Sema kwa Ujasiri
1 Katika miaka ya juzijuzi wahubiri katika maeneo mengine wanaona ikiwa vigumu zaidi kusema na watu nyumbani mwao. Wengi wanaripoti kwamba katika eneo lao watu zaidi ya asilimia 50 hawapo nyumbani wanapozuru nyumba kwa nyumba. Kama tokeo, wakati mwingi unaotumiwa huwa bila matokeo.
2 Miaka mingi iliyopita watu wengi walipatikana nyumbani Jumapili, ambayo kwa ujumla ilikuwa inaonwa kuwa siku ya kupumzika. Desturi zimebadilika. Ni jambo la kawaida leo kwa watu kuwa kwenye kazi za kimwili, kutunza mahitaji ya familia kama vile kununua vitu, au kuhusika katika tafrija, jambo ambalo pia huwaondoa nyumbani. Kwa hiyo hata Jumapili, kuwafikia watu nyumba kwa nyumba kumekuwa tatizo.
3 Watu wanapokosekana nyumbani, bila shaka humaanisha kwamba wapo mahali penginepo. Kwa kuwa mradi wetu ni kuongea na watu, kwa nini tusiseme na wale tunaokutana nao—barabarani, sokoni, au kazini. Ilikuwa desturi ya Paulo kufikia ‘wale aliokutana nao,’ ili awatolee ushahidi. (Mdo. 17:17) Hii ilithibitika kuwa aina ya kutoa ushahidi yenye matokeo wakati huo, na ni aina ya kutoa ushahidi yenye matokeo katika siku yetu.
4 Tunapoenda nyumba kwa nyumba, kwa kawaida sisi huona watu wakitembea kwa starehe au labda wakingoja mtu. Kukiwa na siku nzuri, huenda wakawa wameketi kwenye kiti cha bustani au kurekebisha au kuosha gari lao. Tabasamu ya kijirani na salamu ya kirafiki huenda yakawa tu mambo tunayohitaji ili kuanzisha mazungumzo. Ikiwa wanaishi karibu, hata tunaweza kutaja kwamba yamkini tumewakosa tu nyumbani mwao na sasa tunafurahi kwamba tumepata nafasi hii ya kusema nao. Kwa kuchukua hatua ya kuonyesha ujasiri zaidi, wengi wamefurahia mambo yaliyoonwa yenye kuthawabisha.
5 Ujasiri Hupata Matokeo: Ndugu mmoja alisimulia kwamba yeye hufikia watu wanaosimama, wakingoja basi, wakitembea kwa starehe, au wakiwa wameketi ndani ya gari lao. Akiwa na tabasamu changamfu na sauti yenye shangwe, yeye hutenda kama jirani mwenye urafiki ambaye hutaka tu kuzuru. Kwa njia hii yeye hajaangusha fasihi nyingi tu, bali pia ameanzisha mafunzo ya Biblia kadhaa.
6 Ndugu mwingine pamoja na mke wake walikuwa wakienda mlango kwa mlango walipokutana na mwanamke akitembea huku akibeba mfuko mkubwa wa vyakula. Walianza mazungumzo, wakimpongeza kwa juhudi yake ya kuangalia mahitaji ya familia yake. “Lakini ni nani,” wao wakauliza, “awezaye kuandaa mahitaji ya wanadamu?” Hilo liliamsha kupendezwa kwa mwanamke huyo. Mazungumzo mafupi yaliongoza kwenye mwaliko nyumbani mwake, ambamo funzo la Biblia lilianzishwa.
7 Kwa hiyo wakati ufuatao unapotoa ushahidi mlango kwa mlango, iwe ni Jumapili au siku nyingine ya juma, na unapata kwamba watu hawako nyumbani, kwa nini usijipatie ujasiri zaidi na kusema na watu unaokutana nao—barabarani au kwingineko? (1 The. 2:2) Huenda ukawa na huduma yenye matokeo, na kuwa na shangwe kubwa zaidi katika utumishi wako.