Kuongoza Mafunzo ya Biblia Nyumbani Yenye Maendeleo
1 Mwuguzi katika Tanzania, kijana katika Argentina, na mama katika Latvia wote hushiriki kitu gani kimoja? Kichapo 1997 Yearbook (ukurasa wa 8, 46, na 56) charipoti kwamba kwa sababu ya utayari wao wa kuwa na zaidi ya kipindi kimoja kila juma katika kitabu Ujuzi, wote watatu walifanya maendeleo ya haraka katika mafunzo yao ya Biblia nyumbani. Imependekezwa kwamba wakati wowote iwezekanapo, watangazaji wanapaswa wajitahidi kuzungumzia sura moja ya kitabu wakati wa kila kipindi. Hata hivyo, wengine huona ni vigumu kufanya hivyo. Ijapokuwa mengi zaidi yatategemea hali na wepesi wa kila mwanafunzi, walimu wazoefu wamepata mafanikio kwa kutekeleza madokezo yafuatayo.
2 Kama ilivyozungumziwa katika nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Juni 1996, ni lazima tuzoeze wanafunzi wetu kutayarisha funzo. Kuanzia mwanzo kabisa, ingekuwa vizuri kueleza na kuonyesha jinsi linavyofanywa. Waonyeshe nakala yako ya kibinafsi ya kitabu Ujuzi. Tayarisheni somo la kwanza pamoja. Saidia wanafunzi wapate mambo makuu au mafungu ya maneno ambayo yanajibu swali lililochapwa moja kwa moja kisha apige mstari au kuyatia alama. Watangazaji wengine hata wamepatia wanafunzi wao kalamu za kutia alama zile zenye rangi zinazoacha maandishi yaonekane ili kutumia. Watie moyo wasome maandiko wanapotayarisha funzo lao. Kwa kufanya hivi, pia utakuwa ukimzoeza kutayarisha na kuhudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko na Funzo la Mnara wa Mlinzi.—Luka 6:40.
3 Mwalimu mzuri atamfanya mwanafunzi aongee badala ya yeye mwenyewe kuongea sana. Yeye huepuka kukengeushwa na mambo madogo. Ni mara chache ambapo angeleta habari ya ziada. Badala ya hivyo, yeye hukazia mambo makuu ya somo. Wengine wameandalia wanafunzi fasihi ya ziada ya kuwasaidia wapate majibu ya maswali yao. Zaidi, watu wenye kupendezwa watapokea habari ya ziada yenye kina kupitia kuhudhuria mikutano ya kutaniko.
4 Huenda isiwe lazima kuangalia maandiko yote yaliyotajwa katika somo. Baadhi ya mambo makuu huenda yakaelezewa kutokana na maandiko yaliyonukuliwa katika fungu. Wakati wa pitio, kazia maandiko ya msingi ambayo yalizungumziwa na umtie moyo mwanafunzi akumbuke hayo.
5 Kila Kipindi Chapaswa Kuchukua Muda Gani?: Si lazima funzo liwe la muda wa saa moja tu. Wenye nyumba wengine wana wakati nao wanaweza kutaka kuendelea kwa muda mrefu zaidi. Au mwanafunzi huenda akataka kujifunza zaidi ya mara moja kwa juma. Hili laweza kunufaisha wale wanaoweza kufanya hivyo.
6 Kama Isaya 60:8 linavyofananisha, leo mamia ya maelfu ya wasifaji wa Yehova wapya “[wanaruka] kama wingu, na kama njiwa waendao madirishani kwao” ndani ya makutaniko ya watu wake. Sisi sote na tufanye sehemu yetu kwa kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na Yehova anapohimiza kukusanywa kwa watu wenye mfano wa kondoo.—Isa. 60:22.