Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w12 9/15 kur. 13-17
  • Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • FAIDIKA KUTOKANA NA MAZOEZI YA KITHEOKRASI
  • Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Je, Unajifunza Yote Uwezayo Kutoka kwa Yehova?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2011
  • Mashahidi wa Yehova Wanazoezwa Jinsi Gani ili Kutimiza Huduma Yao?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
  • Njia za Kupanua Huduma Yako
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
w12 9/15 kur. 13-17

Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova

YEHOVA ni ‘Mfundishaji wetu Mkuu.’ (Isa. 30:20) Upendo unamchochea kuwaelimisha na kuwazoeza wengine. Kwa mfano, akichochewa na upendo mwingi sana, Yehova anamwonyesha Yesu “mambo yote anayofanya yeye mwenyewe.” (Yoh. 5:20) Kwa sababu ya upendo wake kutuelekea tukiwa Mashahidi wake, Yehova anatupatia “ulimi wa waliofundishwa,” tunapojitahidi kabisa kumheshimu na kuwasaidia wengine.​—Isa. 50:4.

Kwa kuiga mfano wa Yehova katika kuonyesha upendo, Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza inatumia shule kumi za kitheokrasi ili kuwazoeza wale walio na tamaa na hali zinazowaruhusu kujiunga na shule hizo. Je, unaziona shule hizo kuwa uthibitisho wa upendo wa Yehova?

Furahia maelezo kuhusu shule zilizopo za kitheokrasi na maelezo kutoka kwa baadhi ya wale waliohudhuria shule hizo. Kisha jiulize, ‘Ninawezaje kufaidika na elimu hii ya kimungu?’

FAIDIKA KUTOKANA NA MAZOEZI YA KITHEOKRASI

Akiwa “Mungu wa upendo,” Yehova anatupatia mazoezi yanayofanya maisha yetu yawe yenye kusudi zaidi, yanayotutayarisha kushinda magumu, na kutusaidia kupata shangwe nyingi katika huduma yetu. (2 Kor. 13:11) Sawa na wanafunzi wa karne ya kwanza, tunatayarishwa kikamili ili kuwasaidia wengine, na ‘kuwafundisha kushika mambo yote’ tuliyoamriwa.​—Mt. 28:20.

Huenda tusiweze kuhudhuria shule hizi zote, hata hivyo, tunaweza kufaidika kutokana na shule moja au kadhaa. Nasi tunaweza kuyatumia mafundisho hayo yanayotegemea Biblia. Tunaweza pia kuongeza ustadi wetu katika huduma kwa kuhubiri pamoja na watumishi wa Yehova waliozoezwa vizuri.

Jiulize hivi: ‘Je hali zangu zinaniruhusu kuhudhuria mojawapo ya shule hizo?’

Waabudu wa Yehova wanaona kuwa ni pendeleo kuunga mkono na kujifunza katika shule hizo zenye thamani. Acha mazoezi unayopata yakusaidie kumkaribia zaidi Mungu na kukusaidia kutimiza majukumu yote aliyokupa, hasa kazi yenye uharaka ya kuhubiri habari njema.

MAELEZO KUHUSU SHULE ZA KITHEOKRASI

Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

Kusudi: Kuwazoeza wahubiri watoe ushahidi na kufundisha habari njema kwa njia yenye matokeo.

Muda: Shule hii ni ya kuendelea.

Mahali: Katika Jumba la Ufalme lililo karibu. Sifa za Kustahili: Wote wanaoshirikiana kwa ukawaida na kutaniko, wanaokubali mafundisho ya Biblia, na kuishi kupatana na kanuni za Kikristo.

Kujiandikisha: Mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huandikisha wanafunzi.

Sharon, aliye na ugonjwa wa kupooza unaoitwa amyotrophic lateral sclerosis (ALS), anasema: “Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imenifundisha kufanya utafiti na kutoa habari kwa njia inayoeleweka. Nimejifunza pia kukazia fikira mahitaji ya kiroho ya wengine, na wala si yangu tu.”

Arnie, ambaye amekuwa mwangalizi anayesafiri kwa muda mrefu, anasema: “Nilizaliwa nikiwa na tatizo la kigugumizi na ilikuwa vigumu kwangu kuwatazama wengine usoni. Shule hii imenisaidia kujiamini na kujithamini. Kwa msaada wa Yehova kupitia mazoezi hayo, nimejifunza mbinu zinazonisaidia kukaza fikira na kupumua vizuri. Ninashukuru sana kwa kuwa na uwezo wa kumsifu Mungu katika kutaniko na katika huduma yangu.”

