Onyesha Uthamini kwa Nyumba ya Mungu
1 Katika nyakati za Biblia Yehova aliamuru watu wake wakusanyike pamoja kwa ukawaida katika nyumba yake. (Law. 23:2) Mikusanyiko hii iliwasaidia kuweka akili zao kwa neno la Mungu, ikiandaa wakati wa kutafakari, ushirika, na mazungumzo ya Sheria ya Yehova. Akili zao zilijawa na mawazo ya Mungu, yaliyoleta baraka nyingi za kiroho. Kwa kweli hivi vilikuwa vipindi vyenye furaha. Mpango huo uliendeleza ibada yenye muungano na iliyo safi. Mikusanyiko katika nyumba ya Mungu leo ni ya maana vilevile.
2 Twaweza Kuonyeshaje Tunathamini Mikutano? Makutaniko fulani huripoti hudhurio la chini la mikutano. Pindi kwa pindi hali ya mtu yaweza kumzuia asihudhurie mkutano. Lakini je, umeruhusu matatizo yaonekanayo kuwa madogo yavuruge hudhurio la kawaida la mikutano? Watu fulani huenda wakaamua kukaa nyumbani ikiwa wanaumwa kidogo tu na kichwa au wanahisi wamechoka baada ya siku yenye shughuli. Wengine wamehisi kuwajibika kuwapendeza watu wa ukoo wasioamini wanaotaka kuwatembelea. Watu fulani hata wamekosa mikutano ili watazame kipindi wakipendacho zaidi cha televisheni au tukio fulani la michezo. Kiwango cha uthamini kinachoonyeshwa katika hali hizi kwa wazi si sawa na tamaa iliyohisiwa moyoni iliyoonyeshwa na wana wa Kora: “Nafsi yangu imezionea shauku nyua za BWANA.”—Zab. 84:2.
3 Ingawa kuna wingi wa chakula cha kiroho kilichoandaliwa mikutanoni, wengine wanaohudhuria wana ugumu wa kukaza uangalifu. Huenda wakajipata wakiota ndoto za mchana, wakifikiria mahangaiko ya siku, au hata wakisinzia. Wengi wameona kwamba kuandika maandishi mafupi huwasaidia wawe chonjo na kukazia fikira yanayosemwa. Kuandika mambo pia hukaza habari hiyo kwenye akili. Kwa kuongezea, kujitayarisha mapema ni msaada wa kunufaika kikamili. Tukitayarisha vizuri, tutaweza “kuzingatia kwa makini zaidi.”—Ebr. 2:1, Habari Njema kwa Watu Wote.
4 Watoto vilevile na watu wazima wanahitaji kuyashika maagizo yanayoandaliwa mikutanoni. Yale watoto wajifunzayo yatakuwa ya kadiri ndogo sana ikiwa wazazi wanawapa watoto vitu vya kuchezea au vitabu vya kuchorea ili wawe na shughuli na wanyamaze. Kuna ukosefu wa nidhamu ifaayo watoto wanaporuhusiwa kucheza, kuzungumza, kulia, au kufanya mambo mengine yanayosumbua wale wanaoketi karibu. Ziara za kila mara na zisizo za lazima msalani au kunywa maji wakati wa mikutano mara nyingi hupunguka mtoto ajuapo kwamba mmoja wa wazazi wake ataandamana naye sikuzote.
5 Kuwahi Ni Muhimu: Pindi kwa pindi, hali zisizoepukika huenda zituzuie kufika mkutanoni kwa wakati, lakini kwa kuzoea kufika tukiwa tumechelewa baada ya wimbo na sala ya kufungua huonyesha ukosefu wa heshima kwa kusudi takatifu la mikutano na daraka letu la kuepuka kusumbua wengine. Kumbuka kwamba kuimba na kusali pamoja na ndugu zetu kwenye mikutano ya kutaniko ni sehemu ya ibada yetu. Zoea la kuchelewa mara nyingi huwa tokeo la mpango mbaya au kushindwa kupanga mapema. Kuwahi huonyesha kwamba twaheshimu na kuthamini mikutano yetu.
6 Kadiri siku ile ikaribiapo zaidi, uhitaji wa kukusanyika pamoja wawa mkubwa zaidi. (Ebr. 10:24, 25) Na tuonyeshe uthamini wetu kwa kuhudhuria kwa ukawaida, kutayarisha mapema, kuwahi, kusikiliza kwa makini, na kisha kutumia yale tunayojifunza.