kwamba tutoe uangalifu unaopita ule wa kawaida kwa utu wetu wa Kikristo. Wote wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu mwenendo wao kwenye mkusanyiko na kwingineko katika mahali pa umma, kama vile kwenye malojing’i na mikahawa. Wazee wanapendezwa na ndugu zao wote. (Flp. 2:4) Wanapaswa wawe wenye msaada na wapongeze wengine kwa mwenendo wao mzuri. Wazee wanapaswa pia wajihisi huru kutoa shauri lenye upendo ikiwa linahitajiwa, hata ingawa hawamjui ndugu au dada huyo kibinafsi. Matatizo yoyote makubwa yanayoonwa yapaswa kuripotiwa kwenye Ofisi ya Usimamizi kwenye mkusanyiko.
10 Tunahitaji kukumbuka nini? Wafanyakazi wa lojing’i wanapaswa kutendewa kwa adabu na staha. Idara ya Mahali pa Kulala imefanya kazi kwa bidii ili kupata mahali pa kulala penye bei ya chini kuliko ile ya kawaida. Ikiwa tunadai mno au kuacha mahali hapo pakiwa katika hali isiyopendeza, huenda wasimamizi wasikubali kuwa na Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya mikusanyiko ya wakati ujao. Baadhi yetu bado wanahitaji kukumbushwa juu ya hilo. Ni wachache tu ndio huharibu sifa ya walio wengi.
11 Utu mpya unaotajwa kwenye Waefeso 4:24 unafananishwa na vazi ambalo mtu huvaa baada ya kuondolea mbali utu wa kale. Badiliko hilo la utu lapaswa lionyeshwe katika mavazi yetu halisi pia. Baadhi ya akina ndugu na dada, hasa wachanga, wameonwa wakivaa kizembe sana, hata kwa kukosa kiasi nyakati nyingine. Wengine hutoa viatu vyao na kuweka miguu yao juu ya viti vilivyoko mbele yao au wanatembea wakiwa na soksi. Je! sisi hujiendesha hivyo kwenye Majumba ya Ufalme? Pia, baadhi ya wenye kubatizwa wamevaa T-shati zenye shime na maneno ya kilimwengu au zenye maandishi yanayotangaza bidhaa mbalimbali. Wazee wanaopitia maswali pamoja na wale wanaojitayarisha kubatizwa wanapaswa wahakikishe kwamba wale watakaobatizwa wanaelewa yale ambayo yangeonwa kuwa mavazi yanayofaa kwa ajili ya pindi hiyo.—Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Juni 1, 1985, ukurasa 30, na Machi 15, 1974, ukurasa 143 au (w73-E 4/15, kur. 254-5).
12 Vifaa vya Kurekodia: Ingawa kamera za video zinakubaliwa, tunawahimiza wale wanaozitumia wawafikirie wengine, wawe wateuzi wa yale wanayonasa, na kuwa wenye staha kwa wale ambao huenda wasitake kupigwa picha wakila, wakisikiliza programu, au wakati wa sala. Yeyote anayerekodi kwa video au kwa kaseti apaswa aepuke kukengeusha wasikilizaji au kuzusha makelele. Hakuna ubaya kurekodi baadhi ya programu ukiwa umeketi. Lakini wakati wa vipindi, haingefaa kwa yeyote kuzurura huku na huku kwenye vijia na mbele ya wasikilizaji, akinasa programu. Ikiwa inahitajika, wakaribishaji wazungumze na wowote wanaoshindwa kuonyesha upendo wa kidugu kwa habari hii. Tafadhali kumbukeni kwamba kamera au vifaa vya kurekodia havipaswi kuunganishwa na mfumo wa umeme au wa sauti kwenye mkusanyiko, wala vifaa vyovyote havipaswi kuwekwa kwenye vijia au mahali pa watu kupitia.