Shule ya Wanabetheli Wapya

Kusudi: Kuwasaidia Wanabetheli wapya wafanikiwe katika utumishi wao wa Betheli.

Muda: Dakika 45 kila juma kwa majuma 16.

Mahali: Betheli.

Sifa za Kustahili: Lazima uwe mshiriki wa kudumu wa familia ya Betheli au mjitoleaji wa muda aliyekubaliwa kutumika Betheli kwa mwaka mmoja au zaidi.

Kujiandikisha: Washiriki wapya wa familia ya Betheli wanaandikishwa moja kwa moja.

Demetrius, aliyehudhuria shule hiyo katika miaka ya 1980, anasema: “Shule hiyo iliboresha mazoea yangu ya kujifunza na ilinisaidia kuwa tayari kutumikia Betheli kwa muda mrefu. Walimu, masomo, na mashauri yenye kufaa yalinisaidia kusadiki kwamba Yehova ananihangaikia kwa upendo na anatamani kuona nikifanikiwa katika utumishi wangu wa Betheli.”

Kaitlyn anasema: “Nilisaidiwa kukazia fikira jambo la muhimu zaidi, yaani, kuwa mtu wa kiroho. Shule ya Wanabetheli Wapya imenisaidia kumthamini zaidi Yehova, nyumba yake, na tengenezo lake.”

Shule ya Huduma ya Ufalme

Kusudi: Kuwazoeza waangalizi wanaosafiri, wazee, na nyakati nyingine, watumishi wa huduma kushughulikia madaraka yao ya uangalizi na ya kitengenezo. (Mdo. 20:28) Hali zilizopo, mielekeo, na mahitaji ya makutaniko huzungumziwa. Shule hii hufanywa baada ya miaka michache ikitegemea uamuzi wa Baraza Linaloongoza.

Muda: Katika miaka ya hivi karibuni, shule hii imefanywa kwa kipindi cha siku mbili mpaka mbili na nusu kwa ajili ya waangalizi wanaosafiri, siku moja na nusu kwa ajili ya wazee, na siku moja kwa ajili ya watumishi wa huduma.

Mahali: Kwa kawaida, katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Sifa za Kustahili: Lazima awe mwangalizi anayesafiri, mzee, au mtumishi wa huduma.

Kujiandikisha: Wazee na watumishi wa huduma wanaostahili hualikwa na mwangalizi wa mzunguko. Ofisi ya tawi huwaalika waangalizi wanaosafiri.

“Ingawa shule hii inazungumzia mambo mengi kwa muda mfupi, inawachochea wazee na kuwasaidia kudumisha shangwe yao na ‘kuendelea kuwa kama wanaume’ katika utumishi wa Yehova. Wazee wa zamani na wapya, wanajifunza kufanya uchungaji kwa njia yenye matokeo ili kuunganishwa vyema katika ‘njia ileile ya kufikiri.’”​—Quinn (chini).

“Mazoezi haya yameonyesha usawaziko mzuri tunaopaswa kuwa nao katika kusitawisha uthamini wetu kuelekea mambo ya kiroho, yametuonya kuhusu hatari, na kutuandalia mapendekezo yanayofaa kuhusu kulitunza kundi. Ni jambo la fadhili kama nini kwa Yehova kutusaidia.”​—Michael.

Shule ya Utumishi wa Painia

Kusudi: Kuwasaidia mapainia ‘kutimiza kwa ukamili huduma yao.’​—2 Tim. 4:5.

Muda: Majuma mawili.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme.

Sifa za Kustahili: Ni lazima wawe wametumikia wakiwa mapainia wa kawaida kwa angalau mwaka mmoja au zaidi.a

Kujiandikisha: Mapainia wanaostahili hawahitaji kujiandikisha, wanapata mwaliko kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko.

“Shule hii imenisaidia kukabiliana na magumu ninayopata katika huduma na maishani mwangu,” anasema Lily (kulia). “Njia yangu ya kujifunza, kufundisha, na kuitumia Biblia imekuwa bora zaidi. Niko tayari zaidi kuwasaidia wengine, kuwaunga mkono wazee, na kuchangia ukuzi wa kutaniko.”

Brenda, ambaye amehudhuria shule hii mara mbili, anasema: “Shule hii ilinizoeza kuzama kabisa katika mambo ya kiroho kwa asilimia 100, kuimarisha dhamiri yangu, na kukazia fikira kuwasaidia wengine. Kwa kweli, Yehova ni mkarimu!”

a Ikiwa hakuna mapainia wapya wa kutosha, mapainia ambao walihudhuria shule hiyo zaidi ya miaka mitano iliyopita wanaweza kualikwa ili wahudhurie tena.

