Wenye Sifa za Kustahili na Kuandaliwa Vifaa ili Kufundisha Wengine
1 Musa alipowekwa rasmi kuwa mwakilishi wa Yehova, hakuhisi kustahili kutangazia Farao neno la Mungu. (Kut. 4:10; 6:12) Yeremia alionyesha kukosa kwake uhakika katika kuweza kumtumikia Yehova akiwa nabii, akimwambia Mungu kwamba hakujua jinsi ya kusema. (Yer. 1:6) Ujapokuwa ukosefu wao wa kwanza wa uhakika, manabii wote hao walithibitika kuwa mashahidi wa Yehova wasiohofu. Walikuwa wamestahilishwa na Mungu.
2 Leo, kwa sababu ya Yehova, tuna kile tunachohitaji ili tutimize huduma yetu kwa uhakika. (2 Kor. 3:4, 5; 2 Tim. 3:17) Kama mekanika mwenye seti kamili ya vyombo, tumeandaliwa kwa kufaa vifaa kutimiza huduma yetu tuliyogawiwa kwa njia ya ustadi. Katika Januari tunatoa kitabu chochote chenye kurasa 192 kilichochapishwa kabla ya 1984 na ambacho kutaniko laweza kuwa nacho. Ingawa vyombo hivi vya kiroho si vipya, vichwa vyavyo vya Kimaandiko bado ni vya kisasa na vitabu hivi vitasaidia watu wajifunze kweli. Utoaji mbalimbali ufuatao uliodokezwa waweza kufanywa upatane na kitabu chochote kinachotolewa.
3 Somo la elimu laweza kutumiwa kuanzisha kupendezwa katika Neno la Mungu. Unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema:
◼ “Leo kuna mkazo unaowekwa juu ya ubora wa elimu. Kwa maoni yako, ni aina gani ya elimu ambayo mtu apaswa kufuatia ili kumhakikishia furaha nyingi na mafanikio maishani? [Ruhusu itikio.] Manufaa za milele zaweza kupatwa na wale wanaotwaa ujuzi wa Mungu. [Soma Mithali 9:10, 11.] Kitabu hiki kinachoweza kubebeka kwa urahisi [taja kichwa cha kitabu unachotoa] kinategemea Biblia. Hicho hukazia chanzo pekee cha ujuzi uwezao kuongoza kwenye uhai udumuo milele.” Onyesha kielelezo mahususi katika kitabu na ukitoe kwa mchango wa kawaida. Ukiona upendezi panga ziara ya kurudia.
4 Unaporudi kwa mwenye nyumba ambaye ulizungumza naye umaana wa elimu ya Biblia, unaweza kusema:
◼ “Wakati wa ziara yangu iliyopita, tulizungumza juu ya Biblia kuwa chanzo cha elimu inayoweza kutuhakikishia wakati ujao wa milele. Bila shaka, inahitaji jitihada ili tujifunze yale tunayohitaji kujua kutoka Maandiko. [Soma Mithali 2:1-5.] Watu wengi huona ni vigumu kuelewa baadhi ya sehemu za Biblia. Ningependa kukuonyesha kifupi njia ambayo tumetumia kwa muda mrefu kusaidia watu wajifunze mengi zaidi kuhusu mafundisho ya msingi ya Biblia.” Ukitumia kitabu kilichoachwa, fungua mahali pafaapo na uonyeshe kifupi jinsi ya kufanya funzo la Biblia. Mwenye nyumba akipenda kuwa na funzo la kawaida, eleza kwamba utarudi ukiwa na msaada wetu wa funzo kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele.
5 Watu wengi wanataabishwa na kuteseka kwa mamilioni ya watoto ulimwenguni. Labda unaweza kumsaidia mwenye nyumba aone jinsi ambavyo Mungu huona hali mbaya hiyo, kwa kusema:
◼ “Bila shaka umeona ripoti za habari kuhusu watoto tufeni kote ambao wana njaa, ni wagonjwa, na wameachwa. Kwa nini mashirika yenye kuhusika yameshindwa kuboresha hali hiyo? [Ruhusu itikio.] Mungu anawatakia wanadamu yaliyo bora tu. Ona kile anachoahidi watoto na watu wazima, kama ilivyorekodiwa katika Biblia. [Soma Ufunuo 21:4.] Kitabu hiki [taja kichwa] huandaa mambo kuhusu ulimwengu wa Mungu ambamo kuteseka kutakoma.” Ikiwezekana, fungua kwenye picha ambayo yaonyesha Paradiso, na uizungumzie. Toa kitabu, na upange ziara nyingine.
6 Ikiwa uliongea kuhusu kuteseka kwa watoto mara ya kwanza, katika ziara ifuatayo unaweza kuendeleza mazungumzo kwa kusema:
◼ “Nilipokuwa hapa hivi majuzi, ulionyesha hangaiko kuhusu hali mbaya ya watoto ambao wanateseka kwa sababu ya familia zilizovunjika, njaa, ugonjwa, na jeuri. Inafariji kusoma katika Biblia kuhusu ulimwengu ambamo wala watoto wala watu wazima hawatakuwa wagonjwa, wenye maumivu, au kifo. Unabii katika kitabu cha Isaya unafafanua maisha bora yatakayokuja duniani.” Soma na uzungumzie Isaya 65:20-25. Elekeza kwenye funzo la Biblia la hatima katika kitabu Ujuzi.
7 Kwa kuwa sala ni zoea la kawaida kwa watu wa kidini, unaweza kuanzisha mazungumzo juu ya habari hii kwa kusema:
◼ “Kufikia hatua fulani katika maisha yetu, wengi wetu tumepata matatizo ambayo yametufanya tusali kwa Mungu tupate msaada. Lakini, wengi huhisi kwamba sala zao hazijibiwi. Hata huonekana kwamba viongozi wa kidini wanaosali hadharani kwa ajili ya amani hawasikiwi. Twasema hivyo kwa sababu vita na jeuri huendelea kusononesha wanadamu. Je, kweli Mungu huzisikiliza sala? Ikiwa husikiliza, kwa nini sala nyingi zaonekana kuwa hazijibiwi? [Ruhusu itikio.] Zaburi 145:18 hueleza kinachohitajiwa ikiwa sala zetu zitajibiwa. [Soma andiko.] Kwanza, sala kwa Mungu lazima ziwe za moyo mweupe na zipatane na kweli ipatikanayo katika Neno lake, Biblia.” Onyesha kitabu unachotoa, na ueleze kile kinachosema kuhusu thamani ya sala.
8 Unapofuatia mazungumzo yaliyopita kuhusu sala, unaweza kujaribu mfikio huu:
◼ “Nilifurahia mazungumzo yetu kuhusu sala. Bila shaka utaona mawazo ya Yesu juu ya yale tuwezayo kuomba katika sala kuwa mwongozo wenye msaada.” Soma Mathayo 6:9, 10, linaloonyesha mambo makuu yanayoonyeshwa na Yesu katika sala yake ya kigezo. Onyesha sura ya 16, “Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu,” katika kitabu Ujuzi, na uulize ikiwa unaweza kuonyesha jinsi ya kujifunza habari hiyo.
9 Wakati wa kuwapa wengine ujuzi juu ya Mungu, huenda tukauliza, “Ni nani ambaye ana sifa za ustahili wa kutosha kwa ajili ya mambo haya?” Maandiko yajibu: “Ni sisi.”—2 Kor. 2:16, 17, NW.