Iweni na “Juhudi Katika Matendo Mema” Mwezi wa Aprili!
1 Mwaka jana ushahidi mwingi ulitolewa wakati mamilioni ya trakti Na. 34 Habari za Ufalme yaligawanywa ulimwenguni pote. Watangazaji wa kutaniko na mapainia pia walishiriki kwa bidii katika kazi hii yenye kusisimua. Je, ulikuwa miongoni mwao? Ikiwa ulifanya hivyo, bila shaka ulifurahi sana kushiriki katika kampeni hiyo yenye kutazamisha. Sasa huenda ukawa unajiuliza, Ni ‘tendo gani jema’ lililo mbele yetu mwaka huu?—Tito 2:14.
2 Mwezi wa Aprili na wa Mei, tutakuwa na furaha ya kugawanya toleo la pekee la gazeti Amkeni!, la Aprili 22, 1996, linalokazia “Wakati Vita Havitakuwapo Tena.” Kwa kuwa jambo hili litapendeza wenye nyumba wengi, tutajitahidi kugawanya gazeti hilo kwa kiwango kikubwa. Kwa sababu ya umaana wa habari iliyo ndani yalo, toleo hili la Amkeni! lapaswa kutolewa mwezi wa Aprili na Mei, hadi ugavi wishe.
3 Mradi Wetu—Watangazaji Wote Washiriki: Itatia moyo kwelikweli ikiwa watangazaji wote katika nchi hii watashiriki kazi ya kuhubiri mwezi wa Aprili. Tukiwa tumetoka tu kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo, kwa kweli tutataka kuonyesha uthamini wetu kwa wema wa Mungu kwa kutoa “dhabihu ya sifa” katika huduma ya shambani.—Ebr. 13:15.
4 Jitihada kubwa yapaswa kufanywa ili kutambua mahitaji ya kila mshiriki wa kutaniko ili kwamba wote waweze kushiriki kwa bidii katika huduma mwezi wa Aprili. (Rum. 15:1) Viongozi wa funzo la kitabu wapaswa kujua kabisa mahitaji ya wale walio katika vikundi vyao na kutoa msaada unaohitajiwa. Je, kuna mtu anayehitaji usafiri? Ni nani awezaye kuuandaa? Je, wengine ni waoga au wenye wasiwasi? Je, watangazaji wenye uzoefu zaidi wa kazi wanaweza kuhubiri pamoja nao? Vipi juu ya wasiojiweza walio kitandani au wagonjwa? Je, wanaweza kutoa ushahidi wa simu, kuandika barua, au kushiriki utendaji mwingine wenye matokeo?
5 Wengine ambao wamekuwa wasiotenda wamekuwa wakipokea kitia-moyo cha ukawaida cha kiroho, nao waweza kuchochewa kushiriki katika kazi ya kuhubiri tena. Kampeni hiyo ya Amkeni! ya pekee itawaandalia fursa bora ya kuwa watendaji tena.
6 Zoezeni Wachanga Ili Washiriki: Watoto wengi wa Mashahidi wa Yehova wameandamana na wazazi wao nyumba kwa nyumba kwa miaka mingi, ijapokuwa bado hawatumikii wakiwa watangazaji wasiobatizwa. Je, sasa ni wakati wao kuanza? Je, wanasukumwa kutoka moyoni na wako tayari kushiriki ifaavyo katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba? Vichwa vya familia wapaswa kutumia wakati katika funzo la Biblia la familia kusaidia watoto wao waliostahili kutayarisha utoaji unaopatana na umri na uwezo wa kila mmoja. Walio wakubwa wanaweza kuchagua swali lenye kuvuta fikira ambalo litaamsha kupendezwa kwa mwenye nyumba kisha waonyeshe jibu kwenye gazeti. Watoto walio wachanga wanaweza kutoa ushahidi wenye matokeo kwa maneno machache. Kwa kielelezo, wanaweza kumtia moyo mwenye nyumba “asome gazeti la pekee ambalo latolewa ulimwenguni pote mwezi huu.” Ikiwa sehemu ya utayarishaji wa familia yako, hakikisha kutia ndani madokezo ya kushinda vipingamizi vya kawaida. Utapata baadhi ya maoni yenye kupendeza katika kitabu Kutoa Sababu. Wakati wa chakula na katika pindi nyingine zifaazo, tia moyo washiriki wa familia waeleze mambo yaliyoonwa ambayo wamekuwa nayo katika utumishi wa shambani.
