Je, Unatimiza Huduma Yako Kikamili?
1 Katika kitabu cha Matendo, twaambiwa kwamba wanafunzi wa Yesu walitimiza huduma yao kwa kuwatolea watu “ushahidi kamili.” (Mdo. 2:40; 8:25; 28:23) Hilo hasa ndilo lililokuwa lengo la mtume Paulo. (Mdo. 20:24) Je, huo si mradi wako ukiwa mhudumu wa habari njema? Unaweza kuutimizaje?
2 Tayarisha Utoaji Wako: Ili uwe na matokeo katika huduma yako, ni lazima ujitayarishe. Ndivyo ilivyo hasa katika kutoa magazeti, kwa kuwa habari ya kuzungumziwa hubadilika mara kwa mara. Ili kutusaidia kuwa tayari, toleo hili la Huduma Yetu ya Ufalme linaanzisha sehemu mpya—safu iliyo kushoto, ambayo yaorodhesha mifano ya utoaji mbalimbali wa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Habari inayofaana na wakati itakayovutia watu wengi itakaziwa katika kila toleo. Unaweza kutayarishaje utoaji huo mfupi?
3 Chagua dokezo ambalo unahisi kwamba litakuwa na matokeo zaidi katika eneo lenu. Soma makala inayokaziwa kwa uangalifu na uangalie mambo hususa ambayo labda yatachochea kupendezwa. Tafuta andiko katika gazeti ambalo halijanukuliwa linalohusiana na mazungumzo hayo na ambalo waweza kumsomea mwenye nyumba. Ongezea kifupi maneno ya kumalizia ili umtie moyo msikilizaji wako asome gazeti hilo na ikifaa, umweleze kifupi kuhusu kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Sasa, jizoeze utoaji wako.
4 Panga Kutumia Biblia: Ukipanga vizuri, mara nyingi unaweza kutia ndani andiko katika mazungumzo yako. Kwa mfano, wahubiri wenye ujuzi katika maeneo mengi wamekuwa na mafanikio kwa kumwendea mwenye nyumba wakiwa wameshika Biblia, kisha wanamsalimu na kusema:
◼ “Tunauliza watu kama wanaamini jambo hili . . .” Soma Mwanzo 1:1, kisha uulize: “Je, wakubaliana na maneno hayo?” Mwenye nyumba akikubali, mwambie: “Mimi pia nakubaliana nayo. Hata hivyo, je, wafikiri kwamba kwa kuwa Mungu ndiye aliyeumba vitu vyote, yeye ndiye wa kulaumiwa kwa sababu ya uovu uliopo?” Baada ya kusikiliza jibu la mtu huyo, soma Mhubiri 7:29. Fungua kitabu Ujuzi kwenye ukurasa wa 71, na usome fungu la 2. Mtie moyo mtu huyo asome kitabu hicho.
5 Warudie Wote Waliopendezwa: Huwezi kutimiza kikamili huduma yako ikiwa huwarudii wale wanaopendezwa. Unapokuwa na mazungumzo yenye kupendeza, iwe umewaachia magazeti au vichapo vinginevyo, andika jina na anwani ya mtu huyo. Jitahidi sana kusitawisha upendezi wa mtu huyo kwa kurudi bila kukawia. Kwa hakika, mpendekezee funzo la Biblia.
6 Wanafunzi wa karne ya kwanza walijua kwamba Yesu alikuwa amewaagiza “kutoa ushahidi kamili.” (Mdo. 10:42) Sisi pia tumepewa agizo hilohilo, kwa kuwa ndiyo njia pekee tunayoweza kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Na tufanye yote tuwezayo tutimize huduma yetu kikamili.—2 Tim. 4:5.