13 Kwa Wazazi: Tungependa tena tukazie umaana wa wazazi kuwaangalia watoto wao nyakati zote, iwe ndani ya mahali pa mkusanyiko au katika lojing’i. (Mit. 29:15b; Lk. 2:48) Programu inapokuwa ikiendelea, hakikisha kwamba watoto wako wanasikiliza na kuandika habari. Wakati wa pumziko kuna fursa ya kuzuru marafiki wa makundi mengine.
14 Ili kutoa kielezi cha umaana wa kujua waliko watoto wako nyakati zote, dereva wa teksi katika jiji moja la mkusanyiko aliripoti kwa ndugu mmoja kwamba alibeba wasichana wawili wachanga kutoka mahali pa mkusanyiko. Kwa wazi walikuwa wanapanga kutokuwapo alasiri nzima na wakamwambia dereva kwamba mama yao hangewakosa hadi saa 11 jioni. Dereva huyo wa teksi aliona wasiwasi kuhusu hali njema yao, lakini namna gani mama yao? Ungekuwa msiba ulioje ikiwa jambo baya lingewapata, na kuleta suto kwa jina la Mungu na watu wake!
15 Ushirikiano wenu unaombwa kwa habari ya kuhifadhi viti. Tafadhali kumbukeni kwamba VITI VINAWEZA KUHIFADHIWA TU KWA WASHIRIKI WA KARIBU WA FAMILIA YAKO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Sehemu za pekee kama zinavyohitajiwa kwa ajili ya walio wazee-wazee na wasiojiweza zitapatikana kwenye mikusanyiko yote. Tunawauliza wote tafadhali wasome ishara kwa uangalifu na kufuata mielekezo ya wakaribishaji. Baadhi ya ndugu wenye umri mkubwa wamelazimika kutafuta viti katika sehemu zisizofikiwa kwa urahisi kwa sababu wachanga walijaza viti katika sehemu ya wazee-wazee. Tafadhali fikirieni wazee-wazee. Tunasikitika kwamba haiwezekani kushughulikia maombi ya kupata sehemu au vyumba vya pekee kwa wale wenye matatizo kama vile mizio (allergies).
16 Inadokezwa kwamba vitu vya kibinafsi unavyoleta kwenye mkusanyiko viwe vichache kadiri iwezekanavyo. Ikiwa kifaa hakitoshei chini ya kiti chako, huenda ikawa afadhali kukiacha nyumbani. Vifaa vikubwa vya kuhifadhi baridi ya chakula haviruhusiwi katika vijia kwa sababu ya usalama, na ikiwa vinawekwa juu ya kiti kando yako, mtu fulani huenda akakosa kiti.
17 Utumishi wa Fasihi na Chakula: Inaelekea kwamba Idara ya Fasihi kwenye kila mkusanyiko itakuwa na hesabu fulani ya vichapo vya zamani, kama vile Vitabu-Mwaka mbalimbali, ambavyo unaweza kupata kwa ajili ya maktaba yako binafsi.
18 Mpango wa utumishi wa chakula ulio sahili umepangwa tena kwa ajili ya mwaka huu. Hilo hupunguza sana kazi na huruhusu uangalifu zaidi utolewe kwa mambo ya kiroho ya mkusanyiko, huku wafanyakazi wakiweza kufurahia zaidi programu. (Kut. 12:16b; Kum. 31:12; it Buku 1 kur. 503-4, 821; linganisha Luka 10:38-42.) Orodha ya chakula inaandaa ulishaji unaofaa kwa ajili ya vipindi vya asubuhi na adhuhuri. (Linganisha Mathayo 14:14-20.) Kwa milo ya jioni, kila mtu yuko huru kufanya mipango yake mwenyewe. Inaelekea kwamba mlo wa jioni wenye joto utaandaliwa karibu saa moja baada ya mwisho wa kipindi kwa wale wanaolala kwenye mahali pa mkusanyiko.
