Jinsi ya Kutayarisha Utoaji wa Magazeti
1 Huenda unajiuliza, ‘Kwa nini tutayarishe utoaji wa magazeti wakati mambo ya kusema yanapatikana katika kila toleo la Huduma Yetu ya Ufalme?’ Ingawa wengi wameona mapendekezo hayo ya utoaji kuwa yanasaidia, matayarisho ya kibinafsi ya utoaji yanahitajika. Utoaji ambao unafaa eneo fulani huenda usifae eneo lingine. Hivyo, hatupaswi kudhania kwamba ni lazima tutoe magazeti yetu kwa maneno yaleyale yanayotumiwa kwenye mapendekezo. Hata ingawa tunapenda kutumia mapendekezo hayo, ni vizuri tufanye hivyo kwa maneno yetu wenyewe.
2 Chagua Makala: Baada ya kulisoma gazeti mapema, chagua makala ambayo inakupendeza na inayofaa eneo lenu. Uhakika na uchangamfu wako unapoizungumzia makala hiyo unaweza kumvutia mwenye nyumba atake kuisoma pia. Hata ingawa utapenda kuzungumzia makala ambayo inawavutia watu wengi katika eneo lenu, ni vizuri kuelewa makala nyingine katika gazeti hilo. Hilo litakusaidia kubadili utoaji wako unapokutana na mtu ambaye huenda akapendezwa na habari nyingine kwenye gazeti hilo.
3 Uliza Swali: Kisha, tayarisha utangulizi wako vizuri. Utangulizi wako ni muhimu sana. Ili kuchochea upendezi kuelekea makala uliyochagua, ni vizuri kumuuliza mwenye nyumba swali litakalomfanya afikiri. Mara nyingi maswali ya maoni huwa na matokeo mazuri. Epuka kuuliza maswali ambayo yatamtatanisha mwenye nyumba au kumfanya aanze kujitetea.
4 Soma Andiko: Mwisho, chagua andiko ambalo utasoma ikiwa mwenye nyumba ataruhusu. Linaweza kuwa kwenye makala ambayo utazungumzia. Kusoma andiko kutamsaidia mwenye nyumba aone kuwa ujumbe wetu unatokana na Neno la Mungu. (1 The. 2:13) Hata ingawa hatakubali kuchukua magazeti, andiko hilo litamtolea ushuhuda. Wengine wameamsha upendezi wa wenye nyumba kwa kusoma andiko kabla ya kuwauliza swali. Kabla ya kusoma andiko unaweza kusema hivi, “Ningependa kupata maoni yako kuhusu mstari huu wa Biblia.” Halafu mwelekeze mwenye nyumba kwenye sehemu ambayo inapatana na andiko hilo katika gazeti, na utoe maelezo mafupi ili kuchochea upendezi zaidi kabla ya kumwachia.
5 Hakuna sheria fulani inayopaswa kufuatwa unapotoa magazeti. Kwa ujumla, unapaswa kufanya utoaji wako uwe mfupi na rahisi. Tumia utoaji ambao unajisikia huru kuutumia na wenye matokeo mazuri. Kazia jinsi magazeti yetu yalivyo na thamani na uwe mchangamfu. Ikiwa utajiandaa vizuri, utakuwa na matokeo mazuri unapotoa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa wale ambao wana “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Matendo 13:48.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini ni vizuri tutayarishe utoaji wa magazeti kwa maneno yetu wenyewe badala ya kukariri mapendekezo yanayopatikana kwenye Huduma Yetu ya Ufalme?
2. Unapaswa kufikiria mambo gani unapoamua makala utakayotoa?
3. Ili upate matokeo mazuri ni utangulizi wa aina gani unaoutumia?
4. Ikiwa hali zinaruhusu kuna faida gani ya kumsomea mwenye nyumba andiko?
5. Ni mambo gani unayopaswa kukumbuka unapotayarisha utoaji wa magazeti?