Shule ya Wazee wa Kutaniko

Kusudi: Kuwasaidia wazee washughulikie madaraka yao kutanikoni na kuboresha hali yao ya kiroho.

Muda: Siku tano.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Sifa za Kustahili: Lazima awe mzee aliyewekwa rasmi.

Kujiandikisha: Ofisi ya tawi huwaalika wazee.

Ona baadhi ya maelezo ya wanafunzi wa darasa la 92 nchini Marekani:

“Nimefaidika sana na shule hiyo, imenisaidia kujichunguza mwenyewe na kuona jinsi ninavyoweza kuwatunza kondoo wa Yehova.”

“Sasa niko tayari kujitahidi zaidi kuwatia moyo wote kwa kukazia mambo makuu katika Maandiko.”

“Nitayatumia mazoezi hayo maishani mwangu.”

Shule ya Waangalizi Wanaosafiri na Wake Zao

Kusudi: Kuwasaidia waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wayatumikie makutaniko kwa njia bora zaidi ‘wanapofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha’​—1 Tim. 5:17; 1 Pet. 5:​2, 3.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua.

Sifa za Kustahili: Ni lazima ndugu awe mwangalizi wa mzunguko au mwangalizi wa wilaya.

Kujiandikisha: Ofisi ya tawi huwaalika waangalizi wanaosafiri na wake zao.

“Uthamini wetu kuelekea ukichwa wa Yesu juu ya tengenezo uliongezeka zaidi. Tuliona uhitaji wa kuwatia moyo akina ndugu na dada tunaowatumikia na kuimarisha umoja katika kila kutaniko. Shule ilitusaidia kuelewa kuwa ingawa mwangalizi anayesafiri hutoa mashauri na kuwarekebisha ndugu pindi fulani, lengo lake kuu ni kuwasaidia waone kwamba Yehova anawapenda.”​—Joel, Darasa la 1, mwaka wa 1999.

Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja

Kusudi: Kuwatayarisha wazee na watumishi wa huduma waseja ili kutimiza majukumu zaidi katika Tengenezo la Yehova. Wahitimu wengi watapata migawo mahali popote penye uhitaji katika nchi yao. Wengine wanaweza kutumwa katika nchi nyingine ikiwa watajitolea. Baadhi ya wahitimu wanaweza kutumika wakiwa mapainia wa pekee wa muda ili kuanzisha na kupanua kazi ya kuhubiri habari njema katika maeneo ya mbali na ya mashambani.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Ofisi ya tawi huamua; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Sifa za Kustahili: Ndugu waseja wenye umri wa kati ya miaka 23 na 62 wenye afya nzuri na ambao wangependa kutumika popote pale penye uhitaji mkubwa zaidi. (Marko 10:​29, 30) Lazima wawe wametumikia wakiwa mapainia wa kawaida kwa angalau miaka miwili na pia wawe wametumikia kwa miaka miwili mfululizo wakiwa wazee au watumishi wa huduma.

Kujiandikisha: Mkutano kwa ajili ya wale ambao wangependa kuhudhuria shule hiyo hufanywa katika kusanyiko la mzunguko.

“Shule hiyo imenisaidia kuiruhusu roho ya Yehova kufanya mabadiliko ndani yangu,” anasema Rick, mwanafunzi wa darasa la 23 nchini Marekani. “Unapopewa mgawo na Yehova, anakutegemeza katika mgawo huo. Nilijifunza kwamba nikikazia fikira mapenzi ya Mungu badala ya kujikazia fikira, ataniimarisha.”

“Nilijifunza kulithamini tengenezo la Mungu ambalo ni kama muujiza katika nyakati za kisasa,” akasema Andreas, anayetumikia Ujerumani. “Mazoezi niliyopata yalinitayarisha kwa ajili ya kazi. Pia, mifano mingi iliyo katika Biblia imenifundisha kweli hii ya msingi: Ninaweza kupata shangwe ya kweli kwa kuwatumikia ndugu zangu na Yehova.”

Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo

Kusudi: Kuwapa wenzi wa ndoa mazoezi ya pekee ili waweze kutumiwa kikamili na Yehova na tengenezo lake. Wahitimu wengi watapewa mgawo wa kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi katika nchi yao. Baadhi yao huenda wakapewa mgawo katika nchi nyingine ikiwa wako tayari. Wahitimu wanaweza kutumikia wakiwa mapainia wa pekee wa muda ili kuanzisha na kupanua kazi ya kuhubiri habari njema katika maeneo ya mbali au ya mashambani.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Shule hii inafanywa nchini Marekani, na kuanzia Septemba 2012, itafanywa pia katika maeneo fulani ya ofisi za tawi ulimwenguni pote, kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.

