‘Fuata Hatua Zake kwa Ukaribu’
1. Tunahitaji kufanya nini ili tuwe wahudumu wenye matokeo?
1 Yesu hakuelimishwa katika shule za kirabi, lakini yeye ndiye Mhudumu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Tunashukuru kwamba habari kuhusu huduma ya Yesu zimeandikwa na kuhifadhiwa kwa faida yetu. Ili tuwe wahudumu wenye matokeo, ni lazima ‘tufuate hatua zake kwa ukaribu.’—1 Pet. 2:21.
2. Ni nini kitakachotusaidia kuwapenda watu kama Kristo alivyowapenda?
2 Onyesha Kwamba Unawapenda Watu: Yesu alichochewa na upendo wake na hangaiko lake kwa ajili ya watu. (Marko 6:30-34) Watu wengi katika eneo letu wana “maumivu” na wanahitaji sana kweli. (Rom. 8:22) Tukitafakari kuhusu hali yao mbaya na jinsi Yehova anavyowajali kwa upendo tutachochewa kuendelea kuhubiri. (2 Pet. 3:9) Isitoshe, watu watakuwa tayari kusikia ujumbe wetu wakitambua kwamba tunawajali kikweli.
3. Yesu aliwahubiria watu wakati gani?
3 Zungumza Kila Unapopata Nafasi: Yesu alitumia kila nafasi kuwahubiria wengine habari njema. (Mt. 4:23; 9:9; Yoh. 4:7-10) Vivyo hivyo, tunataka kuwa tayari kuzungumza kuhusu kweli tunapofanya shughuli zetu za kila siku. Wengine hubeba Biblia na vichapo ili wahubiri kazini, shuleni, wanaposafiri, wanaponunua vitu, na wanapofanya shughuli nyinginezo.
4. Tunaweza kufanya nini ili Ufalme uwe kichwa kikuu cha mahubiri yetu?
4 Kazia Fikira Ufalme: Kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu kilikuwa habari njema ya Ufalme. (Luka 4:43) Ingawa huenda tusitaje Ufalme moja kwa moja katika ujumbe wetu, tunakumbuka kumsaidia mwenye nyumba aone kwamba Ufalme unahitajiwa. Hata tunapotaja hali mbaya za ulimwengu zinazoonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho, kazi yetu ya msingi ni ‘kutangaza habari njema ya mambo mema!’—Rom. 10:15.
5. Ili huduma yetu iwe na matokeo, tunapaswa kuitumiaje Biblia?
5 Tegemea Neno la Mungu: Yesu alitumia Maandiko katika huduma yake yote. Hakujitungia mambo aliyofundisha. (Yoh. 7:16, 18) Alijilisha Neno la Mungu na kulitumia maishani aliposhambuliwa na Ibilisi. (Mt. 4:1-4) Ili tuwafundishe wengine kwa matokeo, ni lazima tusome Biblia kila siku na kuitumia maishani. (Rom. 2:21) Tunapojibu maswali katika huduma, tunapaswa kunukuu Maandiko ili kutegemeza yale tunayosema na inapowezekana tusome moja kwa moja kutoka katika Biblia. Tunataka mwenye nyumba aone kwamba hatusemi maoni yetu tu bali tunashikamana na maoni ya Mungu.
6. Yesu alifanya nini ili kufikia mioyo ya wasikilizaji wake?
6 Fikia Moyo Unapofundisha: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Yoh. 7:46) Ndivyo maofisa walivyosema kumhusu Yesu wakati wakuu wa makuhani na Mafarisayo walipowauliza kwa nini walishindwa kumkamata. Badala ya kutaja tu mambo ya hakika, Yesu alifundisha kwa njia iliyofikia mioyo ya wale aliowafundisha. (Luka 24:32) Alitumia mifano ya mambo halisi ili kuwasaidia waelewe maneno yake. (Mt. 13:34) Yesu hakuwalemea wasikilizaji wake kwa habari nyingi sana. (Yoh. 16:12) Badala ya kujielekezea uangalifu, alimwelekezea Yehova. Kama Yesu, tunaweza kuwa walimu stadi ikiwa tu ‘tutaangalia daima kufundisha kwetu.’—1 Tim. 4:16.
7. Kwa nini Yesu aliendelea kutimiza huduma yake?
7 Endelea Kutimiza Huduma Ujapokabili Ubaridi na Upinzani: Ingawa Yesu alifanya kazi nyingi zenye nguvu, wengi hawakumsikiliza. (Luka 10:13) Hata watu wa familia ya Yesu walisema kwamba “amerukwa na akili.” (Marko 3:21) Lakini, Yesu aliendelea kutimiza huduma yake. Alidumisha mtazamo unaofaa kwa sababu alisadiki kabisa kwamba ana kweli inayoweza kuwaweka huru wanadamu. (Yoh. 8:32) Kwa msaada wa Yehova, sisi pia tumeazimia kutokufa moyo.—2 Kor. 4:1.
8, 9. Tunaweza kumwigaje Yesu katika kujidhabihu kwa ajili ya habari njema?
8 Dhabihu Mambo Fulani Ili Ushiriki Kikamili: Yesu alijinyima starehe za kimwili kwa ajili ya huduma. (Mt. 8:20) Alihubiri kwa bidii, na nyakati nyingine alifanya hivyo hadi usiku. (Marko 6:35, 36) Yesu alijua kwamba alikuwa na muda mfupi tu wa kutimiza kazi hiyo. Kwa kuwa “wakati uliobaki umepungua,” sisi pia tunahitaji kudhabihu wakati wetu, nguvu zetu, na mali zetu kama Yesu alivyofanya.—1 Kor. 7:29-31.
9 Wakristo wa karne ya kwanza walipata matokeo kwa sababu walijifunza kutokana na Yesu. (Mdo. 4:13) Sisi pia tunaweza kutimiza kwa ukamili huduma yetu tukimwiga yule Mhudumu mkuu zaidi aliyepata kuishi.—2 Tim. 4:5.