Umewawekea Watoto Wako Miradi Gani?
1 Mafanikio maishani hutegemea kuwekwa na kutimizwa kwa miradi inayofaa. Wale ambao hufuatia miradi hafifu au isiyo ya kihalisi mwishoni hukata tamaa na kuhisi hawakutimiza jambo lolote. Hekima inahitajiwa ili kutambua ni malengo gani ya kufuatiwa ili ‘kupata uhai ulio kwelikweli.’ (1 Tim. 6:19) Twashukuru kama nini kwamba Yehova, kupitia Neno na tengenezo lake, atuonyesha sisi njia barabara ya kwenda!—Isa. 30:21.
2 Katika kuandaa mwongozo huo wenye upendo, Yehova huwawekea wazazi kielelezo chema. Badala ya kuwaacha watoto wao ambao hawajajionea mambo mengi wajichagulie ni njia gani iliyo bora zaidi, wazazi wenye hekima huwazoeza katika njia wapaswayo kwenda, na wanapozeeka, wao ‘hawataiacha.’ (Mit. 22:6) Wazazi Wakristo wanajua kutokana na mambo ambayo wamejionea wenyewe kwamba hawawezi kutumaini uamuzi wao wenyewe; ni lazima wamtegemee Yehova. (Mit. 3:5, 6) Uhitaji huu ni mkubwa hata zaidi kwa watoto, ambao hawana ujuzi mwingi wala hawajajionea mambo mengi.
3 Wazazi waweza kuweka mbele ya watoto wao miradi inayofaa itakayowasaidia kukazia “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Flp. 1:10, NW) Wao waweza kuanza na funzo la familia, wakiwatia moyo watoto kuthamini umaana walo na kujifunza kutoka kwalo. Ni vema kwa watoto kujipatia zoea la kujifunza kimbele kwa ajili ya mikutano ya kutaniko na kujitayarisha ili kutoa maelezo kwa maneno yao wenyewe. Ushiriki wa kawaida katika kazi ya kuhubiri ni jambo la maana. Watoto wachanga waweza kuchangia kwa kutoa trakti, kwa kusoma maandiko, au kwa kutoa magazeti. Wanapoweza kusoma, kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwaweza kuharakisha maendeleo yao ya kiroho. Kustahili kuwa mhubiri asiyebatizwa au kukubaliwa kubatizwa ni hatua kubwa kuelekea mbele.
4 Watoto wao wakaribiapo miaka ya utineja, au hata mapema zaidi, wazazi wapaswa kuongea nao kwa uhalisi juu ya miradi ya kazi-maisha. Washauri wa shule na wanafunzi wenzao waweza kuwavuta kwa urahisi ili kupendelea ufuatiaji mbalimbali wa kilimwengu, wa kufuatia vitu vya kimwili. Wazazi wapaswa kusaidia watoto wao kuchagua mitaala inayoandaa mazoezi ya kutumika, ikiwatayarisha ili watunze mahitaji yao ya kimwili bila kudhabihu masilahi ya Ufalme. (1 Tim. 6:6-10) Wao waweza kutiwa moyo kufuatia “zawadi” ya useja, kisha baadaye, wakiamua kuoa au kuolewa, wao wataweza kuyachukua madaraka mazito ya ndoa. (Mt. 19:10, 11, NW; 1 Kor. 7:36-38) Kwa kuongea kwa njia chanya juu ya kupainia, kutumikia mahali ambako uhitaji ni mkubwa zaidi, utumishi wa Betheli, au utendaji wa mishonari, wazazi waweza kutia katika watoto hata wenye umri wa mapema tamaa ya kutumia maisha zao katika njia inayompendeza Yehova, inayonufaisha wengine, na kuwaletea baraka wao wenyewe.
5 Si kwa aksidenti tu kwamba tuna vijana wengi sana katika tengenezo leo wanaoshikamana na kanuni za juu za Kikristo na kufuatia miradi ya kitheokrasi. Kiasi kikubwa cha mafanikio yao chaweza kuhesabiwa kuwa kwa sababu ya wazazi wenye upendo. Ikiwa wewe ni mzazi, je, yaonekana watoto wako wanaelekea wapi? Je, wanasonga mbele kwa maendeleo kuelekea maisha yanayokazia masilahi ya Ufalme? Kumbuka kwamba, mojapo mambo ya maana zaidi uwezayo kufanya ni kukazia kweli kikiki katika watoto wako, na useme juu yayo kila siku. Huenda ukabarikiwa kuwa na watu wa nyumbani mwako walio waaminifu katika kumtumikia Yehova.—Kum. 6:6, 7; Yos. 24:15.