Mbariki Yehova ‘Mchana Kutwa’
1 Zaburi 145:2 (NW) ina ahadi ambayo Mfalme Daudi alimtolea Yehova: ‘Mchana kutwa nitakubariki, nami nitalisifu jina lako hadi wakati usio dhahiri, hata milele.’ Sisi pia tuna sababu ya kumbariki na kumsifu Baba yetu wa kimbingu! Lakini twaweza kuigaje kielelezo cha Daudi cha kutukuza enzi kuu ya Yehova ‘mchana kutwa’?
2 Jaza Mioyo Yetu na Uthamini kwa Yehova: Funzo la kawaida la Neno la Mungu huongeza shukrani zetu kwa yale ambayo Yehova ametufanyia, anayotufanyia, na atakayotufanyia. Tunapoongeza uthamini wetu kwa matendo yake ya ajabu, twajipata tukisema juu ya wema wake. (Zab. 145:7) Tutamtukuza Yehova kwa bidii katika kila pindi ifaayo.
3 Msifu Yehova Katika Maongeo ya Kila Siku: Tunapoongea na majirani, wanashule wenzetu, wafanyakazi wenzetu, na wengine tunaokutana nao kila siku, twaweza kupata fursa za kushiriki nao tumaini letu. Jirani anaweza kuonyesha hangaiko juu ya uhalifu katika jumuiya hiyo; mwanashule mwenzetu anaweza kuhangaika kuhusu matumizi mabaya ya madawa au ukosefu wa adili; mfanyakazi mwenzetu huenda akatoa maoni kuhusu suala fulani la mahali pao. Twaweza kuelekeza kwenye kanuni na ahadi zilizo katika Neno la Mungu ambazo huonyesha mwendo ufaao kuchukuliwa sasa na utatuzi wa mwisho wa matatizo haya. Maneno hayo yakiongewa “wakati wa kufaa” yanaweza kuwa baraka!—Mit. 15:23.
4 Ongea Juu Ya Yehova Wakati Wote: Mtu mwenye uthamini mwingi kwa Yehova hutaka kushiriki habari njema na wengine wengi iwezekanavyo. (Zab. 40:8-10) Kuhusu hili twapaswa kujiuliza wenyewe, ‘Je, nafanya yote ambayo hali zangu zitaruhusu?’ Wengi wameona kwamba wakifanya marekebisho yafaayo, wameweza kuwa mapainia wa kawaida. Kwa sasa ikiwa hali haziruhusu, je, twaweza kujiandikisha kuwa mapainia-wasaidizi? Kwa kuwa majira yanayokuja ya Ukumbusho ni wakati wa utendaji ulioongezeka, miezi ya Machi na Aprili itakuwa wakati mzuri wa kuongeza utumishi wetu kwa kufanya upania-msaidizi.
5 Saidia Wapya Wajiunge Nasi Kumbariki Yehova: Sherehe ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu sikuzote hutukumbusha sababu za kutufanya tuwe wenye shukrani kwa Yehova na kusifu jina Lake. Huu ni wakati mzuri wa kutia moyo wanafunzi wetu wa Biblia kujiunga nasi kusema peupe kuhusu utawala wa Yehova. Wahimize wafikirie kupitia sala yale yanayosemwa katika mafungu 7-9 kwenye kurasa 173-175 katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Wakistahili, hawana sababu ya kuepuka kuhubiri kwa sababu tu hawana uzoefu. Watangazaji wenye uwezo wako ili wawaonyeshe jinsi kazi ya kuhubiri Ufalme inavyofanywa. Wapya wakiweza kupata ujasiri wa kusema habari njema, wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawasaidia.—Mdo. 4:31; 1 The. 2:2.
6 Sisi wenyewe pamoja na wengine twajiletea manufaa za milele tunapotafuta kumbariki Yehova mchana kutwa.