Twafundishwa na Yehova
1 Kupitia mwelekezo wa Mungu, programu ya kimataifa ya elimu yaendelea sasa katika nchi 233. Hakuna chochote kinachoweza kulinganishwa nayo ambacho ulimwengu waweza kuandaa. Mfunzi wetu Mtukufu, Yehova, anatufundisha jinsi ya kujinufaisha wenyewe sasa na vilevile kutuelimisha kwa ajili ya uhai wetu wa milele.—Isa. 30:20; 48:17.
2 Shule za Elimu ya Kimungu: Fikiria shule zinazoendelea kwa manufaa ya watu wa Yehova. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, inayofanywa kila juma katika makutaniko 87,000 hivi, huzoeza mamilioni ya wahubiri wa Ufalme wawe wahudumu wa habari njema wenye matokeo. Je, umejiandikisha? Je, wewe ni mmojawapo wa maelfu ambao walihudhuria Shule ya Utumishi wa Painia ya majuma mawili? Labda takwa la saa lililopunguziwa mapainia wa kawaida litawezesha wengi zaidi kupainia na wastahili kuhudhuria shule hii. Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ya miezi miwili, sasa ikifanywa katika lugha za msingi ulimwenguni pote, inaandaa wazee na watumishi wa huduma waseja kuchukua madaraka makubwa zaidi ya kitheokrasi. Pindi kwa pindi, wazee na watumishi wa huduma wote hupokea maagizo ya pekee katika Shule ya Huduma ya Ufalme.
3 Majengo yaliyo kwenye Kitovu cha Kielimu cha Watchtower kule Patterson, New York, yanatumiwa kutoa makao ya shule tatu za pekee, zinazotoa mazoezi ya hali ya juu ya kitheokrasi. Mtaala wa miezi mitano wa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower hutayarisha wahudumu kwa kazi ya umishonari katika maeneo ya kigeni. Washiriki wa Halmashauri ya Tawi kutoka ulimwenguni pote huhudhuria mtaala wa miezi miwili kuhusu upangaji wa mambo ya ofisi ya tawi. Katika Mei 1999 shule mpya ya miezi miwili ilianzishwa kwa ajili ya waangalizi wasafirio ikiwa na wanafunzi 48 kutoka Marekani na Kanada. Watumishi wote wa Yehova mwishowe hupokea manufaa mazuri kutokana na mazoezi ambayo Yehova anaandaa kupitia shule hizi mbalimbali.
4 Twafundishwa kwa Kusudi Gani? Mshiriki wa Baraza Linaloongoza alisema hivi: “Programu yetu ya elimu ya kisasa imekusudiwa kuwafanya watu wote wa Yehova kila mahali wawe na hali nzuri ya ukomavu inayofafanuliwa kwenye Mithali 1:1-4.” Yehova na aendelee kumpa kila mmoja wetu “ulimi wa hao wafundishwao.”—Isa. 50:4.