“Kupanda Mbegu za Ufalme” kwa Kupelekea Watu Magazeti kwa Ukawaida
1 Wimbo 133 katika kitabu Mwimbieni Yehova Sifa una kichwa “Kupanda Mbegu za Ufalme.” Wategemea kielezi cha Yesu kinacholinganisha kazi ya kufanya wanafunzi na kupanda mbegu. (Mt. 13:4-8, 19-23) Maneno ya wimbo huo yasema hivi: “Wingi wa mbegu palipo rutuba/Wawategemea sana.” Twaweza kuongezaje matokeo katika huduma yetu? Njia moja ni kwa kutafuta na kudumisha watu wa kupelekea magazeti kwa ukawaida.
2 Malengo mbalimbali yaweza kufikiwa kwa kupelekea watu magazeti kwa ukawaida. (1) Kufanya ziara za kawaida baada ya kila majuma mawili hukuwezesha kujenga uhusiano wa kirafiki pamoja na mtu mwenye kupendezwa. (2) Waendelea kumgawia kwa ukawaida habari za kuokoa uhai zilizo katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! (3) Kupitia mazungumzo yenu huenda ukamsaidia mtu huyo afanyize hamu ya kweli ya Kimaandiko, ambayo yaweza kuongoza kwenye funzo la Biblia.—1 Pet. 2:2.
3 Jinsi ya Kupata Watu wa Kupelekea Magazeti kwa Ukawaida: Mtu aonyeshapo kupendezwa na magazeti, mweleze kwamba makala zenye kupendeza hupatikana katika kila toleo na kwamba ungefurahi kumpelekea kila baada ya majuma mawili. Baada ya kuondoka, andika jina la mtu huyo na mahali anapopatikana, tarehe ya ziara, tarehe za matoleo yaliyoangushwa, makala iliyokaziwa, na mambo ambayo yanampendeza mtu huyo hasa.
4 Waweza kuanza kwa kupelekea watu wachache tu. Kisha jitahidi kuongeza wengine ambao unaangushia magazeti. Watu unaopelekea magazeti kwa ukawaida waongezekapo, waweza kuwapanga kwa utaratibu unaofuata mahali wanakokaa ili iwe rahisi kuwapelekea wote. Weka rekodi sahihi ya matoleo yaliyoangushwa katika kila ziara unayoenda na wakati unapoenda. Tia ndani taarifa za mazungumzo na jinsi ya kuendelea kusitawisha kupendezwa kwa mtu huyo katika kweli katika ziara ifuatayo.
5 Tia Ndani Wafanyabiashara na Wataalamu: Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba wenye duka na wataalamu wengine yamkini watakubali magazeti yetu kwa ukawaida. Hata mzee mmoja alimfanya meya wa mji wake awe mmoja wa watu ambao yeye huwapelekea magazeti kwa ukawaida. Mhubiri alianzisha funzo na mwenye kampuni ya vifaa vya ujenzi aliye na umri wa miaka 80 baada ya kumpelekea magazeti kwa miaka 10 mfululizo!
6 Dada painia aliingia kwenye duka na kukuta wenzi waliooana ambao hawakumkaribisha kwa uchangamfu. Hata hivyo, kwa kuwa walikubali magazeti, aliamua kutia ndani wenzi hao waliooana kwenye orodha yake ya watu wa kupelekea magazeti kwa ukawaida. Baada ya muda, dada huyo alitaka kuacha kuwarudia kwa sababu hawakuwa wenye urafiki na hawakuwa na mengi ya kusema kamwe, hata alipowauliza swali la maoni. Lakini dada huyo alisali kuhusu jambo hilo na mwishowe akawaangushia wenzi hao waliooana kitabu Kuishi Milele. Baada ya kukisoma, mke alisema hivi kwa mshangao: “Hatimaye, nimeipata kweli!” Funzo la Biblia lilianzishwa, na baadaye wenzi hao waliooana wakabatizwa. Ustahimilivu wa painia huyo kwa kweli ulizaa matunda mazuri.
7 Kufanya Ziara za Kurudia: Unapopokea gazeti jipya, soma kila makala. Tafuta mambo yatakayomvutia kila mtu unayempelekea magazeti kwa ukawaida. Kisha urudipo, waweza kusema hivi: “Niliposoma makala hii, nilikufikiria na jinsi inavyoweza kukupendeza.” Wahubiri wa umri wote wanaweza kufurahia kuwa na watu wa kupelekea magazeti kwa ukawaida. Hata mtoto mchanga aweza kusema hivi: “Nimefurahi kukuona tena. Nakala zako za karibuni zaidi za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zimefika. Nafikiri utapenda makala hii yenye kichwa . . . ”
8 Chochea tazamio la makala zinazokuja kwa kuvuta uangalifu kwenye sanduku lenye kichwa “Katika Toleo Letu Linalofuata.” Makala zitokeapo zikiwa mfululizo, mwonyeshe hilo na umtie moyo msomaji asikose sehemu yake yoyote. Usisahau kwamba kila wakati unapomtolea mtu magazeti, mtu ambaye wewe humpelekea magazeti kwa ukawaida, waweza kuihesabu kuwa ziara ya kurudia. Na zaidi ya yote, kumbuka kwamba mradi wetu ni kusitawisha ziara hizi ziwe mafunzo ya Biblia ya nyumbani.
9 Tembelea Watu Ambao Wewe Hupelekea Magazeti kwa Ukawaida: Waweza kuwapelekea watu wote magazeti wakati wowote ufaao—katikati ya juma asubuhi, alasiri, jioni-jioni, au mwisho-juma baada ya kuhubiri nyumba hadi nyumba. Ukishindwa kuwapelekea wote magazeti kwa sababu ya kuwa mgonjwa au kuwa likizoni, mwombe mhubiri mwingine katika familia yako au kutaniko lako akupelekee magazeti hayo. Kwa njia hiyo, wale ambao wewe huwapelekea magazeti kwa ukawaida hawatakosa kupata magazeti kwa wakati.
10 Njia moja ya kupanda mbegu ya Ufalme ni kupeleka Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida kwa watu wote ambao wewe huwapelekea magazeti. Unapowafundisha kweli ya Kimaandiko, huenda wakapata maana ya lile neno la Ufalme na hatimaye kuzaa matunda ya Ufalme pamoja nawe.—Mt. 13:8, 23.