Tayarisha Utoaji Wako Mwenyewe wa Magazeti
1 Twayathamini magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa sababu ya makala zayo za wakati ufaao na zenye kuarifu, ambazo hushughulikia kila jambo kuanzia masuala ya ulimwengu hadi “mambo yenye kina kirefu ya Mungu.” (1 Kor. 2:10, NW) Sote twakumbuka mambo mengi mapya na yenye kujenga ambayo tumesoma katika majarida hayo, ambayo Yehova anatumia ili kufunua kweli hatua kwa hatua. (Mit. 4:18) Twataka kuwa na hamu ya kuyagawanya kwa wingi iwezekanavyo. Hakikisha kutoa maandikisho mwezi huu.
2 Changanua Eneo Lako: Ni watu wa aina gani wanaoishi katika eneo lako? Ikiwa wako mbioni sikuzote, huenda ukahitaji kutayarisha utoaji ambao ni mfupi na wa moja kwa moja. Ikiwa una eneo ambalo katika hilo maisha si ya mbiombio sana, huenda ukaweza kusema zaidi. Ikiwa wenye nyumba wengi wanafanya kazi mchana, huenda ukawa na mafanikio bora ukiwatembelea nyumbani kwao baadaye alasiri au mapema jioni. Waweza kuwasiliana na baadhi yao mchana kupitia ushahidi wa barabarani au kuhubiri duka kwa duka. Wahubiri fulani hupata matokeo mazuri kwa kuwafikia watu kivivi-hivi kwenye maegesho ya magari na mabustani ya jiji.
3 Yafahamu Magazeti: Soma kila toleo mara tu ulipatapo. Teua makala ambazo wahisi zaweza kuwavutia watu katika eneo lako. Ni habari gani zinazowahusu? Tafuta hoja hususa ambayo waweza kunukuu kutoka katika hiyo makala unayokusudia kuonyesha. Fikiria swali uwezalo kuzusha ili kuchochea upendezi. Teua andiko la wakati ufaao la kusoma kwa mwenye nyumba ukipata fursa ya kufanya hivyo. Fikiria uwezalo kusema ili kuwekea msingi ziara ya kurudia.
4 Tayarisha Utangulizi Wako: Chagua kwa uangalifu maneno unayopanga kutumia ili kujijulisha kwake na kuanzisha mazungumzo. Watu fulani wamepata mafanikio kwa kutumia utangulizi huu: “Nimesoma makala yenye kuvutia katika gazeti hili, nami nataka kuishiriki pamoja na wengine.” Wengi huanza kwa swali linalokazia hoja ya kuzungumziwa wanayopanga kutumia. Kwa kielelezo:
5 Ikiwa wakazia makala juu ya mweneo wa uhalifu, ungeweza kuuliza hivi:
◼ “Ni nini kinachohitajiwa ili tuweze kulala usiku bila hofu ya kuibiwa au kudhuriwa?” Eleza kwamba una habari fulani juu ya utatuzi wa tatizo hilo. Karibuni utatuzi huo utaondolea mbali kila aina nyingine ya mchafuko wa kijamii vilevile. Rejezea jambo fulani katika hilo gazeti litoalo tumaini hilo. Urudipo, waweza kuelekeza uangalifu wa mwenye nyumba kwenye sura ya 1 ya kitabu Ujuzi.
6 Unapotoa makala juu ya maisha ya familia, waweza kusema hili:
◼ “Wazazi wengi wanaona ugumu sana wa kutunza familia siku hizi. Vitabu vingi vimeandikwa juu ya habari hii, lakini hata hao wataalamu hawakubaliani. Je, kuna yeyote awezaye kuandaa mwongozo wenye kutegemeka?” Shiriki maelezo hususa kutoka katika hilo gazeti linaloonyesha shauri lenye hekima lipatikanalo katika Biblia. Ufanyapo ziara ya kurudia, zungumzia mawazo ya Kimaandiko juu ya kulea watoto yanayozungumziwa katika kitabu Ujuzi, kurasa 145-148.
7 Unapoonyesha makala juu ya tatizo la kijamii, ungeweza kusema hivi:
◼ “Watu wengi huhisi wakiwa wamesongwa kwa sababu ya nyakati zenye mikazo tunamoishi. Je, wafikiri Mungu alikusudia tuishi hivi?” Elekeza kwenye makala inayoonyesha jinsi ya kukabiliana na matatizo ya leo au inayotoa sababu za kutazamia wakati ujao ambao hautakuwa na mahangaiko. Kwenye ziara yako inayofuata, zungumzia picha na maelezo kwenye kurasa 4-5 za kitabu Ujuzi, kisha uongoze moja kwa moja kwenye funzo la Biblia nyumbani.
8 Badilikana Umfae Mwenye Nyumba: Utakuta watu wenye mapendezi na malezi tofauti. Tayarisha utoaji wa msingi ambao waweza kuubadilisha umfae kila mwenye nyumba. Uwe tayari juu ya uwezavyo kubadili usemayo yamfae mwanamume, mwanamke, mtu mwenye umri mkubwa zaidi, au kijana. Hakuna kanuni ngumu juu ya yale ambayo ni lazima useme. Sema chochote kinachokustarehesha na kinachopata matokeo. Hata hivyo, uwe mwenye shauku, sema kutoka moyoni, na uwe msikilizaji mzuri. Wale wenye “mwelekeo ufaao” wataona moyo wako mweupe nao wataitikia vizuri.—Mdo. 13:48, NW.
9 Saidianeni: Kwa kushiriki pamoja mawazo, twajifunza njia mpya za kujieleza. Kujizoeza pamoja utoaji wetu mbalimbali hutupa uzoefu na uhakika. (Mit. 27:17) Ukijizoeza kimbele yale utakayosema, utahisi ukiwa mtulivu zaidi mlangoni. Ni jambo la maana kwamba wazazi watumie wakati kuwasaidia watoto wao kujitayarisha, kuwasikiliza wakijizoeza utoaji wao, na kutoa madokezo ya kufanyia maendeleo. Wapya waweza kunufaika kwa kuhubiri pamoja na watangazaji wenye uzoefu zaidi.
10 Si lazima iwe vigumu kutayarisha utoaji wako mwenyewe wa magazeti. Kwahitaji tu kutayarisha jambo hususa la kusema kisha kulieleza kwa njia yenye kuvutia. Kwa kuchukua hatua ya kwanza na kufikiri kimbele, waweza kutokeza utoaji mzuri ambao utapata itikio zuri.
11 Kugawanya magazeti ni mojapo njia zetu za msingi za kueneza ujumbe wa Ufalme ulimwenguni pote. Ikiwa waweza kuangushia watu wenye mioyo myeupe Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, hayo magazeti yaweza kujisemea. Sikuzote kumbuka thamani yayo na jinsi ujumbe wayo uwezavyo kuokoa uhai. Aina hii ya “kutenda mema na kushirikiana” ndiyo impendezayo Yehova sana.—Ebr. 13:16.