19 Sosaiti huthamini sana utegemezo mzuri ambao nyinyi ndugu na dada mmekuwa mkitoa kwa mipango ya utumishi wa chakula kwenye mikusanyiko ya wilaya kwa muda wa miaka mingi. Hilo limefanya iwezekane kupata vifaa vizuri vya kukodi na kushughulikia gharama za mkusanyiko. Pia imewawezesha mbaki katika mahali pa mkusanyiko wakati wa pumziko fupi la mchana ili mwepo, bila kuchelewa na mkiwa mmeburudishwa, kwa ajili ya programu ya kiroho iliyo ya muhimu zaidi.
20 Watu wa Yehova huthamini kuweza kukutana pamoja kwenye vifaa vizuri ili kunufaishwa na programu ya kiroho iliyotayarishwa. Tunathamini pia utumishi mwingi na usaidizi mwingine unaotolewa katika vikusanyiko hivyo. Kwa uangalifu mwingi na kwa gharama kubwa kwa Sosaiti, mipango hufanywa kwa ajili ya viti vya kutosha, kuweka mifumo ya sauti yenye gharama sana, kuendesha Idara ya Utumishi wa Chakula yenye mafanikio, na hesabu fulani ya utumishi mbalimbali ambao hufanya kuhudhuria mkusanyiko kuwe jambo la kuonewa shangwe na lenye kuburudisha kiroho.
21 Hudhuria “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya: Kwa kuhudhuria “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya, tutasisimuliwa kusikia kwa nini kuwa wachukuaji nuru ni heshima na pendeleo kubwa. Pia tutakumbushwa kwamba hilo ni daraka zito. Kwa kutoa uangalifu unaopita ule wa kawaida kwa mambo tunayosikia kwenye mkusanyiko, tutafanyia maendeleo stadi zetu na pia uthamini wetu wa daraka letu tukiwa wachukuaji nuru. Fanya mipango yako sasa ili uwepo wakati wa vipindi vyote, kuanzia wimbo wa kufungua siku ya Ijumaa mpaka sala ya kumalizia Jumapili alasiri.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Vikumbusho vya Mkusanyiko wa Wilaya
Mahali pa Kulala: Mipango kwa mwaka huu, kwa sehemu iliyo kubwa, itafuata kigezo cha miaka iliyotangulia. Mikusanyiko iliyo mingi hutumia vyumba vya kulala au vifaa vilivyo mahali pa mkusanyiko ili wote wanaohudhuria wapate mahali pa kulala. Huenda kukawa na mahali pa kulala katika nyumba za watu binafsi. Hata hivyo, tafadhali kumbukeni kwamba, si jambo linalofaa wajumbe watumie vibaya ukaribishaji-wageni wa ndugu zao kwa kutazamia wapewe mahali pa kulala siku za ziada ili waweze kuzuru sehemu fulani wakati wa likizo au kufanya mambo mengine kabla au baada ya mkusanyiko. Vyumba hivi ni kwa ajili ya wakati wa mkusanyiko tu. Wale wanaopata mahali kama hapo pa kulala wahakikishe kwamba wao na watoto wao wanatenda kwa njia yenye staha kuelekea nyumba ya mkaribishaji wao na wasiharibu kitu chochote au kupekua-pekua mali au sehemu za faragha za nyumba hiyo. Wenye nyumba wakiwa na matatizo yoyote kuhusiana na jambo hili wanapaswa kujulisha Idara ya Mahali pa Kulala mara moja kwenye mkusanyiko, na ndugu waliopo watafurahi kusaidia. Mnaweza kupeleka fomu ya maombi ya mahali pa kulala iliyojazwa kupitia mratibu wa mkusanyiko katika kundi lenu.