Sifa za Kustahili: Wenzi wa ndoa wenye umri wa kati ya miaka 25 na 50 ambao wana afya nzuri, na hali zao zinawaruhusu watumikie popote penye uhitaji mkubwa zaidi, na wenye mtazamo huu: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Ni lazima wawe wamefunga ndoa kwa angalau miaka miwili na wawe wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa angalau miaka miwili mfululizo. Ni lazima mume awe amekuwa mzee au mtumishi wa huduma kwa angalau miaka miwili mfululizo.

Kujiandikisha: Mkutano hufanywa katika kusanyiko la wilaya ili kuwapa habari wale ambao wangependa kuhudhuria shule hiyo. Ikiwa hakuna mkutano kama huo katika makusanyiko nchini mwenu na ungependa kutuma ombi, unaweza kuiandikia ofisi yenu ya tawi ili upate habari zaidi.

“Majuma hayo manane yanabadili maisha kama nini na ni nafasi bora kwa wenzi wa ndoa wanaotaka kufanya mengi katika utumishi wa Yehova! Tumeazimia kuishi maisha yenye usawaziko yatakayotuwezesha kutumia wakati wetu kwa hekima.”​—Eric na Corina (juu), Darasa la 1, mwaka wa 2011.

Shule ya Gileadi

Kusudi: Kuwazoeza wanafunzi ili watumikie wakiwa wamishonari shambani katika maeneo yenye wakaaji wengi, watumike wakiwa waangalizi wanaosafiri, au Wanabetheli. Lengo ni kuimarisha na kuitegemeza kazi ya kuhubiri na kupanga mambo katika ofisi za tawi.

Muda: Miezi mitano.

Mahali: Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani.

Sifa za Kustahili: Wenzi wa ndoa ambao tayari wanatumika katika utumishi wa pekee wa wakati wote, yaani, wakiwa wamishonari walio shambani ambao hawajahudhuria shule hiyo, mapainia wa pekee, waangalizi wanaosafiri, au Wanabetheli. Ni lazima wawe wametumikia pamoja katika utumishi wa wakati wote kwa angalau miaka mitatu mfululizo. Wanapaswa kujua kusoma, kuongea, na kuandika lugha ya Kiingereza kwa ufasaha.

Kujiandikisha: Wenzi wa ndoa wanaweza kuombwa na Halmashauri ya Tawi ya kwao wajaze ombi.

Lade na Monique kutoka Marekani sasa wanatumikia Afrika. “Shule ya Gileadi ilitutayarisha kwenda mahali popote ulimwenguni, tukiwa tayari kabisa kufanya kazi na ndugu zetu wapendwa,” anasema Lade.

Monique anaongeza hivi: “Ninapotumia yale niliyojifunza kutoka katika Neno la Mungu, ninapata shangwe nyingi katika mgawo wangu. Ninaona shangwe hiyo kuwa uthibitisho zaidi wa upendo wa Yehova.”

Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Wake Zao

Kusudi: Kuwasaidia wale wanaotumikia kwenye Halmashauri za Tawi ili waweze kusimamia makao ya Betheli, kushughulikia masuala ya utumishi yanayohusu makutaniko, na kusimamia mizunguko na wilaya. Wanajifunza pia kuhusu kazi ya utafsiri, uchapishaji, kupakia na kusafirisha machapisho.

Muda: Miezi miwili.

Mahali: Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani.

Sifa za Kustahili: Ni lazima ndugu awe mshiriki wa Halmashauri ya Tawi au wa Halmashauri ya Nchi au awe amepewa mgawo huo.

Kujiandikisha: Baraza Linaloongoza huwaalika ndugu hao pamoja na wake zao.

Lowell na Cara, wa darasa la 25, wanatumikia Nigeria. “Nilikumbushwa kwamba hata niwe na shughuli nyingi kadiri gani au iwe nimepewa kazi gani, siri ya kumpendeza Yehova ni kuwa na hali nzuri ya kiroho,” anasema Lowell. “Shule hiyo pia ilikazia kwamba njia yetu ya kuwatendea wengine inapaswa kuonyesha kwamba tunaiga upendo wa Yehova kuelekea watumishi wake.”

“Jambo moja ambalo siwezi kusahau ni hili,” anaongeza Cara. “Ikiwa siwezi kueleza jambo kwa njia rahisi, ninahitaji kujifunza jambo hilo kabla ya kujaribu kuwafundisha wengine.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki