Je, Unajifunza Yote Uwezayo Kutoka kwa Yehova?
1. Yehova ana maoni gani kuhusu elimu?
1 Yehova, ‘Mfundishaji wetu mkuu,’ anataka tuwe na elimu. (Isa. 30:20) Alianza kufundisha baada ya kumuumba mwana wake mzaliwa wa kwanza. (Yoh. 8:28) Baada ya uasi wa Adamu, Yehova hakuacha kufundisha, bali kwa upendo aliendelea kuwapa maagizo wanadamu wasio wakamilifu.—Isa. 48:17, 18; 2 Tim. 3:14, 15.
2. Ni programu gani ya elimu inayoendelea sasa?
2 Leo, Yehova anaongoza programu ya kielimu iliyo kubwa kupita zote katika historia. Kama Isaya alivyotabiri, mamilioni duniani kote wanamiminika kwenye ‘mlima wa mfano wa nyumba ya Yehova.’ (Isa. 2:2) Kwa nini twende kwenye mlima wa nyumba ya Yehova? Ili kufundishwa njia za Mungu, ndiyo, kufundishwa na Yehova! (Isa. 2:3) Katika mwaka wa utumishi wa 2010, Mashahidi wa Yehova walitumia zaidi ya saa bilioni 1.6 wakihubiri na kufundisha watu kweli za Biblia. Kwa kuongezea, kila juma maagizo ya kiroho yanatolewa kwa makutaniko zaidi ya 105,000 ulimwenguni pote, na machapisho ya Kikristo yanayoelimisha yanatolewa na mtumwa mwaminifu na mwenye busara katika lugha zaidi ya 500.
3. Wewe binafsi umenufaikaje kutokana na elimu inayoandaliwa na Yehova?
3 Faidika Kikamili: Tumefaidika sana na elimu kutoka kwa Mungu. Tumejifunza kuwa Mungu ana jina na anatujali. (Zab. 83:18; 1 Pet. 5:6, 7) Tumejifunza majibu ya baadhi ya maswali muhimu zaidi maishani: Kwa nini watu huteseka na kufa? Ninaweza kupataje furaha ya kweli? Ni nini kusudi la uhai? Yehova pia ametupa mwongozo kuhusu maadili unaotuwezesha ‘kufanikisha njia yetu.’—Yos. 1:8.
4. Ni fursa gani za elimu zinazopatikana kwa ajili ya watumishi wa Mungu, na kwa nini tunapaswa kujifunza yote tuwezayo kutoka kwa Yehova?
4 Kwa kuongezea, Yehova anaandaa elimu ya pekee ili kusaidia wengi wa watumishi wake waongeze utumishi wao kwake. Katika ukurasa wa 4-6 kuna orodha ya fursa ambazo huenda zikawafaa wahubiri fulani. Hata kama hali zetu zinatuzuia tusipate mazoezi yaliyoorodheshwa, je, tunatumia kikamili elimu tunayopata sasa kutoka kwa Mungu? Je, tunawatia moyo wachanga waweke miradi ya kiroho na kufuatia elimu ya juu inayotoka kwa Mungu badala ya kufuatia elimu ya juu ya kilimwengu ambayo mara nyingi wanashauriwa na walimu na watu wengine kuifuatilia? Kujifunza yote tuwezayo kutoka kwa Yehova kutatusaidia tufurahie maisha yenye furaha sasa na uzima wa milele wakati ujao.—Zab. 119:105; Yoh. 17:3.
Programu Mbalimbali za Elimu Kupitia Tengenezo la Yehova
Madarasa ya Kujifunza Kusoma na Kuandika
• Kusudi: Kuwafundisha watu kusoma na kuandika ili waweze kusoma na kujifunza Biblia na kufundisha wengine kweli.
• Muda: Kulingana na uhitaji.
• Mahali: Jumba la Ufalme lililo karibu.
• Wanaoweza Kuhudhuria: Wahubiri wote na watu wanaopendezwa.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Wazee wa kutaniko hupanga madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika kulingana na uhitaji uliopo, na huwatia moyo wote wanaoweza kufaidika wahudhurie.
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
• Kusudi: Kuwazoeza wahubiri watoe ushahidi na kufundisha habari njema kwa njia yenye matokeo.
• Muda: Shule hii ni ya kuendelea.
• Mahali: Jumba la Ufalme lililo karibu.
• Wanaoweza Kujiandikisha: Wahubiri wote. Pia, wengine wanaoshirikiana na kutaniko kwa ukawaida, wanaokubali mafundisho ya Biblia, na ambao maisha yao yanaambatana na kanuni za Kikristo.
• Jinsi ya kujiandikisha: Zungumza na mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.
Madarasa ya Lugha za Kigeni
• Kusudi: Kuwafundisha wahubiri jinsi ya kuhubiri habari njema katika lugha nyingine.