Ubatizo: Wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa kuwa kwenye viti vyao katika sehemu iliyoonyeshwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Mavazi yenye kiasi na taulo yapasa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Akina dada hasa watataka kuchunguza kimbele waone kama mavazi wanayopanga kuvaa yanaonyesha uchi yanapolowa maji. (Ona Huduma ya Ufalme Yetu, Novemba 1987, ukurasa 3, fungu 6.) Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na msemaji, mwenyekiti wa kipindi hicho atawatolea watakaobatizwa maagizo mafupi kisha ataomba wimbo uimbwe. Baada ya mstari wa mwisho, wakaribishaji watawaelekeza wanaotaka kubatizwa kwenye mahali pa uzamisho au kwenye magari yatakayowapeleka hapo. Kwa kuwa ubatizo kwa kufananisha kujiweka wakfu kwa mtu ni jambo la siri na la kibinafsi kati ya mtu na Yehova, hakuna uandalizi kwa ule unaoitwa eti ubatizo wa shirika ambao watu wawili au zaidi wanaotaka kubatizwa wanakumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
Kitambulisho cha Mapainia: Mapainia wote wa kawaida na wa pekee, na waangalizi wasafirio pia watahitaji kuleta kadi yao ya Kitambulisho na Mgawo kwenye mkusanyiko. Mapainia ambao watakuwa wamekuwa kwenye orodha kwa miezi sita tangu waanze upainia wakati wa mkusanyiko wa wilaya wanaouhudhuria wanaweza kupokea tikiti za chakula za mkusanyiko wakionyesha Kitambulisho chao kwenye mkusanyiko mmoja tu. Hivyo, tunza kadi hiyo kwa uangalifu kama vile ungetunza pesa. Huwezi kupata nyingine kwenye mkusanyiko. Vichapo vyovyote vitakavyotolewa kama zawadi au vingine kwa bei ya painia vitapatikana kwa mapainia katika chumba cha vitabu, kwa kuonyesha tu Kitambulisho chao. Wale walio katika utumishi wa Betheli wanaweza kupokea maandalizi yayo hayo kwa kuonyesha Kitambulisho chao cha Betheli.
Utumishi wa Kujitolea: Msaada wa kujitolea unahitajiwa ili mkusanyiko wa wilaya uendeshwe vizuri. Hata ikiwa unaweza kufanya kazi kwa sehemu fulani tu ya mkusanyiko, utumishi wako utathaminiwa. Ikiwa unaweza kusaidia, tafadhali piga ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea unapowasili kwenye mkusanyiko. Watoto wa umri ulio chini ya miaka 16 waweza kuchangia pia kufanikiwa kwa mkusanyiko, lakini wanatakwa wafanye kazi pamoja na mzazi au mtu mwingine mzima anayeweza kuchukua daraka.
Kadi za Beji: Tafahali vaa kadi ya beji iliyofanyizwa kipekee kwenye mkusanyiko na pia unaposafiri kwenda na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hii hutuwezesha tutoe ushahidi mzuri tunaposafiri. Unapaswa upokee kadi ya beji kupitia kundi lako kwa sababu hazitapatikana kwenye mikusanyiko.
Maneno ya Tahadhari: Hata uwe unaegesha wapi, funga gari lako nyakati zote na usiache ndani kamwe kitu chochote kinachoonekana. Fungia mizigo yako katika mahali pa mizigo, ikiwezekana. Pia, ujilinde dhidi ya wevi na wakwepuzi wa mifuko wanaovutiwa na vikusanyiko vikubwa. Hii inatia ndani kutoacha kitu chochote chenye thamani bila mtu wa kukitunza katika viti kwenye mikusanyiko.
Uangalifu unapaswa pia utolewe ili kuepuka kupakia watu wengi kupita kiasi katika magari yaliyokodiwa au kupangwa na kundi kwa ajili ya usafiri wa kwenda mkusanyikoni. Ni afadhali kupanga kutumia fedha za ziada katika gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au lililo baya hata zaidi kuwahatarisha akina ndugu wapatwe na aksidenti na hata uwezekano wa kupoteza uhai kwa sababu ya kupakia watu wengi kupita kiasi au kumtia shime dereva aongeze mwendo ili mfike mapema zaidi mnakoenda. (Rum. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Ndugu wenye daraka wanaosafiri katika magari kama hayo wajihisi huru kutoa ushauri wenye upendo kuhusu jambo hilo ikiwa inahitajika.