Kigezo cha Kufuata kwa Ukaribu
1 Pasipo na shaka Yesu ndiye aliyekuwa yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Yeye aliweka kielelezo kikamilifu kwa wanafunzi wake. Ingawa hatuwezi kufikia kiwango chake cha ukamilifu, twasihiwa ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Pet. 2:21, NW) Twapaswa kutamani kuwa kama Yesu kwa kadiri iwezekanavyo, tukishiriki kweli pamoja na wengine kwa bidii.
2 Yesu alikuwa zaidi ya mhubiri; yeye alikuwa mwalimu bora zaidi. “Makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake.” (Mt. 7:28) Kwa nini alikuwa mwenye matokeo sana hivyo? Acheni tuangalie sana ‘njia yake ya kufundisha.’
3 Jinsi Tunavyoweza Kumfuata Yesu: Yesu alikuwa amefundishwa na Baba yake. (Yn. 8:28) Nia yake ilikuwa kumheshimu Yehova na kutukuza jina Lake. (Yn. 17:4, 26) Katika kuhubiri na kufundisha kwetu, nia yetu yapasa kuwa pia kumheshimu Yehova na si kuvuta uangalifu kwetu wenyewe.
4 Kila kitu alichofundisha Yesu kilitegemea Neno la Mungu. Kwa kuendelea alirejezea yaliyoandikwa katika Maandiko yaliyopuliziwa. (Mt. 4:4, 7; 19:4; 22:31) Twataka kuelekeza wasikilizaji wetu kwenye Biblia; hivyo twawaacha waone kwamba yale tuhubiriyo na kufundisha yategemea mamlaka iliyo kuu zaidi.
5 Yesu alitumia maelezo mafupi, yenye kutumika, na yasiyo magumu. Kwa kielelezo, katika kueleza jinsi tunavyoweza kupata msamaha wa Mungu, alitutia moyo tuwe tukisamehe wengine. (Mt. 6:14, 15) Twapaswa kujaribu kueleza ujumbe wa Ufalme katika misemo sahili, ya unyenyekevu.
6 Kwa ustadi Yesu alitumia vielezi na maswali ili kuamsha kufikiri kwa wengine. (Mt. 13:34, 35; 22:20-22) Vielezi juu ya mambo ya kawaida, ya kila siku vyaweza kusaidia watu waelewe mafundisho ya Biblia yaliyo magumu. Twapaswa kuuliza maswali ambayo hutia moyo wasikilizaji wetu wafikiri juu ya yale wasikiayo. Maswali yenye kuongoza yanaweza kuwasaidia wafikie mikataa ifaayo.
7 Yesu alitumia wakati kueleza mambo magumu kwa wale waliouliza ili wapate habari zaidi. Wale waliopendezwa kikweli, kama vile wanafunzi wake, waliweza kupata maana ya yale aliyofundisha Yesu. (Mt. 13:36) Sisi pia twapaswa kuwa wenye kusaidia maswali yaulizwapo kwa unyoofu. Ikiwa hatujui majibu, twaweza kufanya utafiti juu ya jambo hilo na kurudi tukiwa na habari baadaye.
8 Yesu alitumia masomo ya vitu ili kufundisha. Kielelezo cha hili kilikuwa kuosha miguu ya wanafunzi wake, hata ingawa alikuwa Bwana-Mkubwa wao. (Yn. 13:2-16) Tukionyesha roho ya unyenyekevu, wale wanaofundishwa watahamasishwa kutumia yale wanayojifunza.
9 Yesu alivutia mioyo ya watu na upendo wao wa uadilifu. Twataka kufikia mioyo pia. Twajaribu kuvutia tamaa ya asili ya wanadamu ya kumwabudu mtu mkuu zaidi na kuishi pamoja na wengine kwa amani na furaha.
10 Wakati wa Desemba twaweza kushiriki na wengine mambo ambayo tumejifunza kuhusu Yesu kwa kutoa kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Kuiga kwetu sifa za kufundisha za Yesu huenda kukahamasisha wanyoofu wasikilize tuelezapo aliyofundisha.—Mt. 10:40.