Saidia Wanafunzi wa Biblia Wajitayarishe Kwa Ajili ya Funzo Lao
1 Wanafunzi wa Biblia wanaojitayarisha kwa ajili ya funzo lao kila juma huonyesha kupendezwa kikweli katika funzo hilo na mara nyingi hufanya maendeleo ya haraka zaidi ya kiroho kuliko wale wasiojitayarisha. Nyakati nyingine huenda mwanafunzi asijitayarishe kwa sababu yeye hajui jinsi ya kufanya hivyo. Huenda ikahitajiwa kumfundisha jinsi ya kutayarisha. Hilo laweza kufanywaje?
2 Tangu mwanzo wenyewe, chukua wakati kidogo kuhakikisha mwanafunzi aelewa kwamba kutayarisha hutia ndani funzo la kibinafsi. Ingawa watu wengi waweza kusoma, wao hawajafundishwa jinsi ya kujifunza. Kurasa 33-43 za kitabu Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huandaa madokezo mengi yenye kusaidia ambayo huenda ukaweza kupitisha kwa mwanafunzi kadiri yahitajiwavyo.
3 Onyesha Mwanafunzi Manufaa ya Kujifunza: Huenda ukamwonyesha mwanafunzi kitabu chako cha funzo ambacho umetia alama ndani au umepiga mstari maneno na mafungu ya maneno makuu. Mwache aone jinsi ambavyo kutupia jicho sehemu zilizotiwa alama kwaweza kumkumbusha mawazo akatayoweza kueleza katika maneno yake mwenyewe. Hivyo yeye hatashawishwa kusoma sehemu nzima-nzima kutoka kwa kitabu anapojibu maswali. Kufikia hatua hii, mazoezi yafaayo yatamsaidia baadaye kutoa maelezo yenye maana katika mikutano ya kutaniko. Maelezo yake yataonyesha uthamini wa habari inayozungumzwa na yaonyeshe kina cha uelewevu wake.
4 Mfundishe Kutumia Biblia: Mwanafunzi huyo ahitaji kujifunza jinsi ya kupata maandiko yaliyorejezewa katika habari ya funzo. Awezapo kufanya hivyo bila shida, yeye atathamini kwa ukamili zaidi kwamba kwa kweli yeye ni mwanafunzi wa Biblia. Ingawa huenda mwanzoni akahitaji kutumia orodha ya vitabu vya Biblia iliyo upande wa mbele wa Biblia, mwanafunzi huyo apaswa atiwe moyo kufahamiana na mfuatano wa vitabu 66 vya Biblia. Afunguapo na kusoma andiko, msaidie kutambua ile sehemu inayotegemeza jambo kuu linalotokezwa katika fungu linalozungumziwa na asikengeushwe na sehemu ambazo hazihusiani moja kwa moja na funzo la sasa.
5 Mwanafunzi afanyapo maendeleo, mtie moyo kusoma Biblia kuanzia mwanzo hadi mwisho. Kazia kwamba Biblia nzima ni Neno la Mungu lililopuliziwa na kwamba ni lazima Wakristo wa kweli walishwe nalo.—Mt. 4:4; 2 Tim. 3:16, 17.
6 Mjulishe juu ya Marejezeo Mengineyo ya Kitheokrasi: Mwanafunzi anapokuwa amefanya maendeleo ya kutosha, yeye aweza kuanza kutumia marejezeo mengineyo ya kitheokrasi. Kwa utambuzi, mtie moyo atafute habari zaidi katika vichapo vya Sosaiti atakavyofahamiana navyo ahudhuriapo mikutano ya kutaniko. Mfundishe jinsi ya kutumia sehemu za pekee za New World Translation, kama vile “Maneno ya Biblia Yaliyofarisiwa.” Yeye aanzapo kujenga maktaba yake mwenyewe ya kitheokrasi, mwonyeshe jinsi ya kutumia vitabu Comprehensive Concordance, Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Index, na mabuku ya Insight.
7 Tukiwafundisha wanafunzi wa Biblia jinsi ya kujitayarisha kwa ajili ya funzo lao la Biblia, tutawasaidia kuendelea kufanya maendeleo katika kweli wakiwa wanafunzi wa Biblia wenye uwezo hata baada ya funzo lao la Biblia nyumbani la kibinafsi kwisha.