• Muda: Miezi minne au mitano. Kwa kawaida wanaojifunza huhudhuria madarasa hayo Jumamosi asubuhi kwa saa moja au mbili.
• Mahali: Kwa kawaida, katika Jumba la Ufalme lililo karibu.
• Wanaoweza Kujiandikisha: Wahubiri wenye msimamo mzuri ambao wangependa kuhubiri katika lugha ya kigeni.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Madarasa hupangwa na ofisi ya tawi kulingana na uhitaji.
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme
• Kusudi: Kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme. Hiyo si shule, lakini chini ya mpango huo wajitoleaji hufundishwa stadi mbalimbali ili waweze kusaidia katika miradi ya ujenzi.
• Muda: Kulingana na hali za mjitoleaji.
• Mahali: Popote katika eneo lililogawiwa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa au katika maeneo mengine wanapotumikia pamoja na Kikundi cha Ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Huenda wajitoleaji wengine wakaombwa wasaidie kazi ya kutoa msaada katika maeneo ya mbali yaliyoathiriwa na msiba.
• Sifa za Kustahili: Ndugu na dada lazima wawe wamebatizwa na kuidhinishwa na baraza la wazee. Wanaweza kuwa mafundi stadi au la.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Jaza fomu ya Kingdom Hall Volunteer Worker Questionnaire (S-82) au Maombi ya Kuwa Mjitoleaji wa Ujenzi wa Majumba ya Ufalme (A-25) inayotolewa na wazee wa kutaniko lenu.
Shule ya Utumishi wa Painia
• Kusudi: Kuwasaidia mapainia ‘kutimiza kwa ukamili huduma yao.’—2 Tim. 4:5.
• Muda: Majuma mawili.
• Mahali: Uamuzi hufanywa na ofisi ya tawi; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme lililo karibu.
• Sifa za Kustahili: Wale ambao wamekuwa mapainia wa kawaida kwa angalau mwaka mmoja.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Mapainia wanaostahili hawahitaji kutuma ombi bali hupata barua ya mwaliko kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko.
Shule ya Wanabetheli Wapya
• Kusudi: Shule hii imekusudiwa kuwasaidia Wanabetheli wapya wafurahie utumishi wao Betheli.
• Muda: Saa moja kila juma kwa majuma kumi na sita.
• Mahali: Betheli.
• Sifa za Kustahili: Lazima wawe Wanabetheli wa kudumu au wajitoleaji wa muda mrefu (mwaka mmoja au zaidi).
• Jinsi ya Kujiandikisha: Washiriki wa familia ya Betheli wanaostahili hujiunga bila kujiandikisha.
Shule ya Huduma ya Ufalme
• Kusudi: Kuwazoeza wazee wa kutaniko na watumishi wa huduma washughulikie madaraka yao ya uangalizi na ya kitengenezo. (Mdo. 20:28) Shule hii hufanywa baada ya kila miaka michache kama inavyoamuliwa na Baraza Linaloongoza.
• Muda: Katika miaka ya hivi karibuni, shule hiyo imefanywa kwa siku moja na nusu kwa wazee na siku moja kwa watumishi wa huduma.
• Mahali: Kwa kawaida, katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko lililo karibu.
• Sifa za Kustahili: Lazima wawe wazee au watumishi wa huduma.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Wazee na watumishi wa huduma wanaostahili wanaalikwa na mwangalizi wa mzunguko.
Shule ya Wazee wa Kutanikoa
• Kusudi: Kuwasaidia wazee washughulikie madaraka yao kutanikoni.
• Muda: Siku tano.
• Mahali: Uamuzi hufanywa na Ofisi ya tawi; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko lililo karibu.
• Sifa za Kustahili: Lazima wawe wazee.
• Jinsi ya kujiandikisha: Wazee wanaostahili wanaalikwa na ofisi ya tawi.
Shule ya Waangalizi Wanaosafiri Pamoja na Wake Zaob
• Kusudi: Kuwawezesha waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wayatumikie makutaniko kwa njia bora zaidi na ‘wafanye kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha’ na kuwachunga wale walio chini yao.—1 Tim. 5:17; 1 Pet. 5:2, 3.
• Muda: Miezi miwili.
• Mahali: Uamuzi hufanywa na Ofisi ya tawi.
• Sifa za Kustahili: Lazima wawe waangalizi wa mzunguko au wilaya.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Waangalizi wanaosafiri wanaostahili na wake zao hualikwa na ofisi ya tawi.
Shule ya Biblia ya Ndugu Wasejac
• Kusudi: Kuwatayarisha wazee na watumishi wa huduma ambao bado hawajaoa kwa ajili ya madaraka ya ziada. Wengi wa wanaohitimu hutumwa mahali penye uhitaji katika nchi yao wenyewe. Huenda wachache wakapokea mgawo katika nchi nyingine iwapo watajitolea.
