Uwe Mwenye Kubadilikana Katika Huduma Yako
1 Imesemwa kuwa unamna-namna ni kiungo cha uhai. Kwa kawaida mfikio tofauti wa jambo fulani waweza kulifanya liwe lenye kupendeza zaidi. Hilo ni kweli kuhusu huduma yetu. Ikiwa sisi si waangalifu, utoaji wetu wa mlango kwa mlango waweza kuwa usiobadilika. Kurudia-rudia utangulizi uleule tena na tena kwaweza kutuchokesha sisi na wenye nyumba pia. Kwa hiyo, uwe mwenye kubadilikana katika huduma yako. Lakini waweza kutimizaje hilo?
2 Badala ya kusema, ‘Habari ya asubuhi. Tunawazuru majirani wetu tukiwa na habari njema za Ufalme,’ kwa nini usifikirie njia za kutofautisha maneno yako ya kuanzia? Kitabu Kutoa Sababu kina wingi wa habari kuhusu tangulizi mbalimbali. Kuna tangulizi mbalimbali kwa vichwa tofauti-tofauti 18 katika kurasa 9-15. Na kuna tangulizi mbili au tatu au zaidi kwa vichwa vingi.
3 Ikiwa unatumia broshua “Je! Kweli Mungu Anatujali?,” utangulizi huu kutoka sehemu ya “Maisha/Furaha” kwenye ukurasa 11 huenda ukawa msaada:
◼ “Tunaongea na watu wanaohangaikia kwelikweli ubora wa maisha leo. Wengi wanataka kujua, Je! inawezekana kuwa na maisha ya furaha kwelikweli? Broshua hii yaandaa maoni yenye kutia moyo na yenye kuchochea mawazo.” Fungua broshua ukurasa wa 25, na usome jambo mmoja au mawili kutoka mafungu 15 na 16.
4 Baadhi ya wahubiri wa Ufalme—wachanga na hasa wapya, lakini wa zamani pia—wameona kwamba mfikio wenye kupendeza milangoni waweza kufanywa kwa kutumia trakti.
Mhubiri mchanga huenda akatumia trakti “Furahia Maisha ya Familia” na kusema:
◼ “Nina habari fupi ya kukueleza kuhusu jinsi Mungu anavyoweza kuziunganisha familia pamoja kwa furaha. Ningependa kukupa trakti hii yenye kichwa Furahia Maisha ya Familia.” Kufikia hapo mhubiri mwenye umri mkubwa anayefanya na kijana huyo mkubwa aweza kuamua ama kuongezea mawazo mengine au maelezo, ikitegemea itikio la mwenye nyumba.
5 Ikiwa mwenye nyumba aonyesha kupendezwa, mhubiri mwenye umri mkubwa aweza kusema:
◼ “Biblia huandaa fundisho juu ya daraka linalofaa la mume, mke, na watoto ndani ya mpango wa familia. Kwa kuwa Mungu ndiye Mwanzilishi wa familia, je! hutakubali kwamba ndiye anayeweza kutuambia jinsi familia inapasa kuwa? Ningependa kusikia maoni yako juu ya shauri lililo wazi la Biblia kwa washiriki wa familia.” Halafu soma Waefeso 5:22, 23, 28-31.
6 Ukitoa kitabu Upeo wa Ufunuo, kwa nini usionyeshe maoni chanya ya wakati ujao yanayoonyeshwa kwenye Ufunuo 21:3, 4? Halafu soma fungu la 7 katika ukurasa 303 wa kitabu hicho. Mwulize mwenye nyumba ikiwa ni jambo halisi kuamini kwamba Mungu atatimiza ahadi hizo. Mazungumzo mafupi ya unabii wa Biblia ambao tayari umetimia yapaswa kutia nguvu uhakika wa mwenye nyumba katika uwezo wa Mungu wa kubariki jamii ya kibinadamu.
7 Wapiga mbiu wote wa Ufalme wataka kushiriki katika kusogeza mbele masilahi ya kitheokrasi, wakipanda mbegu za kweli inapowezekana na kufuatia kupendezwa kunakoonyeshwa. Tukiwa tumefanya sehemu yetu, tunaweza kwa furaha kuacha ukuzi wowote wa wakati ujao mikononi mwa Yehova. Tuna habari njema zaidi za kushiriki na jirani zetu. Tukiwa tumejitayarisha sikuzote, twaweza kuwa wenye kubadilikana katika kutoa ujumbe wa Ufalme na katika kutoa vichapo vyetu.