7 Wanafunzi wa Biblia Waliostahili Hufanya Kazi Aliyofanya Yesu: Yesu hakuwekea mipaka mafundisho yake kwa kutoa maagizo ya kimafundisho. Yeye aliandamana na wanafunzi wake katika huduma na kuwafundisha jinsi ya kuhubiri. (Luka 8:1; 10:1-11) Namna gani leo? Mafunzo ya Biblia zaidi ya 35,000 yanaongozwa katika Afrika Mashariki. Bila shaka, kukiwa na kitia-moyo kifaacho wengi wa wanafunzi hawa wanaweza kuchukua hatua ifuatayo katika mazoezi yao na kustahili kutumikia wakiwa watangazaji wasiobatizwa katika Aprili.
8 Ikiwa unaongoza funzo la Biblia, fikiria maswali haya: Je, mwanafunzi huyo anafanya maendeleo, kupatana na umri na uwezo wake? Je, ameanza kushiriki imani yake kivivi hivi pamoja na wengine? Je, anavaa “utu mpya”? (Kol. 3:10) Je, amefikia sifa za kustahili za mtangazaji asiyebatizwa, zilizo kwenye kurasa 97 hadi 99 za kitabu Huduma Yetu? Ikiwa waamini kwamba anastahili, kwa nini usizungumze jambo hilo pamoja naye? Wanafunzi wengine wanahitaji tu mwaliko wa moja kwa moja ili washiriki katika mahubiri. Bila shaka, kama mwanafunzi yuko tayari, kwanza itakuwa lazima mwangalizi-msimamizi apange kama ilivyo kawaida mazungumzo na wazee wawili. Kwa upande mwingine, huenda jambo fulani likawa lamzuia mwanafunzi. Labda mmoja wa wazee anaweza kuandamana nawe kwenye funzo la Biblia na kumfanya mwanafunzi azungumze kuhusu hisia zake kuelekea kweli. Baada ya kusikiliza yale ambayo mwanafunzi anasema, mzee anaweza kuandaa madokezo yafaayo, pamoja na msaada wa Kimaandiko.
9 ‘Komboa Wakati’ Ufanye Upainia Msaidizi: Kila mwaka wakati wa majira ya Ukumbusho, shukrani kwa fidia huchochea maelfu ‘wakomboe’ wakati wawe mapainia-wasaidizi. (Efe. 5:15-17) Ijapokuwa dhabihu fulani zahitajiwa, thawabu ni kubwa. Idadi yenye kusifika ya vijana hutumia kwa manufaa likizo ili wafanye upainia msaidizi. Watu wazima wanaofanya kazi wakati wote hutumia jioni na miisho-juma kwa manufaa kamili katika utendaji huohuo. Hivyo, familia nzima zimechukua fursa za kufanya upainia msaidizi pamoja! Katika makutaniko mengine wengi wa wazee na watumishi wa huduma na wake zao wamejiandikisha wawe mapainia-wasaidizi. Wakiwa wamechochewa na kielelezo chao cha bidii, wengine wamekifuata, hivi kwamba asilimia kubwa ya kutaniko hutumikia wakiwa mapainia-wasaidizi katika Aprili.
10 Iwe unaweza kufanya upainia msaidizi au la, tafuta njia za kuongeza utumishi wako wa shambani katika Aprili. Jiwekee mradi wa kibinafsi, ule utakaotaka jitihada ili kuufikia lakini unaoweza kufikika. Tamaa yako ya ‘kutumia na kutumiwa kabisa’ katika utumishi wa Yehova, kulingana na hali zako za kibinafsi, itakuwa na baraka zake.—2 Kor. 12:15, NW.
11 Mikutano ya Utumishi wa Shambani: Mikutano ya utumishi wa shambani yapaswa kupangwa kila siku ya kampeni ya Amkeni!, wakati ambao utaruhusu kuanza mapema katika huduma. Uandalizi wapaswa kufanywa pia kwa ajili ya kutoa ushahidi wa jioni. Watangazaji walio wengi watashiriki katika utumishi wa shambani kwenye miisho-juma, hivyo makutaniko yapaswa kuratibu mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani Jumamosi, asubuhi na alasiri vilevile, wakati wa ugawanyaji wa Amkeni! la pekee.