• Muda: Miezi miwili.
• Mahali: Uamuzi hufanywa na ofisi ya tawi; kwa kawaida katika Jumba la Ufalme au Jumba la Kusanyiko.
• Sifa za Kustahili: Ndugu waseja wenye umri wa kati ya miaka 23 na 62 ambao wana afya nzuri na wangependa kutumikia kina ndugu na masilahi ya Ufalme popote penye uhitaji. (Marko 10:29, 30) Lazima wawe wametumikia kwa muda usiopungua miaka miwili wakiwa watumishi wa huduma au wazee wa kutaniko.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Iwapo shule hii iko katika eneo lililo chini ya ofisi ya tawi ya nchi yenu, mkutano kwa ajili ya wale wangependa kuhudhuria hufanywa katika kusanyiko la mzunguko. Habari zaidi hutolewa katika mkutano huo.
Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristod
• Kusudi: Kuwapa wenzi wa ndoa mazoezi ya pekee ili waweze kutumiwa kikamili na tengenezo la Yehova. Wengi wa wanaohitimu watapewa mgawo wa kutumikia mahali penye uhitaji katika nchi yao. Huenda wachache wakapokea mgawo wa kutumikia katika nchi nyingine iwapo watajitolea.
• Muda: Miezi miwili.
• Mahali: Madarasa machache ya kwanza yanafanywa katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani. Baadaye, shule hiyo itafanywa mahali ambapo ofisi ya tawi itaamua, kwa kawaida katika Jumba la Kusanyiko au Jumba la Ufalme.
• Sifa za Kustahili: Wenzi wa ndoa wenye umri kati ya miaka 25 na 50, ambao wana afya nzuri, na hali zao zinawaruhusu watumikie popote penye uhitaji. Wanapaswa pia kuwa na mtazamo wa: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Isitoshe, lazima wawe wamefunga ndoa kwa angalau miaka miwili na wawe katika utumishi wa wakati wote kwa angalau miaka miwili bila kukatiza.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Iwapo kuna shule hiyo katika eneo lililo chini ya ofisi ya tawi ya nchi yenu, mkutano wa wale wanaopendezwa hufanywa katika kusanyiko la pekee. Habari zaidi hutolewa katika mkutano huo.
Shule ya Gileadi
• Kusudi: Kuwazoeza mapainia na watumishi wengine wa wakati wote kwa ajili ya utumishi wa umishonari.
• Muda: Miezi mitano.
• Mahali: Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani.
• Sifa za Kustahili: Wenzi wa ndoa ambao wamebatizwa kwa miaka mitatu na wenye umri kati ya miaka 21 na 38 wanapojaza ombi lao la kwanza. Wanapaswa kujua lugha ya Kiingereza, wawe wamefunga ndoa kwa angalau miaka miwili, na kwa sasa wawe katika utumishi wa wakati wote kwa angalau miaka miwili bila kukatiza. Wanaojaza ombi lazima wawe na afya nzuri. Mapainia wanaotumikia katika nchi za kigeni (kutia ndani wamishonari ambao hawajahudhuria shule ya Gileadi); waangalizi wanaosafiri; washiriki wa familia ya Betheli; na waliohitimu katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja, na Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo wanaweza kujaza ombi ikiwa wanastahili.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Katika ofisi za tawi zilizoteuliwa, mkutano kwa ajili ya wale wangependa kuhudhuria shule hiyo hufanywa katika kusanyiko la wilaya. Habari za ziada hutolewa katika mkutano huo. Iwapo mkutano huo haufanywi katika makusanyiko ya nchi yenu na ungependa kujiandikisha, unaweza kuandikia ofisi yenu ya tawi upate habari zaidi.
Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Wake Zao
• Kusudi: Kuwasaidia wale wanaotumikia kwenye Halmashauri za Tawi washughulikie vizuri zaidi kazi ya kusimamia makao ya Betheli, mambo yanayohusiana na utumishi katika makutaniko, na kushughulikia mizunguko na wilaya katika maeneo yao, kazi ya utafsiri, uchapishaji, kupakia na kusafirisha machapisho na kusimamia idara nyinginezo.—Luka 12:48b.
• Muda: Miezi miwili.
• Mahali: Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani.
• Sifa za Kustahili: Washiriki wa Halmashauri ya Tawi au wa Halmashauri ya Nchi na vilevile akina ndugu ambao kwa sasa si washiriki wa halmashauri hizo lakini watawekwa rasmi baada ya shule.
• Jinsi ya Kujiandikisha: Ndugu wanaostahili na wake zao wanaalikwa na Baraza Linaloongoza.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa sasa shule hiyo haipatikani katika nchi zote.
b Kwa sasa shule hiyo haipatikani katika nchi zote.
c Kwa sasa shule hiyo haipatikani katika nchi zote.
d Kwa sasa shule hiyo haipatikani katika nchi zote.