12 Wale wanaoongoza mikutano ya utumishi wa shambani wapaswa kuhakikisha kwamba kuna eneo la kutosha. Eneo ambalo halijahubiriwa karibuni lapaswa kufanywa kwanza. Hata hivyo, eneo lisilogawiwa lililo chini ya usimamizi wa Sosaiti halipaswi kuhubiriwa bila ruhusa ya Sosaiti. Je, una eneo moja au zaidi ambayo hayajafanywa karibuni? Ikiwa utataka msaada wa kuyahubiri wakati wa kampeni hii, ongea na mwangalizi wa utumishi au ndugu anayeshughulikia eneo nao watafurahia kupanga upate msaada.
13 Utaangusha Magazeti Mangapi? Swali hilo ni la kila mtu mmoja-mmoja kujibu. Ili kujua ni magazeti mangapi utakayoangusha wakati wa kampeni hii, fikiria aina ya eneo utakalokuwa ukihubiri, umri wako, afya yako, na wakati unaoweza kutumia katika kazi hiyo, na mambo mengine. Hata hivyo, angalia kikumbusha kilichotolewa katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1994: “Kama dokezo, wahubiri wanaweza kuwa na mradi wa magazeti 10 hivi kila mwezi, ikitegemea hali zao; huenda mapaina wakajitahidi kufikia 90.” Je, mradi huohuo utafaa kwa upande wako?
14 Wazee—Upangaji Mzuri Wahitajiwa: Ikiwezekana, hakikisha kwamba, eneo lote la kutaniko litahubiriwa mkiwa na toleo la pekee la Amkeni! Uangalifu wapaswa kutolewa ili kuhubiri eneo la kibiashara lolote lililogawiwa kutaniko. Wale wanaolihubiri wanapaswa kujitayarisha vizuri na kuvalia nadhifu. Si lazima kuwa na utoaji ulio mgumu. Unapomfikia mfanya biashara, unaweza kusema kwamba hupati wafanya biashara nyumbani, kwa hiyo unatembelea mahali pake pa biashara wakati huu ukiwa na makala itakayompendeza. Kisha unaweza kushiriki kifupi jambo hususa katika gazeti hilo. Ushahidi wa barabarani na magazeti wapaswa pia kupangwa vizuri katika eneo la kutaniko. Njia yenye matokeo zaidi ya kushiriki katika mahubiri ya barabarani ni kuchukua hatua ya kumfikia mpita-njia, badala ya kungoja wakufikie. Kwa kuwa utakuwa unaonekana na watu hadharani, unapaswa kuangalia kwamba una sura yenye heshima. Huenda kukawa na mahali pengine katika eneo lako ambapo panaweza kuhubiriwa wakati wa kampeni hii, kama vile viwanja vya ndege, hospitali, mahali pa kuegesha magari, bustani, na nyumba za wazee. Baraza la wazee lapaswa kuchunguza ni mipango gani ifaayo inayoweza kufanywa kwa ajili ya ushahidi katika sehemu hizi za maeneo ya kutaniko.
15 Yehova ni mfanyakazi asiyechoka. (Yn. 5:17) Aliumba mbingu na dunia pamoja na mimea na wanyama; lakini aliendelea kufanya kazi hadi alipoumba kazi yake bora ya upeo duniani—mwanadamu. Uhakika wa kwamba tuna uhai ni tokeo la moja kwa moja la utayari wa Mungu kufanya kazi. Tukiwa ‘waigaji wa Mungu,’ twapaswa kusukumwa na upendo kwake tuwe wenye “juhudi katika matendo mema.” (Efe. 5:1, HNWW; Tito 2:14) Kwa kuwa Yehova anastahili kupata jitihada zetu bora kupita zote na kwa kuwa tamaa ya kupata matokeo yatokana na yule aliye na bidii, twapaswa kupendezwa na kufanya kazi bora katika huduma. Bila shaka, Yehova huthamini dhabihu zozote tufanyazo kwake, na kazi yetu si ya bure kamwe. (1 Kor. 15:58) Kwa hiyo, tukiwa na mioyo yenye shukrani, acheni tufanye utendaji wa bidii mwezi wa Aprili, tukiwa na uhakika wa kibali cha Yehova na baraka na mafanikio mengi!